Skip navigation.
Home kabah

Kisa Cha Aswhaabul-Kahf (ًًًWatu Wa Pangoni ) Sehemu Ya 1



Imeandikwa na Alhidaaya.com

 


أَعُوذُ بِاللَّهِ مِنَ الشَّيْطاَنِ الرَّجِيم

  أَمْ حَسِبْتَ أَنَّ أَصْحَابَ الْكَهْفِ وَالرَّقِيمِ كَانُوا مِنْ آيَاتِنَا عَجَبًا ﴿9﴾ إِذْ أَوَى الْفِتْيَةُ إِلَى الْكَهْفِ فَقَالُوا رَبَّنَا آتِنَا مِن لَّدُنكَ رَحْمَةً وَهَيِّئْ لَنَا مِنْ أَمْرِنَا رَشَدًا ﴿10﴾ فَضَرَبْنَا عَلَى آذَانِهِمْ فِي الْكَهْفِ سِنِينَ عَدَدًا ﴿11﴾ ثُمَّ بَعَثْنَاهُمْ لِنَعْلَمَ أَيُّ الْحِزْبَيْنِ أَحْصَى لِمَا لَبِثُوا أَمَدًا ﴿12﴾ نَحْنُ نَقُصُّ عَلَيْكَ نَبَأَهُم بِالْحَقِّ إِنَّهُمْ فِتْيَةٌ آمَنُوا بِرَبِّهِمْ وَزِدْنَاهُمْ هُدًى ﴿13﴾ وَرَبَطْنَا عَلَى قُلُوبِهِمْ إِذْ قَامُوا فَقَالُوا رَبُّنَا رَبُّ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ لَن نَّدْعُوَ مِن دُونِهِ إِلَهًا لَقَدْ قُلْنَا إِذًا شَطَطًا ﴿14﴾ هَؤُلَاء قَوْمُنَا اتَّخَذُوا مِن دُونِهِ آلِهَةً لَّوْلَا يَأْتُونَ عَلَيْهِم بِسُلْطَانٍ بَيِّنٍ فَمَنْ أَظْلَمُ مِمَّنِ افْتَرَى عَلَى اللَّهِ كَذِبًا ﴿15﴾ وَإِذِ اعْتَزَلْتُمُوهُمْ وَمَا يَعْبُدُونَ إِلَّا اللَّهَ فَأْوُوا إِلَى الْكَهْفِ يَنشُرْ لَكُمْ رَبُّكُم مِّن رَّحمته ويُهَيِّئْ لَكُم مِّنْ أَمْرِكُم مِّرْفَقًا ﴿16﴾

 

9. Bali unadhani ya kwamba wale Watu wa Pangoni na Maandishi walikuwa ni ajabu miongoni mwa ishara zetu?

10. Vijana hao walipo kimbilia kwenye pango walisema: Mola wetu Mlezi! Tupe rehema itokayo kwako, na tutengezee uwongofu katika jambo letu

11. Tukayaziba masikio yao kuwalaza humo pangoni kwa muda wa miaka kadhaa wa kadhaa

12. Kisha tukawazindua ili tujue ni lipi katika makundi mawili lilio hisabu sawa muda walio kaa.

13. Sisi tunakusimulia khabari zao kwa kweli. Hakika wao walikuwa ni vijana walio muamini Mola wao Mlezi. Na Sisi tukawazidisha uwongofu.

14. Na tukazitia nguvu nyoyo zao walipo simama na wakasema: Mola wetu Mlezi ni Mola Mlezi wa mbingu na ardhi. Hatutamwita mwenginewe kabisa badala yake kuwa ni Mungu. Hivyo itakuwa tumesema jambo la kuvuka mpaka.

15. Hawa watu wetu wameshika miungu mingine badala yake Yeye. Kwa nini basi hawawatolei uthibitisho ulio dhaahiri? Na nani aliye dhaalimu zaidi kuliko anaye mzulia uwongo Mwenyezi Mungu

16. Na mkijitenga nao na vile wanavyo viabudu badala ya Mwenyezi Mungu, basi kimbilieni pangoni, akufungulieni Mola wenu Mlezi rehema yake, na akutengenezeeni ya kukufaeni katika mambo yenu.

Maelezo kwa ufupi kuhusu kisa hiki:

Kisa hiki ni kuhusu vijana wa kiume waliopata uongofu kutoka kwa Mola wao kwa kuepukana na ibada ya masanamu na kuamini Tawhiyd ya Allaah سبحانه وتعالى.  Vijana hawa walikuwa wakiishi katika mji ambao mfalme wao alikuwa akiabudu hayo masanamu. Alivyojua huyo mfalme kwamba hawa vijana wamekanusha ibada  hiyo ya masanamu na baada ya kujua sababu zao, akataka kuwadhulumu kwa kuwatesa na kuwaua! Wakakimbilia katika pango ambapo humo Allaah  سبحانه وتعالى  Aliwateremshia Rahma Yake kwa kuwahifadhi na kuwaficha humo wasijulikane.  Akawapa  usingizi wa kulala miaka mingi zaidi ya mia tatu, ili watakapoamka  hatokuweko tena huyo mfalme wala kizazi kilichowahi kuwepo wakati huo walipokimbia. Maelezo zaidi ya kisa hiki kizito ni katika kila baada ya aya zake.

