Kisa Cha "Ni Dada Yangu Nuurah"

 

Kisa Cha “Dada Yangu Nuurah”

 

Imetafasiriwa na: Ummu ‘Abdul-Wahaab

 

 

Alhidaaya.com

 

Mashavu yake yalikuwa yamenywea na kuchujuka na kuambatana na mifupa. Hayo hayakumsitisha yeye kabisa katika ibada zake, kwani huwezi kumkuta kakaa tu bure bila ya kusoma Qur-aan. Daima hukesha kwa ajili ya swalaah zake za binafsi katika chumba ambacho baba kamtayarishia. Hurukuu, husujudu, na hunyanyua mikono yake katika swalaah. Hivyo ndivyo alivyo tangu jua linapochomoza hadi kutua na hurudia tena.  Ilikuwa ni kichokesho kwa wengine.

  

Kwa upande wangu sikuvutiwa na kitu ila mitindo katika magazeti na vitabu vya visa. Wakati wote niliifanya nafsi yangu iwe kwenye kuangalia video hadi ikawa safari za kwenda sehemu ya kukodia kanda kuwa ndio biashara yangu. Kama isemwavyo, pindi linapokuwa jambo ni tabia, watu huweza kukutofautisha kutokana na jambo hilo. Nilipuuza majukumu yangu na hufanya uvivu kwenye swalaah.

 

Siku moja wakati wa usiku, nilizima video baada ya kuangalia kwa masaa matatu mfululizo. Sauti nyororo ya adhana ilipaa hewani katika kimya kile cha usiku. Niliteleza pole pole kwenye blankenti langu.

 

Sauti yake ilisikika toka kwenye chumba chake.

 

"Ndio? Unahitajia chochote Nuurah?"

 

Kama vile mfano sindano yenye ncha kali, alitoboa mipangilio yangu.

 

"Usilale kabla ya kusali swalaah ya Alfajiri!"

 

"Ahh …Kuna saa nzima kabla ya Alfajiri! Hiyo ilikuwa ni adhana ya mwazo tu!"

 

Kwa mifunyo yake ya kimapenzi, aliniita niwe karibu yake. Daima hivyo ndivyo alivyokuwa, pamoja na kuwa ugonjwa mkali uliotikisa imani yake uliomshika ulimlaza kitandani kwake.

 

"Hannaan unaweza kuja kukaa pembeni yangu."

 

Sikuweza kukataa wito wake wowote, kwa vile ungeweza kugusa utakatifu na ukunjufu wake.

 

"Ndio, Nuurah?"

 

"Tafadhali kaa hapa."

 

"Sawa nnakaa. Una jambo gani?"

 

Alianza kusoma kwa sauti nzuri:

 

كُلُّ نَفْسٍ ذَائِقَةُ الْمَوْتِ ۗ وَإِنَّمَا تُوَفَّوْنَ أُجُورَكُمْ يَوْمَ الْقِيَامَةِ ۖ

Kila nafsi itaonja mauti. Na hakika mtalipwa kikamilifu ujira wenu Siku ya Qiyaamah. [Al-'Imraan:185]

 

Alisita huku akiwaza. Kisha akaniuliza, "Unaamini mauti?"

 

"Bila ya shaka nayaamini."

 

"Unaamini kwamba utakuwa na jukumu kwa yale yote unayoyatenda, ikiwa ni madogo au makubwa?"

 

"Ndio naamini, lakini Allaah ni Mwenye Kusamehe na ni Mwenye Kurehemu na nna umri mrefu unanisubiri."

 

"Nyamaza Hannaan …huogopi mauti wewe ambayo huja ghafla?  Muangalie Hind, alikuwa mdogo kuliko wewe, lakini alikufa kwa ajali ya gari. Ndivyo hivyo hivyo yalivyotokea kwa wengine, na wengine. Mauti ni kipofua-umri na umri wako hauwezi kuwa na kipimo mpaka ufe."

