Zingatio: Kuwa Bwana Wa Nafsi Yako

 

Zingatio: Kuwa Na Bwana Wa Nafsi Yako

 

Naaswir Haamid

 

Alhidaaya.com

 

 

Nafsi ni kama mtoto mdogo, haichoki wala hailali kutamani mambo. Na kawaida ya nafsi ni yenye kutamani maovu. Mfano mdogo tu, ni namna inavyopenda pumbazo za kidunia kama vile pombe, zinaa, ugomvi na kadhalika. Utaikutia nafsi ipo nyepesi kuyaingia mambo haya lakini ni nzito kujiweka mbali nayo.

 

Nafsi ni toto lisilosikia, kutwa lahitaji pembea.

Haijui halali kuhitajia, daima haramu huindea.

Nafsi Shaytwaani aipalilia, yeye machafu hukuwekea.

Yahitaji vita kuipigania, haramu usije kuyapendelea.

 

Nafsi sio rahisi kuilea kama alivyo mtoto. Mtoto haachi kudai utamu wa peremende, biskuti na vifaa vya kuchezea. Halikadhalika, nafsi nayo haiachi kukuamrisha kuangalia mambo yasiyofaa ili kutumbukia kwenye maasi. Inaamrisha kuyaacha yaliyo halali ili kuingia kwenye haramu.

 

Nafsi yahitaji kulelewa kwa kutenda ‘Ibaada. Na vile vile kupigana nayo ili kujiepusha kwenye kutenda maasi. Kwani kutenda ‘Ibaada sio kazi rahisi, ni kazi yenye kuhitaji subira ya hali ya juu. Lakini hakuna njia rahisi ya mafanikio ila ni kujihimiza kwenye yale mashurti yaliyowekwa ili kufanikiwa na kile unachokitafuta. Hivyo yahitaji juhudi ili nafsi izowee kutenda mema.

 

Tumechagua wetu Uislamu, njia nzuri muafaka.

Njia isio na pekee matamu, inadai jasho kukutoka.

Ndivyo waliopita Waislamu, muda kupoteza hawakutaka.

Maisha yao hatamu, ni damu machozi kuwatoka.

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Anasema kwa wale wenye kujitahidi: 

 

 وَمَن جَاهَدَ فَإِنَّمَا يُجَاهِدُ لِنَفْسِهِ ۚ إِنَّ اللَّـهَ لَغَنِيٌّ عَنِ الْعَالَمِينَ ﴿٦﴾

Na anayefanya juhudi basi hakika hapana isipokuwa anafanya juhudi kwa ajili ya nafsi yake. Hakika Allaah bila shaka ni si Mhitaji wa walimwengu. [Al-‘Ankabuut: 6]

 

Daima tukumbuke kwamba tunapojikubalisha, Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Atatuonesha njia In shaa Allaah. Kasema Mtukufu wa Mbingu na Ardhi:

 
وَالَّذِينَ جَاهَدُوا فِينَا لَنَهْدِيَنَّهُمْ سُبُلَنَا ۚ وَإِنَّ اللَّـهَ لَمَعَ الْمُحْسِنِينَ ﴿٦٩﴾

Na wale waliofanya juhudi kwa ajili Yetu, bila shaka Tutawaongoza njia Zetu. Na hakika Allaah Yu Pamoja na watendao ihsaan. [Al-‘Ankabuut: 69]

 

Tukirudi nyuma kwenye Taariykh ya Uislamu, tunaona kwamba Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba (Radhwiya Allaahu ‘Anhum) na watangu wema walikuwa hawana masikhara kwenye ‘Ibaada, ama kuswali, kufunga na kujishughulisha kwenye elimu na Ijtihaad nyenginezo. Muda mrefu wa usiku ulikuwa ukitumika kwa kuomba toba au kutafuta elimu.

 

Hivi ndivyo inavyotakiwa kwa maisha ya Muislamu na ndivyo kufuzu katika Dunia hii kwa kutarajia kunufaika na maisha ya milele kesho Aakhirah insha Allaah.

 

Tumuombe Allaah Atujaalie tuwe katika wale mabwana wa nafsi zao, sio watumwa wa matamanio yao. (AAMIYN).

 

Share