Fadhila Za Swawm

 

Fadhila Za Swawm

 

Ummu Faraj

 

Alhidaaya.com

 

 

Sifa njema zote Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Rabb wa viumbe wote mwingi wa rehma na mwingi wa kusamehe na rehma na amani zimfikie kipenzi chake Allaah Nabiy wetu Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) Jamaa na Swahaba wake wote.

 

Amma Baa’d:

 

 

Ndugu yangu Muislam ama kwa hakika umetufikia mwezi ulio mtukufu na wenye fadhila kubwa na mavuno kwa wenye mazingatio kwa hayo, nao ni mwezi wa Ramadhwaan ambao Allaah Ameufaradhisha kwa Waislam kwa kauli yake Jalla wa ‘Alaa Aliposema:

 

 يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا كُتِبَ عَلَيْكُمُ الصِّيَامُ كَمَا كُتِبَ عَلَى الَّذِينَ مِن قَبْلِكُمْ لَعَلَّكُمْ تَتَّقُونَ ﴿١٨٣﴾

Enyi walioamini! Mmefaridhishwa Swiyaam kama ilivyofaridhishwa kwa walio kabla yenu mpate kuwa na taqwa. [Al-Baqarah: 183]

 

Na hili la kumcha Allaah ndio lengo kubwa la ibada hii ya funga kwani ni ibada ya siri baina yako na Rabb wako. Na wengi wanaliona gumu jambo hili la kufunga wakati lina fadhila kubwa kabisa wengi wanapitwa na fadhila za kufunga kwa kupenda kula na kunywa. Majuto yatawajia pale watakapokutana na Rabb wao hali hawana kitu.

 

Na ni siku maalum, siku chache katika mwaka mzima zilizowekwa watu hawamuonei hayaa Allaah kwa kula mchana bila ya udhuru wowote wa kisheria. Allaah Anatwambia katika kitabu Chake kitukufu: 

 

أَيَّامًا مَّعْدُودَاتٍ ۚ فَمَن كَانَ مِنكُم مَّرِيضًا أَوْ عَلَىٰ سَفَرٍ فَعِدَّةٌ مِّنْ أَيَّامٍ أُخَرَ ۚ 

(Swiyaam ni) Siku za kuhesabika. Lakini atakayekuwa mgonjwa miongoni mwenu, au yuko safarini, basi (inapaswa kulipa) idadi sawa katika masiku mengineyo. [Al-Baqarah: 184]

 

Ama kwa hakika tumeona umuhimu na wajibu wa kufunga. hivyo basi napenda kuchukua fursa hii adhimu kuwafahamisha ndugu zangu katika imaan fadhila za kufunga, namuomba Allaah Aniwezeshe.

 

Miongoni Mwa Fadhila Hizo ni:

 

 

1- Funga Inamuokoa Mtu Kutokana na Moto

 

Kama ilvyopokewa na imam Ahmad katika Hadiyth sahihi.

 

Kutoka kwa Jaabir (Radhwiya Allaahu ‘anhu) hakika ya Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: "Swawm ni kinga itamukoa mja kutokana na moto (siku ya Qiyaamah)." [Imepokewa na At-Twabaraaniy kutoka kwa ‘Uthmaan bin Abil ‘Aasw]

 

Na katika Hadiyth iliyopokewa na ambayo ni muttafaqun ‘alayhi, inasema:

 

Kutoka kwa Abu Sa’iyd Al Khudhriyy (Radhwiya Allaahu ‘anhu) hakika Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: "Mwenye kufunga siku kwa ajili ya Allaah Allaah Atamuokoa uso wake kutokana na moto kwa umbali wa miaka sabini".

 

Ndugu yangu Muislam ikiwa unafunga siku moja na Allaah Anakuokoa na moto wa Jahannam je, Ukifunga Ramadhwaan yote! Hakika hii ni fadhila kubwa. Na fadhila hizi zinaingia katika funga za lazima na funga za Sunnah.