 

Kiza cha chumba kilifunika ngozi yangu kwa woga. "Naogopa kiza na wewe sasa unanifanya niogope mauti? Unafikiri nitapataje usingizi sasa! Nilifikiri uliahidi kuwa unakwenda na sisi katika mapumziko ya msimu wa joto."

 

Mgongano! Sauti yake ilivunjika na moyo wake ukatetemeka. "Huenda nikenda safari ndefu mwaka huu Hannaan, sehemu nyengineyo. Labda! Sisi sote uhai wetu upo mikononi mwa Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) na sisi ni Milki Yake."

 

Macho yangu yalinilengalenga na machozi yalinititririka kwenye mashavu yangu. Nilifikiria ugonjwa wa dada yangu, kwani madaktari waliwahi kumjulisha baba kwa faragha kuwa hakuna matumaini makubwa kwa Nuurah kuweza kuishi bila ya maradhi. Lakini yeye mwenyewe hakujulishwa hayo. Sasa nani alimjulisha? Au aliwezaje kuwa na hisia za kujua ukweli?

 

"Unawaza nini Hannaan?" Sauti yake ilikuwa kali. “Unafikiri nasema hivi kwa sababu naumwa?  Aah!....Aah! Kwa kweli, huenda nikaishi sana kuliko yule ambaye haumwi. Na wewe Hannaan, unajua utaishi kwa muda gani? Miaka ishirini, labda? Arobaini? Kisha nini?”

 

Kwenye kiza kile aliufikia mkono wangu akaubana kwa utaratibu. “Hakuna tofauti kati yetu; sote tutaondoka katika ulimwengu huu na kwenda kuishi kwenye Jannah au kuangamia mwenye Moto. Sikiliza maneno ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa): 

 

فَمَن زُحْزِحَ عَنِ النَّارِ وَأُدْخِلَ الْجَنَّةَ فَقَدْ فَازَ ۗ وَمَا الْحَيَاةُ الدُّنْيَا إِلَّا مَتَاعُ الْغُرُورِ ﴿١٨٥﴾

Basi atakayewekwa mbali na moto na akaingizwa Jannah kwa yakini amefuzu. Na uhai wa dunia si lolote ila ni starehe ya udanganyifu. [Al-'Imraan:185]

  

Niliondoka kwenye chumba cha dada yangu nikiwa nimepigwa na bumbuwazi, maneno yake yalikuwa yakisikika kwenye masikio yangu: "Allaah Atakulinda Hannaan.  Usisahau kusali"

 

Saa mbili asubuhi mlango wangu uligongwa. Kwa kawaida siamki wakati huu. Kilio! Mbabaiko! "Ee Allah! kitu gani kimetokea?"

 

Hali ya Nuurah ilikuwa mbaya baada ya sala ya Alfajiri, alichukuliwa kwa haraka kupelekwa hospitali.  "Inna liLLlaahi wa innaa Ilayhi raaji'uun" (Hakika sisi sote ni waja wa Allaah na kwa hakika marejeo yetu ni Kwake).

 

Hakukuwa tena na safari ya mapumziko ya msimu wa joto.  Ilikwishaandikwa kwamba nitabakia nyumbani.

 

Baada ya muda …..

 

Ilikuwa saa saba za mchana mama alipopiga simu hospitali. "Ndio. Unaweza kuja sasa kumuona." Sauti ya baba ilibadilika, mama aliweza kuhisi kuwa kuna jambo ambalo limetokea.  Tuliondoka haraka sana.

 

Iko wapi ile njia ambayo nilizowea kuipita na kudhania kuwa ni fupi? Kwanini imekuwa ndefu sana leo?  Uko wapi ule mlolongo wa magari ambao ulikuwa ukinipa fursa ya kukatisha kulia na kushoto? "Hebu ondokeni upande wetu tunaopita". Mama alikuwa akitikisa kichwa chake na mikono yake huku analia na kumuombea du'aa Nuurah.

