056 - Al-Waaqi'ah

 

   الْوَاقِعَة

 

056-Al-Waaqi’ah

 

 

056-Al-Waaqi’ah: Utangulizi Wa Suwrah

 

Alhidaaya.com

 

 

بِسْمِ اللَّـهِ الرَّحْمَـٰنِ الرَّحِيمِ

 

 

إِذَا وَقَعَتِ الْوَاقِعَةُ ﴿١﴾

1. Litakapotokea Tukio! (La Qiyaamah).[1]

 

 

 

 

لَيْسَ لِوَقْعَتِهَا كَاذِبَةٌ ﴿٢﴾

2. Hakuna cha kukadhibisha kutokea kwake.

 

 

 

 

خَافِضَةٌ رَّافِعَةٌ ﴿٣﴾

3. Literemshalo hadhi na linyanyualo hadhi.

 

 

 

 

إِذَا رُجَّتِ الْأَرْضُ رَجًّا ﴿٤﴾

4. Itakapotikiswa ardhi mtikiso mkubwa.

 

 

 

 

وَبُسَّتِ الْجِبَالُ بَسًّا ﴿٥﴾

5. Na milima itakapopondwa pondwa.

 

 

 

 

فَكَانَتْ هَبَاءً مُّنبَثًّا ﴿٦﴾

6. Ikawa chembechembe za vumbi zinazoelea hewani zikitawanyika.  

 

 

 

 

وَكُنتُمْ أَزْوَاجًا ثَلَاثَةً ﴿٧﴾

7. Na mtakuwa namna tatu.[2]

 

 

 

 

فَأَصْحَابُ الْمَيْمَنَةِ مَا أَصْحَابُ الْمَيْمَنَةِ ﴿٨﴾

8. Basi wapo watu wa kuliani; je, ni nani watu wa kuliani?[3]

 

 

 

 

وَأَصْحَابُ الْمَشْأَمَةِ مَا أَصْحَابُ الْمَشْأَمَةِ ﴿٩﴾

9. Na watu wa kushotoni; je, ni nani watu wa kushotoni?[4]

 

 

 

 

وَالسَّابِقُونَ السَّابِقُونَ ﴿١٠﴾

10. Na waliotangulia mbele, watatangulia mbele.[5]

 

 

 

 

أُولَـٰئِكَ الْمُقَرَّبُونَ ﴿١١﴾

11. Hao ndio watakaokurubishwa.

 

 

 

 

فِي جَنَّاتِ النَّعِيمِ ﴿١٢﴾

12. Katika Jannaat za taanisi.

 

 

 

 

ثُلَّةٌ مِّنَ الْأَوَّلِينَ ﴿١٣﴾

13. Kundi kubwa katika wa awali.[6]

 

 

 

وَقَلِيلٌ مِّنَ الْآخِرِينَ ﴿١٤﴾

14. Na wachache katika wa mwishoni.

 

 

 

 

عَلَىٰ سُرُرٍ مَّوْضُونَةٍ ﴿١٥﴾

15. (Watakuwa) juu ya makochi ya fakhari yaliyotariziwa na kutonewa johari za thamani kwa ustadi wa hali ya juu.[7]

 

 

 

 

مُّتَّكِئِينَ عَلَيْهَا مُتَقَابِلِينَ ﴿١٦﴾

16. Wakiegemea juu yake wakielekeana.

 

 

 

 

يَطُوفُ عَلَيْهِمْ وِلْدَانٌ مُّخَلَّدُونَ ﴿١٧﴾

17. Watazungukiwa (kuhudumiwa) na vijana wenye kudumu (katika hali yao milele).

 

 

 

 

بِأَكْوَابٍ وَأَبَارِيقَ وَكَأْسٍ مِّن مَّعِينٍ ﴿١٨﴾

18. Kwa bilauri na mabirika na vikombe vya mvinyo kutoka chemchemu inayobubujika.

 

 

 

 

لَّا يُصَدَّعُونَ عَنْهَا وَلَا يُنزِفُونَ ﴿١٩﴾

19. Hawatoumizwa vichwa kwavyo na wala hawatoleweshwa.

 

 

 

 

وَفَاكِهَةٍ مِّمَّا يَتَخَيَّرُونَ ﴿٢٠﴾

20. Na matunda watakayopendelea.

 

 

 

 

وَلَحْمِ طَيْرٍ مِّمَّا يَشْتَهُونَ ﴿٢١﴾

21. Na nyama za ndege katika watakazozitamani.

 

 

 

 

وَحُورٌ عِينٌ ﴿٢٢﴾

22. Na Hurulaini: Wanawake weupe wazuri wa Jannah wenye macho makubwa ya kupendeza.

 

 

 

 

كَأَمْثَالِ اللُّؤْلُؤِ الْمَكْنُونِ ﴿٢٣﴾

23. Kama mfano wa lulu zilizohifadhiwa.

 

 

 

 

جَزَاءً بِمَا كَانُوا يَعْمَلُونَ ﴿٢٤﴾

24. Jazaa kwa yale waliyokuwa wakitenda.

 

 

 

 

