Umuhimu wa 'Aqiydah: Laiti Wangelijua...

 

Umuhimu Wa ‘Aqiydah

 

Chanzo: ‘Aqiydah  Mambo ya Iymaan - Kwanza ... Laiti Kama Wangalijua

Alhidaaya.com

 

 

 

Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alimtaarifu Mu’aadh bin Jabal, wakati alimpomtuma kwenda nchi ya Yemen, “Wewe unakwenda kwa watu Watu wa Kitabu (Ahlul-Kitaab) Basi jambo la kwanza kuwalingania liwe kumuabudu Allaah. Kama wakilikubali hilo, ndio kisha uwataarifu kwamba Allaah amewajibishia juu yao sala tano wakati wa usiku na mchana.” [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

Hadiyth hii iko wazi kabisa. Na haihitaji maelezo mengi. Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) katumia kanuni hii katika uilinganizi wake wa kuwaita watu ndani ya Uislamu. Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikaa katika mji wa Makkah kwa muda wa miaka kuminatatu akiwafunza watu iymaan na kuwaelimisha Maswahaba zake juu ya nukta hii na kusahihisha iymaan za watu. Huu ndio mfumo waliokuzwa nao Maswahaba (Radhwiya Allaahu ‘anhum).

 

 

Jundub bin ‘Abdillaah Al-Bajaliy akasema, “Tumejifunza iymaan na kisha tukajifunza Qur-aan nayo ikatuongezea iymaan yetu.”

 

'Abdullaah bin ‘Umar alisema, “Sisi tuliishi wakati ambapo mmoja wetu atafunzwa iymaan kwanza kabla ya kufunzwa Qur-aan na wakati Suwrah zikiteremka tulijifunza ni nini kilichoruhusiwa na nini kilichopigwa marufuku na kipi kilichokatazwa na kipi kilichoamriwa na upi unapaswa kuwa msimamo wetu juu yao. Lakini nimeona watu wengi waliofunzwa Qur-aan kabla ya iymaan. nao huisoma kutoka mwanzo wa Kitabu hadi mwisho wake pasi na wao kufahamu nini imeamrisha na nini imekataza na bila ya kuufahamu msimamo wao juu yake. Anakuwa kama mtu ambaye anayezitupa tende (yaani, hafaidiki na kuisoma kwake Qur-aan)."

 

 

Hiyo ndio njia ambayo Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) aliyowaleya nayo Maswahaba wake:

 

Iymaan kwanza kisha Qur-aan.

 

Hii ni sawa na kile alichosema Imaam Abuu Haniyfah: “Elewa Dini kwanza (yaani Tawhiyd) kisha ndio uelewe sayansi yake (yaani Shariy'ah).”

 

 

Iymaan lazima isahihishwe kwanza, kisha ndio yafuate mambo mengine ya Dini.

 

Na Imaam Ash-Shafi'iy akasema, “Yakuwa ni bora mja akutane na Allaah kwa kila aina ya dhambi isipokuwa shirki kuliko kukutana na Allaah hali ya kuwa amezusha jambo katika Dini.”

 

Neno Al-‘Aqiydah asili yake imetokana na neno ‘aqada. Katika lugha ya Kiarabu, panasemwa, “Aqada Al-Habl” kumaanisha wakati kamba imefungwa imara. Na, “’Aqada Al-Bay’” (Mkataba wa Mauzo)” au “Makubaliano ya bei” wakati mtu anapoidhinisha mkataba wa mauzo au makubaliano. Na Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)  Anasema katika Qur-aan:

 

وَالَّذِينَ عَقَدَتْ أَيْمَانُكُمْ فَآتُوهُمْ نَصِيبَهُمْ ۚ  

Na wale mliofungamana nao viapo (vya undugu) basi wapeni fungu lao. [An-Nisaa: 33]

 

 

Na vilevile Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Anataja ‘aqqadtum’:

 

لَا يُؤَاخِذُكُمُ اللَّـهُ بِاللَّغْوِ فِي أَيْمَانِكُمْ وَلَـٰكِن يُؤَاخِذُكُم بِمَا عَقَّدتُّمُ الْأَيْمَانَ ۖ  

Allaah Hatokuchukulieni kwa viapo vyenu vya upuuzi, lakini Atakuchukulieni kwa (kuvunja) viapo mlivyoapa kwa niyyah mlioifunga thabiti. [Al-Maaidah 89]  

 

Na pia:

 

وَأَوْفُوا بِعَهْدِ اللَّـهِ إِذَا عَاهَدتُّمْ وَلَا تَنقُضُوا الْأَيْمَانَ بَعْدَ تَوْكِيدِهَا

Na timizeni ahadi ya Allaah mnapoahidi, na wala msivunje viapo baada ya kuvithibitisha;  [An-Nahl: 91]

 

 

Mfano wa mtu kusema ‘Aqadtu juu ya jambo ni kumaanisha yakuwa moyo wake umekita juu ya hicho alichokidhamiria.

