Skip navigation.
Home kabah

Vipi Kutupa Karatasi Zenye Aayah Za Qur-aan?

SWALI:

assalam aleykum. natanguliza shukrani zangu kwenu na inshAllaah Allaah akulipeni ujira kwa kujitolea kwenu.amma baad, napenda kuuliza...mimi nilipewa kalenda ya sala ya mwaka mzima  na ndani yake ina aya za qur an na majina ya Allaah ,na sasa kalenda hii imemaliza  nataka kwenda kuchukua mpya..suali..je hii ya zamani natakiwa niihifadhi kila ninapokwenda  au naruhusika kuitupa na kama naruhusika basi naomba nifafanulie ni kwa namna gani?shukran..samahani kama sikufahamika maana kidogo nina matatizo ya ufasaha wa lugha.. wabillahi ttawfik.

 




 

JIBU:

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

Bila samahani umefahamika vyema bila ya utata wowote.

Shukrani kwa swali lako hili kuhusu mas-ala ya Aayah za Qur-aan. Inafahamika vyema kuwa Qur-aan ni Kitabu kitukufu chetu na Aayah zake ni Maneno ya Allaah Aliyetukuka na Mwenye Shani.

 

Kitabu hiki ambacho hakina shaka ndani yake, uongofu wa wamchao Allaah Aliyetukuka kinafaa kitukuzwe kwa kusomwa, kuhifadhiwa na kufuatwa maagizo yaliyomo ndani yake. Hivyo, Aayah hizo zikiwa kwenye kalenda, fremu, picha, ukuta ni lazima ziwe ni zenye kupatiwa heshima inayostahili. Ifahamike kuwa Qur-aan haikuteremshwa ili kutiwa katika kalenda bali inatakiwa itiwe ndani ya vifua vya wanaadamu na kusomeshwa kama inavyotakiwa.

 

Zikiwa Aayah hizo tayari zipo katika kalenda ambayo umepatiwa na muda wake umeisha inafaa uzihifadhi sehemu ambayo ni nzuri au uzichome kurasa za kalenda hiyo ili zisiwe ni zenye kukanyangwa, kuchezewa au kutupwa ovyo bila ya kuwekewa heshima inavyopaswa.

 

 Kwa wale ndugu zetu wanaoishi nchi za Kimagharibi ambako kuna nidhamu ya urejelezaji (recylcing) ya karatasi n.k, wanaweza kuziweka karatasi hizo zenye Aayah za Qur-aan au jina la Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) humo. Kwa kuzipa heshima zaidi, ni bora kuziweka katika mfuko wa karatasi pekee kuliko kuzichanganya na makaratasi mengineyo na waziweke juu ya hizo zote nyingine.

 

Natumai pia jibu letu kwako litakuwa limefahamika vizuri.

 Na Allaah Anajua zaidi