Kitoka Nyumba Hupewa Mke Mkubwa Pindi Mume Anapooa Mke Wa Pili?

 

Mut’ah (Kitoka Nyumba) Hupewa Mke Mkubwa Pindi Mume Anapooa Mke Wa Pili?

 

Alhidaaya.com

 

 

 

 

SWALI:

 

Assalam alaikum warahmatullahi wabarakatu..........

 

Swala langu ni kuhusu "Kitoka nyumba" ...hii ni kama ada ambayo watu wanasema kuwa anapewa mke mkubwa na mumewe atakapo kuwa yule mume ameowa mke wa pili......Je hili jambo ni la sawa ama ni uzushi tu.

 

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Rabb wa walimwengu, Swalaah na Salaam zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

 

Kuhusu Kitoka Nyumba au Kupewa mke Mut’ah (Mataa’ kwa wingi) hii Mut’ah ina maana ni kile ‘Kiliwazo’ na pia inajulikana kama ‘Kitoka Nyumba’ au ‘Masurufu Talaka’ ambacho anapewa mwanamke pindi anapoachwa na mumewe   kama Alivyotaja Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) 

 

((وَلِلْمُطَلَّقَاتِ مَتَاعٌ بِالْمَعْرُوفِ حَقًّا عَلَى الْمُتَّقِينَ))

((Na wanawake walioachwa wapewe cha kuwaliwaza kwa mujibu wa Shariy'ah. Haya ni waajibu kwa wenye taqwa)) [Al-Baqarah: 241]

 

Nayo inahusu Talaka ya mke yeyote yule ikiwa wa kwanza au wa pili, au watatu au wane.

 

Na ikiwa hicho Kitoka nyumba au haki katika sehemu nyingine za Afrika Mashariki ni pesa au kitu kingine chochote ambacho anapatiwa mke mkubwa pindi mume anapooa mke mwingine na imezoeleka hivyo, basi hiyo itakuwa ni ada ambayo inatumika katika baadhi ya makabila isiyopingana na Shariy’ah ya Kiislaam. Hili ni chimbuko katika Shariy’ah yetu ya Kiislaam inayojulikana kama ‘Urf (ada au desturi). Hivyo ikiwa wamekubaliana hayo watu wa maeneo fulani basi hakuna tatizo maadam haipingani na Shariy’ah ya Kiislaam. Lakini lisiwe ni jambo la kulazimishana.

 

Bonyeza kiungo kifutacho upate faida ziyada:

 

Mataa'u (Kiliwazo, Kistarehea, Kitoka Nyumba, Masurufu) Ya Kumpa Mke Anayeachwa

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

Share