Imaam Ibn ‘Uthaymiyn: Taratibu Za Hajj Na 'Umra

 Taratibu Za Hajj Na 'Umra

 

 

Imaam Muhammad Bin Swaalih Al-‘Uthaymiyn  (Rahimahu Allaah)

 

 

Imetarjumiwa na  www.alhidaaya.com

 

 

 

AlhamduliLLaah Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salamu zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Hajj ni aina mojawapo ya ‘ibaadah   bora kabisa na ni amali tukufu kabisa kwani ni mojawapo ya fardhi za Kiislamu ambazo Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Amemtuma Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kutuongoza.  Dini ya mja wa Kiislamu haikamiliki bila ya Hajj.  Ni ‘ibaadah inayokubaliwa pindi yafuatayo yatahakikishwa:

 

 

Mtu ataifanyia bidii ya dhati kuwa ni kwa ajili ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Pekee na kwa kutamani Aakhirah na haitowezekana kufanyika kwa ajili ya kumuonyesha mtu au kwa ajili ya maslahi ya dunia.

Inampasa mtu anapotenda ‘ibaadah yake afuate mfano wa Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kwa maneno na vitendo na hii haiwezekani kutimia ila kwa kujifunza na kupata elimu ya mafundisho ya Sunnah.

       

 

Aina Za Hajj

 

Kuna aina tatu za Hajj; Tamattu'u, Ifraad na Qiraan.

 

Tamattu’

 

Hajji anavaa Ihraam ya 'Umrah tu wakati wa miezi ya Hajj (anapokwenda Makkah mapema) ambayo inamaanisha kwamba anapofika Makkah atafanya twawwaaf na Sa'yi ya 'Umrah. Kisha atanyoa au kukata nywele. Siku ya Tarwiyyah ambayo ni siku ya nane Dhul-Hijjah, atavaa nguo zake za Ihraam kwa ajili ya Hajj tu na atatekeleza yote yanayompasa kufanya.

 

Ifraad:

 

Hajji atavaa Ihraam kwa ajili ya Hajj pekee.  Atakapofika Makkah atafanya twawwaaf pamoja na Sa'yi ya Hajj. Hana haja kunyoa au kukata nywele zake kwani hatoki kwenye Ihraam yake. Bali atabakia katika Ihraam mpaka amalize kurusha vijiwe katika Jamrah Al-'Aqabah siku ya 'Iyd. Anaruhusiwa kuchelewesha Sa'yi yake ya Hajj mpaka amalize twawwaaf ya Hajj.

 

Qiraan:

 

Hajji anavaa Ihraam ya zote mbili; 'Umrah na Hajj au anavaa kwanza Ihraam ya 'Umrah, kisha anatia niyyah ya Hajj kabla ya twawwaaf ya Hajj. Wajibu wa anayefanya Ifraad ni sawa sawa na anayefanya Qiraan, isipokuwa tu mwenye kufanya Qiraan inampasa achinje na mwenye kufanya Ifraad haimpasi kuchinja

 

 

Aina ya Hajj iliyo bora kabisa katika hizi ni ya Tamattu'u ambayo ndio Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alisisitiza ummah wake waitekeleze.

 

Hata kama Mweny kuhiji akitia niyyah ya kufanya Qiraan au Ifraad, anaruhusiwa kubadilisha niyyah yake kuingia katika Hajj ya Tamattu'u. Na anaweza kufanya hivi hata kama baada ya kufanya twawwaaf na Sa’yi kwa sababu Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alipofanya Twawwaaf na Sa’yi mwaka wa Hijjah ya Widaa' (Hajj ya kuaga) pamoja na Maswahaba zake, aliamrisha wote ambao hawakuleta mnyama kwa ajili ya kuchinja, wabadilishe niyyah zao za Hajj na kutia niyyah ya 'Umrah, wakate nywele zao, na wavue Ihraam mpaka Hajj.  Akasema:

(("لولا أني سقت الهدي لفعلت مثل الذي أمرتكم به))   البخاري

"Ingelikuwa sikuleta mnyama ningelifanya hivyo nilivyokuamrisheni mfanye" [Al-Bukhaariy]  

 

 

 

'Umrah

 

Akipenda Hajji kuwa katika Twahaara ya 'Umrah, akoge kama josho la janaba. Mwanamume atie manukato mazuri kabisa na apake mafuta mazuri kichwani. Hakuna ubaya harufu ikibakia baada ya Ihraam.

 

Kukoga ili kuingia katika Ihraam ni Sunnah kwa mwanamume na mwanamke pamoja na wanawake wenye hedhi na wale wenye Nifaas (damu ya uzazi). 

 

Baada ya kukoga na kujitayarisha, Mahujjaaj wote isipokuwa wanawake wenye hedhi au nifaas wataswali Swalaah za fardhi inapowadia wakati wake kama kawaida. Na ikiwa sio wakati wa Swalaah ya fardhi basi ataswali Raka'h mbili ambazo ni vizuri mtu kuswali kila anapotia wudhuu.

 

Atakapomaliza kuswali atasema Talbiyah hii:

 

لَبَّيْكَ اللَّهُمَّ عُمْرَة لَبَّيْكَ اللَّهُمَّ لَبَّيْكَ، لَبَّيْكَ لاَ شَرِيكَ لَكَ لَبَّيْكَ، إِنَّ الْحَمْدَ، وَالنِّعْمَةَ، لَكَ وَالْمُلْكَ،لاَ شَرِيكَ لَكَ

Labbayka-Allaahumma ‘Umrah, Labbayka-Allaahumma Labbayk. Labbayka laa shariyka Laka Labbayk. Innal-Hamda Wan-Ni'imata Laka wal-Mulk laa shariyka Lak.

 

"Nimekuitikia (Ee Allaah) 'Umrah, Nimekuitika (Ee Allaah) nimekuitika, nimekuitika (ee Allaah) Huna mshirika, nimekuitika (ee Allaah), hakika Himdi na Neema na  Ufalme ni Vyako Huna mshrika"

 

Mwanamume atasema kwa sauti na mwanamke atasema kiasi cha kumsikia wa pembezoni mwake. (Wanawake wenzake).

