Kulia Wakati Wa Kusoma Qur-aan Kunamaanisha Nini?

 

Kulia Wakati Wa Kusoma Qur-aan Kunamaanisha Nini

 

Alhidaaya.com

 

SWALI:

 

Ningependa kuuliza swali kuhusu quran,unaposoma na ukawa unalia je nini?maana yake ni nini?

 

 

 

JIBU:  

 

AlhamduliLLaah Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na Salaam zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Unaposoma Qur-aan ukalia, bila shaka ni nyongeza ya iymaan katika moyo wa msomaji, kwani hayo ni maneno ya Allaah ('Azza wa Jalla), maneno ambayo nafsi zilimtambua kabla ya kuumbwa duniani na kumuitikia kuwa zitamtii. Dalili ya kuwa ni iymaani ni kutoka katika Qur-aan na Sunnah.

 

Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

إِنَّمَا الْمُؤْمِنُونَ الَّذِينَ إِذَا ذُكِرَ اللَّـهُ وَجِلَتْ قُلُوبُهُمْ وَإِذَا تُلِيَتْ عَلَيْهِمْ آيَاتُهُ زَادَتْهُمْ إِيمَانًا وَعَلَىٰ رَبِّهِمْ يَتَوَكَّلُونَ﴿٢﴾

Hakika Waumini ni wale ambao Anapotajwa Allaah, nyoyo zao zinajaa khofu na wanaposomewa Aayaat Zake huwazidishia iymaan, na kwa Rabb wao wanatawakali.  [Al-Anfaal:4] 

 

 

Vile vile Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

وَإِذَا مَا أُنزِلَتْ سُورَةٌ فَمِنْهُم مَّن يَقُولُ أَيُّكُمْ زَادَتْهُ هَـٰذِهِ إِيمَانًا ۚ فَأَمَّا الَّذِينَ آمَنُوا فَزَادَتْهُمْ إِيمَانًا وَهُمْ يَسْتَبْشِرُونَ﴿١٢٤﴾

Na inapoteremshwa Suwrah, basi miongoni mwao wako wanaosema: Nani kati yenu imemzidishia (Suwrah) hii iymaan? Ama wale walioamini huwazidishia iymaan nao wanafurahia. [At-Tawbah:124]

 

Anasema pia Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)      kwamba kuzidishiwa Iymaan hiyo ni Hidaaya kutoka Kwake.

 

اللَّـهُ نَزَّلَ أَحْسَنَ الْحَدِيثِ كِتَابًا مُّتَشَابِهًا مَّثَانِيَ تَقْشَعِرُّ مِنْهُ جُلُودُ الَّذِينَ يَخْشَوْنَ رَبَّهُمْ ثُمَّ تَلِينُ جُلُودُهُمْ وَقُلُوبُهُمْ إِلَىٰ ذِكْرِ اللَّـهِ ۚ ذَٰلِكَ هُدَى اللَّـهِ يَهْدِي بِهِ مَن يَشَاءُ ۚ وَمَن يُضْلِلِ اللَّـهُ فَمَا لَهُ مِنْ هَادٍ ﴿٢٣﴾

Allaah Ameteremsha kauli nzuri kabisa, Kitabu; zinazoshabihiana ibara zake, zenye kukaririwa kila mara, zinasisimua kwazo ngozi za wale wanaomkhofu Rabb wao, kisha zinalainisha ngozi zao na nyoyo zao katika kumdhukuru Allaah. Huo ndio mwongozo wa Allaah Humwongoza kwao Amtakaye. Na ambaye Allaah Amempotoa basi hana wa kumuongoa.    [Az-Zumar: 23] 

 

 

Kama tunavyoona katika Aayah hiyo tukufu, kwamba kusoma Qur-aan husisimua ngozi na kutia khofu nyoyo na kuulainisha hadi imsababishe mja kutokwa machozi.  Na aghalabu humtokea mja mwema khaswa mwenye elimu ya Qur-aan anapofahamu na kutadabari (kuzingatia).

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Amewasifia waja hao wanaotokwa machozi pindi wanaposoma au kusikiliza Aayah Zake, huzidishiwa iymaan, khofu, unyenyekevu na hulia na huporomoka kuliakumsujudia Allaah :

 

قُلْ آمِنُوا بِهِ أَوْ لَا تُؤْمِنُوا ۚ إِنَّ الَّذِينَ أُوتُوا الْعِلْمَ مِن قَبْلِهِ إِذَا يُتْلَىٰ عَلَيْهِمْ يَخِرُّونَ لِلْأَذْقَانِ سُجَّدًا ﴿١٠٧﴾

Sema: Iaminini au msiamini. Hakika wale waliopewa elimu kabla yake wanaposomewa (Qur-aan) wanaporomoka kifudifudi wanasujudu.

 

وَيَقُولُونَ سُبْحَانَ رَبِّنَا إِن كَانَ وَعْدُ رَبِّنَا لَمَفْعُولًا ﴿١٠٨﴾

Na wanasema: Utakasifu ni wa Rabb wetu; hakika ahadi ya Rabb wetu lazima itimizwe.