 

 

2- Swawm Ni Kinga Kutokana Na Matamanio

 

Imekuja katika Hadiyth

 

Kutoka kwa Ibn Mas’uud (Radhwiya Allaahu ‘anhu) amesema Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) Enyi kundi la vijana miongoni mwenu atakae kuwa na uwezo wa kuoa basi na aoe, (kufanya hivyo) kutampelekea kuinamisha macho yake na kuhifadhi tupu yake. Ikiwa hana uwezo wa kuoa basi na afunge kwani hiyo ni kinga kwake. [Muttafaqun 'Alayhi]

 

Hakika vijana wengi wanashtakia kutokana na matamanio khasa katika zama zetu hizi za wanawake wanaotembea wazi katika masoko, waliowekwa picha zao tupu kwenye magazeti, wanajitoa katika matangazo ya televisheni, hii ndio sababu kubwa inayoleta athari ya uchafu na ufisadi mkubwa katika ardhi. Allaah Atuhifadhi! Na kwa sababu hiyo Nabiy (swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akawanasihi vijana ikiwa mtu hana uwezo wa kuoa basi na afunge.

 

 

3- Swawm Ni Njia Ya Kumpelekea Mtu Jannah

 

Kutoka kwa Abu Umamah (Radhwiya Allaahu ‘anhu) amesema kumwambia Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), “Ee Nabiy wa Allaah Niamrishe mimi jambo litakalonifaa mbele ya Allaah”. Akasema Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), “Ni juu yako kufunga kwa hakika hakuna mfano wake" [An-Nasaaiy]

 

Akabainisha kuwa hakuna kitu kitakacho mkurubisha mja kwa Allaah, na kumuweka mbali na adhabu kama kufunga.

 

Bali ametupa khabari Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) katika Jannah kuna mlango khasa wa wenye kufunga.

 

Kutoka kwa Sahal bin Sa'ad (Radhwiya Allaahu ‘anhu) hakika Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: "Hakika katika Jannah kuna mlango unaitwa Rayyaan,wataingia humo siku ya Qiyaamah wenye kufunga tu, hatoingia yeyote mwingine, utasema wako wapi wenye kufunga? Watasimama kuingia hatoingia yeyote mwingine, wakisha kuingia utafungwa, basi hatoingia mwengine" [Imepokewa na Al-Bukhaariy]

 

Na umepewa jina hilo kunasibiana na sifa ya Swawm ambayo inampata mtu kiu kutokana na athari ya kufunga. mara nyingi mtu anapofunga hatamani chakula kama anavyotamani maji.

 

 

4- Funga Itamuombea Mtu Siku Ya Qiyaamah

 

Kutoka kwa 'Abdullaah bin ‘Amru bin Al-‘Aasw (Radhwiya Allaahu ‘anhumaa) amesema Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) " Funga na Qur-aan zitamuombea mja siku ya Qiyaamah, itasema funga ee Rabb amejizuilia kutokana na chakula chake na matamanio yake wakati wa mchana, basi nnamuombea msamaha, na itasema Qur-aan amejizuilia kutokana na usingizi wake wakati wa usiku ninamuombea msamaha. Akasema wamesamehewa. [Imepokewa na Ahmad na Al-Haakim]

 

 

5- Swawm Ni Kafara Na Msamaha Kutokana Na Madhambi

 

Kwa hakika mema huondosha maovu na Swawm ni katika jambo jema sana. Na Amesema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa): 

 

 ۚ إِنَّ الْحَسَنَاتِ يُذْهِبْنَ السَّيِّئَاتِ ۚ 

"Hakika ya mema huyaondosha maovu" [Huwd: 114]

 

Na katika Hadiyth iliyopokewa na imamu sita.

 

Kutoka kwa Hudhayfah (Radhwiya Allaahu ‘anhu) amesema Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) " Fitna ya mtu kwa mke wake, mali yake na jirani yake itamfidiya kutokana na Swalah, Funga na Sadaqa"

 

Mara nyingi kunakua na upungufu ima katika haki za mkeo kwa njia ya maneno au kuudhi na upungufu mdogodogo na katika makosa ya haki za jirani iwe kwa matendo au qauli na katika kuitakasa mali, vyote hivyo hutakaswa na Swalah, funga na sadaqa. Iwapo mtu atajilazimisha na haya basi atasamehewa madhambi yake madogo.

