Kusujudu Pindi Unapomkumbuka Allaah Inafaa?

 

Kusujudu Pindi Unapomkumbuka Allaah Inafaa?

 

Alhidaaya.com

 

 

 

SWALI:

 

Asalamu alaikum

 

Napenda kuuliza hivi je inafaa kama mtu yu watembea kisha ukamkumbuka Allaah kisha ukasujudu palepale kwa ajili yake. wabilah taufiq

 

 

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salamu zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayahi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

 

Hakika Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alisujudu alipowasomea makafiri Quraysh Suwratun-Najm na alipofika mwisho wa Suwrah alisujudu pamoja na Maswahaba (Radhwiya Allaahu ‘anhum) na Maquraysh wote wakasujudu juu ya mchanga mpaka wengine kwa kukosa nafasi wakasujudu juu ya migongo ya wenziwao. Na hivyo ndivyo ipasavyo unaposoma Aayah zenye Sajdah kutokana na Hadiyth:

 

Kutoka kwa  Abuu Hurayrah (Radhwiya Allahu ‘Anhu) kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)   amesema: ((Anaposoma mwana Adam (Ayah) ya kusujudu kisha akasujudu, shaytwaan atajitenga na kulia, atasema: “Ole wake (akijiambia yeye), ameamrishwa (mwana Aadam) kusujudu akasujudu na ana Pepoo, nami niliamrishwa kusujudu nikaasi na nina moto)) [Muslim, Ibn Maajah na Ahmad]

 

Ama kusujudu unapomkumbuka Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)   hatukupata mafunzo ya haya, hivyo ni vyema kutokusujudu. Bali kumkumbuka Allaah ni aina ya ibaada ya kutafakari, na ina thawabu nyingi, hivyo inatosha kujipatia thawabu kila unapomdhukuru Allaah.

 

Na hali nyengine ya kusujudu ni ile hali ya kuwa mtu yu juu ya kipando kinachokwenda kama walipokuwa Swahaba (Radhwiya Allaahu ‘anhum). Katika hali hiyo unatoa ishara ya kusujudu kwa kuinamisha kichwa na huko kutakuwa sawa kabisa.

 

Kadhalika pindi upatapo habari ya furaha au habari njema unaweza kusujudu kama alivyofanya Ibn ‘Abbaas (Radhwiya-Allaahu ‘anhumaa).

 

Pia, Hadiyth ya Abu Bakrah (Radhwiya Allaahu Anhu) isemayo kwamba Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), alikuwa anaporomoka kwenda kusujudu kwa ajili ya kumshukuru Allaah linapomjia jambo la furaha au jambo alilobashiriwa kheri. [Abu Daawuud (2774), At-Tirmidhy (1578), Ibn Maajah (1394) ]

 

Pia Ka’ab bin Maalik alisujudu ilipomjia habari ya furaha ya kuwa Allaah Kaikubali toba yake. [Hadiyth Swahiyh: Imefanyiwa “ikhraaj” na Al-Bukhaariy (4418) na Muslim (2769)].

 

Na kusujudu huko  waweza kusujudu popote bora pawe hapana najisi juu yake ikiwa unasujudu barabarani au kiwanjani au ofisini.

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

Share