Anaanza Allaah سبحانه وتعالى  kutusimulia kisa hiki cha As-haabul-Kahf  (watu wa pangoni) kwa swali:

 أَمْ حَسِبْتَ أَنَّ أَصْحَابَ الْكَهْفِ وَالرَّقِيمِ كَانُوا مِنْ آيَاتِنَا عَجَبًا ﴿9﴾

{{9. Bali unadhani ya kwamba wale Watu wa Pangoni na Maandishi walikuwa ni ajabu miongoni mwa ishara zetu?}}

Anatuelezea kwamba kisa chao sio jambo la kustaajabisha, ukilinganisha na Uwezo Wake, Nguvu Zake, maumbile ya mbingu na ardhi, kubadilika mchana na usiku, kutiishwa kwa jua na mwezi, vilioko mbinguni vyote, na vinginevyo Alivyoviumba. Vyote vinaonyesha Utukufu na Nguvu Zake Allaah سبحانه وتعالى  na kwamba Yeye anaweza kufanya lolote Alitakalo na sio kwamba hawezi kufanya miujiza ya kisa kama hiki cha As-haabul-Kahf. Akitaka anaweza kufanya miujiza  zaidi ya haya.

Ibn Jurayj alimsikia Mujaahid akisema kuhusu aya hiyo kwamba ina maana:

"Miongoni mwa alama zetu kuna maajabu zaidi ya haya " (At-Twabari 17:601)

Al-'Awf ameeleza maelezo kutoka kwa Ibn ‘Abbaas ambaye alisema: kuhusu aya hiyo kwamba ina maana:  "Yale niliyokupa ya elimu, Quraan na Sunnah ni bora zaidi kuliko kisa cha As-haabul-Kahf na Ar-Raqiim"

Nini maana ya Al-Kahf  na Ar-Raqiim?

Al-Kahf ni pango katika jabali ambalo vijana hao walikimbilia kujificha humo.   Na kuhusu neno la 'Ar-Raqiim' kuna usemi mbali mbali uliopokelewa kama ifuatavyo:

Al'Awfi amemsikia Ibn 'Abbas  kwamba ni bonde karibu na Aylah.  Hii imesimuliwa pia kwengine na 'Atiyah, Al-'Awfi pamoja na Qatada.  

Ad-Dhahhak   kasema,  Al-Kahf ni pango  katika bonde na Ar-Raqiim  ni jina la bonde.

Mujaahid kasema, Ar-Raqiim inakusudiwa  majengo yao.  

Wengine wamesema kuwa ni bonde ambalo lilikuwepo hilo pango lao. 

Ka'ab alikuwa akisema kwamba ni mji.

Ibn Jurayr kaeleza kwamba Ibn 'Abbas kasema Ar-Raqiim ni jabali lilikuwemo hilo pango. 

Sa'id bin Jubayr kasema Ar-Raqim ni ubamba wa jiwe wenye maandiko walioandikia kisa cha As-haabul-Kahf kisha wakaliweka  katika kiingilio cha mlango wa pango. (At-Twabari 17: 601 – 603)

 إِذْ أَوَى الْفِتْيَةُ إِلَى الْكَهْفِ فَقَالُوا رَبَّنَا آتِنَا مِن لَّدُنكَ رَحْمَةً وَهَيِّئْ لَنَا مِنْ أَمْرِنَا رَشَدًا ﴿10﴾

{{10.Vijana hao walipo kimbilia kwenye pango walisema: Mola wetu Mlezi! Tupe rehema itokayo kwako, na tutengezee uwongofu katika jambo letu}}

                                                                                       

Hapa Allaah Anatuambia kuhusu hao vijana wa kiume waliowakimbia watu wao kwa sababu ya dini yao, wamekimbia kwa kuogopa kuuliwa, kwa hiyo wakakimbilia pangoni katika mlima na kujificha humo. Walipoingia pangoni wakamuomba Allaah سبحانه وتعالى Awateremshie Rahma na huruma kwao wakasema:

}}فَقَالُوا رَبَّنَا آتِنَا مِن لَّدُنكَ رَحْمَةً{{

{{Mola wetu Mlezi! Tupe rehema itokayo kwako}}

Kwa maana: Tupe Rahma na utufiche na watu wetu.

