Zipi Mbingu Saba Na Ardhi Saba? Ikiwa Ardhi Ni Tambarare Vipi Dunia Inazunguka?

 

Zipi Mbingu Saba Na Ardhi Saba? Ikiwa Ardhi Ni

Tambarare Vipi Dunia Inazunguka?

 

Alhidaaya.com

 

 

 

SWALI:

Pili ni naswali lingine ambalo nahitaji pia msaada wenu ili niweze kuelewa.

Allah anasema "“Allah is He Who created seven Firmaments and of the earth a similar number…” [Quran 65.12]

Je aridhi saba na mbingu saba ni zipi? naomba nitajie. 

Tatu Allaah anasema "  Earth spread out (like a carpet), mountains firm…Quran 15:19

God made earth like a carpet spread out…20:53 aya hizi nimezinakili kwa kifupi. sasa swali langu ni hili "Ikiwa aridhi imeumbwa tambarare Je dunia ni aridhi ikiwa dunia ni aridhi je vipi kuhusu ukweli wa dunia kua ni duara?

 

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah - Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na Salaam zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho

 

 

Mbingu Saba na Ardhi Saba 

 

Kwa mujibu wa wafasiri mbalimbali, ardhi ziko saba kama vile mbingu zilivyo saba. Na maelezo ya Swahaba kama Ibn Mas'uud yanathibitisha kuwa masafa ya mbingu moja hadi nyingine ni masafa ya miaka mia tano, na baina ya mbingu ya saba na Kursiy hali kadhalika na juu ya Kursiy kuna 'Arsh ambayo iko juu ya maji. (Maelezo hayo ya Kursiy na 'Arsh na Maji ni kwa faida ya nyongeza ingawa hayapo kwenye swali kwa sababu wengi wanashindwa kutofautisha baina ya Kursiy na 'Arsh.

 

Na pia si wengi wetu wanaofahamu kuwa 'Arsh ipo juu ya maji na maji hayo yapo juu ya mbingu saba. Na kwa faida zaidi, tuelewe kuwa Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Yuko juu ya 'Arsh ambayo ipo juu ya Maji na juu ya Kursiy na vilevile juu ya mbingu saba na juu ya viumbe vyote. Hakuna kitu juu Yake, Na Hakifichiki chochote katika matendo yetu  Kwake. Ametukuka na hafanani na chochote. (Maelezo haya yote yanaungwa mkono na kutiliwa nguvu na Qur-aan)

Na kwa faida nyingine kwa mujibu wa wafasiri ni kuwa baina ya hizo ardhi saba kuna viumbe ndani yake kama ilivyo kwenye Aayah hii:

تُسَبِّحُ لَهُ السَّمَاوَاتُ السَّبْعُ وَالْأَرْضُ وَمَن فِيهِنَّ ۚ 

Zinamsabihi mbingu saba na ardhi na waliomo humo. [Israa: 44]

 

Kuhusu Aayah:

اللَّـهُ الَّذِي خَلَقَ سَبْعَ سَمَاوَاتٍ وَمِنَ الْأَرْضِ مِثْلَهُنَّ 

Allaah ni Yule Aliyeumba mbingu saba na katika ardhi mfano wa hizo.. [At-Twalaaq 65:12] 

 

Ni kwamba idadi hiyo ya ardhi saba kama ilivyotajwa kuwa sawa na idadi ya mbingu. Amesema Ibnu Kathiyr katika 'Al-Bidaayah wa An-Nihaayah' kwamba kama vile Anavyosema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kuwa: 

 

إِنَّ عِدَّةَ الشُّهُورِ عِندَ اللَّـهِ اثْنَا عَشَرَ شَهْرًا فِي كِتَابِ اللَّـهِ يَوْمَ خَلَقَ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ مِنْهَا أَرْبَعَةٌ حُرُمٌ ۚ 

Hakika idadi ya miezi mbele ya Allaah ni kumi na mbili katika hukmu ya makadirio ya Allaah, (tangu) siku Aliyoumba mbingu na ardhi. Kati ya hiyo iko minne mitukufu. [At-Tawbah: 36]

 

 

Kwa hiyo idadi hiyo ni sawa kabisa kuwa ziko ardhi saba. Vile vile kama kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

أَلَمْ تَرَوْا كَيْفَ خَلَقَ اللَّـهُ سَبْعَ سَمَاوَاتٍ طِبَاقًا﴿١٥﴾   

Je, hamuoni vipi Allaah Ameumba mbingu saba tabaka tabaka? [Nuwh: 15]

 

Vile vile:

تُسَبِّحُ لَهُ السَّمَاوَاتُ السَّبْعُ وَالْأَرْضُ وَمَن فِيهِنَّ ۚ 

Zinamsabihi mbingu saba na ardhi na waliomo humo. [Israa: 44]

 

Na kauli yake hiyo 

وَمِنْ الْأَرْض مِثْلهنَّ

na katika ardhi mfano wa hizo,[At-Twalaaq:12] 

 