 

Anatakiwa mtu kusema Talbiyah kila mara khaswa anapofika na kubadilisha kituo. Mfano anapopanda na kushuka kipando wakati wa safari au wakati wa usiku unapoingia na asubuhi kunapopambazuka. Pia Amuombe Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) radhi Zake za kupata Jannah na aombe kujikinga na moto kwa Rahmah Za Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa). 

 

Anatakiwa mtu aseme Talbiyah wakati wa 'Umrah tokea anapovaa Ihraam yake hadi anapoanza Twawwaaf. Wakati wa Hajj aseme Talbiyah kutokea mwanzo wakati anapovaa Ihraam yake mpaka anapoanza kupiga mawe Jamarah ya 'Aqabah siku ya 'Iyd.

 

Hajji anapoingia msikitini atangulize mguu wake wa kulia na kusema:

 

أَعُوذُ بِاللَّهِ الْعَظِيمِ، وَبِوَجْهِهِ الْكَرِيمِ، وَسُلْطَانِهِ الْقَدِيمِ، مِنَ الشَّيْطَانِ الرَّجِيمِ,، (بِسْـمِ الله، وَالصَّلاةُ) (وَالسَّلامُ عَلى رَسولِ الله)، اللّهُـمَّ افْتَـحْ لي أَبْوابَ رَحْمَتـِك

A’uwdhu biLlaahil-‘Adhwiym, wabi Wajhihil-Kariym wa-Sultwaanihil-qadiym, minash-shaytwaanir-rajiym (BismiLLaah was-swalaatu) (was-salaamu ‘alaa Rasuwli-Llaah) Allaahummaftah-liy abwaaba Rahmatika

 

“Najikinga na Allaah Mtukufu, na kwa Wajihi Wake Mkarimu, na kwa utawala Wake wa kale, dhidi ya shaytwaan aliyeepushwa na Rahmah za Allaah (Kwa jina la Allaah na Swalaah na salaam zimfikie Rasuli wa Allaah) Ee Allaah nifungulie milango ya Rahmah Yako.”

 

Anakaribia Hajar Al-Aswad (jiwe jeusi) na kuligusa kwa mkono wake wa kulia na kulibusu. Ikiwa hii haiwezekani, basi aelekeze tu uso wake kuelekea kwenye Hajar Al-Aswad na kuashiria kwa mkono wake. (Usibusu mkono wako!) Haifai kusukuma na kusababisha madhara kwake na kwa watu.  

 

Anapoligusa au kuliashiria Hajar Al-Aswad anatakiwa aseme hivi:

 

 

  بسم الله والله أكبر، اللهم إيماناً بك، وتصديقاً بكتابك، ووفاء بعهدك، واتباعاً لسنة نبيك محمد صلى الله عليه وآله وسلم

BismiLLaahi wa-Allaahu Akbar, Allaahumma Iymaanam-Bika, Wa taswdiyqam-bikitaabika, wa wafaa-aan bi'ahdiak, wat-tibaa'al-lisunnati Nabiyyika Muhammad Swalla Allaahu 'Alayhi wasallam.

 

Kwa jina la Allaah, na Allaah ni Mkubwa, Ee Allaah kwa iymani Kwako, na kwa kuamini kitabu Chako, na kwa kutekeleza ahadi yako, na kufuata Sunnah ya Nabii Wako Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam).

 

(Tanbihi: Pamoja na Imaam kutaja ziada ya du'aa baada ya 'BismiLLaahi Wa-Allaahu Akbar' (Kwa jina la Allaah, na Allaah ni Mkubwa),  maelezo yaliyofuatia pamoja na kwamba yananasibishwa na Maswahaba 'Aliy bin Abi Twaalib, Ibn 'Abbaas na Ibn 'Umar, lakini Wanachuoni wengi wa Hadiyth miongoni mwao Ibn Hajr na Al-Albaaniy wameeleza kuwa hazijathibiti kutoka kwao.)

 

Hajji lazima atembee huku Ka'bah liko kushotoni mwake. Anapofika Rukn Al-Yamani aiguse lakini asibusu bali atakapokuwa baina yake na Hajar Al-Aswad aseme:

 

 

 رَبَّنَا آتِنَا فِي الدُّنْيَا حَسَنَةً وَفِي الاَخِرَةِ حَسَنَةً وَقِنَا عَذَابَ النَّارِ 

 

((Rabbanaa Aatinaa fid-duniyaa Hasanatan wafil Aakiharati Hasanatan waqinaa 'adhaaban-naar)).

 

"Rabb wetu, Tupe duniani mema, na Aakhirah mema, na Utulinde na adhabu ya moto"

 

((اللهم إني أسألك العفو والعافية في الدنيا والآخرة))

 

Allaahumma Inniy As-alukal-'afuw wal-'aafiyata fid-duniyaa wal-Aakhirah

 

"Ee Allaah Nakuomba msamaha na al-‘aafiyah (afya, salama amani kutokana na kila shari na ovu) duniani na Aakhirah"

 

Kila mara akilipita Hajar Al-Aswad anatakiwa aseme "Allaahu Akbar"

 

Katika kufanya Twawwaaf zilizobakia anaweza kusema anachopenda katika Du'aa, kumtaja Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kusoma Qur-aan.  Hii kwa sababu twawwaaf, Sa’yi na kurusha vijiwe Jamrah imekhusiwa kwa ajili ya kumdhukuru Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa).  

 

Katika Twawwaaf hii anahitajika mwanamume afanye vitu viwili: 

 

 

Aweke Al-Idhwtwiba'a kutoka mwanzo wa Twawwaaf mpaka mwisho. Al-Idhwtwiba'a ina maana kwamba ni kuweka sehemu ya katikati ya vazi (ridaa) chini ya kwapa lake la kulia na kipande cha ridaa akipitishe juu ya bega la mkono wa kushoto. Anapomaliza kufanya Twawwaaf anaweza kurudisha ridaa yake katika hali yake ya mwanzo kwa sababu wakati wa Idhwtwiba'a ni wakati wa Twawwaaf tu.