 }}وَهَيِّئْ لَنَا مِنْ أَمْرِنَا رَشَدًا {{

{{na tutengezee uwongofu katika jambo letu}}

Maana: Yaelekeze mambo vizuri kwa kutujaalia mwisho mwema. Kama hadithi hii inavyoleta maana kama hiyo.

((وَمَاَ قَضَيْتَ لَنَا مِنْ  قَضَاءٍ فَاجْعَلْ عَاقِِبَتَهُ رَشَداً))

((Na lolote Utakalotuamulia, basi Lijaalie liwe na mwisho mwema))

 فَضَرَبْنَا عَلَى آذَانِهِمْ فِي الْكَهْفِ سِنِينَ عَدَدًا ﴿11﴾

{{11. Tukayaziba masikio yao kuwalaza humo pangoni kwa muda wa miaka kadhaa wa kadhaa}}

Tukawafanya walale walipoingia pangoni, na wakalala miaka mingi.

Allaah سبحانه وتعالى Anasema hapa kuwa Aliwazibua masikio yao, wala Hakusema kuwa Aliwafunga macho yao kama vile ilivyo kawaida ya mtu anapolala kuwa hufunga macho yake.  Basi hapa kuna hikma kubwa Aliyoitumia Allaah سبحانه وتعالى  kutaja kuwazibua  masikio yao, na tutapata  mafundisho mazito ya kuzingatia kuhusu  kiungo cha masikio  na umuhimu wake kwa binaadamu .

Basi tuelezee kidogo maajabu ya Qur'aan na Maumbile ya Allaah سبحانه وتعالى  kuhusu 'masikio' (kusikia) kama alivyotuelezea Sh. Muhammad Mutawalliy Ash-Sha'arawiy  رحمه الله  katika Tafsiyr yake, anasema:

Kwa kupata kufahamu vizuri tuulize na kujibu maswali haya yafuatayo:

1.      Akiuliza mtu kiungo gani baina ya macho na masikio kilicho muhimu kwa binaadamu zaidi ambacho ni tabu zaidi kwake kukikosa? Bila ya shaka atasema mtu ni macho. Kwa sababu kiziwi ni bora kuliko kipofu. Sasa basi kwa nini Allaah سبحانه وتعالى ametanguliza neno السمع  (sikio) kabla ya أبصار  (macho) katika aya alizotaja hayo na hali macho ni muhimu kwa binaadamu zaidi ya masikio?

2.      Kwa nini Allaah سبحانه وتعالى Anataja السمع (sikio) kwa moja (singular )  na أبصار  (macho/maono) kwa wingi (plural)?

Tuzisome aya zinazotaja Usikiaji na Uoni

 

}} وَمَا كُنتُمْ تَسْتَتِرُونَ أَنْ يَشْهَدَ عَلَيْكُمْ سَمْعُكُمْ وَلاَ أَبْصَارُكُمْ وَلاَ جُلُودُكُمْ وَلَكِن ظَنَنتُمْ أَنَّ اللَّهَ لاَ يَعْلَمُ كَثِيرًا  مِّمَّا تَعْمَلُونَ{{

{{Na hamkuwa wenye kujificha hata masikio yenu, na macho yenu, na ngozi zenu, zisikushuhudilieni. Lakini mlidhani kwamba Mwenyezi Mungu hayajui mengi katika mliyo kuwa mkiyatenda}}   Fusswilaat: 22

 Aya hii Ametaja Allaah mara mbili viungo hivyo:

}}وَلَقَدْ مَكَّنَّاهُمْ فِيمَا إِن مَّكَّنَّاكُمْ فِيهِ وَجَعَلْنَا لَهُمْ سَمْعًا وَأَبْصَارًا وَأَفْئِدَةً فَمَا أَغْنَى عَنْهُمْ سَمْعُهُمْ وَلاَ أَبْصَارُهُمْ وَلاَ أَفْئِدَتُهُم مِّن شَيْءٍ إِذْ كَانُوا يَجْحَدُونَ بِآيَاتِ اللَّهِ وَحَاقَ بِهِم مَّا كَانُوا بِهِ يَسْتَهْزِؤُون{{

{{Na bila ya shaka tuliwaweka vizuri sio kama tulivyo kuwekeni nyinyi; na tuliwapa masikio, na macho, na nyoyo. Na hayakuwafaa kitu masikio yao, wala macho yao, wala nyoyo zao kwa lolote. Kwani hao walikuwa wakizikataa Ishara za Mwenyezi Mungu, na yale waliyo kuwa wakiyafanyia maskhara ndiyo yakawazunguka}}  Ahqaaf:  26

}}قُلْ هُوَ الَّذِي أَنشَأَكُمْ وَجَعَلَ لَكُمُ السَّمْعَ وَالأَبْصَارَ وَالأَفْئِدَةَ قَلِيلاً مَّا تَشْكُرُونَ{{

{{Sema: Yeye ndiye aliye kuumbeni tangu mwanzo, na akakupeni masikio na macho, na nyoyo. Ni kidogo kabisa shukrani zenu}} Al-Mulk 23  

Majibu:

·   Sikio ni kiungo cha mwanzo kabisa kufanya kazi katika mwili wa binaadamu anapozaliwa.  Tunajua kuwa mtoto mchanga huchelewa kidogo kuona, lakini hachelewi kusikia kwani anaweza kuamshwa usingizini inapotokea sauti kubwa.

