Skip navigation.
Home kabah

002 - Historia Fupi Ya Mwandishi Wa Kitabu

 

 

Historia Fupi Ya Mwandishi Al-Imaam, Al- Muhadith, Al-‘Allaamah Shaykh Muhammad Naaswirud-Diyn Al-Albaaniy

 

Amezaliwa katika mji wa Ashkodera, mji mkuu wa Albania katika mwaka 1332H (1914 C.E) katika familia ya kimasikini. Baba yake Al-Haaj Nuuh Najjaatiy Al-Albaaniy alimaliza masomo yake ya Sheria Istanbul na akarudi Albania akiwa Mwanachuoni. Baada ya kutekwa Albania na makafiri, familia yake ilihamia Damascus. Huko Shaykh al-Albaaniy alimaliza elimu yake ya kwanza na akafunzwa Qur-aan, Tajwiyd, Sayansi ya lugha ya Kiarabu, Fiqh ya madhehebu ya Hanafiy, akafunzwa matawi mengineyo ya dini na Mashaykh mbali mbali pamoja na marafiki wa baba yake.

 

Amejifunza pia kwa baba yake fani ya saa na kutengeneza kwake na akawa hodari na maarufu, nayo ndiyo iliyompatia rizki yake. Alianza kuchepua katika fani ya Hadiyth pamoja na sayansi yake inayohusiana akiwa na umri wa miaka 20 akiwa ameathirika na makala katika gazeti la Al-Manaar.

 

Alianza kufanya kazi katika fani hii akinakili kumbukumbu za Al-Haafidhw Al-'Iraaqiy 'Al-Mughniy 'An Hamlili-Asfaar Fiyl-Asfaar Fiy Takhriyj Maa Fiyl-Ihyaa Minal-Akhbaar' akiongeza tanbihi humo.

 

Akaendelea kuchimba zaidi katika fani ya Hadiyth pamoja na sayansi yake mbali mbali ingawa alivunjwa moyo na baba yake. Zaidi ya hivyo, vitabu alivyovihitaji havikupatikana katika maktaba ya baba yake ambayo ilikusanya zaidi vitabu vya Fiqh ya Hanafiy. Kwa vile hakuweza kumudu kununua vitabu alivyovihitaji aliazima kutoka maktaba maarufu ya Damascus – 'Al-Maktabat adh-Dhwaahiriyah' au mara nyingine kutoka kwa wauzaji vitabu.

 

Akawa amezama katika Sayansi ya Hadiyth hadi alikuwa akifunga duka lake na kubakia maktaba hadi masaa kumi na mbili akipumzika kwa ajili ya Swalah pekee. Hakupumzika haa kwa ajili ya kula, bali alikuwa akichukua vitafunio viwili vyepesi.

 

Mwishowe wahusika wa maktaba walimpa chumba maalum kwa ajili ya masomo yake na ufunguo wake mwenyewe aweze kuingia maktaba katika nyakati zisizo za kawaida. Mara nyingine alibakia kazini kutoka asubuhi mapema hadi 'Ishaa. Katika muda huu aliweza kuzalisha kazi nyingi za faida ambazo nyinginezo bado zinasubiri kuchapishwa.

 

Masomo ya Hadiyth ya Mjumbe wa Allaah    (صلى الله عليه وآله وسلم)yalimletea athari kubwa kwake iliyomsababisha kuacha kufuata kwa upofu madhehebu yake na badala yake akaamua kufuata na kutenda kutokana na Qur-aan na Sunnah, akifahamu kuwa ndio mwendo wa  Salafus-Swaalih (Wema Waliotangulia). Hivyo bila shaka ilibidi mara nyingine akhitilafiane na Mashaykh wakaazi, ambao walikuwa wakifuata kwa upofu madhehebu ya ki-Hanafiy, hali kadhalika Maimamu wa Kisufi na watu wa bid'ah ambao walianza kumpinga na kuwashawishi watu maarufu dhidi yake wakimuita 'Kombo la Wahaabiy'. Lakini alitiwa nguvu na baadhi ya Mashaykh watukufu wa Damascus ambao walimshikilia kuendelea, miongoni mwao; Shaykh Bahjatul Bayjaar, Shaykh 'Abdul-Fattaah – Imaam na Tawfiyq Al-Barzah (رحمهم الله).

Hivyo Shaykh alikabili upinzanii katika juhudi zake za kusitawisha Tawhiyd na Sunnah lakini alivumilia kwa subira na msimamo madhubuti.

 

Baada ya muda fulani, alianzisha darasa za kila wiki zikihudhuriwa na wanafunzi wa elimu na walimu wa vyuoni. Alifundisha vitabu mbali mbali vya 'Aqiydah, Fiqh, Uswuul na Sayansi ya Hadiyth.

 

Alianza pia kupanga safari za kila mwezi katika miji mbalimbali ya Syria na Jordan kwa ajili ya da'wah.

 

Baada ya kuchapishwa baadhi ya kazi zake, Shaykh alichaguliwa kufundisha Hadiyth katika Chuo Kikuu cha Al-Madiynah, Saudi Arabia kwa miaka mtiatu kutoka 1381 hadi 1383H ambako pia alikuwa mwanachama wa chuo kikuu hicho.

 

Baada ya miaka kadhaa alirudia kufundisha na pia kuendelea kufanya utafiti zaidi katika 'Maktabah adh-Dhwaahiriyyah' akimuachia mmoja wa ndugu zake duka lake.

 

Ametembelea nchi mbali mbali kwa ajili ya da'wah na mihadhara, miongoni mwazo ni; Qatar, Misr, Kuwait, Imarati, Hispania na Uingereza.

 

Alilazimishwa kuhama mara nyingin kutoka Syria kuelekea Jordan, kisha Syria tena, kisha Beirut, kisha Imarati, kisha tena 'Ammaan – Jordan ambako ndiko alikomalizia maisha yake.

 

Kazi zake katika fani ya Hadiyth na Sayansi yake, zinapindukia mia.

Wanafunzi wake ni wengi wanajumuisha Mashaykh wengi wa hivi sasa miongoni mwao; Shaykh Hamdiy 'Abdul-Majiyd As-Salafy, Shaykh Muhammad ‘Iyd ‘Abbaasiy, Dkt. ‘Umar Sulaymaan Al-Ashqar, Shaykh Muhammad Ibraahiym Shaqrah, Shaykh Muqbil bin Haadiy Al-Waadi’iy, Shaykh ‘Aliy Khushshaan, Shaykh Muhammad Jamiyl Zaynuu, Shaykh ‘Abdur-Rahmaan ‘Abdus-Swamad, Shaykh ‘Aliy Hasan ‘Abdul-Hamiyd Al-Halabiy, Shaykh Saalim Al-Hilaaliy na Shaykh 'Abdur-Rahmaan ‘Abdul-Khaaliq.

Hiyo ni historia ya Shaykh kwa ufupi sana, ikiwa mtu atapenda kujua historia ya mwanachuoni huyu, basi aingie kwenye tovuti ya ALHIDAAYA katika kiungo kiitwacho Mwanachuoni Wa Karne - Shaykh Al-Albaaniy na atapata maelezo kwa kirefu niliyoyakusanya kuhusiana na maisha ya Shaykh kwa upana.

 

Abu ‘Abdillaah