011-Hakimu Wa Kiislamu: Sura Ya Tano

 

SURA YA TANO

 

USHAHIDI

 

 

Dhana Ya Ushahidi

 

Ushahidi ni tendo la kisheria na inaangukia chini ya fungu la habari akhbarah. Pale haki inapotokana na tukio la kiasili au tendo la mwanaadamu, Taifa inayoiwakilisha jamii ndio itakuwa na wajibu wa kuelezea ukweli wa namna ilivyotokea. Pale ukweli unapoibua haki ya mtu ulio dhahiri, Taifa linaichukua haki hiyo wenyewe (by its own motion). Kwa mfano, yatambulika kwamba nyumba A, B, X, Y na K zilivunjwa kutokana na kujengwa shule na Taifa hilo. Au, mwananchi Z, S, D, na O waliuawa kutokana na vita vilivyopiganwa na Taifa hilo.

 

Lakini, kwa kesi yoyote, ofisa wa Taifa, ambaye ni Hakimu, kama yeye mwenyewe hana uelewa binafsi wowote wa tukio, ni lazima ategemee maelezo ya shahidi. Habari hii, yaweza kuelezwa kwa njia ya matamshi ya aliyeuona ukweli huo au kwa alama au dalili traces zilizotokea pale pale wakati wa tukio. Ni ukweli ulio dhahiri kwamba haitowezekana kutoa maelezo yakinifu kama dalili au alama zimetoweka au zimeondolewa kwa makusudi. Hivyo, hakutakuwa na njia rahisi ya kupinga ukweli huo, kama ushahidi unajulikana wazi na Taifa au Hakimu.[1]

 

Kama ukweli ulio wazi umesababisha haki fulani kudaiwa, ni haki na pia ni wajibu wa kila mwananchi aliyeona kutoa habari kwa Mahkama na Taifa kwa jumla. Lakini, shahidi anaweza (kutokana na kukosa maadili) kuchagua kutotoa habari sahihi kwa yaliyotokea na tendo hilo pekee laweza kutambulika kuwa ni habari. Wajibu wa kutoa ushahidi sahihi unatambulika kuwa ni wa sifa isiyokamilika kwa namna ambayo binaadamu amejaa kasoro. Kwa mujibu wa wanachuoni wa Kiislamu, kiapo cha uongo hakitambuliki kuwa ni ushahidi, kwa vile lengo kuu la kutoa habari ni kuweka wazi wa lililotokea. Ukweli ni kwamba, kwa mujibu wa hao wanachuoni, kiapo, ushahidi au habari za uongo ni mkanganyo wa ushahidi.

 

Mahitaji ya ushahidi mara nyingi yanaibuka pale ukweli unaojadiliwa unatokana na haki ya A dhidi ya B na B akabisha. Na kwa vile ni uoni halisi wa ushahidi kwamba unatoa habari ya ukweli ili ipatikane athari kwa anayepaswa kuipata kwa uadilifu. Wanachuoni wa Kiislamu, wanasema kwamba kutoa ushahidi ni haki ya mtu aliyeona tukio ili kumuathiri yule anayedaiwa. Kazi ya Hakimu kwa hapa ni kuupa nguvu za kisheria ushahidi uliotolewa ukiwa na habari au thibati. Haki ya Hakimu ni kupatiwa ushahidi wa kweli (shahaadah). Lakini, kwa vile ni kawaida ya wanaadamu kutotoa habari sahihi ama ikiwa kwa makosa ya kuona kwake au kwa sababu ya kukosa maadili mema, ni mzigo mkubwa kwa Shari’ah kuchukua hadhari kwa lengo la kuikinga Mahkama isiburuzwe na uongo.

 

Hakutakuwa na mgongano wa ushahidi iwapo habari zote zilizotolewa ni za ukweli, ingawa kunaweza kutokea mgongano wa matamko, ambapo moja kati ya tamko laweza kuitwa ushahidi, na tamko jengine kuwa ni uongo au kosa. Kwa mnasaba wa uongo au kosa, haiwezekani kuwa ni haki au wajibu wa mtu yeyote kutamka mbele ya Mahkama na wala Mahkama haitakuwa na mamlaka ya kukubali. Hivyo kwa msingi wa wanachuoni wa Kiislamu, ushahidi kuhusiana na ukweli ni lazima uegemee upande mmoja. Kwa kubainisha kanuni hizi, Shari’ah inatengeneza kanuni namna itakayoweza kuondosha makosa na uongo. Baadhi ya mambo haya ni ya mwenendo, lakini mengine yanaonesha asili na umbali wa kiapo kuwa ni tendo la kisheria.

 

 

Kuthibitisha (Onus Of Proof)

 

Hadiyth maarufu na muhimu ambayo inatoa mwangaza juu ya vipengele vya kuthibitisha ni:

 

“Jukumu la kuthibitisha (al-Bayyinah) lipo kwa mdai na kiapo kifanywe kwa mdaiwa.”[2]

 

Neno “Bayyinah” ndani ya Hadiyth linatokana na mzizi wa neno “bayaan”, ambalo linamaanisha kuelezea kwa uwazi kabisa. Hivyo, kwa mujibu wa Hadiyth, inampasa juu ya mdai kuifanya kesi yake kuwa nzuri kwa kutoa maelezo kamili ya madai, kuvipambanua vifungu vyote vya ushahidi vinavyowezekana kutolewa na kutoa hoja za nguvu na za kulazimisha. Maelezo hayo yanatupelekea ya kwamba mdai anaweza kutoa ushahidi wa maandiko (documentary evidence), ushahidi wa mazingira (circumstantial evidence) (mambo yote yapasavyo ambavyo si dhahiri au hakika ila huelekea kuwa kwa mambo na hali zilivyokuwa) na mawazo ya mtaalamu kwa lengo la kuthibitisha madai yake.

