Kuhudhuria Sherehe Za Wanafunzi Zenye Mchanganyiko

 

Kuhudhuria Sherehe Za Wanafunzi Zenye Mchanganyiko 

 

Alhidaaya.com

 

 

Swali:

 

Assalam aleikum,

 

Nimeulizwa kuhuhsu kwenda prom night yafaa? Prom night ni sherehe wanafunzi waenda kusherekea na wanawke kabla ya kuiaga shule kwenda unversity ama college. Naomba uniandikie madhara yake na aya pamoja na hadith.

 

 

Jibu:

 

AlhamduliLLaah - Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salamu zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

 

Inatakiwa tufahamu kuwa sherehe zozote ambazo tutafanya ni lazima ziende sambamba na mafunzo ya Dini yetu tukufu. Katika yale yaliyokatazwa na Dini ni kuwa na sherehe ya kijahiliya ambazo zinakwenda kinyume na maadili ya Uislamu.

 

 

Miongoni mwa yaliyokatazwa ni kuhudhuria michanganyiko baina ya wanaume na wanawake pasi na kuchunga muruwa wa Dini. Katika hali hiyo mwanaume na mwanamke wanakaa na kuzungumza baina yao na hata kuingia katika mengine. Hata ikiwa hawatakaa katika hali hiyo pia itakuwa haifai kwani waliohudhuria watakuwa wameikaribia zinaa iliyokatazwa.  Allaah Aliyetukuka Anasema:

وَلَا تَقْرَبُوا الزِّنَىٰ ۖ إِنَّهُ كَانَ فَاحِشَةً وَسَاءَ سَبِيلًا ﴿٣٢﴾

Na wala msiikaribie zinaa. Hakika huo ni uchafu na njia mbaya kabisa. [Al-Israa: 32].

 

 

Na Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akabainisha kuwa macho yanazini, na zinaa yake ni kutazama ya haramu, masikio yanazini, na zinaa yake ni kusikiliza ya haramu. Miguu, mikono na viungo vyengine vyote vinazini kwa njia moja au nyengine kama kwenda katika haramu, kushika vya haramu na mengineo.

 

 

Mbali na hilo katika sherehe kama hiyo huwa kuna muziki na ulevi vyote vikiwa ni haramu katika Uislamu. Allaah Anasema yafuatayo kuhusu muziki:

 

وَاسْتَفْزِزْ مَنِ اسْتَطَعْتَ مِنْهُم بِصَوْتِكَ وَأَجْلِبْ عَلَيْهِم بِخَيْلِكَ وَرَجِلِكَ وَشَارِكْهُمْ فِي الْأَمْوَالِ وَالْأَوْلَادِ وَعِدْهُمْ ۚ وَمَا يَعِدُهُمُ الشَّيْطَانُ إِلَّا غُرُورًا ﴿٦٤﴾

Na wachochee punde kwa punde kiupumbavu uwawezao miongoni mwao; kwa sauti yako na waitie na wasaliti kwa kikosi chako cha farasi, na askari waendao kwa miguu, na shirikiana nao katika mali na watoto na waahidi. Lakini shaytwaan hawapi ahadi isipokuwa ni ghururi. [Al-Israa: 64} na pia,

 

وَمِنَ النَّاسِ مَن يَشْتَرِي لَهْوَ الْحَدِيثِ لِيُضِلَّ عَن سَبِيلِ اللَّـهِ بِغَيْرِ عِلْمٍ وَيَتَّخِذَهَا هُزُوًا ۚ أُولَـٰئِكَ لَهُمْ عَذَابٌ مُّهِينٌ ﴿٦﴾

Na miongoni mwa watu, yuko ambaye hununua maneno ya upuuzi ili apoteze (watu) njia ya Allaah bila elimu, na huichukulia mzaha. Hao watapata adhabu ya kudhalilisha. [Luqmaan: 6].

 

 

Kuhusu Aayah hii ya pili, Ibn Mas‘uud (Radhwiya Allaahu ‘anhu) aliapa kwa kusema kuwa makusudio yake ni muziki. Na Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikataza suala hilo.

 

 

Na ulevi unafahamika umekatazwa sio kunywa tu bali hata kukaa na anayekunywa huku ukisema mimi nakunywa soda au juisi tu.

 

 

Kwa ufupi ni kuwa mikusanyiko hiyo ya ‘prom night’ ni haramu katika Uislamu.

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share