 

وَيَخِرُّونَ لِلْأَذْقَانِ يَبْكُونَ وَيَزِيدُهُمْ خُشُوعًا ۩﴿١٠٩﴾

Na wanaporomoka kifudifudi huku wanalia na inawazidishia unyenyekevu. [Al-Israa: 107-109]

 

Ndio maana vile vile Anatuambia  Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)    inaposomwa Qur-aan tuwe tunaisikiliza ili tuifahamu na tupate Rahma Yake:

 

وَإِذَا قُرِئَ الْقُرْآنُ فَاسْتَمِعُوا لَهُ وَأَنصِتُوا لَعَلَّكُمْ تُرْحَمُونَ ﴿٢٠٤﴾

Na inaposomwa Qur-aan, basi isikilizeni kwa makini na bakieni kimya (mzingatie) ili mpate kurehemewa.    [Al-A'raaf:204]

 

Na Na Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alipomuomba Swahaba 'Abdullaah bin Mas'uwd (Radhwiya-Allaahu ‘anhu) amsomee Qur-aan, akamsomea hadi alipofika Aayah fulani, Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akatokwa na machozi:

 

 

 عن عبد الله بن مسعود رضي الله عنه  قال: قال لي النبي صلى الله عليه وسلم ((اقرأ علي)) قلت: يا رسول الله، أقرأ عليك وعليك أُنزلَ؟ قال: ((نعم، إني أحب أن أسمعه من غيري)) فقرأت سورة النساء، حتى أتيت إلى هذه الآية: (( فَكَيْفَ إِذَا جِئْنَا مِنْ كُلِّ أُمَّةٍ بِشَهِيدٍ وَجِئْنَا بِكَ عَلَى هَؤُلاءِ شَهِيدًا )) قال: ((حسبك الآن)) فإذا عيناه تَذْرِفَان.

Amesimulia ‘Abdullaah bin Mas‘uwd (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ): Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمَ) aliniambia: “Nisomee!”. Nikamwambia: Ee Rasuli wa Allaah! Nikusomee na hali (Qur-aan) imeteremshwa kwako? Akasema: “Naam! Lakini mimi napenda kusikia wengine wakiisoma.” Nikasoma Suwratun-Nisaa mpaka nilipofikia Aayah:

 

فَكَيْفَ إِذَا جِئْنَا مِن كُلِّ أُمَّةٍ بِشَهِيدٍ وَجِئْنَا بِكَ عَلَىٰ هَـٰؤُلَاءِ شَهِيدًا ﴿٤١﴾

“Basi itakuwaje Tutakapoleta kutoka kila ummah shahidi, na Tukakuleta (ee Muhammad صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمَ) kuwa shahidi juu ya hawa?”

 

Akasema: “Hasbuka! (Inatosha, simama hapo).” Nikaona machozi yamejaa machoni mwake. [Al-Bukhaariy]

 

 

Muumini anapolia pindi anaposoma   Qur-aan akiwa peke yake na akatokwa na machozi, pia ni bishara ya kwamba yeye atakuwa miongoni mwa watu saba waliotajwa kuwa watakuwa katika kivuli cha Allaah   Siku ya Qiyaamah, siku ambayo hakutakuweko kivuli ila kivuli cha Allaah kama  alivyosema Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam):

 

 عَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ عَنْ النَّبِيِّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ قَالَ   ((سَبْعَةٌ يُظِلُّهُمْ اللَّهُ فِي ظِلِّهِ يَوْمَ لا ظِلَّ إِلا ظِلُّهُ: الإِمَامُ الْعَادِلُ، وَشَابٌّ نَشَأ فِي عِبَادَةِ رَبِّهِ، وَرَجُلٌ قَلْبُهُ مُعَلَّقٌ فِي الْمَسَاجِدِ، وَرَجُلَانِ تَحَابَّا فِي اللَّهِ اجْتَمَعَا عَلَيْهِ وَتَفَرَّقَا عَلَيْهِ، وَرَجُلٌ طَلَبَتْهُ امْرَأَةٌ ذَاتُ مَنْصِبٍ وَجَمَالٍ فَقَالَ إِنِّي أَخَافُ اللَّهَ، وَرَجُلٌ تَصَدَّقَ بِصَدَقَةٍ فَأَخْفَاهَا حَتَّى لا تَعْلَمَ شِمَالُهُ مَا تُنْفِقُ يَمِينُهُ، وَرَجُلٌ ذَكَرَ اللَّهَ خَالِيًا فَفَاضَتْ عَيْنَاهُ)) متفق عليه

Imepokelewa kutoka kwa Abuu Hurayrah (رضي الله عنه)  kwamba Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم) amesema: ((Watu saba Allaah  Atawafunika katika kivuli Chake, Siku ambayo hakutokuwa na kivuli ila kivuli Chake: Imaam muadilifu, kijana ambaye amekulia katika ‘Ibaadah ya Rabb wake, Mtu ambaye moyo wake umeambatana na Misikiti, watu wawili wanaopendana kwa ajili ya Allaah; wanakutana kwa ajili Yake na wanafarikiana kwa ajili Yake, mwanamme aliyetakwa na mwanamke mwenye hadhi na mrembo wa kuvutia akasema: "Mimi namkhofu Allaah!" Mtu aliyetoa Swadaqah yake akaificha hadi kwamba mkono wake wa kushoto usijue nini ulichotoa mkono wake wa kulia, na mtu aliyemdhukuru Allaah kwa siri macho yake yakatokwa machozi)) [Al-Bukhaariy, Muslim]

 

Kwa hivyo ndugu yetu tunakupa bishara njema na tunakuombea Allaah Akuzidishie iymaan na taqwa. 

 

Na Allah Anajua zaidi

 

 

Share