 

 

Kufanya Ar-Raml katika Twawwaaf tatu za mwanzo. Ar-Raml ina maana kwamba kuzunguka kwa mwendo wa haraka kwa  hatua ndogo ndogo. Kisha anatakiwa atembee mwendo wa kawaida katika Twawwaaf zake nne za mwisho.

 

 

Atakapomaliza mizunguko saba ya Twawwaaf, atakaribia Maqaam Ibraahiym na atasoma:

 

 وَاتَّخِذُواْ مِن مَّقَامِ إِبْرَاهِيمَ مُصَلًّى

 fanyeni mahali pa kusimama Ibraahiym kuwa ni pahala pa kuswalia. [Al-Baqarah: 125]

 

 

Ataswali Raka'ah mbili fupi, akiwa karibu kiasi iwezekanavyo na nyuma ya Maqaam Ibraahiym. Katika Raka'ah ya mwanzo atasoma Swratul-Kaafiruwn na Raka'ah ya pili atasoma Suwratul-Ikhlaas. Atakapomaliza Raka'ah mbili atarudi kuligusa Hajar Al-Aswad kama itawezekana.   Atakwenda Al-Mas-'aa, atakapofika karibu na As-Swafaa atasoma:

 

إِنَّ الصَّفَا وَالْمَرْوَةَ مِن شَعَائِرِ اللَّـهِ ۖ  

158. Hakika Asw-Swafaa na Al-Marwah ni katika alama za Allaah.  [Al-Baqarah: 158]

 

 

Atapanda (kilima cha) Swafaa mpaka aweze kuona Ka'abah. Aelekee Ka'abah na anyanyue mikono yake, amtukuze Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)  na aombe Du'aa apendayo. Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) aliomba:

 

 لا إِلهَ إلاَّ  اللهُ وَحْدَهُ  لا شَرِيكَ لَهُ، لَهُ المُلْكُ وَلَهُ الحَمْدُ وهُوَ عَلى كُلِّ شَيءٍ قَديرٌ، لا إِلَهَ إلا اللهُ وَحْدَهُ أَنْجَزَ وَعْدَهُ، وَنَصَرَ عَبْدَهُ وَهَزَمَ الأَحْزَابَ وَحْدَهُ

 

Laa iIlaaha illa-Allaah Wahdahu laa shariyka Lah, Lahul-Mulku Walahul-Hamd wa Huwa 'alaa kulli shay-in Qadiyr. Laa ilaaha illa-Allaah Wahdahu, Anjaza Wa'dahu Wanaswara 'Abdahu Wahazamal-Ahzaaba Wahdahu.

 

 “Hapana muabudiwa wa haki ila Allaah, hali ya kuwa Peke Yake, wala Hana mshirika, Ufalme ni Wake na Himdi ni Zake, Naye juu ya kila kitu ni Muweza.  Hapana muabudiwa wa hakii ila Allaah hali ya kuwa Peke Yake, Ametekeleza ahadi Yake, na Amemnusuru mja Wake, na Amevishinda vikosi Peke Yake”

 

 

Atasema mara tatu akiomba Du'aa baina yake.

 

 

Atateremeka As-Swafaa na kuelekea Al-Marwah kwa mwendo wa kawaida mpaka anapofika katika alama ya kijani, hapo atatembea kwa mwendo wa kukimbia mpaka alama ya kijani nyingine.  Ataendelea kuelekea Al-Marwah kwa mwendo wa kawaida. Atakapofikia atapanda (kilima) na kuelekea Qiblah, atanyanyua mikono na kurudia kusema kama alivyosema alipokuwa As-Swafaa. Atateremka Al-Marwah kuelekea As-Swafaa, akihakikisha anatembea sehemu zinazohusika na kukimbia katika sehemu zinazohusika.

 

 

Ataendelea kufanya hivyo hivyo mpaka amalize mizunguko saba. Kutoka As-Swafaa kwenda Al-Marwah ni mzunguko mmoja na kurudi ni mzunguko mwingine. Wakati wa Sa’yi anaweza kusoma anachotaka kama Du'aa, Qur-aan na kumtaja Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa).

 

 

Anapomaliza Sa’yi atanyoa nywele. Mwanamke atakata nywele kiasi cha urefu wa ncha ya kidole. Inapendekezeka kunyoa nywele zote, na kunyoa ni bora kuliko kukata kwani Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) aliwaombea du’aa walionyoa mara tatu na waliokata mara moja. Isipokuwa ikiwa Hajj iko karibu na hakuna wakati wa kutosha kwa nywele kurudi kukua, basi ni bora kukata ili nywele zibakie kwa ajili ya kunyoa wakati wa Hajj, kwa sababu Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) aliwaamrisha Maswahaba kukata nywele katika 'Umrah kwani walifanya asubuhi ya tarehe nne ya Dhul-Hijjah.

 

Baada ya hapo 'Umrah itakuwa imemalizika na Hajji atakuwa huru kuvaa nguo nyingine, kutia manukato (mwanamume) na kurudia hali ya ndoa (kujimai na mkewe) na kadhalika.

 

 

 

 

***************

 

 

 

 

Hajj:

 

 

Siku Ya Tarwiyyah, Tarehe 8 Dhul-Hijjah 

 

 

Siku ya tarehe 8 Dhul-Hijjah, Hajji atajitoharisha tena kwa kukoga kama alivyofanya kabla ya 'Umrah mahali hapo anapokaa.  Atavaa Ihraam yake na kusema:

 

 لَبَّيْكَ حَجّاً  لَبَّيْكَ اللَّهُمَّ لَبَّيْكَ ، لا شَرِيكَ لَكَ لَبَّيْكَ ،إنَّ الْحَمْدَ ،وَالنِّعْمَةَ ،لَكَ وَالْمُلْكُ ، لا شَرِيكَ لَكَ  

Labbayka Hajja Labbayka-Allaahumma Labbayk, Labbayka, laa shariyka Laka Labbayk, innal-Hamda wan-Ni'mata Laka wal-Mulk, laa shariyka Lak

 

"Nimekuitikia (Ee Allaah) Hajj, Nimekuitika (Ee Allaah) nimekuitika, nimekuitika (ee Allaah) Huna mshirika, nimekuitika (ee Allaah), hakika Himdi na Neema na Ufalme ni Vyako Huna mshirika "

 

 

Ikiwa atakhofu kuwa jambo litamzuia kukamilisha Hajj yake basi atie niyyah kwa kusema:

 وإن حبسني حابس فمحلي حيث حبستني

"Ikiwa nitazuiliwa na kizuizi chochote sehemu yangu ni popote nilipozuiliwa" 

 

Ikiwa hana khofu kama hiyo basi hana haja kujishurutisha hivyo.  