 

·     Sikio vile vile ni kiungo cha mwanzo kitakachofanya kazi siku ya Kiyama baada ya Malaika Israafiil  kupiga baragumu (suur), likasikika, na watu wote watafufuka kutoka makaburini mwao, na wengine watazimia kwa ukali wa sauti hiyo ya baragumu. 

}}وَيَوْمَ يُنفَخُ فِي الصُّورِ فَفَزِعَ مَن فِي السَّمَاوَاتِ وَمَن فِي الأَ رْضِ إِلأَ مَن شَاء اللَّهُ وَكُلٌّ أَتَوْهُ دَاخِرِينَ{{

{{Na Siku litapo pulizwa baragumu, watahangaika waliomo mbinguni na katika ardhi, ila amtakaye Mwenyezi Mungu. Na wote watamfikia nao ni wanyonge}}    An-Naml: 87

}}يَوْمَ يُنفَخُ فِي الصُّورِ وَنَحْشُرُ الْمُجْرِمِينَ يَوْمَئِذٍ زُرْقًا{{

{{Siku itakapo pulizwa barugumu, na tukawakusanya wakhalifu Siku hiyo, hali macho yao ya kibuluu}} Taha:102

َ}} وَيَوْمَ يُنفَخُ فِي الصُّورِ فَتَأْتُونَ أَفْوَاجًا{{

{{Siku litapo pulizwa barugumu, nanyi mtakuja kwa makundi}}  

An-Nabaa: 18   

·   Macho yanahitaji mwanga ili kuonea, kwenye giza mtu hawezi kuona kitu, lakini masikio yanafanya kazi yake wakati wowote, mahala popote kama mfano anapolala mtu macho huwa hayafanyi kazi yake ya kuona, lakini masikio yako wazi wakati wote yanafanya kazi yake ya kusikia, ndio maana Allaah سبحانه وتعالى Akaujaalia usiku kuwa mtulivu kwetu  kwa kutufanyia uwe kimya kabisa ili tuweze kulala vizuri.

}}وَجَعَلْنَا اللَّيْلَ وَالنَّهَارَ آيَتَيْنِ فَمَحَوْنَا آيَةَ اللَّيْلِ وَجَعَلْنَا آيَةَ النَّهَارِ مُبْصِرَةً لِتَبْتَغُواْ فَضْلاً مِّن رَّبِّكُمْ{{

{{Na tumefanya usiku na mchana kuwa ishara mbili. Tena tukaifuta ishara ya usiku, na tukaifanya ishara ya mchana ni yenye mwangaza ili mtafute fadhila itokayo kwa Mola wenu Mlezi}}   Al-Israa:12 

 وَجَعَلْنَا نَوْمَكُمْ سُبَاتًا ﴿9﴾ وَجَعَلْنَا اللَّيْلَ لِبَاسًا ﴿10﴾ وَجَعَلْنَا النَّهَارَ مَعَاشًا ﴿11﴾  

{{Na tukakufanya kulala kwenu ni mapumziko?}}

{{Na tukaufanya usiku ni nguo?}}

{{Na tukaufanya mchana ni wa kuchumia maisha?}}

An-Nabaa:9-11

Na ndio maana mwizi anapoingia kuiba hunyata polepole ili mwenyeji asimsikie anapoingia. 

·    Macho huyatumia mtu kwa matamanio yake, yaani anaweza mtu kujizuia asitazame jambo fulani, mfano mtu anatembea njiani kisha akaona jambo baya linatendeka njiani, anaweza kujizuia asilitazame lile jambo kwa kugeuza uso au kubadilisha njia na kadhalika.  Ama masikio, hayana kizibo, inapotokea sauti akitaka asitake itabidi aiisikie tu hiyo sauti.