 

Kwenye kisa maarufu ambacho kilikuwa baina ya Zabriqan bin Badr na Hutay’ah. Ambapo ilidaiwa kwamba Hutay’ah aliandika shairi lenye kumtusi Liwali Zabriqan. ‘Umar (Radhiya Allaahu ‘Anhu) akamwita Hassaan bin Thaabit, mshairi maarufu na mzuri kabisa, kutoa mawazo ya kitaalamu. Hutay’ah ameripotiwa kusema:

 

Weka rehani iliyo juu,

Usisafiri kwenye ujasusi wao huo,

Hakika wewe ndie mtafunaji,

Mvaaji baada ya sura mpya.

 

Hassaan akaamua kwamba Hutay’ah alikuwa mkosa kwa kusingizia uongo. Kwa maamuzi haya, Hutay’ah aliadhibiwa.[3]

 

Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesimuliwa akisema kama ilivyopokewa na Ummu Salamah (Radhiya Allaahu ‘Anha):

 

“Mimi ni binaadamu tu na nyinyi mnaleta migogoro yenu kwangu mimi, mukiwa wenye fasaha katika viapo vyenu kuliko wengine, ili ya kwamba nitoe hukumu kwa niaba yenu kwa mujibu wa ninayoyasikia kutoka kwenu. Hivyo, vyovyote nitakavyoamua kwa yeyote, ambapo kwa haki ni ya ndugu yake, asichukue kwani simpatii chochote ila kipande cha moto.”[4]

 

Kutokana na Hadiyth hii na kwa mujibu wa madai ya wadaawa, inaruhusiwa na ni vyema madai yakapelekwa Mahkamani kwa kesi ambayo inakuwa kubwa siku hadi siku. Hata hivyo, wadaawa wanahimizwa kuwa wakweli kwenye viapo.

 

Sheria inaeleza kuwa mtu yeyote anayehitajia Mahkama kutoa hukumu ya suala lenye haki ama wajibu, atahitajika kuthibitisha kwa kutumia hoja zake alizo nazo mkononi.[5] Mtu yeyote anayelazimika kuthibitisha hoja zake, ndiye atakayeambiwa kwamba mzigo wa kuthibitisha upo juu yake.[6] Ni kusema kwamba, mzigo wa kuthibitisha upo kwa yule ambaye iwapo hajathibitisha hoja zake atashindwa kesi yake.[7] Iwapo kuna mtu yeyote mwenye ushahidi nje ya pande za kesi (mdai au mdaiwa) atawajibika kutoa ithibati.[8] Kwa mtu ambaye hatambuliki iwapo ni yuhai au maiti, na imeelezwa kwamba yupo hai ndani ya kipindi cha miaka 30, mzigo wa kuthibitisha utakuwa juu ya yule mwenye kudai kwamba hayupo hai.[9] Katika suala la kwamba mtu fulani anamiliki mali, mzigo wa kuthibitisha kwamba hamiliki ni kwa yule anayedai hana milki ya mali hiyo.[10]

 

Mahkama inaweza kuthibitisha kuendelea kuwepo kwa kitu ambacho kinaamini kilitendeka, kwa kuzingatia matokeo asili, tabia za kibinaadamu na biashara za binafsi au za umma, katika mahusiano ya suala la kesi hiyo.[11] Kwa mfano kuna dhana kwamba shughuli za kijamii zinatayarishwa vizuri, kwamba kila mtu anayetuhumiwa na kosa la jinai kuwa ni msafi hadi ithibitishwe vyenginevyo, kwamba kitu fulani kinachothibitishwa kuwepo kinatambulika kuwa kipo hadi ithibitishwe kinyume chake.

 

 

Mawazo Ya Mtaalamu (Expert’s Opinion)

 

Ibn Farhuun ameelezea mada mahsusi kwenye fikra za kitaalamu katika kitabu cha Tabsiirah. Anasema kwamba mawazo ya mwandishi wa ramani za majengo/mjenzi katika kesi za ujenzi (migogoro kuhusiana na nyumba, kuta, paa n.k.), mawazo ya mfanyabiashara katika kesi za bei na thamani ya vitu na mawazo ya mtu wa sayansi ya utabibu yanaruhusiwa kwa mujibu wa wanachuoni walio wengi.[12]

 

Muongozo kutoka Sheria unaeleza kwamba Mahkama itakapohitaji kupata mawazo juu ya jambo geni, au la sayansi au sanaa, au uandishi wa hati, au alama za dole, mawazo ya jambo hilo kutoka kwa wataalamu wa jambo hilo yatatambulika kuwa yanafaa. Watu wanaotoa ushahidi wa mambo haya wanaitwa wataalamu.[13]

 

 

Tazkiyah

 

Kuchunguza sifa za shahidi (tazkiyah) ni kazi ya Hakimu, ambayo si rahisi kama inavyoonekana. Aidha, shahidi ni wa tabia nzuri au laa, hawezekani kutambulika kwa jamii zetu za leo. Watu hawasemi kitu kuhusiana na jamii za waovu. Na ni nani aliyelindwa kutokana na dhambi isipokuwa Mitume? Ibn Farhuun kuhusiana na hili anaeleza njia nyepesi kwamba shahidi anapofika mbele ya Hakimu, ni lazima aandike jina lake, wazee wake, anuani yake ya ukaazi, msikiti anaoswali, sura yake, uwezo wake, kazi yake na kama nyumba anayoishi ni ya kwake au laa.[14] Maelezo haya yanarahisisha kazi ya tazkiyah.

 

Sheria inaeleza kwamba, utakuwepo utaratibu wa kuwachunguza mashahidi ndani ya sheria za mwenendo wa jinai au madai.[15]

 

Katika siku ya mwanzo ya kusikiliza kesi, au wakati mwengine wowote, upande wowote wa kesi uliofika Mahkamani unaweza kuchunguza upande wa pili. Hakimu pia atakuwa na fursa ya kuchunguza pande za kesi. Uchunguzi huu unaweza kufanywa kwa wadaawa ama kwa mashahidi wao.[16]

 

 

Mashahidi Wa Mdai Na Mdaiwa

 

Pale mdaiwa anapokataa madai yaliyoletwa na mdai. Mdai ataleta ushahidi kwa mujibu wa Shari'ah. Hakimu baada ya hapo atawafanyia mashahidi tazkiyah (kuwachunguza tabia na ukweli wao) kama iilivyoelezwa vizuri na wanachuoni, baadaye atausikiliza ushahidi wao.