 

Kisha Hajji atakwenda Mina na huko ataswali Swalaah ya Adhuhuri, Alasiri, Magharibi, 'Ishaa na Al-Fajiri na kufupisha Swalaah za Raka'h nne kuwa mbili mbili kila moja bila ya kuziunganisha. (Yaani kuswali kila moja vile kwa wakati wake ila ziwe fupi tu) kwani Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akiswali Qaswran (kufupisha) na sio Jam'an (kujumuisha). 

 

 

 

Tarehe 9 Dhul-Hijjah – Siku ya ‘Arafah

 

Jua litakapochomoza siku ya pili ambayo ni tarehe 9 Dhul-Hijjah, atakwenda 'Arafah na huko ataswali Adhuhuri na Alasiri kwa kuunganisha wakati wa Adhuhuri na kufupisha mbili mbili. Atabakia katika msikiti wa Namirah mpaka jua litakapokuchwa. Atamdhukuru Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)  hapo 'Arafah na kuomba Du'aa nyingi sana awezavyo huku akielekea Qiblah na sio kuelekea Mlima wa 'Arafah.

 

Ikiwa atakuwa hakujaaliwa kuweko katika Msikiti wa Namirah karibu na Jabali la 'Arafah basi popote alipokuweko kwani Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alisimama katika jabali la 'Arafah na akasema:

 

((وقفت هاهنا وعرفة كلها موقف، وارفعوا عن بطن عرنة))

((Nimesimama hapa na 'Arafah yote ni kisimamo (cha 'Arafah) na msisimame katika bonde la 'Uranah))

 

Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akiomba:

 

 لا إِلَهَ إلاَّ اللهُ وَحْدَهُ لا شَريكَ لَهُ، لَهُ المُلْكُ ولَهُ الحَمْدُ وهُوَ عَلَى كُلِّ شَيْءٍ قَديرٌ.

 

 Laa ilaaha iIlla-Allaah Wahdahu laa shariyka Lah, Lahul-Mulku Walahul-Hamd wa Huwa 'alaa kulli shay-in Qadiyr

 

 “Hapana muabudiwa wa haki ila Allaah hali ya kuwa Peke Yake, Hana mshirika, ni Wake Ufalme na ni Zake Himdi, Naye juu ya kila kitu ni Muweza”

 

Atakapochoka anaruhusiwa kuzungumza na wenzake au kusoma vitabu vyenye faida khaswa vile kuhusu ukarimu, utukufu wa Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) na neema kubwa za Allaah kwetu ili apate kuzidi kupata matumaini kutoka kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa). Kisha arudi kuendelea kuomba Du'aa na kuhakikisha kuwa anatumia wakati wake wa mwisho wa siku hiyo katika Du'aa nyingi na nzito kwa sababu Du'aa zilizo bora kabisa ni Du'aa za siku ya 'Arafah. 

 

 

Muzdalifah:

 

Jua litakapozama ataondoka 'Arafah kwenda Muzdalifah na huko ataswali Magharibi, 'Ishaa na Al-Fajiri Ikiwa atachoka au ana uchache wa maji, anaruhusiwa kuunganisha Magharibi na 'Ishaa.  Ikiwa atakhofu kuwa hatofika Muzdalifah mpaka baada ya usiku wa manane, basi aswali kabla ya kufika huko kwani hairuhusiwi kuchelewesha Swalaah mpaka usiku wa manane. 

 

Atabakia huko Muzdalifah akiomba Du'aa na kumtaja Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) mpaka Alfajiri, ataswali Alfajiri mapema kwa adhaan na Iqaamah, kisha ataelekea Mash'aril-Haraam (sehemu tukufu) na atafanya tahliyl, yaani atasema "Laa ilaaha illa Allaah" pia "Allaahu Akbar" na ataomba Du'aa mpaka kupambazuke vizuri. Ikiwa hakujaaliwa kwenda Mash'aril-Haraam, ataomba hapo hapo alipo kutokana na kauli ya Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam):

((وقفت هاهنا وجمع كلها موقف)) 

((Nimesimama hapa na kote hapa ni kisimamo (cha Muzdalifah)) [Muslim]

 

Na atakuwa akiomba Du'aa kwa kuelekea Qiblah na huku akinyanyua mikono. 

 

 

      

Minaa – Ar-Ramiy (Krusha vijiwe) Katika Jamrah

 

 

 

Ikiwa ni mtu dhaifu na hawezi kustahamili  zahma za watu wakati wa Ar-Ramiy (kurusha vijiwe), (kama mwanamke na mtu mzima), basi anaruhusiwa kwenda Minaa mwisho wa usiku huo kupiga Jamrah kabla ya zahma ya watu kuwa kubwa.  

 

 

 

Tarehe 10 Dhul-Hijjah:

 

 

Karibu na jua kuchomoza Hujaji ataondoka Muzdalifah kuelekea Minaa. Atakapofika atafanya yafuatayo:

 

 

 

Atarusha vijiwe saba moja moja katika Jamrah ya 'Aqabah ambayo iko karibu na mnara wa Makkah na kusema :

الله أَكْبَر

Allaahu Akbar

 

Kwa kila kijiwe anachokirusha. 