 

·  Masikio ni kiungo muhimu kwa binaadamu kusikia maneno ya Allaah سبحانه وتعالى na kuweza kuathirika mtu kupata hidaya kwani wapotofu watajilaumu kwa kusema :

}}وَقَالُوا لَوْ كُنَّا نَسْمَعُ أَوْ نَعْقِلُ مَا كُنَّا فِي أَصْحَابِ السَّعِير{{ِ  

{{Na watasema: Lau kuwa tungeli sikia, au tungeli kuwa na akili, tusingeli kuwa katika watu wa Motoni}} Al-Mulk:10

Vile vile uongofu wetu wote unatokana na Qur'aan ambayo tumeamrishwa tuwe tunaisikiliza inaposomwa ili iwe Rehma kwetu:

}}إِذَا قُرِىءَ الْقُرْآنُ فَاسْتَمِعُواْ لَهُ وَأَنصِتُواْ لَعَلَّكُمْ تُرْحَمُونَ{{

{{Na  isomwapo Qur'ani isikilizeni na mnyamaze ili mpate kurehemewa}} 

Al-A'araaf 204

·      Sababu ya kutaja sikio kwa umoja (singular)  na macho kwa wingi (plural) ni kwamba,  mfano, inapotokea mshindo wa sauti kubwa ya ghafla wakati watu wengi wamekaa mahali pamoja, kila mtu atasikia sauti ile kwa usawa, yaani kila mmoja atasikia vile vile ile sifa ya sauti bila ya kuweko tofauti na kusikia kwa wengine.  Lakini kwa kushtuka, kila mmoja atapeleka macho yake kuitafuta sauti inatoka wapi, kwa hivyo kila mmoja atakuwa ametazama sehemu mbali mbali, mwenye kuitafuta sauti kwa kutazama labda juu au upande wa kulia au wa kushoto au mbele au nyuma. Hapo ndipo inapokuja maana nzito kuwa Usikivu ni ule ule , ama Uonaji ni mbali mbali .

Wallaahu A'alam.

Tukiendelea na kisa cha As-haabul-Kahf…..

  ثُمَّ بَعَثْنَاهُمْ لِنَعْلَمَ أَيُّ الْحِزْبَيْنِ أَحْصَى لِمَا لَبِثُوا أَمَدًا ﴿12﴾  

{{12. Kisha tukawazindua ili tujue ni lipi katika makundi mawili lilio hisabu sawa muda walio kaa}}

}}لِنَعْلَمَ أَيُّ الْحِزْبَيْنِ{{

{{ili tujue ni lipi katika makundi mawili}}

Makundi mawili yaliyobishana kuhusu As-haabul-Kahf.

}}أَحْصَى لِمَا لَبِثُوا أَمَدًا{{

{{lilio hisabu sawa muda walio kaa}} 

Inakusudiwa  ubishano wa muda gani waliokaa katika pango.

  نَحْنُ نَقُصُّ عَلَيْكَ نَبَأَهُم بِالْحَقِّ إِنَّهُمْ فِتْيَةٌ آمَنُوا بِرَبِّهِمْ وَزِدْنَاهُمْ هُدًى ﴿13﴾  

{{13. Sisi tunakusimulia khabari zao kwa kweli. Hakika wao walikuwa ni vijana walio muamini Mola wao Mlezi. Na Sisi tukawazidisha uwongofu}} 

Hapa Allaah سبحانه وتعالى Anaanza kusimulia kisa hiki kwa urefu na   kumwambia Mtume صلى الله عليه وسلم  kuwa hiki ni kisa cha kweli kutoka kwake Allaah سبحانه وتعالى ambacho hakina shaka.  

Anasema kuwa walikuwa ni vijana wanaume na walikuwa wamekubali Tawhiyd na walipata uongofu zaidi kuliko wazee waliokuwa wakiishi nao ambao walikuwa wamo katika ukaidi  wa kushikilia dini yao ya upotofu ya kuabudu masanamu.

Aya hii  vile vile inatuonyesha ukweli huu wa vijana kuwa wepesi kukubali  wito  wa Mitume.

فَمَا آمَنَ لِمُوسَى إِلاَّ ذُرِّيَّةٌ مِّن قَوْمِهِ عَلَى خَوْفٍ مِّن فِرْعَوْنَ وَمَلَئِهِمْ أَن يَفْتِنَهُمْ  .....   ﴿83﴾

83. Basi hawakumuamini Musa isipokuwa baadhi ya vijana wa Qaumu yake, kwa kumwogopa Firauni na wakuu wao wasiwatese ........   (Yunus : 83)

 Mara nyingi  Mwenyezi Mungu kabainisha kuwa wanaoanza kuwafuata Mitume ni vijana, si ile mizee, kwani ile mizee huwa imebobea katika ubaya wao, wanaona tabu kuukosa huo ukubwa wao na hayo waliyoyazoelea, japo mabaya kwani 'Mzoea vya kunyonga, vya kuchinja haviwezi' (Qur'ani Takatifu - Sh Abdullah Swaalih Al-Farsiy)

 Ukitazama katika historia ya Mtume صلى الله عليه وسلم  vile vile, utaona kuwa wengi wao waliomuitikia Mtume صلى الله عليه وسلم ni vijana zaidi kuliko wazee kwani wazee wa ki-Quraysh wengi wao walitaka kubakia katika dini yao, ni wachache waliokubali haki na kuingia katika Uislam.