Vile vile ina maana ni ardhi saba kama ilivyothibitika katika Swahiyhayn

 

((مَنْ ظَلَمَ قِيدَ شِبْر مِنْ الْأَرْض طَوَّقَهُ مِنْ سَبْع أَرَضِينَ))

"Atakayechukua ardhi ya mwenzake kwa dhulma, hata kama ni shibri moja, shingo yake itazungushwa (itafungwa) kwenye ardhi saba" [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

Na katika Al-Bukhaariy imesema:

((خَسَفَ بِهِ إِلَى سَبْع أَرَضِينَ))

"Atazamishwa chini katika ardhi saba"

 

 

Kutandazwa Kwa Ardhi

 

Kuhusu Aayah: 

وَالْأَرْضَ مَدَدْنَاهَا وَأَلْقَيْنَا فِيهَا رَوَاسِيَ وَأَنبَتْنَا فِيهَا مِن كُلِّ شَيْءٍ مَّوْزُونٍ﴿١٩﴾  

Na ardhi Tumeitandaza na Tukatupa humo milima iliyosimama thabiti, na Tukaotesha humo kila kitu kwa uwiano[Al-Hijr: 19]

 

Na Aayah:

الَّذِي جَعَلَ لَكُمُ الْأَرْضَ مَهْدًا

Ambaye Amekufanyieni ardhi kuwa tandiko.. [Twaaha: 53]

 

Ni sawa pia na kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) katika Suwrah Ghaafir:

 

وَالْأَرْضَ فَرَشْنَاهَا فَنِعْمَ الْمَاهِدُونَ ﴿٤٨﴾  

Na ardhi Tumeitandaza basi uzuri ulioje wa Wenye kutayarisha. [Adh-Dhaariyaat: 48]

 

Maana ya Farsh ni tandiko kama vile matandiko ya katika nyumba na kauli nyingi zimekuja katika neno hilo mfano:

الَّذِي جَعَلَ لَكُمُ الأَرْضَ فِرَاشاً

Ambaye Amewafanyieni ardhi kuwa ni tandiko [al-Baqarah: 22] 

 

au vile vile: 

مُتَّكِئِينَ عَلَى فُرُشٍ بَطَائِنُهَا مِنْ إِسْتَبْرَقٍ

Wakiegemea kwenye matandiko ya kupumzikia, bitana yake ni kutokana na hariri nzito [Ar-Rahmaan: 54]

 

Vile vile  neno la 'Mahd' lina maana ya 'utandazaji' kama vile kusema 'kutandaza tandiko' au kutandaza vizuri, kama katika Aayah:

وَمَهَّدتُّ لَهُ تَمْهِيدًا﴿١٤﴾   

Nikamtengenezea mambo vizuri kabisa [al-Muddaththir: 14]

 

Na katika Qur-aan imetajwa kutandikwa kwa ardhi katika Aaya mbali mbali zikiwemo hizo tulizozitaja juu. 

 

Ibn Kathiyr amesema kuhusu kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)

 

وَالْأَرْضَ فَرَشْنَاهَا فَنِعْمَ الْمَاهِدُونَ ﴿٤٨﴾  

Na ardhi Tumeitandaza basi uzuri ulioje wa Wenye kutayarisha.  [Adh-Dhaariyaat: 48]

 

Ina maana :Tumeitandaza kwa wakaazi, yaani kwa ajili ya viumbe vyote vinavyoishi ardhini ili iwe wepesi kwao kuishi.  (Na waishi kwa raha kama vile yanavyoleta raha matandiko ya nyumbani, na ndio tukawekewa ardhi kavu na bahari, mito, majabali, miti, mabustani, wanyama n.k ili tuweze kuendesha maisha yetu kwa kupata mahitajio yetu yote na kuishi kwa raha).

 

 

Kuhusu Ardhi Ni Dunia Na Mzunguko Wa Ardhi 

 

Neno la ardhi inavyoelekea kutokana  na kauli za Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) na Nabiy (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) katika Qur-aan na Sunnah ni kwamba hukusudiwa ardhi nzima kwa maana dunia nzima au kama ni nchi, au kipande tu cha ardhi kwa masafa fulani. Baadhi ya dalili katika Qur-aan kama zifuatavyo:

 

Ardhi nzima yaani kama dunia nzima: 

 

Kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) 

 

1)  

لَّقَدْ كَفَرَ الَّذِينَ قَالُوا إِنَّ اللَّـهَ هُوَ الْمَسِيحُ ابْنُ مَرْيَمَ ۚ قُلْ فَمَن يَمْلِكُ مِنَ اللَّـهِ شَيْئًا إِنْ أَرَادَ أَن يُهْلِكَ الْمَسِيحَ ابْنَ مَرْيَمَ وَأُمَّهُ وَمَن فِي الْأَرْضِ جَمِيعًا ۗ وَلِلَّـهِ مُلْكُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَمَا بَيْنَهُمَا ۚ يَخْلُقُ مَا يَشَاءُ ۚ وَاللَّـهُ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ ﴿١٧﴾