 

Iwapo mdai ameshindwa au hakuweza kuleta ushahidi thabiti, Hakimu kwa maelekezo ya mdai, atamlazimisha mdaiwa kuapa kama ilivyotajwa ndani ya Hadiyth na vitabu vya Fiqh. Al-Mawardi ameshauri kwamba ikiwa mdai hatodai kiapo kutoka kwa mdaiwa, madai yake yatatupwa[17].

 

Sheria kwa upande wake inaeleza kwamba mtu yeyote atawajibika kuthibitisha jambo isipokuwa pale anaposhindwa kufahamu suala lililoulizwa au kushindwa kujibu kutokana na suala lenyewe kuwa ni la kumshushia heshima.[18]

 

Mtu aliye na ugonjwa wa akili (mwenda wazimu) hazuiliki kutoa ushahidi iwapo amelielewa suala aliloulizwa. Atazuiliwa iwapo tu haelewi suala aliloulizwa.[19]

 

Shahidi asiyeweza kuzungumza (bubu), atatoa ushahidi wake kwa njia yoyote nyengine inayoweza kueleweka, iwapo kwa ishara au kwa maandishi. Lakini maandishi yake ni lazime yatiwe saini yake mbele ya Mahkama. Ushahidi unaotolewa wa maandishi kutoka kwa bubu unatambulika kuwa ni ushahidi wa mdomo.[20]

 

Upande wowote wa kesi kutoka kwa mdai au mdaiwa unaweza kuwasilisha shahidi. Shahidi huyo atawajibika kujibu masuala yatakayoulizwa kutoka kwa aliyemfikisha Mahkamani. Baadaye atawajibika kujibu masuala kutoka kwa upande wa pili unaopingana naye. Upande uliomfikisha shahidi huyo Mahkamani utapatiwa fursa tena ya kumuuliza masuala. Hii itampatia fursa upande uliomfikisha shahidi Mahkamani kurekebisha kosa lolote.[21]

 

Mfano A ni mdai na B ni mdaiwa, A amemfikisha C kuwa ni shahidi wake, na B amemfikisha D, E na F kama ni mashahidi wake. A ataanza kumuuliza shahidi wake C, baadaye B ataendelea kumuuliza masuala shahidi C, A atapatiwa tena fursa ya mwisho kumuuliza shahidi wake C. Utaratibu huu ndio utatatumika kwa A dhidi ya mashahidi D, E na F.

 

 

Nukuul (Kiapo)

 

Kanuni kuu iliyopo kwa Shari’ah ya Kiislamu kuhusiana na ushahidi ni kwamba, agizo au amri ya Mahkama iegemezwe inavyowezekana kwenye uhakika na sio kubahatisha. Wale ambao ni wazoefu wa mfumo wa mwenendo wa kileo, wameganda kufikiria kwamba kanuni hizi, ambazo zinaacha kidogo au kutokana na nguvu yoyote Mahkama katika kuzichunguza sifa na uaminifu wa kiapo. Hata hivyo, mengi ambapo wanajaribu kudhania kuyabania, yanapelekea kwa upande fulani kuwa na athari kwenye kesi nyingi katika kuyakataa malengo yao wenyewe. Kwa upande mwengine, inaweza kuzungumzwa kwamba kanuni za mwenendo wa Shari'ah za Kiislamu zinapelekea kumaliza haraka migongano na madai, ambapo mifumo ya sasa ya mwenendo na kesi umebanwa kutofanikisha hili.

 

Pale itakapotokezea kuwepo majibizano ya madai na tuhuma nyenginezo, pande zote mbili watalazimika kuleta ushahidi na kutoa kiapo iwapo hawakuweza kuleta ushahidi thabiti. Lakini nini itakuwa khatamu ya kesi? Hii itategemea na uzuri wa kesi na asili ya kila kesi. Na hakuna utaratibu maalum kuhusiana na viapo vya pamoja (tahaluf).

 

Mdai anapokataa kuchukua kiapo, kesi itahukumiwa dhidi yake. Hata hivyo, Imaam ash-Shafi’iy anaeleza kuwa kwenye kesi hii, hukumu, haitatolewa kumpendelea mdai mpaka yeye mwenyewe (mdai) aape[22]. Katika ushahidi wao, ash-Shafi’iy anatumia Hadiyth maarufu ya Sayyidna ‘Uthmaan kupeleka malalamiko mbele ya Khaliyfah Sayyidna ‘Umar dhidi ya Miqdaad (Radhiya Allaahu ‘Anhum). Miqdaad akashikilia ‘Uthmaan athibitishe. Sayyidna ‘Umar akakubaliana naye kwa kusema: “Miqdaad ametenda (amesema) kwa mujibu wa haki (kweli).

 

Kwa upande wa Hanafi, wanatumia Hadiyth inayosema “Jukumu la kuthibitisha ni juu ya mdai na kiapo kichukuliwe na mdaiwa.”[23]

 

Kwa ushahidi wa Hanafi, wametumia kesi ya Hadhramawt iliyoletwa mbele ya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na ni vyema ikaelezwa kama ilivyopokelewa na Muslim:

 

Watu wawili, mmoja kutoka Hadhramawt, na mwengine kutoka Kindah walifika mbele ya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam). Muhadhrami akasema: Ewe Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) mtu huyu amevamia ardhi yangu! Yule Mkindi akajibu: “Ardhi hii inayodaiwa ni ya kwangu ndani ya mamlaka yangu na Muhadhrami hana haki ya kudai kutokana na ardhi hiyo.” Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akamwambia Muhadhrami: “Una ushahidi wowote?” Akasema “Hapana” Mtume akasema “Utahukumiwa kwa kiapo cha mdaiwa” Muhadhrami akasema, “Ewe Mtume wa Allaah! Mtu huyo sio muadilifu, hivyo kiapo cha uongo hakina tofauti kwake.” Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akasema: “Hata hivyo, ni lazima ukubali maelezo yake chini ya kiapo.”[24]

