Mwanaume Kamuingilia Kwa Nguvu Hadi Ametokwa Damu, Je, Amevunja Bikra?

SWALI:

 

Assalam alaikoum!

Mimi nina rafiki yangu ambaye jina lake nalihifadhi. Alikua na mchumba wake na walimaliza siku kadhaa wakiwa pamoja lakini bila kufanya kitendo cha kujamihiyana. Lakini siku moja mchumba wake huyo alimkamata kwa nvuvu na kumbikiri (alitokwa damu lakini kijana huyo hakumuingilia kama wanavyo fanya mapenzi wengine). Yeye anaamini kama alibikiriwa kwa vile alitokwa na damu, lakini hakuingizwa chochote ndani ya utupu wake. Na tangu siku hiyo hadi sasa, hakurudi tena kufanya kitendo hicho. Ni muda wa mwaka mmoja sasa. Sasa kila mara anajiuliza, je! Akimpata mume mwengine atamkuta bikra? Mimi nimesha olewa, na niliolewa nikiwa bado bikra. Naomba mnijibu swali hilo tafadhalini! Assalam alaikoum!


 

JIBU:

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Shukrani zetu za dhati kwa swali lako kuhusu uchumba ya wapendanao. Mara nyingi nyingi matatizo yanatufikia kwa sababu ya kuyachuma kwa mikono yetu miwili kama Alivyosema Aliyetukuka:

 

Na misiba inayokusibuni ni kwa sababu ya vitendo vya mikono yenu. Naye Anasamehe mengi” (42: 30).

 

Matatizo haya na majuto baadaye yanatufikia kwa sababu ya kuacha mafunzo ya Dini na maadili yake. Uislamu umetukataza kabisa kuwa na urafiki baina ya mvulana na msichana ambao wanaweza kuoana. Lakini kwa kutosikia kwetu hayo tunafikiwa na majanga na tunajuta lakini majuto hayo hayafalii chochote. Huwa wakati huo maji yashamwagika na inakuwa ni vigumu kuyazoa na hayawezi tena kutumiwa. Mara nyingi wasichana kwa udhaifu wao mkubwa huwa wanadanganywa na wavulana kuwa hawatofanya chochote na akadanganywa kuwa ataolewa naye n.k.. lakini baada ya muda inafikia kupigwa teke na kuachwa baada ya kubikiriwa.

 

Huwa tunapambiwa na Shaytwaan kuwa sisi hatutafanya lolote. Je, nyinyi ni Malaika? Jawabu linakuja ni la. Na ndio Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akasisitizia sana mwanamke na mwanamme wasikae pake yao kwani wakifanya hivyo watatu wao ni Shaytwaan. Na tunajua Shaytwaan hawi mahali popote isipokuwa kunapatikana maangamivu na hasara kubwa.

 

Kutokwa na damu si lazima awe amebikiriwa, kwani hukutuelezea kiasi cha damu ambayo huyo msichana ametoka. Huenda ikawa ni damu kutoka sehemu nyingine kwani damu ya kubikiriwa inakuwa kidogo sana sio nyingi. Kwa hiyo kitu ambacho anaweza kufanya ni kwenda kwa daktari mwanamke mwenye kuaminika akamuangalie kama ubikira umeondoka au bado upo.

 

Hiyo ndiyo nasaha ambayo twaweza kumpatia ili aweze kujijua hali yake. Hata hivyo anatakiwa ajichunge sana na arudi kwa Allaah Aliyetukuka kwa kutubia na asirudie tena kosa na huku anafanya mazuri mengi ya kujikurubisha kwa Allaah Aliyetukuka.

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

Share