 

Na kutoka kwa Abu Hurayrah (Radhwiya Allaahu ‘anhu) hakika Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema "mwenye kufunga Ramadhwaan kwa imani na akatarajia malipo atasamehewa madhambi yake aliyoyatanguliza"

 

Imani ni kumuamini Allaah na funga ukamkusudia Allaah Aliyetukuka na ukataraji malipo ambayo Allaah Ameyatolea ahadi kwa wenye kufunga.

 

Kwani kuna baadhi ya watu bado wanamshirikisha Allaah katika ibada zake. Wafunga, waswali kwa ajili ya majini, n.k. nayo ni makosa makubwa sana.

 

Na katika Hadiyth nyingine:

 

Kutoka kwa Abu Hurayrah (Radhwiya Allaahu ‘anhu) amesema Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam): "Swalah tano, na ijumaa mpaka ijumaa, na Ramadhwaan mpaka Ramadhwaan, zitamfidia baina yake madamu atakua ni mwenye kujiepusha na madhambi makubwa" [Imepokewa na Muslim]

 

Kufunga mwezi wa Ramadhwaan ni sababu ya kusamehewa madhambi ambayo umeyatanguliza katika kipindi cha mwaka mzima uliopita lakini basi imewekewa sharti ni kwamba ujiepushe na madhambi makubwa kwani madhambi makubwa hayafutiki mpaka ulete tawbah, na hili wamekubaliana wanavyuoni wote. Na vilevile Allaah Amesema katika Kitabu Chake kitukufu:

 

إِن تَجْتَنِبُوا كَبَائِرَ مَا تُنْهَوْنَ عَنْهُ نُكَفِّرْ عَنكُمْ سَيِّئَاتِكُمْ وَنُدْخِلْكُم مُّدْخَلًا كَرِيمًا ﴿٣١﴾

Mkijiepusha na madhambi makubwa mnayokatazwa Tutakufutieni madhambi yenu madogo na Tutakuingizeni katika mahali patukufu. [An-Nisaa: 31]

 

 

6- Swawm Ni Sababu Ya Kupata Furaha Ya Nyumba Mbili

 

Kama ilivyokuja katika hadiyth

 

Kutoka kwa Abu Hurayrah (Radhwiya Allaahu ‘anhu) amesema Nabiy (swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam): “Mwenye kufunga ana furaha mbili; furaha ya kwanza anapofungua na furaha ya pili atakapokutana na Rabb wake". [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

Amma kwa hakika katika furaha ya kwanza ni pale Allaah Alipotuhalalishia wakati wa jioni kula na kunywa kwani ni vitu ambavyo tunavipenda kwa hivyo tukamuabudu Allaah kwa kujizuilia kula, kunywa na matamanio wakati wa mchana.

Amma furaha ya pili ni pale Allaah Alipotuwafiqisha kuitimiza Swawm hadi jioni kwani mara nyingine unakuwa taabani mpaka ikifika jioni unamshukuru Allaah, ‘Alhamdulillahi nimeifikisha Swawm hadi jioni na nimeikamilisha ibada’

 

 

7- Harufu Ya Mdomo Wa Mwenye Kufunga Mbele Ya Allaah Ni Nzuri Kuliko Harufu Ya Miski

 

Harufu ya mdomo ambayo inatoka ni kutokana na kutokula chakula. Nayo ni harufu iwachukizayo watu lakini mbele ya Allaah ni yenye kupendeza:

 

Amesema Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam):  "Naapa kwa yule ambaye nafsi ya Muhammad iko mikononi Mwake; harufu ya mdomo wa mfungaji ni nzuri mbele ya Allaah kuliko harufu ya miski". [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

Share