 

 

Atachinja mnyama, na kula baadhi ya nyama na atatoa nyingine kuwapa masikini. Kuchinja ni fardhi kwa wale wanaofanya Hajj ya Tamattu'u na Qiraan. (Kwa hali ilivyo sasa huwa haiwezekani kufanya hivi, hivyo anaweza kutekeleza kama anavyoamrishwa yaani kulipa na kuacha jukumu hili kwa serikali ifanye kazi ya kuchinja) 

 

  

 

Atanyoa au kukata nywele. Inapendekezwa kunyoa kuliko kukata (kama alivyosema Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) katika maelezo ya 'Umrah hapo juu). Mwanamke atakata nywele zake urefu wa ncha ya kidole.

 

 

Mambo matatu hayo yafanywe kama ilivyo taratibu yake ikiwezekana, lakini hakuna kikwazo au sharti ikiwa mtu atatanguliza kitendo chochote kabla ya chengine.

 

Akimaliza hayo mambo matatu anaruhusiwa kujitoa katika Ihraam. Na anaweza kuvaa nguo zake za kawaida na kufanya kila jambo la halaal ila kuingia katika kitendo cha ndoa.   

 

Atakwenda Makkah kufanya Twawwaaful-Ifaadhwah na Sa’yi kwa ajili ya Hajj. Ni Sunnah kujitia manukato kabla ya kwenda Makkah (kwa wanaume) kutokana na kauli ya ‘Aaishah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) kwamba:

 

((كنت أطيب النبي صلى الله عليه وسلم لإحرامه قبل أن يحرم، ولحله قبل أن يطوف بالبيت )) البخاري و مسلم

((Nilikuwa nikimpaka manukato Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)  kabla ya kuingia katika Ihraam na na baada ya kutoka katika Ihraam kabla ya kutufu Ka'aba)) [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

Atakapomaliza Twawwaaf na Sa’yi, Hujaji anaruhusiwa kufanya kila kitu kilicho halali hata tendo la ndoa. 

 

 

 

Tarehe 11 na 12 Dhul-Hijjah:

 

 

Baada ya kufanya Twawwaaf na Sa’yi atarudi Minaa kulala huko usiku wa tarehe kumi na moja na wa kumi na mbili Dhul-Hijjah.

 

Atarusha vijiwe Jamrah tatu jioni zote za siku ya tarehe kumi na moja na kumi na mbili Dhul-Hijjah. Ataanza kwanza Jamrah ya kwanza ambayo iko mbali na Makkah, kisha ya katikati, kisha ya mwisho Jamrah Al-Aqabah. 

 

Katika kila moja ya Jamrah atarusha vijiwe saba moja moja na huku atasema Takbiyr kwa kila kijiwe anachokirusha.

 

Atasimama baada ya kurusha vijiwe Jamrah ya kwanza na ya katikati kufanya Du'aa akielekea Qiblah akiwa amenyanyua mikono na kuomba Du'aa ndefu akiweza kufanya hivyo, au asimame kadiri atakavyoweza. Wala haimpasi kuacha kuomba Du'aa kwani ni Sunnah na watu wengi sana hawatekelezi hivi aidha kwa kutokujua au kupuuza. Na kila inapokuwa Sunnah haitekelezwi huwa kutangazika kwake kwa watu na kutendeka huenda ikaachwa kabisa na kupotea. 

  

Hairuhusiwi kurusha vijiwe kabla ya Adhuhuri katika siku mbili hizi. 

 

Ni bora kabisa kutembea kwenda kurusha vijiwe, ingawa kipando kinaruhusiwa. 

 

Ikiwa mtu ana haraka baada ya kurusha vijiwe siku ya kumi na mbili Dhul-Hijjah, anaweza kuondoka Minaa lakini iwe kabla ya jua kuzama. Lakini akipenda kuzidisha makazi yake, ambayo ni bora zaidi, basi alale Minaa usiku wa kumi na tatu na arushe mawe jioni kama alivyofanya siku ya kumi na mbili.

 

 

 

Twawaaful-Widaa’ (Twaaf Ya Kuaga):

 

Atakapokuwa tayari kurudi kwao, atafanya twawwaaful-Widaa' ambayo ni mizunguko saba katika Ka'abah kutokana na kauli ya Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam):

 

((لا ينفر أحد حتى يكون آخر عهده بالبيت ((مسلم

((Asikimbie mtu (asiondoke zake) mpaka iwe shughuli yake (kitendo chake cha mwisho) katika Nyumba (Ka'abah)) [Muslim]

 

Wanawake wenye hedhi na nifaas hawana lazima kufanya Twawwaaful-Widaa'i kama ilivyo katika Hadiyth ifuatayo:

 

((أمر الناس أن يكون آخر عهدهم بالبيت إلا أنه خفف عن الحائض)) البخاري و مسلم

((Aliamrisha watu iwe shughuli zao za mwisho ni Ka'abah isipokuwa waliruhusiwa (wanawake) wenye hedhi)). [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

Ikiwa baada ya twawwaaful-Widaa'i umebakia wakati wa kusubiri wenzake au kipando chake au kununua kitu njiani hakuna neno juu yake, wala hana haja ya kurudia kufanya Twawwaaful-Widaa'i isipokuwa akitia niyyah ya kuchelewesha safari yake, mfano akitaka kuondoka mwanzo wa siku akatufu Ka'abah, kisha akachelewesha safari yake hadi mwisho wa siku, basi itamlazimu arudie kufanya Twawwaaf ili kiwe kitendo chake cha mwisho ni Ka'abah.

 

 

 

****************

 

 

 

 

Kutemebele Msikiti Wa Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam):

 

 

 

Hajji atakwenda Madiynah kabla au baada ya Hajj kwa niyyah ya kutembelea msikiti wa Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na kuswali humo na sio  kwa niyyah ya kutembelea kaburi kutokana na Hadiyth ya Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam):

 

((لا تشد الرحال إلا إلى ثلاثة مساجد: المسجد الحرام، ومسجدي هذا، والمسجد الأقصى)) البخاري ومسلم

 

((Msifanye ziara ila kwa misikiti mitatu; Masjidul-Haraam [wa Makkah], na Msikiti wangu [wa Madiynah], na Masjidul-Aqswaa [wa Palestina])) [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

Swalaah moja humo ni bora kuliko Swalaah elfu mahali pengine isipokuwa msikiti wa Makkah.