 

Tuliwasili kwenye mlango mkuu wa kuingilia hospitali. Tulimkuta mtu mmoja akiwa anahuzunika. Mwengine alikuwa amepatwa na ajali na watatu wao macho yake yametulia tuli hayatikisiki! Huwezi kusema kuwa ni yuhai au amekwisha kufa.

 

Tulizikiuka ngazi kuelekea ghorofa aliyokuwa Nuurah. Alikuwa kwenye chumba cha wagonjwa mahututi.

 

Muuguzi alitukaribia. "Acha nikupelekeni alipo." Tulipokuwa tunapita kwenye ujia kuelekea kule alipo, Muuguzi alielezea jinsi ya uzuri wa msichana Nuurah. Alimuhakikishia mama kuwa hali ya Nuurah ilikuwa ina afadhali kulinganisha na alivyokuwa asubuhi.

 

"Samahani!"  "Sio zaidi ya mtu mmoja kwa wakati!"  Kilikuwa ni chumba cha wagonjwa mahututi. Kupitia kidirisha kidogo cha mlango na uwazi wa mapazia meupe, niliyafuma macho ya dada yangu. Mama alisimama pembezoni mwake. Baada ya dakika mbili, mama alikuja nje huku akishindwa kukizuia kilio chake.

 

"Unaweza kuingia na kumsalimia lakini kwa sharti ya kuwa hutozungumza nae kwa muda mrefu". Hivyo ndivyo walivyonambia mimi.  "Dakika mbili zinatosha".

"Unajisikiaje Nuurah? Ulikuwa hujambo jana usiku dada yangu, kitu gani kimetokea?"

 

Tulishikana mikono, alinibinya mikono yangu lakini si kwa kunidhuru. "Hata hivi sasa, AlhamduliLLah, naendelea vizuri".

 

"AlhamduliLLaah".  Lakini …mikono yako ibaridi sana!

 

Nilikaa pembezoni mwa kitanda chake na kuweka vidole vyangu kwenye vifundo vyake vya miguu. Alivirusha vidole vyangu. "Samahani ... nimekuumiza?"

 

"Hapana! Ila nimekumbuka maneno ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa): 

 

وَالْتَفَّتِ السَّاقُ بِالسَّاقِ﴿٢٩﴾

Na utakapombatanishwa muundi kwa muundi. [Al-Qiyaamah:29]  [Mguu mmoja utakunjwa juu ya mwengine (katika sanda)]

 

"…… Hannaan niombee du'aa. Hivi punde tu huenda nikakutana na siku ya kwanza ya maisha ya Aakhirah. Ni safari ndefu na sikutayarisha vya kutosha sanduku langu kwa amali njema".

 

Machozi yalitoroka kwenye macho yangu kukimbilia kwenye mashavu yangu. Nililia na yeye aliungana na mimi tukalia pamoja. Michirizi ya machozi yalitawanyika kwenye mashavu ya dada yangu ambapo nilimshikilia kwa mikono yangu yote miwili. Baba aliingiwa na wasiwasi sana kwa jinsi nilivyolia kwa sababu sikuwahi kulia kama vile kabla yake.

 

Nilipokuwa nyumbani, juu kwenye chumba changu, nililiangalia jua likitua kwenye siku ya huzuni. Kimya kilichanganyika katika njia za ndani ya nyumba yetu. Ndugu na jamaa walikuja katika chumba changu. Watu wengi walihudhuria na sauti zilisikika zikichanganyika kutoka sehemu ya chini ya nyumba yetu. Kitu kimoja tu ndicho kilichosikika kwa uwazi wakati ule……..  Nuurah alikwishafariki!

 

Nilishindwa kutofautisha ni nani aliyeingia na nani aliyetoka.  Sikuweza kukumbuka walichokisema.  Ee Allah, nilikuwa wapi? Nini kiliendelea? Sikuweza hata kulia tena!

 

Baadaye, walinielezea kitu gani kilitokea. Baba alinishika mkono kunipeleka kwenda kumuaga dada yangu kwa mara ya mwisho, nilikibusu kichwa cha Nuurah.