Hali kadhalika utaona kwamba ni vigumu sana kwa wengi wa wazee wetu siku hizi kukubali kufuata Sunnah na kuacha Bid'aa, ni wachache ukilinganisha na vijana, na yote ni  kwa vile wameshikilia mila za mababu, na wengi wanaokubali kufuata Sunnah kwa wepesi ni vijana zaidi.

 }} وَزِدْنَاهُمْ هُدًى{{

{{Na Sisi tukawazidisha uwongofu}}

Kama alivyosema katika aya hizi nyingine  kuhusu kuwaongezea uongofu wale wanaotaka uongofu:

 

}}وَالَّذِينَ اهْتَدَوْا زَادَهُمْ هُدًى وَآتَاهُمْ تَقْواهُمْ{{

{{Na wale walio ongoka anawazidishia uongofu na anawapa uchamngu wao}}   Muhammad:17

}}فَأَمَّا الَّذِينَ آمَنُواْ فَزَادَتْهُمْ إِيمَانًا وَهُمْ يَسْتَبْشِرُونَ{{

{{Ama wale walio amini inawazidishia Imani, nao wanafurahi}}

At-Tawbah: 124 

}}هُوَ الَّذِي أَنزَلَ السَّكِينَةَ فِي قُلُوبِ الْمُؤْمِنِينَ لِيَزْدَادُوا إِيمَانًا مَّعَ إِيمَانِهِمْ{{

{{Yeye ndiye aliye teremsha utulivu katika nyoyo za Waumini ili wazidi Imani juu ya Imani yao}}  Al-Fath:4

 

Tunaendelea na kisa cha As-haabul-Kahf ……

  وَرَبَطْنَا عَلَى قُلُوبِهِمْ إِذْ قَامُوا فَقَالُوا رَبُّنَا رَبُّ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ لَن نَّدْعُوَ مِن دُونِهِ إِلَهًا لَقَدْ قُلْنَا إِذًا شَطَطًا ﴿14﴾

{{14. Na tukazitia nguvu nyoyo zao walipo simama na wakasema: Mola wetu Mlezi ni Mola Mlezi wa mbingu na ardhi. Hatutamwita mwenginewe kabisa badala yake kuwa ni Mungu. Hivyo itakuwa tumesema jambo la kuvuka mpaka}}

Allaah سبحانه وتعالى Aliwapa nguvu na imani zaidi kwenda kinyume na watu wa mji wao na kuacha maisha ya starehe waliyokuwa wakiishi. 

Wafasiri wengi wamesema kuwa walikuwa wana wa wafalme na wakubwa wa Byantium, na kwamba siku moja walikwenda katika  sikukuu ya watu wao waliokuwa wakikusanyika  mara moja kwa mwaka nje ya mji kisha wakiabudu  masanamu na kuwachinjia.  Mfalme wao alikuwa dhalimu, mjeuri, akiitwa Decianus  na alikuwa akiwashikilia (akiwalazimisha) watu waende kwenye sherehe hizo.  

Vijana hao walipokwenda na wazee wao katika sherehe hizo na walipoona yale yanayotendeka kwa ajili ya masanamu, walitambua kuwa  kusujudu na kuchinja haipasi  kutendewa kwa chochote wala mtu yeyote isipokuwa Allaah سبحانه وتعالى  Ambaye ameumba mbingu na ardhi.  Mmoja mmoja akawa anaondoka na kujitenga mbali na watu wao. Wa kwanza aliyejitenga alikwenda kukaa chini ya mti wenye kivuli. Kisha akaja mwengine kukaa naye, kisha akaja mwengine tena, kisha wakafuatia  wengine wanne, na wote walikuwa hawajuani lakini wamekusanywa pamoja na Allaah سبحانه وتعالى  Ambaye aliwagusisha imani katika nyoyo zao.  Na mfano ni kama hadithi iliyosimuliwa na Al-Bukhari kutoka kwa Bibi 'Aisha رضي الله عنها   kwamba Mtume صلى الله عليه وسلم kasema:

((  عَنْ عَائِشَةَ رَضِيَ اللَّهُ عَنْهَا قَالَتْ سَمِعْتُ النَّبِيَّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ يَقُولُ : " الأَرْوَاحُ جُنُودٌ مُجَنَّدَةٌ فَمَا تَعَارَفَ مِنْهَا ائْتَلَفَ وَمَا تَنَاكَرَ مِنْهَا اخْتَلَفَ (( صحيح البخاري : كتاب أحاديث الأنبياء : باب الأرواح جنود مجندة .