 

 

Anapofika msikitini atatanguliza mguu wa kulia na kusema:

 

 أعوذ بالله العَظيـم وَبِوَجْهِـهِ الكَرِيـمِ وَسُلْطـانِهِ القَدِيـمِ مِنَ الشّيْـطانِ الرَّجِـيمِ،[ بِسْـمِ الله، وَالصَّلاةُ] [وَالسَّلامُ عَلى رَسولِ الله]، اللّهُـمَّ افْتَـحْ لي أَبْوابَ رَحْمَتـِكَ

 

A'uwdhu BiLLaahil-'Adhwiym, wa Biwajhihil-Kariym wa Sultwaanihil-Qadiym minash-shaytwaanir-rajiym, BismiLLaahi wasw-Swalaatu was-Salaam 'alaa Rasuli-LLaah, Allaahuumaf-tah-liy abwaaba Rahmatik.

 

“Najilinda na Allaah Aliye Mtukufu, na kwa Wajihi Wake, mtakatifu, na kwa utawala Wake wa kale, kutokana na shatywaan aliyeepushwa na Rahma za Allaah, (kwa Jina la Allaah na Swalaah) (Na salaam zimfikie Rasuli wa Allaah) Ee Allaah nifungulie milango ya Rahmah Zako"

 

Anatakiwa aswali Raka'ah mbili za Sunnah ya kuamkia msikiti au aswali Swalaah za fardhi ikiwa ameingia katika wakati wake.

 

Atakwenda katika kaburi la Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na atasimama mbele yake, atamsalimia kwa kusema:

 

 السَّلاَمُ عَلَيْكَ أَيُّها النَّبِيُّ وَرَحْمَةُ اللَّهِ وَبَرَكَاتُه  

 

Amani zishuke juu yako ee Nabiy na rahmah za Allaah na baraka Zake

 

 اللّهُـمَّ صَلِّ عَلـى مُحمَّـدٍ  وَعَلـى آلِ مُحَمَّد كَمـا صَلَّيْـتَ عَلـى آلِ إبْراهـيم  وَعَلـى آلِ إبْراهـيم إِنَّكَ حَمـيدٌ مَجـيد

 

   اللّهُـمَّ  بارِكْ عَلـى مُحمَّـدٍ  وَعَلـى آلِ مُحَمَّد  كَمـا بارِكْتَ عَلـى  إبْراهـيم وَعَلـى آلِ إبْراهـيم  إِنَّكَ حَمـيدٌ مَجـيد

 

Allaahumma Swalliy 'alaa Muhammad wa 'alaa aali Muhammad kamaa Swallayta 'alaa Ibraahiym wa 'alaa aali Ibraahiym Innaka Hamiydun-Majiyd. 

 

Allaahumma Baarik 'alaa Muhammad wa 'alaa aali Muhammad kamaa Baarakta 'alaa Ibraahiyma wa 'alaa aal Ibraahiym Innaka Hamiydun-Majiyd.

 

“Ee Allaah Mswalie Muhammad, na aila ya Muhammad kama Ulivyomswalia Ibraahiym na aila ya Ibraahiym hakika Wewe Umesifika na Umetukuka"

 

"Ee Allaah Mbariki Muhammad, na aila ya Muhammad, kama ulivyombariki Ibraahiym na aila ya Ibraahiym, hakika Wewe Umesifika na Umetukuka.

 

أشْهَد أنَّكَ رَسُولُ الله حَقاً، وَأنَّكَ قَدْ بَلَّغْتَ الرِّسَالَةَ، وَأدَّيْتَ الأَمَانَةَ، وَنَصَحْتَ الأُمَّةَ، وَجَاهَدْتَ فِي اللهِ حَقَّ جِهَادِه، فَجَزاكَ اللهُ عَنْ أُمَّتك أَفْضَل ما جَزَى نَبِيَّا عَنْ أُمَّتِه.

 

Ash-hadu Annaka Rasuwlu-Allaah haqqan, wa Annaka qad ballaghtar-Risaalah, wa addaytal-amaanah, wa naswahtal-Ummah, wa jaahadta fil-Llaahi haqqa jihaadih, fa-Jazaaka-Allaahu 'an Ummatika afdhwal Maa jazaa Nabiyyan 'an Ummatih

 

"Nashuhudia kwamba wewe hakika ni Rasuli wa Allaah, Na kwamba umefikisha ujumbe, na umefikisha amana. Na umenasihi Ummah, na umefanya jihaad kwa njia ya Allaah ipasavyo hakika, basi Allaah Akulipe kwa Ummah wako bora kuliko Alivyomlipa Nabiy (yeyote) kwa Ummah wake"

 

Kisha atasogea hatua moja au mbili upande wa kulia kujiweka mbele ya Abu Bakar na kumsalimia kwa kusema :

 السَّلاَمُ عَلَيْكَ

Assalaamu 'alayka

 

"Amani zishuke juu yako"

 

Na akipenda amuombee Du'aa munaasib kama kusema:

 

رَضِيَ اللَّهُ عَنْكَ وَجَزَاكَ اللَّهُ  عَنْ أُمَّة مُحَمَّد  أَفْضَل جَزَاء

 

Radhiya-Allaahu 'anka wa Jazaaka-Allaahu 'an Ummati Muhammad afdhwal jazaa

 

"Allaah Aridhike na wewe na Akulipe malipo bora kwa niaba ya Ummah wa Muhammad" 

 

Kisha asogee hatua moja au mbili upande wa kulia kidogo na kuelekea kwa 'Umar na kumsalimia kwa kusema:

 

السَّلاَمُ عَلَيْكَ

Assalaamu 'alayka

 

"Amani zishuke juu yako"

 

رَضِيَ اللَّهُ عَنْكَ وَجَزَاكَ اللَّهُ  عَنْ أُمَّةَ مُحَمَّد  أَفْضَل جَزَاء

 

Radhiya-Allaahu 'anka wa Jazaaka-Allaahu 'an Ummati Muhammad afdhwal jazaa

 

"Allaah Aridhike na wewe na Akulipe malipo bora kwa niaba ya Ummah Wa Muhammad"

 

Haifai mtu kujikurubisha kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kwa kugusa ukuta wa chumba cha Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) au kufanya twawwaaf (kuzunguka). Pia haelekei mtu huko bali anaelekea Qiblah wakati wa kuomba Du'aa.  Kwa sababu kujikurubisha kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) haiwi ila kama Alivyotuwekea shariy’ah Yeye pamoja na Rasuli Wake (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na ‘ibaadah zinatakiwa zifuatwe sio zianzishwe.

