Ufafanuzi Wa Aayah Kuhusu Kupandishwa Nabiy 'Iysaa (عَلَيْهِ السَّلام) Mbinguni

 

Ufafanuzi Wa Aayah Kuhusu Kupandishwa Nabiy 'Iysaa (عَلَيْهِ السَّلام) Mbinguni

 

Alhidaaya.com

 

 

SWALI:

 

Assalaamu Alaykum Warahmatullah.

 

Nashukuru kwa majibu yenu mazuri. Allaah awabariki kwa kazi nzuri mnayoifanya ya kutuelimisha, Ahsanteni sana. Kuna Aya katika Qur-ani inaelezea kurufaishwa kwa Nabii Issa (kupandishwa mbinguni) lakini kuna nyengine inaelezea kuwa, Nabii Issa anamjibu Allah kuwa na uliponifisha wewe ulikuwa shahidi juu yao. Suala langu ni kuwa, nahisi Aya hizi zinapingana au sijazielewa

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah - Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na Salaam zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho

 

Ufafanuzi wa Aayah hizo mbili ulizozifupisha ambazo zinaonekana kuwa ni kinzani ilhali hazipingani kabisa.

 

Allaah Aliyetukuka Anatueleza:

بَل رَّفَعَهُ اللَّـهُ إِلَيْهِ ۚ وَكَانَ اللَّـهُ عَزِيزًا حَكِيمًا ﴿١٥٨﴾

 Bali Allaah Alimnyanyua Kwake. Na Allaah daima ni Mwenye enzi ya nguvu Asiyeshindika, Mwenye hikmah wa yote. [an-Nisaa’: 158].

 

Hii Aayah inatuonyesha kuwa vile vitimbi vya Mayahudi vya kutaka kumsulubu Nabiy ‘Iysa (‘Alayhis-salaam) havikufaulu kwani Allaah Aliyetukuka Alimrufaisha Kwake kwa wakati walipotaka kumshika. Hiyo inaonyosha nguvu Zake Aliyetukuka kufanya Analotaka, bila ya kuwa na wasiwasi wa aina yoyote.

 

Ama tukija katika Aayah ya pili uliyoitaja:

 

.. وَكُنتُ عَلَيْهِمْ شَهِيدًا مَّا دُمْتُ فِيهِمْ ۖ فَلَمَّا تَوَفَّيْتَنِي كُنتَ أَنتَ الرَّقِيبَ عَلَيْهِمْ ۚ وَأَنتَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ شَهِيدٌ ﴿١١٧﴾

Na nilikuwa juu yao shahidi wakati nilipokuwa nao. Uliponichukua kikamilifu juu Ulikuwa Wewe Mwangalizi juu yao. Na Wewe juu ya kila kitu ni Mwenye kushuhudia. [Al-Maa’idah: 117].

 

Tatizo kwa wengi kuhusu Aayah hii ya pili ni lile neno: “Tawaffaytaniy”. Neno hilo limetafsiriwa na Maqadiyani kumaanisha “uliponifisha”, ilhali Shaykh Abdallah Swaalih al-Farsiy amesema: "Wanavyuoni wanasema kwa tamko la Tawaffaa sio maana yake ya asili ‘kutoa roho’; na wao wanajua, basi tu. Na mwenye Ruuhul Ma’aaniy ambaye wanajidai wamemfuata; ameandika: ‘Uliponichukua kwa kunipeleka mbinguni’. Na akaendelea kusema kuwa neno hilo katika lugha ya Kiarabu ya asili ni kutekeleza" (Qu-raani Takatifu, uk. 169).

 

Na ukitazama Tafsiyr ya Fat-hul Qadiyr ya Imaam Ash-Shawkaaniy ameeleza: "Hiyo ina maana uliponinyanyua mbinguni, na hapa al-Wafaat haina maana ya mauti. Bali ‘Iysa (‘Alayhis Salaam) alibaki mbinguni katika hali ya uhai kama alivyokuwa duniani mpaka arudi tena ardhini mwisho wa wakati kabla ya Qiyaamah. Uliponinyanyua mbinguni".

 

Kwa hiyo, ufafanuzi huo utakuwa wazi In shaa Allaah kuweza kuelewa Aayah hizo mbili.

 

Bonyeza viungo vifuatavyo kupata manufaa zaidi:

 

Nini Ukweli Kuhusu Kupandishwa Nabii 'Iysa عليه السلام

 

Nani Aliyesulubiwa Badala ya Nabii 'Iysa ('Alayhis Salaam)?

 

Je, Nabii 'Iysa Alisulubiwa?

 

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share