لَا يَسْمَعُونَ فِيهَا لَغْوًا وَلَا تَأْثِيمًا ﴿٢٥﴾

25. Hawatosikia humo upuuzi na wala yanayosababisha dhambi.

 

 

 

 

إِلَّا قِيلًا سَلَامًا سَلَامًا ﴿٢٦﴾

26. Isipokuwa itasemwa: Salama, salama!  

 

 

وَأَصْحَابُ الْيَمِينِ مَا أَصْحَابُ الْيَمِينِ ﴿٢٧﴾

27. Na watu wa kuliani, je, ni nani watu wa kuliani?

 

 

 

 

فِي سِدْرٍ مَّخْضُودٍ ﴿٢٨﴾

28. (Watakuwa) kwenye mikunazi iliyokatwa miba.

 

 

 

 

وَطَلْحٍ مَّنضُودٍ ﴿٢٩﴾

29. Na migomba ya ndizi iliyopangwa matabaka.

 

 

 

 

وَظِلٍّ مَّمْدُودٍ ﴿٣٠﴾

30. Na kivuli kilichotandazwa.

 

 

 

 

وَمَاءٍ مَّسْكُوبٍ ﴿٣١﴾

31. Na maji yenye kumiminwa.

 

 

 

 

وَفَاكِهَةٍ كَثِيرَةٍ ﴿٣٢﴾

32. Na matunda mengi.

 

 

 

 

لَّا مَقْطُوعَةٍ وَلَا مَمْنُوعَةٍ ﴿٣٣﴾

33. Hayana kikomo na wala hayakatazwi.

 

 

 

 

وَفُرُشٍ مَّرْفُوعَةٍ ﴿٣٤﴾

34. Na matandiko ya kupumzikia yaliyoinuliwa.

 

 

 

 

إِنَّا أَنشَأْنَاهُنَّ إِنشَاءً ﴿٣٥﴾

35. Hakika Sisi Tutawaumba (hurulaini) upya tofauti na mwanzo.

 

 

 

 

فَجَعَلْنَاهُنَّ أَبْكَارًا ﴿٣٦﴾

36. Tuwafanye mabikra.

 

 

 

 

عُرُبًا أَتْرَابًا ﴿٣٧﴾

37. Wenye mahaba, ashiki na bashasha kwa waume zao, hirimu moja.

 

 

 

 

لِّأَصْحَابِ الْيَمِينِ ﴿٣٨﴾

38. Kwa ajili ya watu wa kuliani.

 

 

 

 

ثُلَّةٌ مِّنَ الْأَوَّلِينَ ﴿٣٩﴾

39. Kundi kubwa katika wa awali.

 

 

 

 

وَثُلَّةٌ مِّنَ الْآخِرِينَ ﴿٤٠﴾

40. Na kundi kubwa katika wa mwishoni.[8]

 

 

 

 

وَأَصْحَابُ الشِّمَالِ مَا أَصْحَابُ الشِّمَالِ ﴿٤١﴾

41. Na watu wa kushotoni, je, ni nani watu wa kushotoni?[9]

 

 

 

 

فِي سَمُومٍ وَحَمِيمٍ ﴿٤٢﴾

42. (Watakuwa) kwenye moto ubabuao na maji yachemkayo.

 

 

 

 

وَظِلٍّ مِّن يَحْمُومٍ ﴿٤٣﴾

43. Na kivuli cha moshi mweusi mnene wa joto kali mno.

 

 

 

 

لَّا بَارِدٍ وَلَا كَرِيمٍ ﴿٤٤﴾

44. Si cha baridi na wala si cha kunufaisha.

 

 

 

 

إِنَّهُمْ كَانُوا قَبْلَ ذَٰلِكَ مُتْرَفِينَ ﴿٤٥﴾

45. Hakika wao walikuwa kabla ya hayo wanaostareheshwa kwa anasa za dunia.

 

 

 

 

وَكَانُوا يُصِرُّونَ عَلَى الْحِنثِ الْعَظِيمِ ﴿٤٦﴾

46. Na walikuwa wakishikilia kufanya dhambi kubwa mno.

 

 

 

 

وَكَانُوا يَقُولُونَ أَئِذَا مِتْنَا وَكُنَّا تُرَابًا وَعِظَامًا أَإِنَّا لَمَبْعُوثُونَ ﴿٤٧﴾

47. Na walikuwa wakisema: Je, hivi tutakapokufa na tukawa udongo na mifupa, je hivi sisi hakika tutafufuliwa?[10]

 

 

 

 

أَوَآبَاؤُنَا الْأَوَّلُونَ ﴿٤٨﴾

48. Au, je na baba zetu wa awali pia?

 

 

 

 

قُلْ إِنَّ الْأَوَّلِينَ وَالْآخِرِينَ ﴿٤٩﴾

49. Sema: (ee Muhammad صلى الله عليه وآله وسلم): Hakika wa awali na wa mwishoni.

 

 

 

 

لَمَجْمُوعُونَ إِلَىٰ مِيقَاتِ يَوْمٍ مَّعْلُومٍ ﴿٥٠﴾

50. Bila shaka watajumuishwa katika wakati na mahali pa siku maalumu.

 