 

Hata hivyo nakumbuka kitu kimoja, kumuona dada yangu alivyolala kwenye kile kitanda, kitanda ambacho ndicho alichofia juu yake. Naikumbuka Aayah aliyoisoma: 

 

وَالْتَفَّتِ السَّاقُ بِالسَّاقِ﴿٢٩﴾

Na utakapombatanishwa muundi kwa muundi. [Al-Qiyaamah:29]  [Mguu mmoja utakunjwa juu ya mwengine (katika sanda)]

 

Na nilikuwa nnaijuia vizuri ukweli wa Aayah inayofuata:

إِلَىٰ رَبِّكَ يَوْمَئِذٍ الْمَسَاقُ﴿٣٠﴾ 

Siku hiyo kuendeshwa ni kwa Rabb wako tu. [Al-Qiyaamah: 30]

 

Nilinyatia usiku ule kuelekea chumba chake cha kusalia. Nikapigwa na bumbuwazi nilipoyatazama makabati na vioo ambayo yalikuwa kimya. Nilimthamini yule ambaye alishirikiana na mimi katika tumbo la mama yangu. Ni dada yangu Nuurah ambaye alikuwa ni pacha wangu!

 

Namkumbuka yule ambaye alikuwa akizibadilisha huzuni zangu. Ni yeye ambaye alikuwa akinifariji wakati wa shida.  Namkumbuka yule ambaye alikuwa akiniombea muongozo na aliyatumia machozi yake mengi katika katika nyusiku nyingi akinielezea kuhusu mauti na kuhesabiwa. Huenda Allaah atatuokoa sote.

 

Usiku wa leo ni usiku wake wa mwanzo ambao Nuurah atautumia kwenye kaburi. "Ee Allah, Mrehemu na Mtilie nuru kaburi lake"

 

Hii ilikuwa ni Qur-aan yake, msala wake, na kanzu ya wardi ambayo aliniambia ataificha mpaka atakapoolewa ili aje amvalie mumewe.

 

Nilimkumbuka dada yangu na nililia siku zote kwa ajili ya kumkosa. Nilimuomba Allaah Anirehemu, Anitakabalie du’aa zangu na Anisamehe.  Nilimuomba Allaah Ampe Qawluth-thaabit (kauli thabiti kuweza kujibu maswali ya Malaika; Munkar na Nakiyr) katika kaburi lake kama alivyozoea kusema katika du'aa zake.

 

Nilisita kwa wakati ule, nikajiuliza: "Je! Ingelikuwa ni mimi niliyekufa?  Ningelielekea upande gani?"  Woga ulinivaa na machozi yakaanza kunitoka tena.

 

Allaahu Akbar, Allaahu Akbar …!

 

Sauti nyororo ya adhana ya kwanza ilipaa hewani kutoka msikitini. Uzuri ulioje kusikia sauti ya adhana wakati ule. Nilitulizana kimya nikawa nayakariri maneno ya muadhini. Nilivaa nguo zangu za kusalia nikasali sala ya Alfajiri. Nilisali kama kwamba ilikuwa ni sala yangu ya mwisho, sala ya kuaga, kama Nuurah alivyofanya. Alfajiri ilikuwa ni sala yake ya mwisho.

 

Kutoka sasa mpaka mwisho wa maisha yangu, ikiwa nitaamka asubuhi, basi sitojihesabu tena kuwa nitakuwa hai ifikapo jioni, na itapokaingia jioni (vile vile) sitojihesabu kama nitakuwa hai ifikapo asubuhi. Sisi sote tunakwenda safari aliyokwenda Nuurah. Je! Tumejitayarisha vipi na safari hiyo?

