Ukilala Peke Yako Chumbani Unapata Jini Wa Mahaba?

 

Ukilala Peke Yako Chumbani Unapata Jini Wa Mahaba?

 

Alhidaaya.com

 

 

SWALI:

 

Assalamu Aleykum 

 

Natowa Shukurani Nyingi Kwa Allaah Pia Na Toa Shukurani Kwa Ndugu Zangu Wote Wa Al Hidaaya Allaah Awajazi Majazi Mema In shaa Allaah Kwa Kutuelimisha Ndugu Zenu Wa Kislam.

 

Sifa Zote Anastahiki Allaah Ambae Ameniwezesha Kuuliza Swali Iliyojaa Moyoni Sikunyingi Na Mi Hii Mara Yangu Ya Kwanza Kujitokeza  Al Hamdulillah.

 

BISMILLAH.. Mimi ni msichana wa miaka 22 ambae sijaolewa bado nimeka miaka 2 sasa nalala peke yangu pia nimefurahi kuwa nachumba peke yangu maana nafanya ibada kwa utulivu na swali, na soma qur.an na soma dua ya kujikinga nyiradi na kwa kweli na mtegemea  ALLAH zaidi ya kila kitu sasa bibi yangu alikuja kututembelea sasa tangu aje sina raha maana namsikia kila mara akimwambia mama msichana sio vizuri kulala peke yake.. sasa mama analala na mimi kweli na mpenda mama yangu na si kama na kata kulala na mimi isipokuwa na mpenda zaidi ALLAH na naogopa adhabu yake ndio maana nimeuliza suali ili nitumie hikma kumwambia mama yangu. mama yangu analala nami nawakati yuko na baba tangu miaka kadhaa mama halali na baba  sasa analala na mi nami najua nivibaya nikimwacha nitapata dhambi maana baba saa ingine anakuja katika hali ya matamanio kumtaka nami nashindwa lakufanya najifanya nimelala na mama anamkatalia kumpa haki yake jee ni sawa nimwache tu alale kwangu...? pia huyo jida yangu anataka nilale na mdogo wangu wakike sikatai ila hafanyi ibada ata niki mpa nasaha  na shindwa kuelewa  pia si kulala tu ata saa zozote nikika ndani  kufanya ibada huyu jida{bibi} yangu ana gomba pia mama anagomba eti nitapata majini nashindwa kuelewa nifanyaje sina raha nashindwa kumu abudu ALLAH Vizuri ata kufanya ibada ya usiku nashindwa nahofia kum bughudhi mama kalala pia ana kaa mpaka saa 6 ama 7 za usiku kuangalia tv kuamka alfajir nikimwamsha ananinyamazia 

 

ninge penda munijibu mapema ili nitatue hii mtihani pia ningependa muni send kwenye e-mail yangu iwe uwepesi kwangu kusoma. pia wasome waislam wenzangu

 

Shukran Wa Fi Amanillah

 

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah - Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na Salaam zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho

 

Kwanza tunapenda na sisi kutoa shukurani kwa du'aa zenu nzuri mnazotuombea nyote mnaotuma maswali yenu pamoja na wengineo wanaoingia Al Hidaaya kutafuta faida mbali mbali. Tunamuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta'aala)   Atutakabalie hizo du'aa na Atuzidishie uwezo wa kuelimishana kwa kadiri Anavyotujaalia. Aamiyn

 

Shukran dada yetu kwa swali lako hilo ambalo limemgusa kila mmoja kati yetu. Pia tunakuombea kila la kheri katika kupata ufumbuzi wa haraka na nasaha za kweli. Pia ni shukrani kwako kutambua kuwa sisi ndugu zako katika Al Hidaaya tunaweza kukupatia nasaha hizo zinazohitajika kwa udi na uvumba katika wakati wetu huu. Tunamuomba Allaah Aliyetukuka Atupatie tawfiki katika hilo. 

 

 

Nasaha yetu ya kwanza katika tatizo hilo nyeti na linaonekana gumu ni kuendelea na kumkumbuka Allah (Subhaanahu wa Ta'aalaa), kunyenyekea Kwake na kumuomba kwa hima zaidi. Hakika Yeye Ndiye Mwenye kuondosha tatizo au shida yoyote ile na hakuna anayeweza kufanya hilo ila Yeye. Ukimtegemea Allah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) na kumcha Yeye basi Atakutolea njia ambayo hata hujaifikiria. Allah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Anasema:

 

وَمَن يَتَّقِ اللَّـهَ يَجْعَل لَّهُ مَخْرَجًا

Na yeyote anayemcha Allaah; Atamjaalia njia ya kutoka (shidani). [Atw-Twalaaq: 2].