 

Sarakhsi alipojadili mada hii, ametoa maelezo mazuri kwamba kiapo sio dalili ya kuthibitisha madai. Ni ushahidi pekee utakaokubaliwa kuthibitisha ukweli wa madai. Pale mdaiwa anapochukua kiapo, inamaanisha kwamba madai ya mdai hayajakubaliwa (na mdaiwa). Vivyo hivyo, kwa mdai kutoa kiapo, hakitothibitisha kesi yake.[25]

 

Kiapo kinaruhusiwa chini ya Sheria ya Fafanuzi – Interpretation Decree, Cap. 1, Laws of Zanzibar.[26] Sheria inaeleza kwamba, Mahkama inaweza kwa wakati unaoona unafaa, kuamuru maelezo ya hoja fulani yatolewe kwa kiapo, au kwamba kiapo cha shahidi yoyote kilichoandikwa kitolewe kwa kusomwa.[27]

 

 

Masharti Ya Kuwa Shahidi

 

Ukirudia sababu za watu kudanganyika hadi kusema uongo au yale mazingira yanayomzuia kutoa habari sahihi na yenye kufaa. Abu Yuusuf ana maoni kwamba, mtu yeyote mwenye tabia njema na mkweli ataruhusika kuwa ni shahidi hata akiwa ni masikini mwenye maisha duni.

 

Shari’ah inasisitiza juu ya masharti kadhaa ambayo Hakimu wa Kiislamu anatakiwa ayaangalie:

 

(1) Uhuru wa upendeleo na kuchukia; hivyo kiapo hakikubaliki kwa baba juu ya mtoto na kinyume chake, cha mtumwa juu ya bwana wake, kwa pande ambazo wanategemea kesi yao moja, cha mtu ambaye ana uhasidi wa upande wa pili, cha asiyekuwa Muislamu dhidi ya Muislamu na vyenginevyo.

 

(2) Utegemezi wa jumla kuhusu tabia; hivyo watu wenye shughuli zenye maadili mabaya, kama vile wataalamu wa kucheza miziki, watu wanaojulikana kuwa ni waongo, walevi au wacheza kamari, watu wasiokuwa na tabia njema kwa kujihusisha na vitendo vilivyo nje ya misingi ya Uislamu vinavyotolewa adhabu ya hadd, kama mtu ambaye ni faasiq kinyume na a’adil. Au mfano wa wale ambao tabia zao mbovu zipo juu ukilinganisha na zile nzuri. Maafisa wala rushwa walioajiriwa kwa malengo ya kunyanyasa, hawakubaliki kuwa ni mashahidi.

 

(3) Ufahamu na uwezo wa kuelewa; hivyo, mtoto mdogo, mwenda wazimu, au kipofu kwenye masuala ambayo yanahitaji kuthibitishwa kwa kiapo cha kuona, wote hawa wanakuwa hawafai kutoa ushahidi.

 

Kwa kuzuia maafa zaidi dhidi ya uwezekano wa makosa au kiapo cha uongo na pia kwa sababu huenda kwa upande mwengine kukawa na majibizano yasio na lazima. Kiapo cha shahidi mmoja kwa kawaida kinatambulika kuwa hakitoshelezi kuthibitisha dai. Hivyo, madai yaliomo kwenye masuala ya haki za watu, kwa mfano uzuiaji wa biashara isiyo na maadili haitumii kiapo hicho cha ahad. Ama baadhi ya masuala ambayo wanawake pekee wanaelewa, kama vile mtoto fulani amezaliwa na mwanamke fulani, yanaweza kuthibitishwa hata kwa kiapo cha mwanamke mmoja.

 

Masuala ambayo yanaangukia kwenye haki za umma na kuhitaji uthibitisho kamili ulio wa kweli, kama vile makosa yanayopelekea adhabu ya hadd yanaweza tu kuthibitishwa kwa ushahidi wa mashahidi wawili wa kiume na kwa kesi nyengine, ambayo ni ya uzinifu kwa mashahidi wanne wa kiume. Mwanamke anatambulika kuwa na uwezo wa chini katika masuala ya kutoa ushahidi kwa sababu ya sifa yake dhaifu.

 

Sheria inaeleza kwamba shahidi anaweza kukanywa na upande wa pili wa kesi au kwa upande uliomuita. Kukanywa huku ni katika njia zifuatazo:

 

a)    kwa ushahidi wa mtu ambaye amethibitisha kwamba shahidi huyo hafai kuaminiwa.

 

b)    amepokea hongo, rushwa au aina nyengine yoyote ya laghai ili kutoa ushahidi wake

 

c)     kwa maelezo yake yoyote ya hapo kabla yanayoonesha kukhitalifiana na maelezo anayoendelea kuyatoa sasa

 

d)    anapohusishwa na tuhuma za kuwa ni mwenye tabia mbaya kabisa kwa mfano ubakaji.[28]

 

 

Kuulizia Uwezo Wa Shahidi

 

Jambo muhimu ni Mahkama kupata maelezo ya kanuni ambazo zimewekwa kwa lengo la kuiongoza Mahkama kuelewa sifa zinazofaa kwa shahidi na ukweli wa matamko yake, pia kwa lengo la kuongoza dhidi ya uwezekano wa Mahkama kuyumbishwa kutokana na kiapo chake. Juhudi pia zinafanyika ili kuzuia uwezekano wa Mahkama kuitwa ili kuamua baina ya madai yenye viapo vyenye mgongano kwenye kesi ambapo wadaawa wanatoa tuhuma zenye mgongano na kila mmoja anaelemea kutetea tuhuma zake, kanuni zimewekwa kwa ule ushahidi unaoweza kukubalika.

