Maonyo Ya Allaah (سبحانه وتعالى) Kujiepusha Na Kughafilika Kwa Nafsi

 

Maonyo Ya Allaah (سبحانه وتعالى)

Kujiepusha Na Kughafilika Kwa Nafsi

 

www.Alhidaaya.com

 

 

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Ametuonya tusije kufikia hali ya nafsi kujuta kwa kutokana na kushughulika na mambo ya dunia ambayo ndio sababu kubwa ya kujikuta mtu yuko kwenye 'ghaflah' (kughafilika na Aakhirah), kusahau kama mauti yako tayari kwa yule iliyomfikia ajali yake bila ya kujua lini au wapi ameandikiwa, kama Anavyosema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

 وَمَا تَدْرِي نَفْسٌ مَّاذَا تَكْسِبُ غَدًا ۖ وَمَا تَدْرِي نَفْسٌ بِأَيِّ أَرْضٍ تَمُوتُ ۚ إِنَّ اللَّـهَ عَلِيمٌ خَبِيرٌ ﴿٣٤﴾

“Na nafsi yoyote haijui nini itachuma kesho, na nafsi yoyote haijui itafia katika ardhi gani, hakika Allaah ni Mjuzi wa yote, Mwenye upeo wa khabari za dhahiri na za kufichika.” [Luqmaan: 34].

 

Kwa hiyo inapomfikia mtu ajali yake na roho inapotoka hapo nafsi tena hutambua kuwa yale yaliyokuwa yakimshughulisha duniani hayana tena faida naye wala hayawezi kumsaidia wakati huu, ndipo hubaki kujuta na kutambua kuwa yupo katika hasara kubwa!  

   

Tunaona jinsi gani Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) anavyotoa onyo au tanabahisho kwa mwanaadam kwa kughafilika na dhikr (ukumbusho) wa Allaah, na kuendekeza dunia na mapambo yake. 

 

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَا تُلْهِكُمْ أَمْوَالُكُمْ وَلَا أَوْلَادُكُمْ عَن ذِكْرِ اللَّـهِ ۚ وَمَن يَفْعَلْ ذَٰلِكَ فَأُولَـٰئِكَ هُمُ الْخَاسِرُونَ﴿٩﴾

“Enyi walioamini! Zisikupurukusheni mali zenu na wala watoto wenu mkaacha kumdhukuru Allaah. Na yeyote atakayefanya hivyo basi hao ndio waliokhasirika.” [Al-Munaafiquwn: 9]

 

Bali mwana Aadam ni mwingi wa kusahau na kughafilika, pamoja na maonyo na tanbihi zote hizo za Mola wake lakini dunia imemzamisha na kuyanywa maji yake yaliyomlewesha na hadi kutojitambua, mwisho wake ni majuto yale yale ya  kutamani kurudishwa duniani afanye mema:

 

وَأَنفِقُوا مِن مَّا رَزَقْنَاكُم مِّن قَبْلِ أَن يَأْتِيَ أَحَدَكُمُ الْمَوْتُ فَيَقُولَ رَبِّ لَوْلَا أَخَّرْتَنِي إِلَىٰ أَجَلٍ قَرِيبٍ فَأَصَّدَّقَ وَأَكُن مِّنَ الصَّالِحِينَ﴿١٠﴾

“Na toeni katika yale Tuliyokuruzukuni kabla hayajamfikia mmoja wenu mauti akasema: Rabb wangu! Lau Ungeliniakhirisha mpaka muda wa karibu hivi, basi ningetoa swadaqah na ningelikuwa miongoni mwa Swalihina.” [Al-Munaafiquwn: 10].

 

Lakini wapi! 

 

وَلَن يُؤَخِّرَ اللَّـهُ نَفْسًا إِذَا جَاءَ أَجَلُهَا ۚ وَاللَّـهُ خَبِيرٌ بِمَا تَعْمَلُونَ﴿١١﴾

“Lakini Allaah Haiakhirishi kamwe nafsi yeyote inapokuja ajali yake na Allaah ni Mwenye upeo wa khabari za dhahiri na za kufichika kwa yale myatendayo.” [Al-Munaafiquwn: 11].

 

Na vilevile Kama Anavyosema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) tena katika Suratul-Muuminuwn:

 

 حَتَّىٰ إِذَا جَاءَ أَحَدَهُمُ الْمَوْتُ قَالَ رَبِّ ارْجِعُونِ ﴿٩٩﴾ لَعَلِّي أَعْمَلُ صَالِحًا فِيمَا تَرَكْتُ ۚ كَلَّا ۚ إِنَّهَا كَلِمَةٌ هُوَ قَائِلُهَا ۖ وَمِن وَرَائِهِم بَرْزَخٌ إِلَىٰ يَوْمِ يُبْعَثُونَ ﴿١٠٠﴾

 “Mpaka itakapomfikia mmoja wao mauti, atasema: Rabb wangu! Nirejeshe (duniani). Ili nikatende mema katika yale niliyoyaacha. (Ataambiwa) Laa hasha! Hakika hilo ni neno alisemaye yeye tu.  Na nyuma yao kuna barzakh mpaka Siku watakayofufuliwa.”. [Al-Muuminuwn: 99-100].

 

 

 

Share