 

 

Kwa hiyo, Al-‘Aqiydah au Al-I’tiqaad kulingana na Wanachuoni wa Kiislamu ni: iymaan imara iliyokita ndani ya moyo wa mtu pasi na kutetereka au kuwa na shaka yoyote. Na inaoondosha dhana, shaka au wasiwasi.

 

Imaam Abuu Haniyfah kaliita somo hili adhimu Al-Fiqh Al-Akbar (Ufahamu ulio Adhimu) na ndio ufahamu wa Dini. Aliita sayansi ya Shariy’ah; ufahamu wa sayansi.

 

Wanachuoni wengi wa Kiislamu hulitumia neno Tawhyid kwa mambo yote ambayo mtu lazima ayaamini. Hii ni kwa sababu kilicho muhimu zaidi katika mambo yote ni msingi wa Tawhyid uliomo ndani ya maneno ya shahaadah: “Laa ilaaha illa Allaah” (hakuna muabudiwa wa haki isipokuwa Allaah)   

 

Tawhiyd, kulingana na wao, inaweza kugawanywa katika makundi mawili:

 

Tawhiyd ya utambuzi na uthibitisho na Tawhiyd ya makusudio na matendo.

 

Tawhiyd ya utambuzi na uthibitisho ni Tawhiyd ya Upweke wa Muumbaji na Tawhiyd ya Majina Yake na Sifa (yaani Yeye ni Mpweke na Ndiye Muumba na ni Mpweke katika Majina na Sifa Zake).

 

Tawhiyd ya makusudio na matendo ndio Tawhiyd ya Uluwhiyyah yaani: Laa ilaaha illa Allaah (hakuna muabudiwa wa haki isipokuwa Allaah).   

 

Wanatheolojia ‘Kalaamiyyuwn’ - na nini kitachokujuza wewe hao wanatheolojia ni wepi? – Wameliita somo hili adhimu “mzizi wa dini” na wakaiita shariy’ah “matawi ya dini.” Hii ni istilahi yao. Sisi hatuafikiani nao katika jambo hili lakini hapa si pahala pake pa kulijadili. Wote wameipatia jina au kivumishi kulingana na mahitaji yao.

 

Lakini ni jina gani Qur-aan imelipa jambo hili?

 

Qur-aan imeliita jambo hili kwa jina la Iymaan. Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)  Anasema katika Qur-aan:

 

 

وَكَذَٰلِكَ أَوْحَيْنَا إِلَيْكَ رُوحًا مِّنْ أَمْرِنَا ۚ مَا كُنتَ تَدْرِي مَا الْكِتَابُ وَلَا الْإِيمَانُ وَلَـٰكِن جَعَلْنَاهُ نُورًا نَّهْدِي بِهِ مَن نَّشَاءُ مِنْ عِبَادِنَا ۚ وَإِنَّكَ لَتَهْدِي إِلَىٰ صِرَاطٍ مُّسْتَقِيمٍ﴿٥٢﴾

Na hivyo ndivyo Tulivyokuletea Ruwh (Qur-aan) kutoka amri Yetu. Hukuwa unajua nini Kitabu wala iymaan, lakini Tumeifanya ni Nuru, Tunaongoa kwayo Tumtakaye miongoni mwa waja Wetu. Na hakika wewe (ee Muhammad صلى الله عليه وآله وسلم) bila shaka unaongoza kuelekea njia iliyonyooka. [Ash-Shuwraa: 52]

 

Kwa ujumla moyo wa Muumin lazima uwe thaabit kuhusu “nguzo” hii ya iymaan. Lakini mtu hatoitwa Muumin tu kwa kujua na kuelewa nguzo hizi lakini ni lazima aridhiye na atekeleze kile kinachoelezewa, katika Hadiyth ya Jibriyl, kama ndio Uislamu. Iymaan, kwa namna hii, inajumuisha Uislamu.

 

 

Kama Iymaan ingekuwa inatosha kwa mtu kujua ukweli katika moyo wake tu, basi kuna tofauti gani baina yake na shaytwaan au Fir’awn (Kumbuka: Shaytwaan alikuwa mwenye elimu kubwa juu ya Rabb wake lakini aliangamizwa kwa sababu ya kiburi chake na wivu. Na Fir’awn, ingawa yeye alidai Uilaah (mwabudiwa) alijua kwamba Ilaah wa kweli  ni Allaah na kwamba hakuna muabudiwa wa haki ila Yeye. Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)  Anasema:

 

قَالَ لَقَدْ عَلِمْتَ مَا أَنزَلَ هَـٰؤُلَاءِ إِلَّا رَبُّ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ بَصَائِرَ وَإِنِّي لَأَظُنُّكَ يَا فِرْعَوْنُ مَثْبُورًا ﴿١٠٢﴾

 (Muwsaa) Akasema: “Kwa yakini umekwishajua kwamba hakuna Aliyeteremsha haya isipokuwa Rabb wa mbingu na ardhi kuwa ni dalili za kuonekana dhahiri.. [Al-Israa: 102]

 

 

Ingawa walijua ukweli, hawakukubali kuielekeza ‘ibaadah yao kwa Allaah Pekee).