 

Ni moja kati ya kanuni muhimu kwa Hakimu, kama shahidi aliyeletwa mbele na upande wa kesi kwa kutoa ushahidi utakaotambulika kuwa wa kweli, ametoa ushahidi unaotakikana dhidi ya upande wa pili na huo upande wa pili ukapinga ushahidi huo kwa madai kwamba ushahidi wake ni wa uongo au kwa hoja ya shahidi kusahau tukio, kuulizia kuhusiana na uwezo wa shahidi na zaidi ni ukweli wa yeye kuwa ni mtu wa kusahihisha. Kuulizia huku kufanywe na yeye Hakimu aidha binafsi au Mahkamani kwa msaada wa watu anaowatambua kuwa wanaweza kutegemewa na wenye kuielewa hali ya maisha na sifa za shahidi aliyetajwa. Upande mwengine pia unao uhuru wa kutoa dharura au pingamizi (jarh, ta’an) kwa ushahidi huo. Kwa kuonesha kwamba shahidi huyo hakubaliki kwa sababu ya kuwa na upendeleo, chuki binafsi au sababu nyenginezo. Uchunguzi ulio wazi kwa sifa za shahidi kwa kutumiwa kigezo cha namna ulivyo Uislamu siku za mwanzo, inasemekana kwamba ushahidi wake utatolewa kwa sababu ya kubishana na bughudha.[29]

 

Kama shahidi ni mgeni kwenye sehemu anayoishi Hakimu huyo na ndani ya mipaka yake ya Kishari'ah, basi Hakimu atalazimika kufanya uchunguzi kwa kumuulizia. Mahakimu pia wanalazimika kuweka kumbukumbu (register) za watu wanaotambulka kuwa ni ‘aadil au watu wenye kusahihisha. Pia Hakimu alipitie register hilo kila baada ya kipindi fulani.

 

Hakuna Sheria ya moja kwa moja kuhusiana na uwezo wa shahidi katika kesi. Wala hakuna kanuni juu ya kueleza uzito wa ushahidi pamoja na kupata maelezo yake. Kila kesi ina sifa yake maalum, na kila moja ni lazima isomwe vyema ili kufikia haki.[30]

 

Lengo la kesi ni kufikia kwenye ukweli, na ukweli unapatikana ndani ya ushahidi wa mashahidi. Katika kuamua iwapo Hakimu amuamini ama asimuamini shahidi, Hakimu anasaidiwa pamoja na mambo mengine, kuangalia khulqa ya shahidi. Hii ni namna ya shahidi anavyojitambulisha na anavyozungumza wakati wa kutoa ushahidi wake. Pia Hakimu anaweza kuangalia kujiamini kwa shahidi, utulivu, uoni na mfano wa hayo.

 

 

Kiapo Cha Moja Kwa Moja Na Tetesi

(Direct And Hearsay Testimony)

 

Kwa ujumla, kiapo cha moja kwa moja peke yake kina thamani ya kuthibitisha. Hivyo, kama ni jambo linawezekana kuonekana, au kama lina matamshi ya maneno kwa mtu aliyezisikia, ni lazima ushahidi uthibitishwe na shahidi aliyeona kwa macho (eyewitness). Lakini mara nyengine kiapo kisichokuwa cha moja kwa moja pia kinatumika. Kwa mfano, ukweli wa ubaba, uzazi, kifo, ndoa, uteuzi wa Hakimu, inawezekana kuthibitishwa na mtu aliyepokea habari kwa mnasaba wake kutoka kwa watu wenye sifa za kutegemewa.[31] Hata kwa masuala ya matamko mepesi ya shahidi kwamba amesikia kadha na kadha, hayatokubalika lakini aweza kuelezea ukweli wenyewe. Kwa mfano, kwamba siku ya tarehe kadha na kadha, alikuwepo Hakimu wa sehemu fulani, au fulani na fulani alikufa katika tarehe fulani. Ijapokuwa maarifa yake yataegemezwa kwenye tetesi. Kwa maneno mengine, habari zake ni lazima ziwe zimeleta imani fulani ndani ya akili yake ili kukubalika na yeye mwenyewe kama ni maarifa. Pia, kama atasema: “Sikuona hili, lakini ninalitambua” na ikabainika ni kweli, maelezo hayo yatakubalika. Ushahidi kama huo, pia unakubalika kuthibitisha ukweli wa mali kuwa ni waqfu, lakini sio kuthibitisha masharti ya ruzuku hiyo.[32] Kama mtu atamuona mwengine amehodhi mali asiyekuwa mtumwa, atalazimika kuthibitisha hilo kwa kueleza kwamba; inamilikiwa na mtu aliyehodhi, kwa sababu kuhodhi kuna maanisha umiliki.[33]

 

Inawezekana kutokea mara nyengine kwamba watu hao walioshuhudia mauziano au mabadilishano, hawatokuwepo kwa hoja ya kufariki kwao au kuwa kwao masafa ya mbali na kwamba haiwezekani kuwafikisha Mahkamani. Basi ushahidi unawezekana kupokewa kutoka kwa mtu aliyewasiliana na hao mashahidi waliofariki kama wapo mbali, kwamba walishuhudia mauziano hayo. Huu unaitwa “ushahidi juu ya kiapo” (shahaadatu ‘ala shahaadat), na unaruhusika na wanachuoni kwenye kutenda uadilifu kwa sababu ya dharura.[34]

 

Katika Sheria, ushahidi wa moja kwa moja ni ule ambao unalingana na tukio. Kwa mfano kusikika kwa sauti ya mlipuko ni ushahidi wa hoja ya nyumba kuingia moto. Pia, iwapo mtu ameona huo mlipuko ukitokea na kutolea kiapo basi itatambulika kuwa ni ushahidi wa moja kwa moja.[35]

 

Maandishi yanaweza kuthibitishwa na shahidi aliye na maandishi hayo. Ushahidi wa kutumia mdomo (oral) unaweza kuthibitishwa na mtu ambaye ameambiwa hayo maneno.