 

 

 

ثُمَّ إِنَّكُمْ أَيُّهَا الضَّالُّونَ الْمُكَذِّبُونَ ﴿٥١﴾

51. Kisha hakika nyinyi enyi wapotovu mnaokadhibisha.

 

 

 

 

لَآكِلُونَ مِن شَجَرٍ مِّن زَقُّومٍ ﴿٥٢﴾

52. Bila shaka mtakula katika mti wa zaqquwm.[11]

 

 

 

 

فَمَالِئُونَ مِنْهَا الْبُطُونَ ﴿٥٣﴾

53. Na kwa huo mtajaza matumbo.

 

 

 

 

فَشَارِبُونَ عَلَيْهِ مِنَ الْحَمِيمِ ﴿٥٤﴾

54. Na mtakunywa juu yake maji ya moto yachemkayo mno.

 

 

 

 

فَشَارِبُونَ شُرْبَ الْهِيمِ ﴿٥٥﴾

55. Tena mtakunywa kama wanywavyo ngamia wenye kiu mno!

 

 

 

 

هَـٰذَا نُزُلُهُمْ يَوْمَ الدِّينِ ﴿٥٦﴾

56. Haya ndio mapokezi yao Siku ya Malipo!

 

 

 

 

نَحْنُ خَلَقْنَاكُمْ فَلَوْلَا تُصَدِّقُونَ ﴿٥٧﴾

57. Sisi Tumekuumbeni, basi kwa nini hamsadiki?

 

 

 

 

أَفَرَأَيْتُم مَّا تُمْنُونَ ﴿٥٨﴾

58. Je, basi mnaona manii mnayoimwagia kwa nguvu?

 

 

 

 

 

أَأَنتُمْ تَخْلُقُونَهُ أَمْ نَحْنُ الْخَالِقُونَ ﴿٥٩﴾

59. Je, nyinyi ndio mnayoiumba au Sisi ndio Waumbaji?

 

 

 

 

نَحْنُ قَدَّرْنَا بَيْنَكُمُ الْمَوْتَ وَمَا نَحْنُ بِمَسْبُوقِينَ ﴿٦٠﴾

60. Sisi Tumekadiria baina yenu mauti, Nasi Sio Wenye Kushindwa.

 

 

 

 

عَلَىٰ أَن نُّبَدِّلَ أَمْثَالَكُمْ وَنُنشِئَكُمْ فِي مَا لَا تَعْلَمُونَ ﴿٦١﴾

61. Kwamba Tuwabadilishe wengine mifano yenu, na Tukuumbeni katika umbo msilolijua.

 

 

 

 

وَلَقَدْ عَلِمْتُمُ النَّشْأَةَ الْأُولَىٰ فَلَوْلَا تَذَكَّرُونَ ﴿٦٢﴾

62. Na bila shaka mmejua umbo la awali, basi kwa nini hamkumbuki?

 

 

 

 

أَفَرَأَيْتُم مَّا تَحْرُثُونَ ﴿٦٣﴾

63. Je, mnaona mbegu mnazozipanda? 

 

 

 

 

أَأَنتُمْ تَزْرَعُونَهُ أَمْ نَحْنُ الزَّارِعُونَ ﴿٦٤﴾

64. Je, ni nyinyi ndio mnaziotesha, au Sisi Ndio Wenye Kuotesha mimea?

 

 

 

 

 

لَوْ نَشَاءُ لَجَعَلْنَاهُ حُطَامًا فَظَلْتُمْ تَفَكَّهُونَ ﴿٦٥﴾

65. Lau Tungelitaka, Tungeliifanya mabua yaliyonyauka na kupondekapondeka, mkabaki mnashangaa na kusikitika.

 

 

 

 

إِنَّا لَمُغْرَمُونَ ﴿٦٦﴾

66. (Mkisema): Hakika sisi tumegharimika.

 

 

 

 

بَلْ نَحْنُ مَحْرُومُونَ ﴿٦٧﴾

67. Bali sisi tumenyimwa.

 

 

 

 

أَفَرَأَيْتُمُ الْمَاءَ الَّذِي تَشْرَبُونَ ﴿٦٨﴾

68. Je, mnaona maji ambayo mnakunywa?

 

 

 

 

أَأَنتُمْ أَنزَلْتُمُوهُ مِنَ الْمُزْنِ أَمْ نَحْنُ الْمُنزِلُونَ ﴿٦٩﴾

69. Je, ni nyinyi ndio mliyoyateremsha kutoka katika mawingu ya mvua au Sisi Ndio Wateremshaji?

 

 

 

 

لَوْ نَشَاءُ جَعَلْنَاهُ أُجَاجًا فَلَوْلَا تَشْكُرُونَ ﴿٧٠﴾

70. Lau Tungelitaka, Tungeliyafanya ya chumvi kali chungu, basi kwa nini hamshukuru?!

 

 

 

 

أَفَرَأَيْتُمُ النَّارَ الَّتِي تُورُونَ ﴿٧١﴾

71. Je, mnaona moto ambao mnauwasha?

 

