Skip navigation.
Home kabah

Nini Hukmu Ya Wudhuu Wangu Ikiwa Natokwa Na Pumzi Kila Mara?

SWALI:

Asalam Aleikum

Mimi ninatatizo la kutokwa na pumzi   kila mara.  Wakati wa sala inanibidi niache sala nikatawadhe upya maana ukijamba udhu umetenguka hali hii inanichukua zaidi ya mara nne mpaka tano kukata sala na kwenda kutawadha upya. Nimekwenda hospitali tatizo wameniambia nina gesi ya tumbo. Dawa nimeshatumia sana sana lakini nafuu sikupata. Naomba unipe ushauri nifanyeje hali hii.  Kuna jambo lolote ambalo ninaweza kulitanguliza ili hata nikitoa pumzi niendelee na sala na hiyo sala itakubalika?

WABILAHI TAUFIQ

 

 



JIBU:

Sifa zote njema anastahiki Allah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Salah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allahu 'Alayhi Wa Aalihi Wasallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu 'Anhum)  na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho

Shukrani kwa swali lako zuri kuhusu mas-ala ya udhu na Swalah. Hili ni jambo ambalo linaonekana kuwa dogo lakini ni kubwa kwa sababu ya umuhimu wake kama nguzo ya msingi ya Uislamu. Kutokubaliwa Swalah zetu ni kumaanisha ya kwamba tumekhasirika sana hapa duniani na Kesho Akhera.

Hili swali linaonyesha muamko wa kidini ambao upo katika ulimwengu hasa kwa vijana mbali na mitihani na vikwazo chungu nzima. Inafahamika kuwa hapana udhuru kwa Swalah kwani tunatakiwa tuswali katika hali zote isipokuwa kwa wanawake wakiwa katika hedhi au nifasi. Na wengine ambao hawachukuliwi ni wenda wazimu na watoto wadogo (japokuwa wanatakiwa wafundishwe).

Allah (Subhaanahu wa Ta'ala) Ametusahilishia mambo mengi na hasa katika mas-ala ya Swalah. Muislamu anatakiwa aswali kwa kusimama, lakini ikiwa hawezi basi kwa kukaa, kwa kulala na hata kwa ishara. Hii yote ni kuonyesha cheo, daraja na umuhimu wa Swalah katika Uislamu. Kwa kuwa Allah (Subhaanahu wa Ta'ala) hataki kututia katika uzito Anatuelezea: “Mwenyezi Mungu anakutakieni yaliyo mepesi wala hakutakieni yaliyo mazito” (2: 187).

Na tena, “Mwenyezi Mungu haikalifishi nafsi yoyote ila kwa kadiri ya iwezavyo” (2: 286).

Na pia, “Wala hakuweka juu yenu mambo mazito katika Dini. Nayo ni mila ya baba yenu Ibrahim” (22: 78).

Katika matatizo wapo wale wanawake wenye kutokwa na damu isiyo ya kawaida na kupita mipaka (inayojulikana kama Istihaadhwah), au wale wasioweza kuzuia mikojo. Hawa huwa wanatakiwa watawadhe kwa kila Swalah na wafunge kitu ambacho kitazuilia damu au mikojo kuingia katika nguo. Baada ya kutawadha kabla kidogo ya kuswaliwa na kuingia katika Swalah damu au mkojo unaotoka hauathiri chochote Swalah yenyewe. Na Swalah inakuwa sahihi. Tatizo lako ni kama la hao, hivyo unatakiwa nawe utawadhe tu kabla ya Swalah na kisha uingie katika Swalah. Wakati huo ukitokwa na gesi utaendelea na Swalah pia kuirudia tena. Ikiwa kuna kitu ambacho kinaweza kuwekwa katika sehemu yako ya siri ili sauti isitoke ya nguvu au harufu itakuwa bora zaidi ikiwa haiwezekani basi utaswali hivyo hivyo.

Nasaha yetu kwako ni kuwa usivunjike moyo na uwe na hakika kuwa utapona, kwani Mtume (Swalla Llaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema, “Allah (Subhaanahu wa Ta'ala) Hakuleta maradhi yoyote isipokuwa Ameweka na dawa yake”. Muombe Allah (Subhaanahu wa Ta'ala) katika dua na ‘Ibadah zako nyenginezo (katika Swalah na unapofunga) na kwa idhini ya Allah utapona.

Jaribu sana usile vyakula vya hamidhi (vikali) na utumie vitu ambavyo ni tiba kwa magonjwa tofauti kama Habbatus Sawdaa na asali. Habbatus Sawdaa inaweza kutiwa katika chai, supu na vinywaji vyengine na inasaidia sana katika magonjwa tofauti, kwani Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema kuwa Habbatus Sawdaa ni dawa ya kila ugonjwa isipokuwa mauti.

Tunamuomba Allah (Subhaanahu wa Ta'ala) Akupatie shifaa ya haraka na Atuweke sote katika siha na afya nzuri.

Na Allah Anajua zaidi