Zingatio: Ikhlaasw Ndio Mafanikio Yetu

Zingatio: Ikhlaasw Ndio Mafanikio Yetu

 

 Naaswir Haamid

 

Alhidaaya.com

 

 

Ikhlaasw (kumtakasia nia) katika kumuabudu Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa), kukhofu shirki na kupinga machafu ndio msingi mkuu wa kuimarika Uislamu. Yanapokosekana haya ndio huzama mizizi ya Uislamu na kutositawi matawi yake. Hii ndiyo Ikhlaasw aliyokuja nayo Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), wakaishughulikia Swahaba (Radhwiya Allaahu ‘Anhum) katika kuithibitisha na kuimakinisha. Kinyume chake ni kufanya Shirki.

 

 

Shirki ni kwa mtu kumjaaliya Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) mshirika katika mambo ambayo ni haki Yake peke Yake, kama kujifanyia waabudiwa au miungu mingineyo pamoja Naye, anayaabudu au kuitii au kuitegemea au kuipenda na mambo kama haya ambayo hayastahiki kufanyiwa mwengine ila Yeye tu.

 

 

Na hili ni dhambi lisilosamehemwa kwa njia yoyote ile:

 

 إِنَّ اللَّـهَ لَا يَغْفِرُ أَن يُشْرَكَ بِهِ وَيَغْفِرُ مَا دُونَ ذَٰلِكَ لِمَن يَشَاءُ ۚ وَمَن يُشْرِكْ بِاللَّـهِ فَقَدْ ضَلَّ ضَلَالًا بَعِيدًا ﴿١١٦﴾

Hakika Allaah Haghufurii kushirikishwa; lakini Anaghufuria yasiyokuwa hayo kwa Amtakae. Na yeyote atakayemshirikisha Allaah basi kwa yakini amepotoka upotofu wa mbali. [An-Nisaa: 116]

 

 

Naye Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) hakuwa nyuma katika kupinga ushirikina, kwani ameeleza ya kwamba “Shirki ni miongoni mwa mambo saba yenye kuangamiza” [Imepokelewa na Al-Bukhaariy na Muslim] 

 

 

Halikadhalika, amesema: Mwenye kumwendea mpiga bao (mpiga ramli) akamuuliza kuhusu jambo lolote, kisha akamsadiki aliyoyasema, hazikubaliwi Swalaah zake kwa siku arobaini” [Muslim]

 

 

Hapana shaka yoyote kwamba ujumbe aliokuja nao Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ni kwa ulimwengu wote. Ni kwa sababu hii, Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) aliusambaza ujumbe wa Uislamu kwa Kosroisi – Mfalme wa Fursi na Kaizari – Mfalme wa Rumi. Alikuwa akiwaandikia:

 

 قُلْ يَا أَهْلَ الْكِتَابِ تَعَالَوْا إِلَىٰ كَلِمَةٍ سَوَاءٍ بَيْنَنَا وَبَيْنَكُمْ أَلَّا نَعْبُدَ إِلَّا اللَّـهَ وَلَا نُشْرِكَ بِهِ شَيْئًا وَلَا يَتَّخِذَ بَعْضُنَا بَعْضًا أَرْبَابًا مِّن دُونِ اللَّـهِ ۚ فَإِن تَوَلَّوْا فَقُولُوا اشْهَدُوا بِأَنَّا مُسْلِمُونَ ﴿٦٤﴾

Sema: Enyi Ahlal-Kitaabi! Njooni katika neno lililo sawa baina yetu na baina yenu, kwamba tusiabudu isipokuwa Allaah Pekee, na wala tusimshirikishe na chochote, na wala wasichukue baadhi yetu wengine kuwa miola badala ya Allaah. Wakikengeuka; basi semeni: Shuhudieni kwamba sisi ni Waislamu. [Al-‘Imraan: 64]

 

 

Inashangaza mno kuona Muislamu anamshirikisha Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Aliye Mmoja na Asiye na Mshirika. Utakuta Muislamu anapiga bao kujidanganya kuona yaliyo ghaibu! Subhaana min dhaalik. Tunaziweka nafsi zetu wapi enyi Waislamu? Ghadhabu za Rabb wetu twazijua? Wasiokuwa Waislamu wamshirikishe Rabb, basi hadi sisi Waislamu? Lahaula! Tuelewe kuwa mwenye kumwendea kahini na akamsadiki aliyoyasema, huwa amekanusha yale aliyoteremshiwa Muhammad. [Hadiyth ya Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) iliyopokelewa na al-Bazzaar]

 

 

Sehemu tofauti na wenye rika kadha wa kadha, wanashiriki kwenye vitendo hivi vichafu. Si mashamba wala mijini, si masikini wala tajiri, wote wamedhalilishwa kwa kumuachia Ibiliys kuwa ndie nahodha wa jahazi yao. Tukumbuke kuwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ameeleza: “Haingii Peponi mwenye kuamini uchawi.” (Ibn Hibbaan).

 

 

Swahaba (Radhwiya Allaahu ‘Anhum) na wale waliowafuata kwa wema (Rahimahum Allaahu), walikuwa wakiitambua ikhlaasw hii na wajibu wao juu yake, kwani wakati Rustum mkubwa wa jeshi la Kifursi alipomuuliza Rab’i bin A’amir kwenye vita vya Qaadisiya: ‘Nani nyinyi na nini ujumbe wenu?’ Rab’i alimjibu kwa kumwambia kuwa: Sisi ni watu tulioletwa na Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) kuwatoa watu kwenye ibada ya waja kuwatia kwenye ibada ya Allaah Peke Yake na kutoka kwenye dhiki ya dunia kuwatia kwenye wasaa na nafasi yake, na kutoka kwenye jeuri za dini kuwatia katika uadilifu wa Uislamu.’

 

 

Hayo ndio malengo yetu ya kuufuata Uislamu, sio sisi Waislamu kuwa ni wenye kumshirikisha Allaah kwa uganga na uchawi, kuwa na mashaka ya ulimwengu huu na kushughulika mno na kuchuma mali bila ya kubagua halali wala haramu. Uislamu ndio njia yetu iliyo nadhifu inayokubalika na nyoyo zetu, tuwe na Ikhlaasw madhubuti ili tupate kuondokana na dhulma tunayotendewa Waislamu.

 

 

 

 

Share