 

 

 

أَأَنتُمْ أَنشَأْتُمْ شَجَرَتَهَا أَمْ نَحْنُ الْمُنشِئُونَ ﴿٧٢﴾

72. Je, ni nyinyi ndio mliouanzisha mti wake, au Sisi Ndio Waanzilishaji?

 

 

 

 

نَحْنُ جَعَلْنَاهَا تَذْكِرَةً وَمَتَاعًا لِّلْمُقْوِينَ ﴿٧٣﴾

73. Sisi Tumeufanya kuwa ni ukumbusho na manufaa kwa wasafiri katika jangwa na wahitaji.

 

 

 

 

فَسَبِّحْ بِاسْمِ رَبِّكَ الْعَظِيمِ ﴿٧٤﴾

74. Basi sabbih kwa Jina la Rabb wako Mwenye U’adhwama.[12]

 

 

 

 

فَلَا أُقْسِمُ بِمَوَاقِعِ النُّجُومِ ﴿٧٥﴾

75. Basi Naapa kwa maanguko ya nyota.[13]

 

 

 

 

وَإِنَّهُ لَقَسَمٌ لَّوْ تَعْلَمُونَ عَظِيمٌ ﴿٧٦﴾

76. Na hakika hicho ni kiapo adhimu lau mngelijua.

 

 

 

 

إِنَّهُ لَقُرْآنٌ كَرِيمٌ ﴿٧٧﴾

77. Hakika hii bila shaka ni Qur-aan Tukufu.

 

 

 

 

فِي كِتَابٍ مَّكْنُونٍ ﴿٧٨﴾

78. Katika Kitabu kilichohifadhiwa.[14]

 

 

 

 

لَّا يَمَسُّهُ إِلَّا الْمُطَهَّرُونَ ﴿٧٩﴾

79. Haigusi isipokuwa waliotakaswa kabisa.

 

 

 

 

تَنزِيلٌ مِّن رَّبِّ الْعَالَمِينَ ﴿٨٠﴾

80. Ni uteremsho kutoka kwa Rabb wa walimwengu.

 

 

 

 

أَفَبِهَـٰذَا الْحَدِيثِ أَنتُم مُّدْهِنُونَ ﴿٨١﴾

81. Je, basi kwa (unafiki na kujipendekeza) maneno haya nyinyi mnayakanusha na kuyabeza?

 

 

 

 

وَتَجْعَلُونَ رِزْقَكُمْ أَنَّكُمْ تُكَذِّبُونَ ﴿٨٢﴾

82. Na mnafanya kuruzukiwa kwenu kuwa ndio mnakadhibisha?!

 

 

 

 

 

فَلَوْلَا إِذَا بَلَغَتِ الْحُلْقُومَ ﴿٨٣﴾

83. Basi mbona roho ifikapo kooni.[15]

 

 

وَأَنتُمْ حِينَئِذٍ تَنظُرُونَ ﴿٨٤﴾

84. Nanyi wakati huo mnatazama.

 

 

وَنَحْنُ أَقْرَبُ إِلَيْهِ مِنكُمْ وَلَـٰكِن لَّا تُبْصِرُونَ ﴿٨٥﴾

85. Nasi Tuko karibu naye zaidi kuliko nyinyi, lakini hamuoni.

 

 

 

فَلَوْلَا إِن كُنتُمْ غَيْرَ مَدِينِينَ ﴿٨٦﴾

86. Basi je, -mnaweza- ikiwa mnadai kwamba hamtohisabiwa wala kulipwa (na kwamba hamko chini ya Mamlaka Yetu).

 

 

 

 

تَرْجِعُونَهَا إِن كُنتُمْ صَادِقِينَ ﴿٨٧﴾

87. Kuirudisha roho (mwilini mwake), mkiwa ni wakweli?

 

 

 

 

فَأَمَّا إِن كَانَ مِنَ الْمُقَرَّبِينَ ﴿٨٨﴾

88. Basi akiwa miongoni mwa waliokurubishwa. [16]

 

 

 

 

فَرَوْحٌ وَرَيْحَانٌ وَجَنَّتُ نَعِيمٍ ﴿٨٩﴾

89. Basi mapumziko ya raha na manukato na Jannah ya neema.

 

 

 

 

وَأَمَّا إِن كَانَ مِنْ أَصْحَابِ الْيَمِينِ ﴿٩٠﴾

90. Na kama akiwa miongoni mwa watu wa kuliani.

 

 

 

 

فَسَلَامٌ لَّكَ مِنْ أَصْحَابِ الْيَمِينِ ﴿٩١﴾

91. Basi (ataambiwa): Salaam juu yako uliye katika watu wa kuliani.

 

 

 

 

وَأَمَّا إِن كَانَ مِنَ الْمُكَذِّبِينَ الضَّالِّينَ ﴿٩٢﴾

92. Na kama akiwa miongoni mwa wakadhibishaji waliopotoka.

 

 

 

 

فَنُزُلٌ مِّنْ حَمِيمٍ ﴿٩٣﴾

93. Basi mapokezi yake ni maji ya moto yachemkayo.

 