Kwa yakini, wamekufuru wale waliosema: Hakika Allaah Ndiye Al-Masiyh mwana wa Maryam. Sema: Nani anayemiliki chochote mbele ya Allaah, Akitaka kumhilikisha Al-Masiyh mwana wa Maryam na mama yake na walioko ardhini wote? Na ufalme ni wa Allaah wa mbingu na ardhi na vyote vilivyo baina yake, Anaumba Atakacho. Na Allaah juu ya kila kitu ni Muweza.   [Al-Maaidah: 17] 

 

2) 

 وَإِذْ قَالَ رَبُّكَ لِلْمَلَائِكَةِ إِنِّي جَاعِلٌ فِي الْأَرْضِ خَلِيفَةً ۖ قَالُوا أَتَجْعَلُ فِيهَا مَن يُفْسِدُ فِيهَا وَيَسْفِكُ الدِّمَاءَ  

Na pindi Rabb wako Alipowaambia Malaika: Hakika Mimi Nitaweka katika ardhi khalifa. Wakasema: Utaweka humo atakayefanya ufisadi humo na kumwaga damu,.. [Al-Baqarah: 30]

 

Kwa maana Ataumba binaadamu na kuwaweka katika hii dunia.

 

Ardhi kama ni nchi

 

Kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)

 

1)

وَنَجَّيْنَاهُ وَلُوطًا إِلَى الْأَرْضِ الَّتِي بَارَكْنَا فِيهَا لِلْعَالَمِينَ ﴿٧١﴾

Na Tukamuokoa na Luutw kuelekea ardhi ambayo Tumeibariki humo kwa walimwengu. [Al-Anbiyaa: 71]

 

(ardhi ya Shaam)

2)

يَا قَوْمِ ادْخُلُوا الْأَرْضَ الْمُقَدَّسَةَ الَّتِي كَتَبَ اللَّـهُ لَكُمْ وَلَا تَرْتَدُّوا عَلَىٰ أَدْبَارِكُمْ فَتَنقَلِبُوا خَاسِرِينَ ﴿٢١﴾

Enyi kaumu yangu! Ingieni ardhi iliyotakaswa ambayo Amekuandikieni Allaah kwenu, na wala msirudi kugeuka nyuma kukimbia (kupigana) hapo mtageuka kuwa wenye kukhasirika. [Al-Maaidah: 21]

 

(Jerusalem)

 

Ardhi kama ni kipande tu cha masafa fulani:

 

Kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)

 

a)

فَبَعَثَ اللَّـهُ غُرَابًا يَبْحَثُ فِي الْأَرْضِ لِيُرِيَهُ كَيْفَ يُوَارِي سَوْءَةَ أَخِيهِ ۚ 

Kisha Allaah Akamleta kunguru akifukua katika ardhi ili amwonyeshe vipi asitiri maiti ya ndugu yake. [Al-Maaidah: 31]

 

b)

وَلَا تَمْشِ فِي الْأَرْضِ مَرَحًا ۖ إِنَّكَ لَن تَخْرِقَ الْأَرْضَ وَلَن تَبْلُغَ الْجِبَالَ طُولًا ﴿٣٧﴾

Na wala usitembee katika ardhi kwa majivuno. Hakika wewe huwezi kupasua ardhi, na wala huwezi kufikia urefu wa milima. [Al-Israa:37]

 

Mzunguko Wa Dunia:

 

Amesema Dkt. Zaghluul (Mtaalamu wa Qur-aan na Sayansi) kwamba masafa ya ardhi ni ni taqriban Milioni 510 Square Kilo Meter ikiwa ni Milioni 149 Square Meter ardhi kavu.   Hivyo kutandikwa kwa ardhi huko tunaona kuwa ni sehemu kubwa au masafa marefu sana, kwa hiyo juu ya kwamba ardhi inazunguka kama tunavyojua, kutandikwa hukuhusiani au hakuambatani na mzunguko wa dunia kwa vile masafa kutoka Kazkazini hadi Kusini na kutoka Mashariki hadi Magharibi ni makubwa sana. Na Aayah ifuatayo inathibitisha pia usemi huu kuwa Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Amejaalia ardhi kuwa ya kutua:

أَمَّن جَعَلَ الْأَرْضَ قَرَارًا وَجَعَلَ خِلَالَهَا أَنْهَارًا وَجَعَلَ لَهَا رَوَاسِيَ

Au nani Aliyeijaalia ardhi kuwa mahali pa matulio na Akajaalia baina yake mito, na Akaiwekea milima... [An-Naml: 61] 

 

Na kuhusu ardhi kutandazwa au kufanywa kuwa kama tandiko, haina maana kuwa ni flat tambarare au bapa na si umbo la 'yai',  bali  ardhi au Dunia kwa maana maarufu, umbo lake ni umbo kama tufe au kama ule mpira wanaochezea wachezaji wa rugby au American football kama wanavyoita huko mchezo huo.

 

 

Na Allah Anajua zaidi

 

Share