Malaika Wanahudhuria Vikao Kwa Maumbile Ya Kibinaadam?

  

Malaika Wanahudhuria Vikao Kwa Maumbile Ya Kibinaadam?

 

Alhidaaya.com

 

SWALI:

 

Assalaam 'Alaykum Warahmatullah,

Tunaamini kweye vikao vyema malaika huwa wanatuzunguka, tunauliza jee wakati huu tulionao malaika wanaweza kuwa na sisi kwa kujitokeza kwa njia ya kiumbe kama binaadamu au vyenginevyo hata bila kuwajua kama ilivyokuwa nyakati za Rusuli (kuja kwa Jubril kufundisha dini), kwenda kwa watu wa Luutw nakadhalika??

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah - Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na Salaam zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho

 

Bila ya shaka Malaika wanatuzunguka tunapokuwa katika vikao vya madarasa ya kujifunza Dini yetu. Ama kujitokeza kwao katika hali ya ubinaadamu, hatukupata mafunzo yenye dalili kuwa huenda hali ikawa hivyo kwetu. Tuliyojifunza ni kama ulivyotaja yaliyotokea zama za Mitume na katika Siyrah ya Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) mfano mmoja ulioutaja na mwingine katika vita vya Badr walipoteremka Malaika zaidi ya elfu kupigana na makafiri na wakawaua makafiri kwa kuwakata shingo zao.

 

“Kwenye Hadiyth iliyopokewa na Al-Bayhaqiy, mama wa waumini Khadiyjah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) alimwambia Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amjulishe wakati Jibriyl (‘Alayhis-salaam) atakapomjia yeye (Nabiy). Kila Jibriyl (‘Alayhis-salaam) alipowasili, mama wa waumini Khadiyjah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) hakuweza kumuona na akawa kila mara anamuuliza Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kama keshakuja na kama  (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) anamuona , Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akawa anamuitikia kwa kukubali kuwa anamuona, kisha akamwambia Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akae karibu yake na akawa bado Nabiy  (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) anamuona Jibriyl (‘Alayhis-salaam), na kisha akamtaka Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akae kwenye mapaja yake ili kuhakikisha kuwa kama bado Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) atakuwa anamuona (maana yeye hakuwa anaweza kumuona Jibriyl), na Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akamuhakikishia kuwa bado anamuona, hata mama wa waumini Khadiyjah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) alipofunua kichwa chake wakati bado Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kakaa kwenye mapaja yake, na huku akiendelea kumuuliza Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ikiwa bado anamuona Jibriyl (‘Alayhis Salaam), hapo Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akamjibu hapana, na kusema kuwa yeye (Jibriyl) si shetani; bali ni Malaika…”

 

Kwenye Hadiyth hii tunaona kuwa mama wa waumini Khadiyjah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) hakuweza kumuona Malaika huyo, bali Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa Sallam) tu peke yake. Na pia tunapata kujua kuwa Malaika ni wenye staha kubwa na hayaa na ndio sababu ya Jibriyl (‘Alayhis-salaam) kuondoka kwa kuwa mama wa waumini alifunua kichwa chake na hivyo yeye kuona hayaa na kuondoka. Hadiyth hiyo hata hivyo, haijatujulisha alikuwa katika umbo lipi japokuwa hakuwa katika umbo la kibinaadam, kwani kama angekuwa kwenye umbo la kibinaadam, bila shaka mama wa waumini Khadiyjah (Radhwiya Allaahu ‘anha) angelimuona.

 

Pia kuna Hadiyth mbalimbali ambazo tumejua kuwa Jibriyl (‘Alayhis-salaam) alimwendea Nabiy kama mwanaadam, mfano wa Hadiyth maarufu ambayo alimwendea Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa Sallam) kumuuliza masuala ya Uislam, Iymaan na Ihsaan. Pia Hadiyth nyingine ambayo inatuonyesha alijigeuza kama mmoja wa Swahaba wa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) aitwaye Duhyah bin Khaliyfah Al-Kalbiy (Radhwiya Allaahu ‘anhu) ambaye alikuwa na sura ya kupendeza na kwenda kwenye nyumba ya Mtume na akawa anazungumza naye na mama wa waumini ‘Aaishah (Radhwiya Allaahu ‘anha) akaweza kumuona lakini hakujua kuwa ni Malaika hadi Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa Sallam) alipomjulisha hivyo.