 

 

 

وَتَصْلِيَةُ جَحِيمٍ ﴿٩٤﴾

94. Na kuunguzwa na moto uwakao vikali mno.

 

 

 

 

إِنَّ هَـٰذَا لَهُوَ حَقُّ الْيَقِينِ ﴿٩٥﴾

95. Hakika hii bila shaka ni haki yenye yakini.

 

 

 

 

فَسَبِّحْ بِاسْمِ رَبِّكَ الْعَظِيمِ ﴿٩٦﴾

96. Basi sabbih kwa Jina la Rabb wako Mwenye U’adhwama.[17]

 

 

 

 

[1] Matukio Ya Siku Ya Qiyaamah:

 

Suwrah inaanza kwa kutaja tukio la Siku ya Qiyaamah, ikafuatia kutaja matukio yake mengineyo kama ardhi kutingishwa, na milima kupondwapondwa, Aayah namba (3-6). Na matukio kama haya na mengineyo, yametajwa katika Suwrah zifuatazo: An-Naazi’aat (79:6-14), At-Takwiyr (81:1-13), Al-Infitwaar (82:1-4), Al-Inshiqaaq (84:1-5), Az-Zalzalah (99), Al-Qaari’ah (101:1-5).

 

[2] Watu Watagawanyika Makundi Matatu Siku Ya Qiyaamah:

 

Kuanzia Aayah hii namba (7) hadi namba (11), Tafsiyr yake ni ifuatayo:

 

Watu watagawanywa katika magurupu matatu kulingana na amali zao njema na ovu. [Tafsiyr As-Sa’diy]

 

Watu watawaganyika katika aina tatu za makundi: (i) Watu wa kuliani mwa ‘Arsh, na hao ni wale waliotolewa ubavuni mwa Aadam upande wa kulia. Hawa watapewa Vitabu vyao kuliani mwao na watapelekwa upande wa kulia. As-Suddi amesema: Hao ndio wengi katika watu wa Jannah. (ii) Aina nyengine la kundi ni wale watakaowekwa upande wa kushoto wa ‘Arsh. Na hawa ni wale waliotolewa ubavu wa kushoto wa Aadam. Na hawa watapewa Vitabu vyao kushotoni mwao na watapelekwa upande wa kushoto. Hao wengi wao ni watu wa motoni, Allaah Atuepushe na matendo yao. (iii) Kundi la tatu linajumuisha wale waliotangulia mbele na waliokaribu zaidi mbele ya Allaah. Hao wamo katika daraja bora na hadhi, na ndio walio karibu zaidi na Allaah kuliko walio upande wa kulia. Hao ndio walio juu ya wote kwa sababu wao ni Rusuli, Manabii, wakweli wasadikishaji na Shuhadaa, nao ni wachache katika watu wa upande wa kuliani. [Tafsiyr Ibn Kathiyr]

 

Rejea Faatwir (35:32) kwenye faida nyenginezo.

 

Rejea pia At-Takwiyr (81:7).

 

[3] Hali Za Watu Walio Kuliani:

 

Kisha Allaah (سبحانه وتعالى) Akabainisha hali za makundi matatu:

 

فَأَصْحَابُ الْمَيْمَنَةِ مَا أَصْحَابُ الْمَيْمَنَةِ ﴿٨﴾

“Basi wapo watu wa kuliani; je, ni nani watu wa kuliani.”

 

Kutukuzwa hadhi zao na daraja lao la juu. [Tafsiyr As-Sa’diy]

 

Hii ni sawa na Kauli za Allaah (سبحانه وتعالى) za Suwrah Al-Haaqqah (69:19-24), Al-Inshiqaaq (54:7-9).

 

[4] Hali Za Watu Wa Kushotoni:

 

وَأَصْحَابُ الْمَشْأَمَةِ مَا أَصْحَابُ الْمَشْأَمَةِ ﴿٩﴾

“Na watu wa kushotoni; je, ni nani watu wa kushotoni.”

 

Swali hapa pia limekuja ili kuzindusha jinsi gani hali mbaya watakayokuwa nayo.

 

Hii ni sawa na Kauli za Allaah (سبحانه وتعالى) za Suwrah Al-Haaqqah (69:25-37), Al-Inshiqaaq (54:7-9).

 

[5] Hali Za Waliotangulia Mbele:

 

وَالسَّابِقُونَ السَّابِقُونَ ﴿١٠﴾

“Na waliotangulia mbele, watatangulia mbele.”