 

Huu ni mtihani ambao unakumbana nao, na kila mmoja anajaribiwa kulingana na Imani yake aliyonayo. Rusuli na Manabii ndio walipata mitihani mikubwa zaidi kisha wale walio chini yao kwa Imani. Kutahiniwa ndio dalili ya kwamba unapendwa na Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala), lakini inatakiwa uupite mtihani huo wala usilegee na kurudi nyuma. Ukishindwa katika mtihani basi inaonyesha kuwa wewe huna istiqaamah (kwenda mwendo wa sawa, kunyooka, kuwa na msimamo). Na hilo ndilo alilousiwa Nabiy (Swalla Llaahu 'alayhi wa sallam) na Waumini na Allah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

فَاسْتَقِمْ كَمَا أُمِرْتَ وَمَن تَابَ مَعَكَ وَلَا تَطْغَوْا ۚ إِنَّهُ بِمَا تَعْمَلُونَ بَصِيرٌ﴿١١٢﴾

Basi thibitika imara kama ulivyoamrishwa na aliyetubia pamoja nawe, na wala msiruke mipaka. Hakika Yeye kwa myatendayo ni Mwenye kuona. [Huwd: 112].

 

Na Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alimwusia Sufyaan ibn ‘Abdillahi (Radhwiya Allaahu ‘anhu) kwa kumwambia: "Sema: Nimemuamini Allah, kisha uwe na msimamo" [Muslim].

 

 Subira mara zote inaleta kheri ndio Waswahili wanasema: “Subira huvuta kheri”. Tutambue kuwa hakuna dhiki ambazo zinadumu milele katika maisha ya mwanadamu, kwani baada ya dhiki inakuja faraja. Allah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Anasema:

 

إِنَّ مَعَ الْعُسْرِ يُسْرًا ﴿٦﴾

Hakika pamoja na kila ugumu kuna wepesi. [Ash-Sharh: 6].

 

Na Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: "Muhifadhi Allaah, utampata Yuko mbele yako. Mjue Allaah katika neema, Atakujua katika shida. Ujue kwamba hakika lenye kukukosa halikuwa ni la kukupata, na la kukupata halikuwa ni lenye kukukosa. Na ujue kwamba ushindi waja kwa kusubiri na kwamba faraja yaja baada ya dhiki, na hakika baada ya mazito huja mepesi" [Ahmad]. 

 

Kwa hivyo, awali ya yote usijitie dhiki kwa yanayokukumba katika mitihani kwani hiyo ni Sunnah ya Allah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kwa waja wake. Ukilinganisha mtihani wako huu na wengine kama wewe utajikuta kuwa wewe wako ni mdogo sana. Utajikuta unapofanya hayo kuwa ni mwepesi wewe katika hayo yote unayokumbana nayo na utapambana nayo kwa moyo mkunjufu na uso wa bashasha ni kama kwamba hakuna lolote.

 

Nasaha ya pili, usitoke katika utii kwa mamako maadamu hajakuamrisha kumuasi Allah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) na Nabiy wake (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam). Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Anasema:

 

وَوَصَّيْنَا الْإِنسَانَ بِوَالِدَيْهِ حَمَلَتْهُ أُمُّهُ وَهْنًا عَلَىٰ وَهْنٍ وَفِصَالُهُ فِي عَامَيْنِ أَنِ اشْكُرْ لِي وَلِوَالِدَيْكَ إِلَيَّ الْمَصِيرُ ﴿١٤﴾وَإِن جَاهَدَاكَ عَلَىٰ أَن تُشْرِكَ بِي مَا لَيْسَ لَكَ بِهِ عِلْمٌ فَلَا تُطِعْهُمَا ۖ وَصَاحِبْهُمَا فِي الدُّنْيَا مَعْرُوفًا ۖ 

Na Tumemuusia insani kwa wazazi wake wawili. Mama yake ameibeba mimba yake kwa udhaifu juu ya udhaifu, na kumwachisha ziwa katika miaka mwili; ya kwamba, unishukuru Mimi, na wazazi wako; Kwangu ndio mahali pa kuishia. Lakini wakikushikilia kuwa Unishirikishe na ambayo huna elimu nayo, basi usiwatii. Na suhubiana nao kwa wema duniani.. [Luqmaan: 14 – 15].