 

Allaah (Subhaananu wa Ta’aalaa) Amewapa Malaika uwezo wa kujibadili kwa njia mbalimbali. Kama Alivyomtuma Jibriyl (‘Alayhis-salaam) kwa Maryam (‘Alayhas-salaam) akiwa katika umbile la kibinaadam kama tunavyoona katika Aayah ifuatayo: 

وَاذْكُرْ فِي الْكِتَابِ مَرْيَمَ إِذِ انتَبَذَتْ مِنْ أَهْلِهَا مَكَانًا شَرْقِيًّا ﴿١٦﴾فَاتَّخَذَتْ مِن دُونِهِمْ حِجَابًا فَأَرْسَلْنَا إِلَيْهَا رُوحَنَا فَتَمَثَّلَ لَهَا بَشَرًا سَوِيًّا ﴿١٧﴾قَالَتْ إِنِّي أَعُوذُ بِالرَّحْمَـٰنِ مِنكَ إِن كُنتَ تَقِيًّا ﴿١٨﴾قَالَ إِنَّمَا أَنَا رَسُولُ رَبِّكِ لِأَهَبَ لَكِ غُلَامًا زَكِيًّا ﴿١٩﴾ 

Na mtaje katika Kitabu Maryam alipojiondosha kutoka kwa ahli zake, mahali pa Mashariki. Akafanya pazia kujitenga nao, Tukampelekea Ruwh Wetu (Jibriyl عليه السلام) akajimithilisha kwake kama bin Aadam timamu. (Maryam) Akasema: Najikinga kwa Ar-Rahmaan dhidi yako ukiwa ni mwenye taqwa. (Jibriyl عليه السلامAkasema: Hakika mimi ni Mjumbe wa Rabb wako ili nikubashirie tunu ya ghulamu aliyetakasika. [Maryam: 16-19]

 

Na pia tunaona Malaika walivyokwenda kwa Nabiy Ibraahiym (‘Alayhas-salaam) kwa maumbile ya wanaadam, kama anavyosema Allaah katika Qur-aan:

وَلَقَدْ جَاءَتْ رُسُلُنَا إِبْرَاهِيمَ بِالْبُشْرَىٰ قَالُوا سَلَامًا ۖ قَالَ سَلَامٌ ۖ فَمَا لَبِثَ أَن جَاءَ بِعِجْلٍ حَنِيذٍ﴿٦٩﴾

Na kwa yakini walimjia Ibraahiym Wajumbe Wetu kwa bishara, wakasema: Salaam! (Naye) Akasema: Salaam.  Basi hakubakia ila alikuja na ndama aliyebanikwa. Alipoona mikono yao haifikii (chakula) aliwashangaa na ikamuingia khofu kutokana nao. Wakasema: Usiogope! Hakika Sisi Tumetumwa kwa kaumu Luutw. [Huwd: 69-70]

 

Pia tunaona kwenye Aayah nyingine kuwa Malaika walitumwa kwa Nabiy Luutw (‘Alayhis- salaam) wakiwa katika sura za binaadam wenye kuvutia sana. Anasema Allaah:

وَلَمَّا جَاءَتْ رُسُلُنَا لُوطًا سِيءَ بِهِمْ وَضَاقَ بِهِمْ ذَرْعًا وَقَالَ هَـٰذَا يَوْمٌ عَصِيبٌ﴿٧٧﴾ 

Na Wajumbe Wetu walipomjia Luutw alisononeka kwa ajili yao na akadhikika na kushindwa (la kufanya); akasema: Hii ni siku ngumu. [Huwd: 77]

 

Na ingawa katika Qur-aan wametajwa kuwa Malaika huteremka kwetu katika hali mbali mbali, lakini hatuwezi kujua wanatajuia katika umbile gani. Hapa katika Suwrah Al-Qadr, Allaah katubainishia kuwa wanashuka katika usiku Laylatul Qadr lakini Hajatujulisha maumbile yao wanayoshuka nayo: 