((Roho ni kama askari waliokusanyana, zile zinazotambuana zinakutana pamoja, na zile zisizotambuana zinatengana))

Kila mmoja wa hao vijana alijaribu kuficha  aliyoyaaamini kwa mwenzake, kwa kuogopana, bila ya kujua wote kumbe imani yao ni moja. Kisha mmoja wao akaanza kusema "Enyi watu, bila ya shaka mnajua kuwa ni sababu fulani iliyokufanyeni mujitenge na watu wetu, basi hebu kila mmoja aelezee sababu yake".  Mmoja akasema "Mimi kwa hakika nilivyoona wanayoyatenda watu wangu, nimetambua ni makosa, na kwamba apasae kutendewa hayo ni Allaah سبحانه وتعالى  Pekee bila ya kumshirikisha na chochote, Ambaye ameumba mbingu na ardhi na vilivyomo baina yake vyote".   Wa pili akasema "Mimi hali kadhalika ni sababu  hiyo hiyo"  Kisha wengine wote wakakubaliana kuwa ni sababu hiyo hiyo moja iliyowafanya kutengana na watu wao na ibada zao za masanamu.   

Wakatafuta sehemu maalumu ya kufanya ibada yao ya kumuabudu Allaah سبحانه وتعالى , lakini watu wao wakaja kujua, wakamwambia mfalme ambaye aliamrisha  waletwe mbele yake na kuwauliza kuhusu itikadi yao. Vijana hao hawakuogopa bali Allaah سبحانه وتعالى  aliwapa nguvu na imani waseme ukweli kwamba  Mola wao ni Yule mwenye kuumba mbingu na ardhi kama aya hii inavyoeleza:

 وَرَبَطْنَا عَلَى قُلُوبِهِمْ إِذْ قَامُوا فَقَالُوا رَبُّنَا رَبُّ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ لَن نَّدْعُوَ مِن دُونِهِ إِلَهًا لَقَدْ قُلْنَا إِذًا شَطَطًا ﴿14﴾

{{14. Na tukazitia nguvu nyoyo zao walipo simama na wakasema: Mola wetu Mlezi ni Mola Mlezi wa mbingu na ardhi. Hatutamwita mwenginewe kabisa badala yake kuwa ni Mungu. Hivyo itakuwa tumesema jambo la kuvuka mpaka}}

 

}}لَقَدْ قُلْنَا إِذًا شَطَطًا{{

{{Hivyo itakuwa tumesema jambo la kuvuka mpaka}}

Maana kwamba: tutasema jambo sio la ukweli na kusema uongo.

 هَؤُلَاء قَوْمُنَا اتَّخَذُوا مِن دُونِهِ آلِهَةً لَّوْلَا يَأْتُونَ عَلَيْهِم بِسُلْطَانٍ بَيِّنٍ فَمَنْ أَظْلَمُ مِمَّنِ افْتَرَى عَلَى اللَّهِ كَذِبًا ﴿15﴾  

 

{{15. Hawa watu wetu wameshika miungu mingine badala yake Yeye. Kwa nini basi hawawatolei uthibitisho ulio dhaahiri? Na nani aliye dhaalimu zaidi kuliko anaye mzulia uwongo Mwenyezi Mungu}}

Maana kwamba: kwa nini hawatoi uthibitisho ulio dhahiri wa halisi kwa tabia yao hiyo?

}}فَمَنْ أَظْلَمُ مِمَّنِ افْتَرَى عَلَى اللَّهِ كَذِبًا{{

{{Na nani aliye dhaalimu zaidi kuliko anaye mzulia uwongo Mwenyezi Mungu}}

Imesemekana kwamba walivyomwambia mfalme  amuamini Allaah سبحانه وتعالى  alikataa na akawaonya na kuwatisha. Aliamrisha wavuliwe nguo na  wavalishwe mapambo ya  watu wao, kisha akawapa muda  wafikirie hali zao huku akitumainia kuwa watarudi katika dini yao. Na ndio maana Allaah سبحانه وتعالى  Aliwaonesha huruma, kwani walikimbia kuepukana na kuuliwa kwa sababu ya dini yao.   Na hii ndio sheria ya kiislamu ilivyoruhusu wakati wa hali ya fitna na kukimbia kuuliwa kwa khofu ya kupoteza dini yake kama katika hadithi ifuatayo:

((عن أبي سعيد الخدري رضي الله عنه قال : قال رسول الله صلى الله عليه وسلم :يوشك أن يكون خير مال المسلم غنم يتبع بها شعف الجبال ومواقع القطر يفر بدينه من الفتن )) رواه البخاري

((Inakaribia kuwa mali bora kabisa ya Muislamu itakuwa ni kondoo hufuatwa juu ya milima na sehemu zinazomwagika maji  (anakimbia) asiuliwe kwa sababu ya dini yake)) Al-Bukhari

Kwa hali kama hizi inaruhusiwa kujitenga mbali na watu ama kwa hali nyingine haifai kwa sababu Muislamu atapoteza faida za Swalah za Jamaa na Swalah ya Ijumaa. 

