Rajab: Swawm Katika Mwezi Wa Rajab Ipi Ni Sunnah; Kufunga Mwezi Mzima Au Siku Maalumu?

 

Swawm Katika Mwezi Wa Rajab Ipi Ni Sunnah; Kufunga Mwezi Mzima Au Siku Maalumu?

 

Alhidaaya.com

 

 

 

 

 

SWALI:

 

Kwajina la Allah mwingi wa rehema, napenda kuuliza maswali yangu ambayo kidogo yananitatiza.  Jee kuna suna ya kufunga swaumu katika mwezi wa Rajabu?

 

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salaam zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.  

 

Kwanza kabisa tujue kuwa mwezi wa Rajab hakika ni katika miezi mitukufu minne Aliyotuwekea Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kama Anavyosema: 

 

إِنَّ عِدَّةَ الشُّهُورِ عِندَ اللَّـهِ اثْنَا عَشَرَ شَهْرًا فِي كِتَابِ اللَّـهِ يَوْمَ خَلَقَ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ مِنْهَا أَرْبَعَةٌ حُرُمٌ ۚ ذَٰلِكَ الدِّينُ الْقَيِّمُ ۚ فَلَا تَظْلِمُوا فِيهِنَّ أَنفُسَكُمْ ۚ وَقَاتِلُوا الْمُشْرِكِينَ كَافَّةً كَمَا يُقَاتِلُونَكُمْ كَافَّةً ۚ وَاعْلَمُوا أَنَّ اللَّـهَ مَعَ الْمُتَّقِينَ﴿٣٦﴾

Hakika idadi ya miezi mbele ya Allaah ni kumi na mbili katika hukmu ya makadirio ya Allaah, (tangu) siku Aliyoumba mbingu na ardhi. Kati ya hiyo iko minne mitukufu. Hivyo ndiyo Dini iliyo nyoofu. Basi msijidhulumu humo nafsi zenu, na piganeni vita na washirikina wote kama wao wanavyokupigeni vita nyote. Na jueni kwamba Allaah Yu Pamoja na wenye taqwa.   [At-Tawbah: 36]

 

 

Na katika Hadiyth Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) imethibitisha kuwa miongoni mwa miezi minne hiyo ni mwezi wa Rajab:

  

 

عَنْ أَبِي بَكْرَةَ، أَنَّ النَّبِيَّ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ خَطَبَ فِي حَجَّة الْوداع فَقَالَ: ((إِنَّ الزَّمَانَ قَدِ اسْتَدَارَ كَهَيْئَتِهِ يَوْمَ خَلَقَ اللَّهُ السَّمَوَاتِ وَالْأَرْضَ، السَّنَةُ اثْنَا عَشَرَ شَهْرًا، مِنْهَا أَرْبَعَةٌ حُرُمٌ، ثَلَاثٌ مُتَوَالِيَاتٌ: ذُو الْقِعْدَةِ، وَذُو الْحِجَّةِ، وَالْمُحَرَّمُ، وَرَجَبُ مُضَرَ الَّذِي بَيْنَ جُمَادَى وَشَعْبَانَ))   رواه البخاري

Kutoka kwa Abuu Bakrah (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alitoa Khutbah katika Hajj ya mwisho akasema: "Wakati umemaliza mzunguko wake kama vile siku Allaah Alipoumba mbingu na ardhi. Mwaka ni miezi kumi na mbili, ambayo ndani yake kuna minne ni mitukufu, mitatu inafuatana, Dhul-Qa’dah, Dhul-Hijjah na Muharram na Rajab upo baina ya Jumaadah na Sha'baan)) [Al-Bukhaariy] 

 

Miezi mitukufu hiyo inapaswa kuadhimiwa kwa kutenda mema na kujiepusha na maasi kutokana na amri za Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) na Rasuli Wake (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam).  Lakini katika kutenda mema, hakuna dalili kwamba tunatakiwa tufunge siku maalumu au mwezi mzima, kwa sababu hakuna aliyefunga Swawm makhsusi kwa ajili ya mwezi huu; si Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) wala Maswahaba zake (Radhwiya Allaahu ‘anhum) wala Salaf wengineo. Na hakuna kabisa dalili kwamba  kuna Swawm siku ya Israa wal-Mi'iraaj. Bali hata siku hiyo, hakuna uthibitisho wa uhakika kwamba siku hii ni tarehe 27 kama wanavyodhania baadhi ya watu.   

 

Tafadhali bonyeza viungo vifuatavyo upate faida ziyada:

 

Mwezi Wa Rajab: Fadhila Zake Na Yaliyozuliwa Ndani Yake

'Amali Za Kutenda Na Mambo Ya Kujiepusha Nayo Katika Miezi Mitukufu

Imaam Ibn Baaz-Kuhusisha Mwezi Wa Rajab Kwa ‘Ibaadah

Uzushi Wa Kuomba Maghfirah Katika Mwezi Wa Rajab

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

 

Share