(تَنَزَّلُ الْمَلَائِكَةُ وَالرُّوحُ فِيهَا بِإِذْنِ رَبِّهِم مِّن كُلِّ أَمْرٍ ﴿٤﴾

Wanateremka humo Malaika na Ar-Ruwh (Jibriyl) kwa idhini ya Rabb wao kwa kila jambo. [al-Qadr: 4]

 

Mfano mwingine katika hali ya sakaraatul-mawt ya waja wema ambapo kutokana na Aayah hizi hapa chini kwamba Malaika huzungumza nao wanapowatoa roho zao, hatuwezi kujua vipi wanazungumza nao; katika maumbile ya ki Malaika au ya kibinaadamu au ya kutoonekana kabisa: 

إِنَّ الَّذِينَ قَالُوا رَبُّنَا اللَّـهُ ثُمَّ اسْتَقَامُوا تَتَنَزَّلُ عَلَيْهِمُ الْمَلَائِكَةُ أَلَّا تَخَافُوا وَلَا تَحْزَنُوا وَأَبْشِرُوا بِالْجَنَّةِ الَّتِي كُنتُمْ تُوعَدُونَ﴿٣٠﴾نَحْنُ أَوْلِيَاؤُكُمْ فِي الْحَيَاةِ الدُّنْيَا وَفِي الْآخِرَةِ ۖ وَلَكُمْ فِيهَا مَا تَشْتَهِي أَنفُسُكُمْ وَلَكُمْ فِيهَا مَا تَدَّعُونَ﴿٣١﴾نُزُلًا مِّنْ غَفُورٍ رَّحِيمٍ﴿٣٢﴾

Hakika wale waliosema: Rabb wetu ni Allaah. Kisha wakathibitika imara; Malaika huwateremkia: (kuwaambia): Msikhofu, na wala msihuzunike, na pokeeni bishara njema ya Jannah ambayo mlikuwa mkiahidiwa. Sisi ni rafiki zenu walinzi katika uhai wa dunia na katika Aakhirah. Na mtapata humo yale yanayotamani nafsi zenu, na mtapata humo yale mtakayoomba. Ni mapokezi ya takrima kutoka kwa Mwenye kughufuria, Mwenye kurehemu.

[Fusw-Swilat: 30-32]

 

Au katika hali ya sakaraatul-mawt ya watu waovu wanapowapiga nyuso na migongo yao, hatujui vipi hali ya maumbile yao huwa, na vipi wanawapiga:  

وَلَوْ تَرَىٰ إِذْ يَتَوَفَّى الَّذِينَ كَفَرُوا ۙ الْمَلَائِكَةُ يَضْرِبُونَ وُجُوهَهُمْ وَأَدْبَارَهُمْ وَذُوقُوا عَذَابَ الْحَرِيقِ﴿٥٠﴾  

Na lau ungeliona pale Malaika wanapowafisha wale waliokufuru, wanawapiga nyuso zao na migongo yao na (wanawaambia): Onjeni adhabu iunguzayo. [Al-Anfaal: 50].

 

Hayo ndiyo yaliyotajwa na yaliyothibiti, vinginevyo ni lazima kuwe na maelekezo kama Malaika huwa wanakuja kwenye vikao vyetu na mikusanyiko yetu ya kusoma na kusomeshana Qur-aan au mafunzo mengineyo ya Dini kwa maumbile ambayo sisi tunaweza kuwaona. Na maadam hakuna mafundisho kama hayo, basi ni waajib wetu kutosheka na yale tuliyoyapata na kuyaamini kuwa wanahudhuria vikao kama hivyo bila kuwa na haja ya kujua kama wanaonekana au hawaonekani, au wanakuja kwa maumbo ya kibinaadam au hapana. Na Hadiyth ifuatayo iliyosimuliwa na Imaam Muslim haikutujulisha jinsi walivyo, Anasema Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam):

 

"…Hawakutaniki watu katika nyumba ya Alllaah wakisoma kitabu cha Allaah  na wakasomeshana pamoja ila watashukiwa na utulivu (sakina). Rehema (za Allaah) huwafunika, na Malaika huwazunguka na Allaah Huwakumbuka kwa wale walioko pamoja Nae… "

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share