Nini Hukmu Ya Wudhuu Wangu Ikiwa Natokwa Na Pumzi Kila Mara?

Nini Hukmu Ya Wudhuu Wangu Ikiwa Natokwa Na Pumzi Kila Mara?

 

Alhidaaya.com

 

 

 

SWALI:

 

Asalam Aleikum

Mimi ninatatizo la kutokwa na pumzi   kila mara.  Wakati wa sala inanibidi niache sala nikatawadhe upya maana ukijamba udhu umetenguka hali hii inanichukua zaidi ya mara nne mpaka tano kukata sala na kwenda kutawadha upya. Nimekwenda hospitali tatizo wameniambia nina gesi ya tumbo. Dawa nimeshatumia sana sana lakini nafuu sikupata. Naomba unipe ushauri nifanyeje hali hii.  Kuna jambo lolote ambalo ninaweza kulitanguliza ili hata nikitoa pumzi niendelee na sala na hiyo sala itakubalika?

 

WabiLlahi taufiq 

 

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Rabb wa walimwengu, Swalaah na Salaam zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

 

Hili ni jambo ambalo linaonekana kuwa dogo lakini ni kubwa kwa sababu ya umuhimu wake kama nguzo ya msingi ya Uislaam. Kutokubaliwa Swalaah zetu ni kumaanisha ya kwamba tumekhasirika sana hapa duniani na kesho Aakhirah.

 

Hili swali linaonyesha muamko wa kidini ambao upo katika ulimwengu hasa kwa vijana mbali na mitihani na vikwazo chungu nzima. Inafahamika kuwa hapana udhuru kwa Swalaah kwani tunatakiwa tuswali katika hali zote isipokuwa kwa wanawake wakiwa katika hedhi au nifasi. Na wengine ambao hawachukuliwi ni wenda wazimu na watoto wadogo (japokuwa wanatakiwa wafundishwe).

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)  Ametusahilishia mambo mengi na hasa katika mas-ala ya Swalaah. Muislaam anatakiwa aswali kwa kusimama, lakini ikiwa hawezi basi kwa kukaa, kwa kulala na hata kwa ishara. Hii yote ni kuonyesha cheo, daraja na umuhimu wa Swalaah katika Uislaam. Kwa kuwa Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) hataki kututia katika uzito Anatuelezea:

 

يُرِيدُ اللّهُ بِكُمُ الْيُسْرَ وَلاَ يُرِيدُ بِكُمُ الْعُسْرَ

Allaah Anakutakieni yaliyo mepesi wala hakutakieni yaliyo mazito [Al-Baqarah: 285]

 

 

Na Anasema pia Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

لَا يُكَلِّفُ اللَّـهُ نَفْسًا إِلَّا وُسْعَهَا ۚ    

Allaah Hakalifishi nafsi yoyote ila kwa kadiri ya uwezo wake.  [Al-Baqarah: 286]

 

 

Na pia,

 

وَمَا جَعَلَ عَلَيْكُمْ فِي الدِّينِ مِنْ حَرَجٍ ۚ مِّلَّةَ أَبِيكُمْ إِبْرَاهِيمَ ۚ  

Na Hakukufanyieni ugumu wowote ule katika Dini. Mila ya baba yenu Ibraahiym .[Al-Hajj: 78]

 

Katika matatizo wapo wale wanawake wenye kutokwa na damu isiyo ya kawaida na kupita mipaka (inayojulikana kama Istihaadhwah), au wale wasioweza kuzuia mikojo. Hawa huwa wanatakiwa watawadhe kwa kila Swalaah na wafunge (Swawm) kitu ambacho kitazuilia damu au mikojo kuingia katika nguo. Baada ya kutawadha kabla kidogo ya kuswaliwa na kuingia katika Swalaah damu au mkojo unaotoka hauathiri chochote Swalaah yenyewe. Na Swalaah inakuwa sahihi.

 

Bonyeza kiungo kifuatacho upate maelezo na faida tele kuhusu Twahara.

 

Swahiyh Fiqh As-Sunnah: Mlango Wa Twaharaah

 

Tatizo lako ni kama la hao, hivyo unatakiwa nawe utawadhe tu kabla ya Swalaah na kisha uingie katika Swalaah. Wakati huo ukitokwa na gesi utaendelea na Swalaah pia kuirudia tena. Ikiwa kuna kitu ambacho kinaweza kuwekwa katika sehemu yako ya siri ili sauti isitoke ya nguvu au harufu itakuwa bora zaidi ikiwa haiwezekani basi utaswali hivyo hivyo.

 

Nasaha yetu kwako ni kuwa usivunjike moyo na uwe na hakika kuwa utapona, kwani Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema katika Hadiyth:

 

عَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ رضى الله عنه عَنِ النَّبِيِّ صلى الله عليه وسلم قَالَ: ((مَا أَنْزَلَ اللَّهُ دَاءً إِلاَّ أَنْزَلَ لَهُ شِفَاءً)) رواه البخاري   

Imepokelewa kutoka kwa Abuu Hurayrah (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Allaah Hakuteremsha maradhi isipokuwa Ameyateremshia shifaa)) [Al-Bukhaariy]

 

Basi muombe Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) katika du'aa na ‘Ibaadah zako nyenginezo (katika Swalaah na unapofunga) na kwa idhini ya Allaah utapona.

 

Jaribu sana usile vyakula vya hamidhi (vikali) na utumie vitu ambavyo ni tiba kwa magonjwa tofauti kama Habbat Sawdaa na asali. Habbat Sawdaa inaweza kutiwa katika chai, supu na vinywaji vyengine na inasaidia sana katika magonjwa tofauti, kwani Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema katika Hadiyth:

 

عَنْ عَائِشَةَ (رضي الله عنها) أَنَّهَا سَمِعَتْ النَّبِيَّ (صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ) يَقُولُ: ((إِنَّ هَذِهِ الْحَبَّةَ السَّوْدَاءَ شِفَاءٌ مِنْ كُلِّ دَاءٍ إلاَّ مِنْ السَّام))ِ قُلْتُ وَمَا السَّامُ؟  قَالَ: ((الْمَوْتُ))

Kutoka kwa ‘Aaishah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) kwamba amemsikia Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akisema: ((Hakika Habbat Sawdaa hii ni shifaa kwa kila maradhi isipokuwa sumu)) Nikasema: Nini sumu? Akasema: ((Mauti)) [Al-Bukhaariy, Muslim, Ibn Maajah, Ahmad]

 

 

Tunamuomba Allaah ('Azza wa Jalla) Akupatie shifaa ya haraka na Atuweke sote katika siha na afya nzuri.

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

Share