Hadi Lini Utakuwa Mwenye Kughafilika?

Hadi Line Utakuwa Mwenye Kughafilika?

 

Alhidaaya.com

 

 

 

 

Anasema Allaah  (Subhaanahu wa Ta’aalaa):

 

وَلَقَدْ ذَرَأْنَا لِجَهَنَّمَ كَثِيرًا مِّنَ الْجِنِّ وَالْإِنسِ ۖ لَهُمْ قُلُوبٌ لَّا يَفْقَهُونَ بِهَا وَلَهُمْ أَعْيُنٌ لَّا يُبْصِرُونَ بِهَا وَلَهُمْ آذَانٌ لَّا يَسْمَعُونَ بِهَا ۚ أُولَـٰئِكَ كَالْأَنْعَامِ بَلْ هُمْ أَضَلُّ ۚ أُولَـٰئِكَ هُمُ الْغَافِلُونَ ﴿١٧٩﴾

“Kwa yakini Tumeumba Jahannam kwa ajili ya wengi katika majini na wana Aadam. Wana nyoyo, lakini hawafahamu kwazo. Na wana macho, lakini hawaoni kwayo. Na wana masikio, lakini hawasikii kwayo. Hao ni kama wanyama, bali wao ni wapotovu Zaidi. Hao ndio walioghafilika.” [Al-A'araaf: 179]

 

Ni onyo la kutisha kwa walioghafilika kumdhukuru Allaah (‘Azza wa Jalla) na onyo pia kwa  wale ambao hawana khofu ya adhabu ya moto Siku ya Qiyaamah.  Ni watu  ambao wameshughulishwa katika starehe za dunia wakaathirika nayo na wakaiuza Aakhirah yao  kwa dunia.  

 

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Ametaja katika Aayah hiyo tukufu, kuwa Jahannam itajaa watu na majini ambao Amewafananisha kama wanyama, bali Amewaona kuwa wao ni wapotofu zaidi kuliko wanyama kwani wanyama angalau wanajua yepi ya kuwafaa na yepi  ya kuwadhuru kisha hujiepusha nayo.

 

Ee ndugu Muislamu unayelala huku Swalaah za fardhi zikakupita au ukazichelewesha Swalaah zako bila ya sababu, mpaka lini utakuwa katika kughafilika?  Je, hushtuki au huingiwi na khofu kutokana na  maneno ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Asemayo:

 

فَوَيْلٌ لِّلْمُصَلِّينَ ﴿٤﴾ الَّذِينَ هُمْ عَن صَلَاتِهِمْ سَاهُونَ ﴿٥﴾
 

“Basi Ole kwa wanaoswali. Ambao wanapuuza Swalaah zao” [Al-Maa’uwn: 4-5]

 

 

Ndugu Muislamu uliyetega sikio lako kwa kusikiliza nyimbo, na kushughulishwa na mambo yaliyo ya upuuzi na mambo yenye kukuchumia dhambi kama ghiybah, umbea na kadhalika mpaka lini utakuwa katika kughafilika? 

 

 

Ndugu Muislamu unayetazama mambo yaliyoharamishwa mpaka lini utakuwa katika kughafilika?  

 

Ndugu Muislamu unayeyasoma haya na ukatambua mabaya yako na tukatambua sisi mabaya yetu, tujiulize sote mpaka lini tutakuwa katika kughafilika? 

 

 

Tuamke na kujikurubisha kwa Allaah (‘Azza wa Jalla) ili kuepukana na maradhi haya ya kughafilika kabla haijafika Siku ya majuto, siku ambayo kila mtu atatamani irudi nyuma ili apate kujirekebisha lakini haitowezekana! 

 

 

 

 

Share