Vijana hawa waliazimia kuwakimbia watu wao na Allaah سبحانه وتعالى  Alikwishawakidhia kufanya hivyo na kuwaambia:

 وَإِذِ اعْتَزَلْتُمُوهُمْ وَمَا يَعْبُدُونَ إِلَّا اللَّهَ فَأْوُوا إِلَى الْكَهْفِ يَنشُرْ لَكُمْ رَبُّكُم مِّن رَّحمته ويُهَيِّئْ لَكُم مِّنْ أَمْرِكُم مِّرْفَقًا ﴿16﴾

{{16. Na mkijitenga nao na vile wanavyo viabudu badala ya Mwenyezi Mungu, basi kimbilieni pangoni, akufungulieni Mola wenu Mlezi rehema  yake, na akutengenezeeni ya kukufaeni katika mambo yenu}}.

Maana kwamba:  mkijitenga nao kwa sababu ya kuikanusha dini yao ya kuabudu asiye Allaah سبحانه وتعالى,  basi jitengeni nao kwa kuwa mbali nao kabisa, hivyo kimbilieni kwenye  pango.

}}يَنشُرْ لَكُمْ رَبُّكُم مِّن رَّحمته{{

{{akufungulieni Mola wenu Mlezi rehema yake}}

Atakuteremshieni Rahma Yake ambayo ni kuwaficha ili msijulikane na watu wenu.

}}ويُهَيِّئْ لَكُم مِّنْ أَمْرِكُم مِّرْفَقًا{{

{{na akutengenezeeni ya kukufaeni katika mambo yenu}}

Atakupeni yale mnayoyahitaji. 

Wakakimbia kwenda kujificha katika pango.  Kisha watu wao wakaanza kuhisi kupotea kwao.  Mfalme akatuma watu kuwatafuta, lakini Allaah سبحانه وتعالى Aliwaficha wasionekane, na hawakuweza kupata hata alama yao yoyote au habari yao yoyote baada ya hapo.   

Mfano huu ni kama mfano wa alivyofichwa Mtume صلى الله عليه وسلم na Abubakar رضي الله عنه  katika pango la Thawr walipokuwa wanahama kwenda Madina na makafiri walivyokuwa wanawatafuta lakini hawakuwaona, japokuwa walipita chini yao katika hilo pango la Thawr. Mtume صلى الله عليه وسلم alipomuona Abubakar ana khofu ya ujulikana  alipomwambia Mtume صلى الله عليه وسلم  "Ewe mjumbe wa Allaah, mmoja  wao akitazama chini  sehemu ya miguu yake atatuona" Mtume صلى الله عليه وسلم alimjibu Abubakar

((يَا أَبا بَكْرٍ مَا ظَنُّكَ بِإثْنَيْنِ اللَّهُ ثاَلِثُهُماَ؟))

((Ewe Abubakar, unafikiriaje wawili ambao wanaye Allaah سبحانه وتعالى kuwa ni watatu wao?))

Allaah سبحانه وتعالى akataja kunusurika kwao katika ayah hii: 

 إِلاَّ تَنصُرُوهُ فَقَدْ نَصَرَهُ اللّهُ إِذْ أَخْرَجَهُ الَّذِينَ كَفَرُواْ ثَانِيَ اثْنَيْنِ إِذْ هُمَا فِي الْغَارِ إِذْ يَقُولُ لِصَاحِبِهِ لاَ تَحْزَنْ إِنَّ اللّهَ مَعَنَا فَأَنزَلَ اللّهُ سَكِينَتَهُ عَلَيْهِ وَأَيَّدَهُ بِجُنُودٍ لَّمْ تَرَوْهَا وَجَعَلَ كَلِمَةَ الَّذِينَ كَفَرُواْ السُّفْلَى وَكَلِمَةُ اللّهِ هِيَ الْعُلْيَا وَاللّهُ عَزِيزٌ حَكِيمٌ ﴿40﴾

{{Ikiwa nyinyi hamtamnusuru Mtume, basi Mwenyezi Mungu alikwisha mnusuru walipo mtoa walio kufuru, naye ni wa pili katika wawili walipo kuwa katika pango, naye akamwambia sahibu yake: Usihuzunike. Hakika Mwenyezi Mungu yu pamoja nasi. Mwenyezi Mungu akamteremshia utulivu wake, na akamuunga mkono kwa majeshi msiyo yaona, na akalifanya neno la walio kufuru kuwa chini, na Neno la Mwenyezi Mungu kuwa ndilo juu. Na Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye nguvu Mwenye hikima}} At-Tawbah: 40

 

Kisa kitaendelea....../2