 

Na mwanamke haimpasi kuzuru kaburi la Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) wala kaburi la yeyote mwingine kwa sababu Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amelaani wanawake wanaozuru makaburi. Lakini aswali na kumsalimia mahali hapo hapo alipo kwani zinamfikia salamu kama alivyosema:

 

)) صلوا علي فإن صلاتكم تبلغني حيث كنتم" وقال: "إن لله ملائكة سياحين في الأرض يبلغوني من أمتي السلام((  النسائي و أحمد

 

((Niswalieni kwani Swalaah zenu zinanifikia popote mlipo. Na akasema: ''Hakika Allaah Anao Malaika wanazunguka katika ardhi na kunitumia salamu kutoka kwa ummah wangu'')) [An-Nasaaiy na Ahmad]

 

 

Akiwa Katika hali ya Twahaarah atakwenda kuswali katika Msikiti wa Qubaa.

 

 

Atakwenda Al-Baaqiy'i kutembelea kaburi la 'Uthmaan (Radhwiya Allaahu ‘anhu) atasimama mbele yake na kumsalimia kwa kusema:

 

السَّلاَمُ عَلَيْكَ

Assalaamu 'alayka

 

"Amani zishuke juu yako"

 

رَضِيَ اللَّهُ عَنْكَ وَجَزَاكَ اللَّهُ  عَنْ أُمَّةَ مُحَمَّد  أَفْضَل جَزَاء

 

Radhiya-Allaahu 'anka wa Jazaaka-Allaahu 'an Ummati Muhammad afdhwal jazaa

 

"Allaah Aridhike na wewe na Akulipe malipo bora kwa niaba ya Ummah Wa Muhammad" 

 

Kisha atawasalimia Waislamu wengine waliofariki waliopo hapo makaburini Al-Baaqiy'i kwa kusema:

 

السَّلامُ عَلَـيْكُمْ أَهْلَ الدِّيارِ مِنَ المؤْمِنيـنَ وَالْمُسْلِمينَ، وَإِنّا إِنْ شاءَ اللهُ بِكُـمْ لاحقون، ( وَ يَرْحَمُ اللَّهُ الْمُسْتَقْدِمِينَ مِنَّا وَالْمُسْتَأْخِرِينَ) نَسْـاَلُ اللهَ لَنَـا وَلَكُـمُ العَـافِيَةَ.

 

Assalaamu 'alaykum ahlad-diyaari minal-Muuminiyna wal-Muslimiyn, wa In Shaa-Allaah bikum laahiquwn, wayarhamu Allaahu ahul-mustaqdimiyna minnaa walmusta-akhiriyn) nas-alu-Allaaha lanaa wa lakumul-'aafiyah

 

Amani ishuke juu yenu watu wa nyumba za Waumini na Waislamu, nasi Apendapo Allaah tutakutana nanyi, [Na Allaah Awarehemu wa mwanzo na wa mwisho] namuomba Allaah Atupe sisi nanyi Al-‘Aafiyah (afya, salama, amani kutokana na kila ovu na shari)”    

 

 

Atakwenda Uhud na kutembelea kaburi la Hamza (Radhwiya Allaahu 'anhu), pamoja na Mashuhadaa waliozikwa hapo.  Atawatolea salaam  na kuwaombea hivyo hivyo Du'aa ya kuzuru makaburi.

 

 

Tanbihi Muhimu: 

 

 

Zifuatazo ni Tanbihi muhimu kwa mwenye kufanya Hajj au 'Umrah

 

 

1

Ajishurutishe katika fardhi za Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) za dini zinazompasa kama kuswali kwa wakati wake na kuswali Jama'ah

 

2

Ajiepusha na yote yaliyoharamishwa kama uchafu, dhulma, utovu wa adabu kama Anavyosema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

 الْحَجُّ أَشْهُرٌ مَّعْلُومَاتٌ ۚ فَمَن فَرَضَ فِيهِنَّ الْحَجَّ فَلَا رَفَثَ وَلَا فُسُوقَ وَلَا جِدَالَ فِي الْحَجِّ ۗ  

Hajj ni miezi maalumu. Na atakayekusudia kuhiji (akahirimia), basi asifanye tendo la ndoa wala ufasiki wala mabishano katika Hajj.   [Al-Baqarah: 197]

 

3

Ajiepushe na kuwadhuru Waislamu wenziwe kwa maneno au vitendo katika sehemu tukufu na kwengine kote.

 

 

4

Ajiepushe na yote aliyozuiliwa kufanya katika Ihraam kama yafuatayo:

 

 

Kwa Hajji wa kiume na wa kike

 

a) Asikate nywele. Hapana ubaya kukuna kichwa au kuchana nywele na ikiwa zitatoka kwa ajili hiyo hakuna ubaya. 

 

b) Asikate kucha. Ikikatika kucha na ikiwa inamuudhi hakuna ubaya kuikata.

 

c) Asijitie manukato mwilini, au katika nguo zake baada ya kuingia katika Ihraam. Ama kabla ya Ihraam inafaa (kama ilivyoelezwa mwanzo). Vile vile katika chakula kama kutia zaafarani kwani zaafarani ni katika harufu nzuri. Vilevile ajiepushe na kuoga sabuni iliyo na manukato.  Hakuna ubaya ikiwa manukato aliyotia kabla ya Ihraam yamebakia katika nguo zake.