 

Hadi hapa, ushahidi wa kuthibitisha usio moja kwa moja ni wa tetesi. Kifungu 60 cha Sheria ya Ushahidi kinahitaji kwamba ushahidi wa mdomo katika kesi zote uwe ni wa moja kwa moja, hivyo ni kusema, shahidi ni lazima awe na ufahamu wa moja kwa moja wa hoja anayoyathibitisha. Kwa mfano, suala ni namna moto ulivyoanza kuwaka. Mtu aliyeuona moto ukianza kwa mlipuko anaweza kutoa ushahidi wa tukio hili, kwa sababu yeye ana ufahamu wa tukio hilo. Iwapo katika pita pita zake amemwambia mtu kuhusiana na mlipuko, mtu huyo aliyeelezwa hawezi kutoa ushahidi wa mlipuko kwa sababu ufahamu wake si chochote ila ni tetesi. Ila tu anaweza kutoa ushahidi kwamba aliambiwa kuhusu huo moto.

 

 

Kiapo Ni Lazima Kiendane Na Madai

 

Kiapo cha kisheria ni lazima kiendane na madai, vyenginevyo hakitakuwa na athari. Kwa mfano, pale dai ni kwamba mali imekuwa ikihodhiwa na mdai kwa miaka isiyozidi miwili na mashahidi wake wanasema kwamba, imekuwa mali yake kwa zaidi ya miaka miwili, hakitoruhusiwa. Ingawa, kama wangelisema kwamba mali hiyo inahodhiwa na mdai kwa chini ya miaka miwili, kiapo hicho kisingelikataliwa. Kwa sababu, ujuzi wao unawezekana umepunguwa.

 

Vile vile, kama mdai anadai shilingi milioni moja na mashahidi wanasema ni nusu yake, ushahidi utakaokubalika ni wa shilingi laki tano, na hautokubaliwa kama watasema ni zaidi ya milioni. Chukulia mfano, dai la A ni shilingi milioni moja kwa mali iliyouzwa, na mashahidi wakaeleza kwamba B anadaiwa zaidi ya shilingi milioni moja kwa A kama ni deni, hautakubaliwa.[36] Vile vile, kama kutakuwa na mgogoro wa kiapo miongoni mwa mashahidi wa mdai, ushahidi huo utatupiliwa mbali. Kama ushahidi utapingana na ukweli ulio wazi au unaonekana, hautakuwa na nguvu.

 

Kwa upande wa Sheria inaeleza kwamba kiapo ni lazima kiendane na hoja (madai) zilizoletwa kutoka kwa mdai ama mdaiwa, na hayo madai yawe yale ambayo anaweza kuyathibitisha hata kwa kiapo.[37]

 

 

Kuchagua Ushahidi

 

Chukulia mfano, wadaawa wote wanafanya tuhuma zenye kugongana ulio sahihi na asili kwa mnasaba wa jambo hilo hilo, na wote wapo tayari kutoa ushahidi. Suala linalokuja hapa; ni ushahidi wa nani utakaochukuliwa au kusikilizwa? (Tarji’uilil-bayyinah). Kwa ujumla, kanuni ni kwamba, ushahidi wa yule ambaye tuhuma inaendana na hali iliyo hakika (istis-haab al-haal) utakubaliwa. Kama tulivyoona, Mahkama haiwezi kusikiliza ushahidi kwa kukubaliana na madai ya wote. Kwa sababu, madai ya mmoja ni lazima yatakuwa ni uongo ama dhaifu na kiapo cha ushahidi huo, hakiwezi kuwa ni taarifa au habari au ushahidi.

 

Hivyo, kama mtu atapendelea kutoa ushahidi kwamba mtu alikuwa na afya nzuri kipindi fulani na yule anayepingana anataka kuthibitisha kwamba baadaye alizidiwa na homa na kupelekea kifo. Ikiwa hakuna ushahidi mwengine, ushahidi wa mwanzo utakubaliwa dhidi ya ushahidi wa pili. Sababu ni kwamba; kutokana na kutokuwepo ushahidi wa suala hilo, mtu huyo atatambulikana kuwa yuhai. Vile vile, ushahidi wa mtu anayetaka kuthibitisha kwamba mtu aliyekuwa na uwezo wa kuelewa, atasikilizwa kama ni uchaguzi dhidi ya yule anayedai kwamba alikuwa ni mwendawazimu au mpungufu wa akili katika kipindi fulani. Ushahidi kwamba bidhaa fulani ilinunuliwa, utakubaliwa kama ushahidi kwamba ilikuwa ni zawadi au amana au kodi. Na ushahidi kwamba ilikodiwa utakuwa ni uchaguzi dhidi ya kwamba ilikuwa ni amana.

 

Kama pande zote mbili wanahodhi bidhaa fulani na mmoja wao akadai kwamba bidhaa hiyo ni yake peke yake na mwengine akadai kwamba ni yao wote, ushahidi wa mwanzo utasikilizwa. Sababu ni kwamba, haki yake inakubaliwa na ushahidi wa pili. Kama, kwa upande mwengine, wote wanadai kila mmoja ana haki peke yake, wataamuliwa kuwa ni dai la wamiliki kwa pamoja, kwani hakuna hoja ya uchaguzi wa ushahidi wa mmoja dhidi ya mwengine.

 

Ndani ya Sheria, inaeleza kwamba hoja (ushahidi) ni zile ambazo zinathibitishwa mbele ya Mahkama. Kwa mfano, mtu amesikia sauti ya kitu au kuona mtu ni hoja. Au kwamba kuna vitu fulani vimehifadhiwa katika mfumo maalum katika sehemu maalum ni hoja. Hoja yenye mgogoro ni ile ambayo inabishaniwa na pande zote mbili. Hivyo, ni kazi ya Hakimu kuchagua maelezo anayoamini kuwa ni sahihi. Kwa mfano, A anaeleza kuwa hataki kuirejesha amana aliyompatia B. Kwa upande wa B, yeye anasema kuwa hana hiyo amana kabisa.[38]

 

Ni lazima Hakimu aweke kumbukumbu pale ambapo suala linapokataliwa kuulizwa (objection) kwa shahidi kutoka kwa pande yoyote au na wakili, na Mahkama ikaruhusu kufanya hilo. Kumbukumbu atakayoiweka Hakimu ni lazima ioneshe suala, jibu na pingamizi.[39]

 

Hakimu ni lazima azingatie mwenendo wa shahidi na aweke kumbukumbu maelezo yake anayotoa wakati wa kuulizwa masuala.[40] Iwapo atashindwa kuweka kumbukumbu ya maelezo, Hakimu ni lazima aandike sababu ya kushindwa huko.[41]

 

 

Ushahidi Wa Hali Halisi (tahkiymul-haal)

 

Kwenye baadhi ya kesi, ambapo pande zote mbili hawakufanikiwa kuwasilisha ushahidi wa kutosha, lakini kuna uwezekano wa mmoja wao kuwa na ushahidi wa kukusanya vipande vipande vya tokeo kwenye hali halisi (tahkiymul-haal). Basi huo ushahidi unaotokana na hali halisi utakubaliwa.

