Skip navigation.
Home kabah

Wanawake Kuvaa Swiming Costume (Nguo Za Kuogelea) Pwani Wakiwa Na Wanaume

 

SWALI:

SWALI LANGU NIKUHUSU KAMA UNAOLEWA NA FAMILY, NA UKENDA BEACH WAO WAKAOGA NA SWIMMING COSTUME NA WEWE PIA NAWE UKAVAA NA FAMILY MCHANGANYIKO YA WAKE NA WAUME JE UNAPATA DHAMBI?  PLEASE NIJIBU KWA SABABAU NIPATE KUMWAMBIA DADA YANGU. ASANTENI

 



JIBU:

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

Shukrani zetu za dhati kwa swali lako zuri kuhusu mas-ala ya kuoga ufukweni na mavazi ya kuogelea. Mwanzo tufahamu ya kuwa Uislamu umehimiza sana mas-ala ya mazoezi na hasa kuogelea kwani Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ametuhimiza tuwafunze watoto wetu kuogolea, kulenga shabaha na kupanda vipando (farasi, ngamia, punda, gari, na kadhalika).

Hata hivyo, tufahamu kuwa Uislamu una misingi na kanuni zake kuhusu mambo tofauti. Katika kila jambo ambalo Muislamu anafanya anafaa achunge maadili ya Kiislamu.

Uislamu katika hilo umemhimiza mwanamke awe ni mwenye kujisitiri kwa kuvaa mavazi ya Kiislamu hasa anapotoka nje na hata akiwa ndani kukiwa na wanaume ambao si maharimu zake basi anafaa ajitande kabisa. Allaah Aliyetukuka Anasema:

Ewe Nabii! Waambie wake zako, na binti zako, na wake za Waumini wajiteremshie nguo zao. Hivyo ni karibu zaidi kuweza kutambulikana wasiudhiwe” (33: 59).

Hakika ni kuwa mavazi ya kuogelea huwa hayana sitara kabisa. Pia tufahamu kuwa Allaah Aliyetukuka hataki wanawake wawe ni wenye kutoka ovyo ovyo kama walivyokuwa wakitoka nje wanawake katika nyakati za ujahili kwa kujirembesha, kuwa uchi au karibu kuwa uchi na mengineo. Ikiwa hapana budi mwanamke atoke nje basi hana budi kuvaa nguo za heshima kinyume na hivyo ataingia katika ujinga. Anasema Aliyetukuka:

Na kaeni majumbani kwenu, wala msijishauwe kwa majishauwo ya kijahilia ya kizamani” (33: 33).

Jamaa za mume, hasa wa kiume ni watu ambao kisheria hawafai kuona uchi wako (mwanamke) na uchi mwanamke ni mwili mzima isipokuwa uso na viganja vya mkono. Ni vyema ikiwa mke hana budi kwenda beach basi asiogelee kabisa kwani atakuwa ameruka mipaka iliyowekwa na Allaah Aliyetukuka na Mtume Wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) wala isiwe beach ya mchanganyiko wa wanawake kwa wanaume ambapo ataona wanaume waliovaa nguo za kuogelea na hivyo kuona maeneo ya uchi yao.

Tusome makala ifuatayo tuone madhara na ubaya wa kuchanginyikana wanawake na wanaume wasio Maharimu.

Ikhtilaatw (Kuchanganyika Wanaume Na Wanawake)

Tunamuomba Allaah Aliyetukuka Amsaidie huyo dada yako na sisi sote katika kufuata maagizo ya sheria ya Kiislamu.

Na Allaah Anajua zaidi