 

Na Akasema tena:

 

وَقَضَىٰ رَبُّكَ أَلَّا تَعْبُدُوا إِلَّا إِيَّاهُ وَبِالْوَالِدَيْنِ إِحْسَانًا ۚ إِمَّا يَبْلُغَنَّ عِندَكَ الْكِبَرَ أَحَدُهُمَا أَوْ كِلَاهُمَا فَلَا تَقُل لَّهُمَا أُفٍّ وَلَا تَنْهَرْهُمَا وَقُل لَّهُمَا قَوْلًا كَرِيمًا ﴿٢٣﴾وَاخْفِضْ لَهُمَا جَنَاحَ الذُّلِّ مِنَ الرَّحْمَةِ وَقُل رَّبِّ ارْحَمْهُمَا كَمَا رَبَّيَانِي صَغِيرًا ﴿٢٤﴾

Na Rabb wako Amehukumu kwamba: Msiabudu isipokuwa Yeye Pekee na (Ameamrisha) kuwafanyia ihsaan wazazi wawili. Kama mmoja wao akifikia uzee naye yuko pamoja nawe, au wote wawili basi usiwaambie, Uff! Na wala usiwakemee; na waambie maneno ya heshima. Na wainamishie bawa la unyenyekevu kwa huruma, na useme: Rabb wangu! Warehemu kama walivyonilea udogoni. [Al-Israa: 23 – 24]. 

 

Hizi ni ayah ambazo zinatuhimiza sana kuwatendea wema wazazi wawili na hasa mama. Jambo hilo la kulala chumba kimoja nawe hakuna tatizo wala si shida kamwe. Tatizo kubwa zaidi kama ulivyo eleza ni yeye (mamako) kutoweza kutekeleza wajibu wake kwa mumewe (babako). Hili ni tatizo kubwa sana na lau halitatuliwa basi linaweza kupelekea talaka au matatizo mengine ya kindoa na kuvunjika kwa nyumba hiyo.

 

Ni muhimu zaidi kutatua tatizo la mamako, kwani hilo likitatuliwa hayo mengine yatafuata. Katika hilo ni muhimu upate mwanamke msomi katika mas-ala ya Dini ili akusaidie au upate jamaa yako ambaye unafahamiana naye vilivyo ili ampatie nasaha mamako. Hiyo ni kuwa kila usiku babako akilala na huku amemkasirikia mamako anakuwa ni mwenye kulaaniwa na Malaika na walimwengu wote mpaka atakaporudi katika twaa. Hiyo ni njia moja na njia nyengine ni kutia kaseti au CD za mawaidha zinazoelezea kuhusu haki za mume au kijitabu kuhusu jambo hilo na uwe ni mwenye kukiweka sehemu ambayo anaweza kukiona. Hili ni jambo ambalo unaweza kufanya kumtoa yeye kulala na wewe.

 

Hata ikiwa hatakuwa ni mwenye kubadilika muache alale huko chumbani nawe ukiinuka usiku unaweza kwenda sehemu ambayo kuna nafasi ili kufanya ibada yako. Au pale pale chumbani bila ya kuwasha taa ili usimsumbue mamako au kuwasha kandili au mshumaa. Ikiwa yeye haswali hata ukimuamsha hilo lisikutie tatizo endelea kumkumbusha na kumwamsha na siku moja atakuwa ni mwenye kubadilika kwa njia ambayo ni nzuri zaidi. Kitu muhimu ni kuwa usife moyo na Allaah Aliyetukuka Yu pamoja nawe.

 

Njia nyengine ni kukubali dada yako alale nawe chumba kimoja kwani hilo litakuondolea mengi. Hilo lake la kutotaka kusikiliza unapompatia mawaidha lisikutishe kwani nasaha unazotoa huenda asiathirike sasa lakini zinakaa kwenye akili na siku moja atajirudi na kuwa msichana mwema. Ukilala naye itakuwa sahali kwako kwani utakuwa umemuondoa mama na kumpatia fursa kuweza kumtimizia haki mumewe na hilo peke yake litakuwa kubwa mbele ya Allah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) na thawabu kwa amali hiyo kubwa.

 

Muombe Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) sana na Inshaa Allaah haya yote yataondoka kama kwamba hayakuwepo katika maisha yako.

 

Tunamuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Akuepushe na balaa, shida na huo mtihani ukuondokee na uwe katika hali nzuri hapa duniani na Kesho Aakhirah. Tunamuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Akupe subira ya kuweza kukumbana na mitihani hiyo.

 

 

Na Allah Anajua zaidi

 

 

Share