 

Kwenye kesi kama hizo, Shari’ah inaweza kumlazimisha mtu aliyetoa ushahidi huo, kufanya kiapo na mara nyengine hatolazimika.

 

Kwa mfano, pale ambapo kuna mgogoro baina ya mume na mke kuhusiana na bidhaa fulani ndani ya nyumba, kama ni bidhaa ya panga na mshale na mfano wake. Vitadhaniwa kuwa ni vya mume na tamko lake litakubaliwa na hukumu itatolewa kwa faida yake. Hukumu itatolewa ikiwa tu mke ameshindwa kuwasilisha ushahidi wowote na mume yupo tayari kula kiapo. Mfano huo huo unaweza kudhaniwa kwa faida ya mke kwa mnasaba wa vifaa vya jikoni, zulia na mfano wake.

 

Kama mfadhili atafungua kesi ya kurudishiwa zawadi aliyoitoa na aliyefadhiliwa akasema zawadi imemalizika (perished) tamko la mfadhiliwa litakubaliwa bila ya kiapo. Kama ni mdhaminiwa, tamko lake litakubaliwa kama atakula kiapo. Kama mjane atadai kuwa ni Muislamu kabla ya kifo cha mumewe aliyekuwa ni Muislamu, lakini warithi wakasema kwamba alikuwa si Muislamu tokea kabla ya kifo, tamko la warithi litakubaliwa. Sababu ni kwamba, tamko la mjane akiwa yeye ni Muislamu litashikana na madai ya warithi pale atakapofika Mahkamani na kutoa ushahidi.[42]

 

Mara nyengine, pande za kesi kuhusiana na mauziano haziwezi kukubaliana na wala yeyote kati yao hayupo tayari kutoa ushahidi, lakini wote wapo tayari kula kiapo kwa mnasaba wa kutilia nguvu madai. Mahkama itatupilia mbali mauziano hayo. Kwa mfano, mnunuzi na muuzaji wa bidhaa hawawezi kukubaliana na dai la bei ya kilichouzwa, na hamna aliye tayari kutoa ushahidi, lakini wote wapo tayari kula kiapo kutilia nguvu madai yao, Mahkama itatupilia mbali madai hayo. Sababu ni kwamba, hakuna msingi wa kupendelea tamko dhaifu la mmoja dhidi ya mwengine.


Imeamuliwa ndani ya Sheria kwamba, mazingira ambayo yatamtia mtu hatiani ni lazima yathibitishwe, na mazingira hayo yakhitimishe asili ya kosa. Kusiwe na pengo baina ya tokeo moja na jengine (mnyororo wa ushahidi – chain of evidence). Pia, mazingira yanayothibitishwa ni lazima yaendane pamoja tu na dhana ya kosa la jinai la mtuhumiwa na wala isiwe inagongana na usafi wake (innocence).[43]

 

Ushahidi Wa Kimazingira (Circumstantial Evidence)

 

Ukiacha ushahidi wa mwanaadamu, ukweli na kimazingira Qariynah inawezekana kutegemewa kama ni ushahidi. Lakini ushahidi wa kimazingira utachukuliwa kuwa na nguvu, pale tu ambapo unafikia kikomo cha uhalisi (Qaati’atan). Kwa mfano, kama mtu ameonekana akitoka kwenye nyumba isiyokaliwa na watu, mwenye khofu na wasiwasi huku amekamata kisu chenye damu, na ndani ya nyumba kuna mwili wa mtu aliyeuawa kwa kukatwa shingo. Mazingira yote haya, yatachukuliwa kuwa ni ushahidi kwamba, mtu huyo aliyeonekana akitoka, amemuua.[44]

 

Mahkama inaweza kwa upande wa Sheria, kuamini hoja fulani ingalipo. Ushahidi huo unaweza kuwa umetokana na tukio asili, tabia za mwanadamu na biashara za kibinafsi au kijamii kwa mnasaba wa kesi iliyo mkononi. Kwa mfano, mtu aliye na bidhaa zilizoibiwa mara tu baada ya kutokezea wizi atakuwa ama ni mwizi au amepokea mali ya wizi.[45]

 

 

Kutengua Kiapo/Ushahidi (Retraction)

 

Kiapo kinaweza kutenguliwa na shahidi mwenyewe kwa kubadili kile alichotolea ushahidi. Kutengua huko ni lazima kufanywe Mahkamani, vyenginevyo, hautakuwa na nguvu yoyote. Kama mashahidi watabadili ushahidi kabla ya amri kutolewa, ushahidi utabadilishwa. Lakini baada ya maamuzi kutolewa, hautaathiri amri. Kama kutengua kumefanyika pale ambapo amri ishatolewa, na kwa upande fulani ushahidi uliotolewa na kutumika kutolea amri, umesababisha hasara yoyote, mashahidi watahusika ipasavyo na hasara hiyo.