 

Ambao wametanguliza katika khayraat duniani basi watatangulizwa Aakhirah kuingia Jannah. [Tafsiyr As-Sa’diy]

 

[6] Kundi Kubwa La Awali:

 

Ni watu wengi waliotangulia katika Ummah huu na wengineo. [Tafsiyr As-Sa’diy]

 

[7] Miongoni Mwa Neema Za Jannah:

 

Kuanzia Aayah hii namba (15) hadi Aayah namba (37), zinatajwa neema katika neema za Jannah. Na zimetajwa sifa na hali za wakaazi wake zitakavyokuwa. Aayah nyingi zimetaja kuhusu watu wa Jannah, hali zao, sifa zao na starehe zao pamoja na neema tele. Rejea pia Faatwir (35:33) kwenye neema nyenginezo za watu wa Jannah. Hali kadhaalika, zipo Hadiyth nyingi ambazo zimetaja hayo. Miongoni mwazo ni hizi zifuatazo:

 

حَدَّثَنَا مُحَمَّدُ بْنُ مُقَاتِلٍ، أَخْبَرَنَا عَبْدُ اللَّهِ، أَخْبَرَنَا مَعْمَرٌ، عَنْ هَمَّامِ بْنِ مُنَبِّهٍ، عَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ ـ رضى الله عنه ـ قَالَ قَالَ رَسُولُ اللَّهِ صلى الله عليه وسلم ‏ "‏ أَوَّلُ زُمْرَةٍ تَلِجُ الْجَنَّةَ صُورَتُهُمْ عَلَى صُورَةِ الْقَمَرِ لَيْلَةَ الْبَدْرِ، لاَ يَبْصُقُونَ فِيهَا وَلاَ يَمْتَخِطُونَ وَلاَ يَتَغَوَّطُونَ، آنِيَتُهُمْ فِيهَا الذَّهَبُ، أَمْشَاطُهُمْ مِنَ الذَّهَبِ وَالْفِضَّةِ، وَمَجَامِرُهُمُ الأَلُوَّةُ، وَرَشْحُهُمُ الْمِسْكُ، وَلِكُلِّ وَاحِدٍ مِنْهُمْ زَوْجَتَانِ، يُرَى مُخُّ سُوقِهِمَا مِنْ وَرَاءِ اللَّحْمِ، مِنَ الْحُسْنِ، لاَ اخْتِلاَفَ بَيْنَهُمْ وَلاَ تَبَاغُضَ، قُلُوبُهُمْ قَلْبٌ وَاحِدٌ، يُسَبِّحُونَ اللَّهَ بُكْرَةً وَعَشِيًّا ‏"‏‏.‏

Amesimulia Abuu Hurayrah (رضي الله عنه): Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) amesema: “Kikundi cha kwanza (cha watu) kuingia Jannah (Peponi) watakuwa waking’ara kama mwezi unapokuwa umekamilika. Hawatatema mate humo wala kuchemua wala kwenda haja. Vyombo vyao vitakuwa ni vya dhahabu, vichana vyao ni vya dhahabu na fedha. Katika vyetezo vyao kutakuwa na uluwwah (mti wenye harufu nzuri unapochomwa) na majasho yao yatanukia kama miski (manukato). Kila mmoja wao atakuwa na wake wawili. Uboho ulio ndani ya mifupa ya miguu ya wake zao utaonekana kupitia nyama zao kwa uzuri wao uliopita kiasi. Wao (yaani watu wa Jannah) hawatakuwa na tofauti baina yao wala chuki. Nyoyo zao zitakuwa kama moyo mmoja, nao watakuwa wanamtakasa Allaah asubuhi na jioni.”

[Al-Bukhaariy Kitaabu Cha Hadiyth Za Uanzishaji Wa Uumbaji (59)]

 

Riwaaya kama hiyo imo katika [Al-Bukhaariy Kitabu Cha Hadiyth Za Manabii (60). Na pia katika Muslim Kitabu Cha Jannah Sifa Zake Na Neema Zake Na Watu Wake]

 

عن أبي موسى رضي الله عنه : أنَّ النبيَّ صلى الله عليه وسلم  قال : (( إنَّ لِلمُؤْمِنِ فِي الجَنَّةِ لَخَيْمَةً مِنْ لُؤْلُؤَةٍ وَاحِدَةٍ مُجَوَّفَةٍ طُولُها في السَّمَاءِ سِتُّونَ مِيلاً . لِلمُؤْمِنِ فِيهَا أَهْلُونَ يَطُوفُ عَلَيْهِمُ المُؤْمِنُ فَلاَ يَرَى بَعْضُهُمْ بَعْضاً )) مُتَّفَقٌ عَلَيهِ

Amesimulia Abuu Muwsaa (رضي الله عنه):  amesema: “Hakika, Muumini katika Jannah atakuwa na  hema la lulu ambalo liko mviringo, urefu wake ni maili sitiini kwenda juu. Muumini atakuwa na familia yake humo, Muumini atakuwa akiwazunguka humo nao hawaonani (jinsi lilivyo kubwa).”  [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

عن أبي هريرة رضي الله عنه : أنَّ رسولَ اللهِ صلى الله عليه وسلم قال : (( إنَّ أدْنَى مَقْعَدِ أَحَدِكُمْ مِن الجَنَّةِ أنْ يَقُولَ لَهُ : تَمَنَّ ، فَيَتَمَنَّى وَيَتَمَنَّى فَيقُولُ لَهُ : هَلْ تَمَنَّيتَ ؟ فيقولُ : نَعَمْ ، فيقُولُ لَهُ : فَإنَّ لَكَ ما تَمَنَّيتَ وَمِثْلَهُ 