 

Katika Hadiyth ya Jibriyl, Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alielezea nguzo za hii iymaan ambayo kila mwan Aadamu lazima aamini, na alipoulizwa, “Ni nini Iymaan?”, Alisema: “Ni kumuamini Allaah na Malaika Wake, na Vitabu Vyake na Rusuli Wake na Siku ya Mwisho na Kheri na Shari vyote vinapatikana kwa Qadar  ya Allaah.”

 

Ni lazima kwa kila mtu kuzijua nguzo hizi na kujifunza ufahamu ulio sahihi na kuamini katika ufahamu wa wema wetu waliotangulia walivyofahamu na kuamini, kwa namna walivyofahamu wao kutoka kwa Maswahaba wa Nabiy (Radhwiya Allaahu ‘anhum) na wale wote waliowafuata katika njia hiyo. Hii inajumuisha pamoja na ma-Imaam wanne, na Sufyaan Ath-Thawriy, Sufyaan bin 'Uyaynah, ‘Abdullaah bin Al-Mubaraak na wengine sawa na wao, kama vile Muhammad bin Isma’iyl’ Al-Bukhaariy, Muslim bin Al-Hajjaaj, Shaykh Al-Islaam Ibn Taymiyyah na Al-Haafidhw Ibn Al-Qayyim. Na Wanachuoni wote walio sawa nao katika ufahamu ambao waliofuata mwenendo  ule ule katika kufahamu na kuziamini nguzo hizi.

 

Huu ni wajibu wa kwanza juu kiumbe mwenye dhima. Hakuna tofauti ya maoni juu ya suala hili miongoni mwa wasomi ambao maoni yao yanastahiki kufuatwa. Imaam Abuu Haniyfah kasema: “Kuelewa iymaan ni bora kuliko ufahamu wa sayansi.”

 

Alichokusudia katika usemi huu kuwa; Iymaan ni Tawhiyd na sayansi ni Shariy’ah. Kwa hiyo katanguliza ufahamu wa Tawhiyd kabla ya mtu kufahamu Shariy’ah.

 

Na Shaykh Al-Islaam Al-Haruwi Al-Answaariy (Aliyefariki 481 H) amesema katika mwanzo wa kitabu chake ‘I’tiqaad Ahl As-Sunnah’: “Wajibu wa kwanza juu mja ni maarifa juu ya Allaah. Hii inathibitishwa na Hadiyth ya Mu’aadh, wakati alipoambiwa na Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), “Wewe unakwenda kwa watu Watu wa Kitabu (Ahlul-Kitaab) Basi jambo la kwanza kuwalingania liwe kumuabudu Allaah. Kama wakilikubali hilo, ndio kisha uwataarifu kwamba Allaah amewajibishia juu yao sala tano wakati wa usiku na mchana.” [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

 

Kutokana na  uadhimu wa nguzo hii ndio ‘Ulamaa wakubwa wa Kiislamu wameitanguliza. Tafakari, kwa mfano, kile Imaam Muhammad bin Ismaa’iyl Al-Bukhaariy alivyofanya katika kitabu chake Al-Jaami’ Asw-Swahiyh, ambayo ni kitabu sahihi zaidi baada ya Kitabu cha Allaah, Utaweza kuona kwamba kutokana na elimu yake ya kina na ufahamu wake wa Dini hii. Imaam huyu mkubwa alianza kitabu chake kwa “Mwanzo wa Wahyi” na kisha ikifuatiwa na mlango juu ya iymaan, na kufuatiwa na mlango juu ya maarifa. Kama kwamba alikuwa akimaanisha (Rahimahu Allaah), kwa uhakika wajibu wa kwanza juu ya mwana Adamu ni iymaan na njia ya kuifikia iymaan ni maarifa. Na chanzo cha iymaan na maarifa ni ufunuo. Hivyo, alianza kwa kuonyesha jinsi Wahyi ulivyotokea na namna ulivyokuwa. Kisha akafuatia kutaja iymaan na maarifa. Utaratibu huu si ajali; na kwayo ametutengenezea baadhi ya nukta muhimu.

 

 

Hii ni jumla ya kile ambacho tunataka kukutaarifuni na kwayo ndio tunapaza sauti zetu juu. kipaumbele cha kwanza ni suala la ‘Aqiydah. Iymaan na maarifa ni njia ya kuifikia. Na chanzo cha maarifa na iymaan ni Kitabu na Sunnah.

 

 

Share