Suwrat Yaasiyn Na Al-An'aam Zina Fadhila?

 

Suwrat Yaasiyn Na Al-An'aam Zina Fadhila?

 

Alhidaaya.com

 

 

SWALI:

 

Naomba kupewa faida za Suwarah Yasin na Al-An'aam, kwani nimeambiwa usome ukiwa na shida au dhiki, ama nitukio gani lilitokea kuteremshwa Suwrah hizi? Shukran, Allaahu Barik, In Shaa Allaah.

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah - Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salaam zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Suwrah Yaasiyn

 

Tunaweka wazi Hadiyth ambazo zimeenea sana kuonyesha fadhila na utukufu wa Suwrah hii. Tunaona katika jamii zetu jinsi watu wanavoitukuza Suwrah hii pekee kuliko Suwrah zingine za Qur-aan kwa kuisoma kila siku na kuacha kusoma Qur-aan kwa mpangilio wake. Vilevile husomwa ki bid’ah kama vile mtu anapokata roho au hata baada ya kufa kwake na pia kuisoma  makaburini n.k.

 

Hadiyth zisizo sahihi kuhusu Suwrah Yaasiyn:

 

عن أبي هريرة رضي الله عنه عن النبي صلى الله عليه وسلم:  "إن الله تبارك وتعالى قرأ  طه  و يّس   قبل أن يخلق آدم بألفي عام ، فلما سمعت الملائكة القرآن قالوا  طوبى لأمة ينزل هذا عليهم ، وطوبى لألسن تتكلم بهذا ، وطوبى لأجوف تحمل هذا" ابن القيسراني, سلسلة الأحاديث الضعيفة  1248

Kutoka kwa Abuu Hurayrah (Radhwiya Allaahu 'anhu)  kwamba Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Allaah (Tabaaraka wa Ta’aalaa) Amesoma Suwrah Twaahaa na Yaassiy kabla ya kumuumba Aadam miaka elfu, na waliposikia Malaika Qur-aan wakasema "pongezi  kwa umma inayowashukia (Suwrah) hii, pongezi kwa ulimi utakaoizungumza Suwrah hii, pongezi kwa tumbo (mwili) utakaobeba.”    [Ibn Al-Qiysaraaniy  

Imechambuliwa kuwa ni dhaifu -  Silsilatul-Ahaadiyth Adhw-Dhwa'iyfah 1248]

 

 عن أنس بن مالك رضي الله عنه:   من دخل المقابر فقرأ سورة   يّس   خفف عنهم يومئذ ، وكان له بعدد من فيها حسنات )) السخاوي - موضوع - سلسلة الأحاديث الضعيفة  1246   ..

Kutoka kwa Anas Bin Maalik (Radhwiya Allaahu 'anhu): “Atakayeingia makaburini na akasoma Suwrat  Yaasiyn atawafanyia wepesi (maiti) siku ya masiku, na ataandikiwa mema idadi ya walio humo makaburini.” [As-Sakhaawiy – Hadiyth dhaifu  Silsilatul-Ahaadiyth Adhw-Dhwa'iyfah 1246]

 

 عن أنس بن مالك رضي الله عنه : إن لكل شيء قلبا، وقلب القرآن  يس، ومن قرأ  يس كتب الله له بقراءتها قراءة القرآن عشر مرات)) الذهبي -  موضوع  - ضعيف الترغيب و الترهيب  885

Kutoka kwa Anas Bin Maalik (Radhwiya Allaahu 'anhu): “Kila kitu kina moyo, na moyo wa Qur-aan ni Suwrat Yaasiyn, atakayesoma Yaasiyn ataandikiwa thawabu za kusoma Qur-aan yote mara kumi.” [Adh-Dhahabiy – Hadiyth dhaifu - At Targhiyb wat-Tarhiyb 885]

 

من قرأ يس ابتغاء وجه الله ، غفر الله له ما تقدم من ذنبه، فاقرؤوها عند موتاكم )) ضعيف الجامع الصغير 5785  

 

“Atakayesoma Yaasiyn kwa kutaka Radhi za Allaah ataghufuriwa madhambi yaliyomtangulia, basi isomeni kwa maiti wenu.” [Hadiyth dhaifu Al-Jaami’ Asw-Swaghiyr 5785]

 

 من قرأ  يس  في صدر النهار  قضيت حوائجه  ضعيف مشكاة المصابيح  2118

 

“Atakayesoma Yaasiyn katikati ya mchana atakidhiwa haja yake.”  [Hadiyth dhaifu - Mishkaat Al-Maswaabiyh 2118]  

 

Imaam Ad-Daaraqutwniy kasema hakuna Hadiyth yeyote iliyosihi fadhila za Suwrat Yaasiyn

 

 

Suwrah-Al-An'aam

 

Hakuna Hadiyth zilotajwa fadhila ya Suwrah hii isipokuwa kutajwa kwake jinsi ilivyoteremshwa ambayo hamaanishi kuwa inapaswa kuisoma kwa namna fulani:

 

عن ابن عمر قال : قال رسول الله صلى الله عليه وسلم" نزلت علي سورة الأنعام جملة واحدة وشيعها سبعون ألفا من الملائكة لهم زجل بالتسبيح والتحميد  رواه الطبراني في " الأوسط

Kutoka kwa Ibn 'Umar ambaye amesema: Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Imeteremka Suwrah ya Al-An'aam kwa mteremko mmoja na imefuatana na Malaika elfu sabiini  wakimtukuza Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kwa kumsabihi na kumhimidi kwa sauti za juu.”  [At-Twabraaniy]

 

Yaliyothibiti kuondosha shida na dhiki ni du’aa ambazo zimo katika Hiswnul-Muslim na Hiswnul-Muumin.

Bonyeza viungo vifuatavyo:

 

034-Hiswnul-Muslim: Du’aa Ukiwa Na Wahka Na Huzuni

 

 

035-Hiswnul-Muslim: Du’aa Unapopatwa Janga Au Balaa

 

 

075-Kuomba Qur-aan Kuwa Ni Uhuisho Wa Moyo Na Nuru, Kuondokewa Huzuni,Wahka

 

10 - Yanayosahilisha Kuvumilia Mitihani

 

Pia ni kuamka usiku thuluthi ya mwisho kumuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Ambaye Huteremka mbingu ya kwanza kuwatakabalia waja Wake haja zao.

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share