مَعَهُ )) . رواه مسلم

Amesimulia Abuu Hurayrah (رضي الله عنه): Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) amesema: “Hakika daraja ya chini mno ya mmoja wenu Jannah, ni kuwa Allaah Atamwambia Tamani! Atatamani kila atakalo. Allaah Atamuuliza: Umeshamaliza kutamani? Atajibu: Ndio. Allaah Atamwambia: Nimekupa ulichotamani na Nimekupa kingine kama hicho.” [Muslim]

 

Bonyeza viungo vifuatavyo kwenye faida nyenginezo:

 

Neema Za Jannah (Pepo) Tuliyoahidiwa

 

Al-Jannah (Pepo)

 

Jazaa Ya Waja Wema Na Neema Za Jannah

 

[8] Kundi Kubwa Katika Wa Mwishoni:

 

Huu ni mgawanyo wa watu wa kuliani ambao idadi yao ni kubwa ya wtu wa awali na idadi kubwa ya watu mwishoni. [Tafsiyr As-Sa’diy]

 

[9] Watu Wa Kushotoni Ni Watu Wa Motoni Na Maelezo Yao:

 

Aayah hii namba (41) hadi Aayah namba (56) zinataja watu wa motoni na sababu za kuwa kwao watu wa motoni, hali zao zitakvyokuwa motoni na adhabu zao.

 

Rejea An-Nabaa (78:21) kwenye uchambuzi na rejea mbalimbali kuhusu watu wa motoni, hali zao, mateso na adhabu zao, vyakula na vinywaji vyao.

 

Rejea pia Faatwir (33:36) kwenye faida nyenginezo kuhusu maudhui hii na rejea zake.

 

[10] Makafiri Hawakuamini Kwamba Watafufuliwa:

 

Rejea Al-Israa (17:49-52), Yaasiyn (36:77-83).

 

[11] Mti Wa Zaqquwm:

 

Zaqquwm ni mti wa motoni ambao utakuwa ni chakula cha wakaazi wake. Rejea Al-Israa (17:60).

 

[12] Kumsabbih Allaah (سبحانه وتعالى) Katika Aayah Za Kumsabbih, Kuomba Rahmah, Jannah (Pepo) Kuomba Kinga Na Kadhaalika.

 

 

عَنْ حُذَيْفَةَ، قَالَ صَلَّيْتُ مَعَ النَّبِيِّ صلى الله عليه وسلم ذَاتَ لَيْلَةٍ فَافْتَتَحَ الْبَقَرَةَ فَقُلْتُ يَرْكَعُ عِنْدَ الْمِائَةِ ‏.‏ ثُمَّ مَضَى فَقُلْتُ يُصَلِّي بِهَا فِي رَكْعَةٍ فَمَضَى فَقُلْتُ يَرْكَعُ بِهَا ‏.‏ ثُمَّ افْتَتَحَ النِّسَاءَ فَقَرَأَهَا ثُمَّ افْتَتَحَ آلَ عِمْرَانَ فَقَرَأَهَا يَقْرَأُ مُتَرَسِّلاً إِذَا مَرَّ بِآيَةٍ فِيهَا تَسْبِيحٌ سَبَّحَ وَإِذَا مَرَّ بِسُؤَالٍ سَأَلَ وَإِذَا مَرَّ بِتَعَوُّذٍ تَعَوَّذَ ثُمَّ رَكَعَ فَجَعَلَ يَقُولُ ‏"‏ سُبْحَانَ رَبِّيَ الْعَظِيمِ ‏"‏ ‏.‏ فَكَانَ رُكُوعُهُ نَحْوًا مِنْ قِيَامِهِ ثُمَّ قَالَ ‏"‏ سَمِعَ اللَّهُ لِمَنْ حَمِدَهُ ‏"‏ ‏.‏ ثُمَّ قَامَ طَوِيلاً قَرِيبًا مِمَّا رَكَعَ ثُمَّ سَجَدَ فَقَالَ ‏"‏ سُبْحَانَ رَبِّيَ الأَعْلَى ‏"‏

Amesimulia Hudhayfah (رضي الله عنه): Niliswali pamoja na Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم) usiku usiku mmoja, akaanza kusoma Suwrah Al-Baqarah, nikadhania kuwa atarukuu atakapofikia mwishoni mwa Aayah mia lakini akaendelea. Kisha nikadhania kuwa ataisoma (Suwrah) nzima katika Rakaa lakini akaendelea. Nikadhania kuwa atarukuu atakapoimaliza (Suwrah). Kisha akaanza An-Nisaa akaisoma, kisha akaanza Aal-‘Imraan akaisoma kwa utulivu. Akawa kila anapopita Aayah yenye tasbiyh alisabbih, na alipopita Aayah ya kumuomba Allaah aliomba, na alipopita katika kuomba kinga aliomba kinga, kisha akarukuu akasema:

سُبْحَانَ رَبِّيَ الْعَظِيمِ ‏

Rukuu yake ilidumu kwa urefu sawa na kusimama kwake (kisha akarudi kwenye kisimamo baada ya kurukuu) akasema: 