 

Sheria inaeleza kwamba njia kuu ya kuuangusha ushahidi unaotolewa na shahidi ni kwa kuoanisha maelezo yake yanayojigonga. Iwapo matamshi yake aliyotoa hapo kabla yanagongana na ushahidi, matamshi hayo ni lazima yaandikwe.[46]

 

Utenguzi wa ushahidi pia unafanywa kwa ushahidi uliotolewa na pande za kesi ukiwa tofauti. Kwa mfano, shahidi mmoja anaeleza kwamba tokeo lilitokea mchana, na mwengine anasema limetokea wakati wa usiku, na ilikuwa giza sana wala haiwezekani kuona kitu.

 

 

Kizuio (Estoppel)

 

Mara nyengine, hakuruhusiwi kutolewa ushahidi au ukweli fulani kwa mnasaba wa tabia ya anayetaka kutoa ushahidi huo. Hii inaitwa (Bayaanu adh-Dharuurah) lenye kuendana na kizuio. Kwa mfano, kama mmiliki wa mali fulani, amemuona mtu mwengine, akiuza mali hiyo na kunyamaza kimya, hataruhusiwa kuthibitisha kwamba mtu huyo aliyekuwa akiuza hakumpa mamlaka ya kufanya hivyo.

 

Sheria inaeleza kwamba, pale ambapo mtu kwa tamko au tendo kwa makusudi kabisa ameruhusu mtu mwengine kuamini jambo kuwa ni kweli na kulitendea kazi kwa kuamini huko, iwapo yeye mwenyewe ama ni wakala wake, hataruhusiwa katika kesi yoyote kukataa ukweli wa jambo hilo.[47]

 

Mfano, kwa makusudi kabisa, A anampelekea B kuamini kwamba ardhi aliyonayo A ni ya kwake na hivyo kumtapeli B kuingia kwenye mauziano na kulipia hiyo ardhi. A hataruhusiwa katika kesi hii kukataa ukweli wa kujaribu kumtapeli B.

 

 

Tafsiri

 

Kwa mujibu wa al-Hilli na Ibn Qudaamah, tafsiri ya maandiko iliyofanywa na watu wawili walio waadilifu inaruhusiwa kutumika Mahkamani.[48]

 

Sheria kwa upande wake pia inaruhusu kufasiriwa hati pale itakapoona kuna haja ya kufanya hivyo.[49] Pale ushahidi utakapowekwa kumbukumbu kimaandishi kwa lugha ya Kiingereza, Mahkama inaweza kuamuru kufasiriwa kwa maandishi hayo kwa yule wakili au mtu asiyeelewa Kiingereza.[50] Kazi ya kufasiri maandishi pia utafanywa kwa shahidi ambaye haelewi lugha iliyoandikwa kwenye hati.[51]

 





[1] Al-Majallah, uk. 289.

[2] Al-Bayhaqi, as-Sunan al-Kubra, X, uk. 250.

[3] Ahmad Hassan az-Zayyat; Tariykh Adab ‘Arbai, uk. 209.

[4] Bukhari, ash-Shaib, II, uk. 1085.

[5] Sheria ya Ushahidi, S. 101

[6] Sheria ya Ushahidi, S. 102

[7] Sheria ya Ushahidi, S. 103

[8] Sheria ya Ushahidi, S. 106

[9] Sheria ya Ushahidi, S. 107

[10] Sheria ya Ushahidi, S. 110

[11] Sheria ya Ushahidi, S. 114

[12] Ibn Farhuun, Tabsirah, II, uk. 74-77.

[13] Sheria ya Ushahidi, S. 45

[14] Ibn Farhuun, Tabsirah, I, uk. 243.

[15] Sheria ya Ushahidi, S. 138

[16] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. XII, r. 2

[17] Al-Mawardi; Adab al-Qaadhi, uk. 350.

[18] Sheria ya Mwenendo wa Madai, S. 118 (1)

[19] Sheria ya Mwenendo wa Madai, S. 118 (2)

[20] Sheria ya Mwenendo wa Madai, S. 119

[21] Sheria ya Mwenendo wa Madai, S. 137 na 138

[22] Al-Mawardi; Adaab al-Qaadhi, uk. 350.

[23] Al-Marghinanani; al-Hidayah, II, uk. 203. Angalia pia Sahihi Muslim.

[24] Shaih, I, uk. 80.

[25] As-Sarkhasi; K. al-Mabsuut, XVI, uk. 116-120.

[26] Angalia ukurasa wa 6, S. cha 2 cha Sheria hii.

[27] Sheria ya Mwenendo wa madai, O. XXII, r. 1

[28] Sheria ya Ushahidi, kifungu 155 (1)

[29] Fathul-Qaadir, Juzuu ya VI, uk. 458-459; Hidayah, Juzuu ya VI, uk. 458-459.

[30] R. V. Madhub Chunder (1874) 21 W. R. Cr. 13, 19 (India).

[31] Hidayah, Juzuu ya VI, uk. 466-467; pia angalia al-Majallah, uk. 287-288.

[32] Hidayah, Juzuu ya VI, uk. 469.

[33] Hidayah, Juzuu ya VI, uk. 522-523.

[34] Hidayah, Juzuu ya VI, uk. 522-523.

[35] Sheria ya Ushahidi, S. 3

[36] Al-Majallah, uk. 291.

[37] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. XXII, r. 3 (1)

[38] Sheria ya Ushahidi, kifungu 3

[39] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. XXI, r. 11

[40] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. XXI, r. 12

[41] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. XXI, r. 13

[42] Hidayah, Juzuu ya VI, uk. 425.

[43] R. V. Harishchandra Ladaku Thange, Supreme Court of India, Justices Arijit Pasayat and P.  P. Naolekar, India's National Newspaper, 04/Sept/2007.

[44] Al-Majallah, uk. 297.

[45] Sheria ya Ushahidi, S. 114

[46] Angalia kesi ya Matofali V. R. (20 E. A. C. A. 232)

[47] Sheria ya Ushahidi, S. 115

[48] (a) Ibn Qudamah; Akhbar al-Qudat, IX, uk. 100 (b) Ibn Farhuun; Tabsirah, I, uk. 86-88.

[49] Sheria ya Ushahidi, S. 162 (3)

[50] Sheria ya Mwenendo wa Madai, S. 117

[51] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. XXI, r. 9

Share