Wasia Muhimu Kwa Hujaji

 

Wasia Muhimu Kwa Hujaji

 

 Imekusanywa na: Ummu Faraj

 

Alhidaaya.com

 

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Rabb wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Aali zake na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho. Ammaa ba’ad:

  

1.    Unatakiwa kuwa karibu na watu wema na wenye elimu ili uweze kufaidika nao katika mambo yanayo husu Hijjah.

 

2.    Kujizoesha subira, na kuvumilia pale utakapoudhiwa, na kutokuwaudhi ndugu zako na kutolipiza mabaya bali ufanye wema.

 

3.  Kujiweka mbali na uongo, udanganyifu, kuiba, kusengenya, kufitinisha na istihzai (kuwacheza shere watu na kuwadharau).

 

4.     Kujihadhari na kuwagusa wanawake kwa makusudi, kuwaangalia, na uwastiri wanawake wako uliofatana nao (wavae hijabu zao vizuri itakiwavo na shari’ah) pindi kunapokuwa na wanaume.

 

5.    Kuwa mpole wakati wa kuuza na kununua, kutoa kauli nzuri bila kuzozana na matendo yako yawe ni mazuri mpaka Allaah Akurehemu.

 

6.      Kutumia mswaki kwani kunamridhisha Allaah. Kasema Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam):

 

“Kupiga mswaki kunatwaharisha mdomo na kunamridhisha Rabb Mtukufu”. [Imepokewa na Al-Bukhaariy]

 

7.    Na uchukue zawadi pamoja na tende, maji ya zamzam; Amesema Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)

 

“Maji ya zamzam ni kwa ile Niyyah uliyonywea” [Sahihi imepokewa na Ahmad]

 

8.     Jihadhari na uvutaji sigara, kwa sababu inadhuru afya na kuwaudhi walio karibu yako pia kupoteza mali, kwa kufanya hivyo ni haramu kwa kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)

 

وَيُحِلُّ لَهُمُ الطَّيِّبَاتِ وَيُحَرِّمُ عَلَيْهِمُ الْخَبَائِثَ

Na anawahalalishia vizuri na anawaharamishia maovu, [Al-A’raaf: 157]

 

9.    Ndevu ni pambo la wanaume, basi jihadhari na kuzinyoa usije ukavunja amri ya Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)Amesema Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam):

 

“Kateni masharubu na fugeni ndevu kutofautiana na Majuus”. [Imepokewa na Muslim]

 

(Majuus (waabudu moto) ni watu wakisifika kwa tabia mbovu wakati wa Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam).

 

10.  Kukithirisha sana kusoma Qur-aan tukufu na kuzingatiya pamoja na kuyafanyia kazi yaliyokuwemo ndani ya Qur-aan, na kumtaja Allaah kwa wingi, kuomba duaa, swala na kusikliza durusu zenye faida.

 

11.   Usiache kuamrisha mema na kukataza maovu lakini basi kwa hikma na mawaidha mazuri pamoja na upole na maneno laini.

 

12.   Pindi utakapoona mijadala isiyokuwa na faida basi achana nayo hata wewe ukiwa katika haki, kwani kuna watu waovu hutafuta sababu au wapate nafasi ya kuitukana Dini si kwa ujinga kwamba wanauliza ili wajue bali ni ubishi wa dhaahir hata akipewa dalili ya sawa bado kang'ang'ana, kwa namna kama hiyo Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amekataza; kwa kauli yake (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam):

 

“Mimi nitamdhamini nyumba katikati ya pepo kwa yule mtu atakaye cha mijadala hata ikiwa yuko katika haki.” [Sahihi imepokewa na Abu Daawuwd]

 

13.   Harakisha kufanya Hijjah pindi tu pale utapokuwa na mali ya kutosha kwenda na kurudi huko, wala usifikirie matumizi baada ya Hijjah kama vile zawadi n.k. ukaacha kwenda Hijjah hali uwezo wakwenda na kurudi unao lakini ukafikiria nikirudi nitatumia nini au sina pesa ya kununua zawadi wakati Allaah hakubali udhuru huo.

 

Basi fanya haraka kabla hujakuwa mgonjwa au kuishiwa na mali au kufa hali yakuwa uko katika maaswi, kwa sababu Hijjah ni nguzo miongoni mwa nguzo za Kiislamu, na ndani yake kuna faida kubwa katika dunia na Aakhirah.

 

14.    Muhimu kabisa ni kujikurubisha na kujilazimisha katika kila matatizo kwa Allaah peke Yake, kumuomba Yeye pasipo mungu mwengine, kama Alivyosema Allaah:

 

قُلْ إِنَّمَا أَدْعُو رَبِّي وَلَا أُشْرِكُ بِهِ أَحَدًا﴿٢٠﴾

Sema: (ee Muhammad صلى الله عليه وآله وسلم): Hakika mimi namuomba Rabb wangu na wala simshirikishi na yeyote. [Al-Jinn: 20]

 

15.   Ukumbuke nawe ukiwa Makkah kwamba Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alikaa Makkah muda wa miaka kumi na tatu (13) akiwaita watu katika kumpwekesha Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala).

 

(Tawhiyd: Laa Ilaaha Illa Allaah) Na maana yake: Hakuna apasae kuabudiwa kwa haki isipokuwa Allaah peke Yake. Na kwa hakika hiyo Tawhiyd ni itikadi sahihi anayo itakidi mtu kwamba Allaah yuko juu ya ‘Arshi.

 

Kama Alivyosema Allaah:

الرَّحْمَـٰنُ عَلَى الْعَرْشِ اسْتَوَىٰ ﴿٥﴾

Ar-Rahmaan; Yuko juu (Istawaa) ya ‘Arsh. [Twahaa: 5]

 

16.    Imekatazwa kwa Mwanamke kusafiri kwenda Hijjah bila ya kuwa na Mahrim au awe na mumewe (Mahrim, ni ndugu anayemuhusu mwanamke kwa karibu zaidi katika wanaume, mfano: Mwanamume ambae ni haramu kumuoa).

 

Kwa kauli ya Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam):

 

Amesema:

 

 

“Wala asisafiri mwanamke isipokuwa awe na Mahrim”

 

Share