سَمِعَ اللَّهُ لِمَنْ حَمِدَهُ ‏

Kisha akasimama kwa muda mrefu kama muda ule ule alotumia katika kurukuu. Kisha akasujudu na akasema:

سُبْحَانَ رَبِّيَ الأَعْلَى

Na kusujudu kwake kulidumu karibu urefu sawa na kisimamo chake. [Muslim]

 

[13] Sababun-Nuzuwl (Sababu Ya Kuteremshwa) Aayah Au Suwrah:

 

Bonyeza kiungo kifuatacho:  

 

056-Asbaabun-Nuzuwl: Al-Waaqi’ah Aayah 75-82: فَلَا أُقْسِمُ بِمَوَاقِعِ النُّجُومِ

 

[14] Kitabu Kilichohifadhiwa (Al-Lawh Al-Mahfuwdhw):

 

Kimewekewa pazia kisiweze kuonwa na macho ya viumbe. Na Kitabu hiki kilichohifadhiwa hivyo ni Al-Lawh Al-Mahfuwdhw (Ubao Uliohifadhiwa), yaani: Qur-aan hii imeandikwa katika Al-Lawh Al-Mahfuwdhw, imetukuka mbele ya Allaah na Malaika Wake wenye hadhi kubwa Kwake. Pia inawezekana kwamba Kitabu kilichohifadhiwa kinachomaanishwa hapa, ni Kitabu ambacho kiko mikononi mwa Malaika ambao Allaah Anawateremshia Wahy Wake na Uteremsho Wake (Qur-aan Yake), na kwamba muradi wa kuhifadhiwa ni kuwekewa pazia mashaytwaan wasiweze kukifikia na wasiwe na uwezo wa kukibadilisha, wala kukiongeza, kukipunguza, wala kukidukua. [Tafsiyr As-Sa’diy]

 

[15] Sakaraatul-Mawt (Mateso Ya Adhabu Inapotolewa Roho):

 

Rejea Qaaf (50:19) kwenye faida kadhaa.

 

[16] Hali Za Aina Tatu Za Watu Mauti Yanapowafikia:

 

Mwanzoni mwa Suwrah, Allaah (سبحانه وتعالى) Ametaja aina tatu za watu watakavyokuwa Aakhirah ambayo ni makazi ya milele,: (i) Waliokurubishwa. (ii) Watu wa kuliani. (iii) Waliokadhibisha Wapotovu. Na mwishoni mwa Suwrah kuanzia Aayah hii namba (88) hadi namba (94) Anataj hali zao katika kutolewa roho zao. [Tafsiyr As-Sa’diy]  

 

Rejea mwanzoni mwa  Suwrah hii Aayah namba (7). 

 

Kuhusu Waumini wanapotolewa roho zao, rejea  Qaaf (50:19) kwenye faida kadhaa.

 

Na kuhusu neema za kuingizwa Jannah (Peponi), rejea  Faatwir (35:33).

 

Ama kuhusu makafiri, rejea An-Nabaa (78:21) kwenye uchambuzi na rejea mbalimbali, kuhusu mateso na adhabu zao motoni, hali zao, vyakula na vinywaji vyao.  

 

[17] Kumsabbih Allaah:

 

Kumsabbih Allaah (عزّ وجلّ)   kwa

سُبْحَانَ اللهِ العظيمِ

ni katika Adhkaar za kurukuu kwenye Swalaah. Bonyeza kiungo kifuatacho kupata maelezo, na kuisoma kwa sauti:

017-Hiswnul-Muslim: Du’aa Za Wakati Wa Kurukuu

Na Hadiyth kadhaa zimetaja fadhila za kumsabbih Allaah ambazo miongoni mwazo ni Hadiyth hii ifuatayo:

 

 عن أَبي هريرة رضي اللهُ عنه قَالَ : قَالَ رسُولُ الله صلى الله عليه وسلم : (( كَلِمَتَانِ خَفِيفَتَانِ عَلَى اللِّسَانِ ، ثَقِيلَتَانِ فِي المِيزَانِ ، حَبِيبَتَانِ إِلَى الرَّحْمانِ : سُبْحَانَ اللهِ وَبِحَمْدِهِ ، سُبْحَانَ اللهِ العظيمِ )) متفقٌ عَلَيْهِ

 

Amesimulia Abuu Hurayrah (رضي الله عنه): Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) amesema: "Maneno mawili ni mepesi ulimini, mazito katika mizani na yanapendwa na Ar-Rahmaan (Mwingi wa Rehma):

 

سُبْحَانَ اللهِ وَبِحَمْدِهِ ، سُبْحَانَ اللهِ العظيمِ

Ametakasika Allaah na Himdi zote Njema Anastahiki, Ametakasika Allaah Mtukufu."

[Al-Bukhaariy, Muslim na At-Tirmidhiy]

 

Rejea pia kiungo kifuatacho chenye kutaja fadhila za kumsabbih Allaah (سبحانه وتعالى):

130-Hiswnul-Muslim: Fadhila Za Tasbiyh, Tahmiyd, Tahliyl Na Takbiyr

 

 

 

Share