 

d)  Asimguse na kumbusu mke/mume wake kwa hamu na baya zaidi asifanye naye jimai (kitendo cha ndoa).

 

e) Asifunge Nikaah (Ndoa) au kupeleka posa kwa mwanamke kwa ajili yake au mwenzake.

 

f)  Asivae glavu, lakini hakuna ubaya kufunika mikono yake kwa nguo yake.

 

 

Tanbihi kwa Hajjah mwanamume pekee:

 

 

 

a) Asivae nguo zilizoshonwa kama fulana, shati, suruwali, soksi, viatu na kadhalika ila tu ikiwa hakuweza kupata Izaar na makubadhi au malapa ndio anaweza kuvaa suruwali na viatu.   Anaruhusiwa kuvaa saa, miwani visaidizi vya kusikia au kuzungumzia.

 

b)  Haifai kujifunika kichwa kama kuvaa kofia, kilemba, ghutra na kadhalika. Ama kujifunika mwavuli kwa ajili ya kujihifadhi jua hakuna ubaya. Pia hakuna ubaya akibeba begi lakekichwani.

 

 

 

Tanbihi kwa mwanamke pekee:

 

 

 

a) Asivae niqaab na glavu.  Kuna ‘Ulamaa waliosema kuwa haifai kujifunika uso wake kwa niqaab au chochote kingine ila kama kuna wanaume karibu yake, basi inambidi ajifunike uso wake (kuepusha fitna) na hatakiwi kulipa fidia akifanya hivyo.

 

 

 

Wa Swalaatu was-Salaam ‘alaa Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na ahli zake na Maswahaba zake.

 

 

 

 

Faharasa

 

 

 

Al-Baaqiy'i

Sehemu Madiynah ambako kuna makaburi ya Maswahaba

 

Al-Idhwtiba'a

Kuweka sehemu ya katikati ya shuka (Ridaa) Chini ya kwapa ya mkono wa kulia na ncha zake juu ya bega la mkono wa kushoto katika twawwaaf

 

Al-Ikhlaas

Suwrah Namba 112 katika Qur-aan.   

 

Al-Kaafiruwn

Surah Namba 109 katika Qur-aan.  

 

Al-Marwah

 

Jina la kilima ambako Muislamu anaanza Sa’yi.

Ar-Raml

Kwenda mwendo wa mbio mbio kwa hatua ndogo ndogo katika mizunguko mitatu ya mwanzo kwenye twawwaaf

 

'Arafah

Sehemu muhimu kabisa ya kusimama katika Hajj iliyoko baada ya Muzdalifah

 

Ar-Ramiy

Kurusha vijiwe

 

As-Swafaa

Jina la kilima ambako Muislamu anamalizia Sa’yi yake ya mwisho

 

Dhul-Hijjah

Mwezi wa kumi na mbili katika kalenda ya Kiislamu

Hajar Al-Aswad

Jiwe Jeusi lililoko pembeni mwa Ka'abah

 

Hajji

Mwanaume mwenye kutekeleza fardhi ya Hijjah huko Makkah

 

Hajjah

Mwanamke mwenye kutekeleza fardhi ya Hijjah huko Makkah

 

Hamzah

'Ami yake Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam aliyekufa Shahiyd katika vita vya Uhud.

 

Hedhi

Damu anayopata mwanamke kila mwezi

 

Ifraad

Aina ya Hajj ya iliyo pekee

 

Ihraam

Hali ya kuingia katika tendo la kufanya ‘ibaadah ya Hajj, au pia nguo za Hajj zinaitwa hivyo.

 

 Jamrah

 

Mnara katika Minaa

Jamrah Al-Aqabah

Mnara ulio karibu na Makkah

 

Ka'abah

 

Nyumba tukufu iliyoko katika msikiti mtukufu wa Makkah.

Maqaamu Ibrahiym

Jiwe alilokanyaga Nabiy Ibraahiym na kusimama kuomba Du'aa baada ya kujenga Ka'abah

 

Mas-'aa

Sehemu iliyonyooka baina ya Swafaa na Marwah

 

Minaa

Bonde karibu na Makkah na mahali patukufu wanapokwenda kulala wanaofanya Hijjah kutekeleza baadhi ya vitendo vya fardhi (za) Hijjah.

 

Muzadalifah

Sehemu tukufu wanapolala waislamu katika ’ibaadah ya Hajj, ipo baina ya 'Arafah na Minaa

 

Namirah

Msikiti uliopo 'Arafah.  

 

Nifaas

 

Damu ya uzazi

Niqaab

Kifuniko cha uso wanachovaa wanawake waislamu

 

Qiraan

 

Aina ya Hajj ya kusindikizwa.

 

Qubaa

Msikiti wa mwanzo waliojenga waislamu pamoja na Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) walipoingia Madiynah kutoka Makkah pamoja na  

 

Ridaa

Sehemu ya nguo (shuka) ya juu wanayovaa wanaume katika Ihraam

 

 

Rukn Al Yamaani

Pembe katika Ka'abah inayoelekea Yemen.

 

Sa’yi

 

Kutembea baina ya Swafaa na Marwah

Sunnah

Mwenendo wa Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) katika kauli na matendo, au pia Hadiyth za Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam). 

 

 

Takbiyr

 

Kusema Allaahu Akbar (Allaah Mkubwa)

Talbiyah

Du'aa ya Muislamu anayosema anapoingia katika Ihraam baada ya kutia Nia.

 

 Tamattu'

Aina ya Hajj ya kustarehe (mapumziko)

 

Tarwiyyah

Tarehe nane ya Dhul-Hijjah

 

Twawwaaf

Mzunguko katika Ka'abah

 

Twaaful-Ifaadhwah

Twawwaaf ya Hajj ambayo ni moja ya fardhi katika taratibu za Hijjah.

 

Twawwaaful-Widaa'

Twawwaaf ya kuaga

 

Uhud

Mlima ulioko Madiynah umeitwa hivyo kutokana na vita vilivyotokea hapo.

 

'Umrah

Hijjah ndogo inayofanywa kwa twawwaaf na Sa’yi pekee.

 

 

 

 

Share