Skip navigation.
Home kabah

Hatari Ya Kuihama Qur-aan

16 Shawwaal1426  17-11-2005

Anasema Allaah سبحانه وتعالى   

}}وَقَالَ الرَّسُولُ يَا رَبِّ إِنَّ قَوْمِي اتَّخَذُوا هَذَا الْقُرْآنَ مَهْجُورًا{{

{{Na Mtume alikuwa akisema: Ee Mola wangu Mlezi! Hakika watu wangu wameifanya hii Qur'aan ni kitu kilichoachwa (kilichohamwa)}} Al-Furqaan: 30

Allaah سبحانه وتعالى Anatuambia jinsi Mtume صلى الله عليه وآله وسلم Alivyokuwa akilalamika kuwa watu wake wameihama na kuipuuza hii Qur'aan. Makafiri Quraysh walikuwa hawataki kusikiliza Qur'aan, na ilipokuwa ikisomwa walikuwa wakizungumza upuuzi au kuzungumza kwa sauti za juu mazungumzo mengine ili wasiisikie  na Allaah سبحانه وتعالى Akasema,

}}وَقَالَ الَّذِينَ كَفَرُوا لاَ تَسْمَعُوا لِهَذَا الْقُرْآنِ وَالْغَوْا فِيهِ لَعَلَّكُمْ تَغْلِبُون{{

{{Na waliokufuru walisema: Msiisikilize Qur'aan hii, na timueni zogo, huenda mkashinda}} Fusswilat: 26 

Hali hii ya kuipuuza Qur'aan vile vile iko miongoni mwa Waislamu hali kadhalika, ingawa Waislamu tofauti yake ni kuwa wameiamini na sio kama Makafiri Quraysh ambao ilikuwa ni dhaahiri  kuwa waliikanusha na kutoiamini.

Ma'ulamaa waliofasiri Qur'aan wameifafanua aya hiyo ya kwanza inayosema,

}}إِنَّ قَوْمِي اتَّخَذُوا هَذَا الْقُرْآنَ مَهْجُورًا{{

{{Hakika watu wangu wameifanya hii Qur'aan ni kitu kilichoachwa (kilichohamwa)}}

kuwa kuihama na kupuuza Qur'aan inawahusu watu wa aina hizi:

1)     Wasioisoma kabisa.

2)     Wanaoisoma lakini hawajifunzi maana yake.

3)    Wanaoisoma na kujifunza maana yake lakini hawafuati maamrisho yake na hawajiepushi na makatazo yake.

Kuihama Qur'aan na kuipuuza ni hatari kubwa kabisa na Mola wetu Mtukufu Ametuonya na Kututisha  katika aya nyingi kupuuza Qur'aan hii na mojawapo wa maonyo hayo ni kuwa mtu anayefanya hivyo basi atakuwa na maisha ya dhiki na hufufuliwa siku ya Qiyaamah akiwa kipofu kama ifuatavyo:

}}وَمَنْ أَعْرَضَ عَن ذِكْرِي فَإِنَّ لَهُ مَعِيشَةً ضَنكًا وَنَحْشُرُهُ يَوْمَ الْقِيَامَةِ أَعْمَى{{  

}}قَالَ رَبِّ لِمَ حَشَرْتَنِي أَعْمَى وَقَدْ كُنتُ بَصِيرًا{{

}}قَالَ كَذَلِكَ أَتَتْكَ آيَاتُنَا فَنَسِيتَهَا وَكَذَلِكَ الْيَوْمَ تُنسَى{{

{{Na atakayejiepusha na mawaidha Yangu, basi kwa yakini atapata maisha yenye dhiki, na Siku ya Qiyaamah Tutamfufua hali ya kuwa kipofu}}

{{Aseme: Ewe Mola wangu Mlezi! Mbona Umenifufua kipofu, nami nilikuwa nikiona?}}

{{(Mwenyezi Mungu) Atasema: Ndivyo vivyo hivyo. Zilikufikia ishara Zetu, nawe ukazisahau; na kadhaalika leo unasahauliwa}}

Twaaha: 124-126

Ndugu Waislamu tunaona hatari ya kuipuuza Qur'aan na kuihama basi na tujitahidi kuisoma, kujifunza maana yake na kufuata maamrisho yake na kujiepusha na makatazo yake ili tuwe miongoni mwa wale Aliowasifu Allaah سبحانه وتعالى  katika hii Qur’aan kuwa wanaisoma 'ipasavyo kusomwa' katika Aya:

}}الَّذِينَ آتَيْنَاهُمُ الْكِتَابَ يَتْلُونَهُ حَقَّ تِلاَوَتِهِ أُوْلَئِكَ يُؤْمِنُونَ بِهِ{{

{{Wale Tuliowapa Kitabu, wakakisoma kama ipasavyo kusomwa, hao ndio kweli wanakiamini}} Al-Baqarah:121

Zifuatazo ni kauli za Maswahaba رضي الله عنهم  kuhusu  'kuisoma  ipasavyo kusomwa':

Amesema Ibn Mas'uud رضي الله عنه "Naapa kwa Yule Nafsi yangu iko mikononi Mwake, Tilaawa ya kweli ni kufuata yaliohalalishwa na kuacha yaliokatazwa, kusoma kama ilivyoteremshwa, kutokubadilisha maneno katika sehemu zake na kutokuifasiri vingine na ilivyopasa kutafsiriwa" (At-Twabariy 2.567)

Ibn 'Abbaas رضي الله عنهما  amesema "Wenye kuhalalisha yaliyo halali na kukataza yalioharimishwa na hawabadilishi maneno yake".

(At-Twabariy 2.567)

'Umar bin Al-Khattwaab رضي الله عنه "Ni wale ambao inaposomwa Aya inapotajwa Rahma wanamuomba Allaah سبحانه وتعالى Rahma Yake, na wanaposoma Aya inayotaja ya adhabu, wanajikinga kwa Allaah سبحانه وتعالى nayo". (Al-Qurtubiy 2:95)

Hii ni kama alivyokuwa akifanya Mtume صلى الله عليه وآله وسلم alipokuwa akisoma aya ya Rahma alikuwa akimuomba Allaah سبحانه وتعالى Rahma Yake, na alipokuwa akisoma Aya ya adhabu alikuwa akijikinga kwa Allaah سبحانه وتعالى na adhabu.

Tunamalizia kwa maneno ya busara ya Mshairi aliyesema kuhusu Qur'aan tukimuomba Allaah سبحانه وتعالى Atujaalie kuandamana na Kitabu Chake hiki ambacho ndio uongofu wetu kamili na mwangaza utakaotutoa katika kiza na kutuingiza katika Nuru (mwanga), na ndio itakayokuwa sababu ya kufuzu kwetu Duniani na Akhera.   Aamiyn.

الله أكبر إن دين محمد               وكتابه أقوى وأقوم قيلا

Mwenyeezi Mungu Mkubwa, hakika Dini ya Muhammad na Kitabu Chake ni vitu viwili vyenye nguvu na maneno yake yanatua zaidi.

لا تتذكر الكتب السوالف عنده              طلع الصباح فأطفئوا القندنيلا

Havitajiki tena vitabu vilivyopita (Kuja kwa Qur'aan)   kumechomoza Asubuhi Basi zimeni taa

(Kwani Qur'aan ndio mwangaza hamuhitaji tena taa nyingine)

 

 ************