 

اللَّـهُ نُورُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ ۚ مَثَلُ نُورِهِ كَمِشْكَاةٍ فِيهَا مِصْبَاحٌ ۖ الْمِصْبَاحُ فِي زُجَاجَةٍ ۖ الزُّجَاجَةُ كَأَنَّهَا كَوْكَبٌ دُرِّيٌّ يُوقَدُ مِن شَجَرَةٍ مُّبَارَكَةٍ زَيْتُونَةٍ لَّا شَرْقِيَّةٍ وَلَا غَرْبِيَّةٍ يَكَادُ زَيْتُهَا يُضِيءُ وَلَوْ لَمْ تَمْسَسْهُ نَارٌ ۚ نُّورٌ عَلَىٰ نُورٍ ۗ يَهْدِي اللَّـهُ لِنُورِهِ مَن يَشَاءُ ۚ وَيَضْرِبُ اللَّـهُ الْأَمْثَالَ لِلنَّاسِ ۗ وَاللَّـهُ بِكُلِّ شَيْءٍ عَلِيمٌ ﴿٣٥﴾ 

Allaah ni Nuru ya mbingu na ardhi. Mfano wa Nuru Yake kama shubaka ndani yake mna taa yenye mwanga mkali. Taa hiyo yenye mwanga mkali iko katika (tungi la) gilasi. Gilasi hiyo ni kama kwamba nyota inayong’aa na kumeremeta, inawashwa kutokana na mti wa baraka wa zaytuni, hauko Mashariki wala Magharibi. Yanakaribia mafuta yake yang’ae japokuwa moto haujayagusa; Nuru juu ya Nuru. Allaah Anamwongoza kwa Nuru Yake Amtakaye. Na Allaah Anapiga mifano kwa watu. Na Allaah kwa kila kitu ni Mjuzi. [An-Nuwr: 35]

 

Alhidaaya Intaoa Mafunzo Yanayopatikana Katika Kisa Hiki:

 

1-  Kuacha mambo ya upuuzi na kujitayarisha na safari ndefu ya Aakhirah kwa kuwa na taqwa (ucha wa Allaah) kufanya amali nyingi njema.

 

2-     Kuthamini mapenzi ya undugu wakati tuko hai kabla ya mauti ya mmoja wetu.

 

3-     Kupokea nasiha za dini tunapopewa na sio kuzipuuza.

 

4-    Kujifunza maana na tafsiyr ya Qur-aan ili kujua mafunzo yaliyokuwemo humo na kuweza kuyatumia katika kupeana nasiha iwe kama ukumbusho na mazingatio ya maneno ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa), kwani huenda Aayah moja tu ikamzindua mtu akatanabahi na kutafakari akatambua haki.

 

5-     Kuombeana du'aa.

 

6-    Nafsi haijui lini itarudi kwa Rabb wake. Hatujui wapi tutafia. Mauti hayana mdogo wala mkubwa, wala hayana ugonjwa au uzima kama alivyosema mshairi: 

 

تزود من التقوى فإنك لا تدري                   

Zidisha taqwa kwani hujui

إذا جن عليك ليل هل تعيش إلى الفجر

Usiku utakapokufunika, je, utaishi hadi Alfajiri

فكم من صحيح مات بغير علة                

Kwani wangapi waliokuwa na siha zao wamekufa bila ya maradhi

 وكم من سقيم عاش حينا من الدهري

Na wangapi walio wagonjwa wameishi miaka?  

وكم من صغار يرتجى طولة عمرهم               

Na Wangapi miongoni mwa wadogo wana matumaini ya maisha marefu

وقد دخلت أجسادهم ظلمة القبر

Na miili yao Imekwishaingia katika kiza cha kaburi

 فكم من فتى يمسي ويصبح ضاحكا       

Na vijana wangapi wameamka huku wanacheka

وقد نسجت أكفانه وهو لايدري

Na hali sanda yake inashonwa (inaandaliwa) naye hajui

  

Tunamuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Atuongoze sote katika kutambua kuwa mauti hayana budi ila kumfikia kila mmoja wetu, ili tuwe daima katika kujitayarisha kukutana na Mola wetu kwa kutenda mema mengi. Aamiyn.

 

Share