Mke Kumsamehe Mume Mahari

SWALI:

Sheikh,

Mimi nina swali langu kama ifuatavyo:-

kuna shoga yangu mmoja aliposwa na walipotaka kudaiwa mahari alisema anataka aolewe kwa laki moja tu. Lakini Sheikh mzee wake mmoja alisema mimi nitadai nitakavyo, akadai laki 3 na nusu yule mwanamme alitoa laki 1 na akaoa na nyengine akasema atammalizie mkewe mahari yake. Suali lipo hapa yule mwanamke alimwambie mumewe kama nimekusamehe mahari yangu kwa uradhi wangu, nimeridhika na ulichotoa. Jee sheikh hii ni halali au afanye vipi?

Naomba majibu kupitia address yangu ahsante,


 

 

JIBU:

AlhamduliLlaah - Himdi Na Sifa Zote Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Mola wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu 'anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

 

Mara nyingi suala la mahari linapojitokeza huwa kuna mushkili hasa wazazi wakiwa wanataka kuchukua tunu hiyo huku wakidai kuwa wao wana haki zaidi kwa sababu wamemlea binti yule kwa kumsomemesha, kumvisha na kumlisha na kumfanyia mengineo. Tujue kuwa hayo ni majukumu ya mzazi kumfanyia mwanae na kama hakumfanyia basi atakuwa anapata dhambi mbele ya Allah. Na kukiwa na Dola ya Kiislamu basi atalazimishwa kumtekelezea hayo. Kwa sasa tunaona kuwa hata dola za kikafiri pia wanafanya hivyo kwa kumshitaki na kumlazimisha mzazi awe ni mwenye kumtekelezea mahitaji hayo yote.

Mahari kwa hakika ni haki ya binti anayeolewa na si haki ya mwengine yeyote hata mzazi. Na ndio Allah Anatuelezea:

“Na wapeni wanawake mahari yao hali ya kuwa ni kipawa” (4: 4).

Allah Ametumia neno Nihlah ambalo lina maana ya kwa roho ya zawadi bila kutarajia chochote kutoka kwake (Muhammad Asad na Zamakhshari), kwa kupenda kwako kama wajibu (Maalik), zawadi ya bure (Muhammad Marmaduke Pickthall na Abdulla Yusuf Ali).

Sheria haijaweka kima maalumu kwa waume kuwapa wake zao ila inatakiwa iwe kwa maridhiano baina yao wawili na inaweza kuwa hata pete ya chuma au kumsomesha Qur’ani kwa mujibu wa Hadithi zilizo sahihi. Hivyo, haifai baada ya kuwaoa na yametokea matatizo iwe mume anataka haki yake isipokuwa ikiwa mke amepatikana na makosa ya uchafu (uzinifu). La si hivyo wawili hawa wakiachana vitu vyote ambavyo mume amempatia mke ni haki yake kabisa ambayo amepatiwa na sheria. Allah Anasema:

“Enyi mlioamini! Si halali kwenu kuwarithi wanawake kwa nguvu. Wala msiwadhikishe ili mwapokonye baadhi ya mlivyowapa - isipokuwa wakifanya uchafu ulio wazi” ().

Na kuchukua mali iwe kidogo au nyingi ambayo umempatia mke ni dhulma na kosa kubwa. Allah Anasema:

 “Na mkitaka kubadilisha mke mahali pa mke, na hali mmoja wao mmempa chungu ya mali, basi msichukue katika hayo kitu chochote. Je, mtachukua kwa dhulma na kosa lilio wazi? Na mtachukuaje na ilhali mmekwisha ingiliana nyinyi kwa nyinyi, na wao wanawake wamechukua kwenu ahadi iliyo madhubuti?” (4: 20 – 21).

Na baada ya kuagana kuhusu mahari mke ana uwezo kumsamehe mume na wala hataulizwa na mtu yeyote kwa haki yake hiyo. Allah Anasema:

 “Lakini wakikutunukieni kitu katika mahari, kwa radhi yao, basi kileni kiwashuke kwa raha” (4: 4).

 Na mume kisheria anafaa kutoa mahari walioridhia si zaidi hapa, lakini akitoa kumpatia mkewe zaidi ni hiari yake na ana uhuru kamili wa kufanya hivyo. Ama nyongeza anayoitaka mama au baba au babu wa mke haipo katika mizani ya sheria na lau kama akitoa kuwapatia kama tunu na sio kwa kutendeshwa nguvu itakuwa ni hiari yake.

Na Allaah Anajua zaidi.

 

Share