075 - Al-Qiyaamah

 

   الْقِيَامَة

 

075-Al-Qiyaamah

 

075-Al-Qiyaamah: Utangulizi Wa Suwrah

 

Alhidaaya.com

 

 

بِسْمِ اللَّـهِ الرَّحْمَـٰنِ الرَّحِيمِ

 

 

 

لَا أُقْسِمُ بِيَوْمِ الْقِيَامَةِ﴿١﴾

1. Naapa kwa Siku ya Qiyaamah.[1]

 

 

 

وَلَا أُقْسِمُ بِالنَّفْسِ اللَّوَّامَةِ﴿٢﴾

2. Na Naapa kwa nafsi inayojilaumu sana.[2]

 

 

 

أَيَحْسَبُ الْإِنسَانُ أَلَّن نَّجْمَعَ عِظَامَهُ﴿٣﴾

3.  Je, anadhani binaadam kwamba Hatutoikusanya mifupa yake?[3]

 

 

 

 

بَلَىٰ قَادِرِينَ عَلَىٰ أَن نُّسَوِّيَ بَنَانَهُ﴿٤﴾

4. Sivyo hivyo! Bali Tuna Uwezo wa kusawazisha sawasawa ncha za vidole vyake.

 

 

 

بَلْ يُرِيدُ الْإِنسَانُ لِيَفْجُرَ أَمَامَهُ﴿٥﴾

5. Bali anataka binaadam aendelee kutenda dhambi na kukanusha umri wake ulobakia.

 

 

 

يَسْأَلُ أَيَّانَ يَوْمُ الْقِيَامَةِ﴿٦﴾

6. Anauliza ni lini hiyo siku ya Qiyaamah?[4]

 

 

 

فَإِذَا بَرِقَ الْبَصَرُ﴿٧﴾

7. Basi jicho litakapoduwaa.

 

 

 

وَخَسَفَ الْقَمَرُ﴿٨﴾

8. Na mwezi utakapopatwa.[5]

 

 

 

وَجُمِعَ الشَّمْسُ وَالْقَمَرُ﴿٩﴾

9. Na jua na mwezi vitakapojumuishwa.

 

 

 

يَقُولُ الْإِنسَانُ يَوْمَئِذٍ أَيْنَ الْمَفَرُّ﴿١٠﴾

10. Atasema binaadam siku hiyo: Wapi pa kukimbilia?

 

 

 

كَلَّا لَا وَزَرَ﴿١١﴾

11. Laa hasha! Hapana mahali pa kimbilio.

 

 

 

إِلَىٰ رَبِّكَ يَوْمَئِذٍ الْمُسْتَقَرُّ﴿١٢﴾

12. Kwa Rabb wako siku hiyo ndio makazi ya kustakiri.

 

 

 

 

يُنَبَّأُ الْإِنسَانُ يَوْمَئِذٍ بِمَا قَدَّمَ وَأَخَّرَ﴿١٣﴾

13. Siku hiyo binaadam atajulishwa yale aliyoyakadimisha na aliyoyaakhirisha.[6]

 

 

 

بَلِ الْإِنسَانُ عَلَىٰ نَفْسِهِ بَصِيرَةٌ﴿١٤﴾

14. Bali binaadam ni shahidi dhidi ya nafsi yake.[7]

 

 

 

وَلَوْ أَلْقَىٰ مَعَاذِيرَهُ﴿١٥﴾

15. Japo akitoa nyudhuru zake zote.[8]

 

 

 

لَا تُحَرِّكْ بِهِ لِسَانَكَ لِتَعْجَلَ بِهِ﴿١٦﴾

16. Usiutikisie (huu Wahy) ulimi wako ili kuiharakiza (Qur-aan ee Muhammad صلى الله عليه وآله وسلم).[9]

 

 

 

إِنَّ عَلَيْنَا جَمْعَهُ وَقُرْآنَهُ﴿١٧﴾

17. Hakika ni juu Yetu Kuikusanya na Kukuwezesha kuisoma kwake.

 

 

 

فَإِذَا قَرَأْنَاهُ فَاتَّبِعْ قُرْآنَهُ﴿١٨﴾

18. Basi Tunapoisoma (kupitia Jibriyl), fuata kusomwa kwake.

 

 

 

ثُمَّ إِنَّ عَلَيْنَا بَيَانَهُ﴿١٩﴾

19. Kisha ni juu Yetu Kuibainisha (kwako).

 

 

 

كَلَّا بَلْ تُحِبُّونَ الْعَاجِلَةَ﴿٢٠﴾

20. Laa hasha! Bali mnapenda uhai wa dunia.

 

 

 

وَتَذَرُونَ الْآخِرَةَ﴿٢١﴾

21. Na mnaiacha Aakhirah.

 

 

 

وُجُوهٌ يَوْمَئِذٍ نَّاضِرَةٌ﴿٢٢﴾

22.  Nyuso siku hiyo zitanawiri.

 

 

 

إِلَىٰ رَبِّهَا نَاظِرَةٌ﴿٢٣﴾

23. Zikimtazama Rabb wake.[10]

 

 

                                                                      

وَوُجُوهٌ يَوْمَئِذٍ بَاسِرَةٌ﴿٢٤﴾

24. Na nyuso (nyenginezo) siku hiyo zitakunjana.

 

 

 

تَظُنُّ أَن يُفْعَلَ بِهَا فَاقِرَةٌ﴿٢٥﴾

25. Zikiwa na yakini kuwa zitafikiwa na msiba unaovunja uti wa mgongo.

 

 

 

 

كَلَّا إِذَا بَلَغَتِ التَّرَاقِيَ﴿٢٦﴾

26. Laa hasha! Itakapofika (roho) mafupa ya koo.

 

 

 

وَقِيلَ مَنْ ۜ رَاقٍ﴿٢٧﴾

27. Na itasemwa:  Ni nani tabibu wa kumponya?

 

 

 

وَظَنَّ أَنَّهُ الْفِرَاقُ﴿٢٨﴾

28. Na atakuwa na yakini kwamba hakika hivyo ni kufariki.

 

 

 

وَالْتَفَّتِ السَّاقُ بِالسَّاقِ﴿٢٩﴾

29. Na muundi utakapoambatana na muundi.

 

 

 

إِلَىٰ رَبِّكَ يَوْمَئِذٍ الْمَسَاقُ﴿٣٠﴾

30. Siku hiyo ni kuendeshwa na kupelekwa kwa Rabb wako tu.

 

 

 

 

فَلَا صَدَّقَ وَلَا صَلَّىٰ﴿٣١﴾

31. Kwani hakusadiki (Qur-aan na Rasuli) na wala hakuswali.

 

 

 

وَلَـٰكِن كَذَّبَ وَتَوَلَّىٰ﴿٣٢﴾

32. Lakini alikadhibisha na akakengeuka.

 

 

 

ثُمَّ ذَهَبَ إِلَىٰ أَهْلِهِ يَتَمَطَّىٰ﴿٣٣﴾

33. Kisha akaenda kwa watu wake akijigamba.

 

 

 

أَوْلَىٰ لَكَ فَأَوْلَىٰ﴿٣٤﴾

34. Ole kwako! Tena ole kwako (ewe kafiri)!

 

 

 

ثُمَّ أَوْلَىٰ لَكَ فَأَوْلَىٰ﴿٣٥﴾

35. Kisha ole kwako! Tena ole kwako!

 

 

 

 

أَيَحْسَبُ الْإِنسَانُ أَن يُتْرَكَ سُدًى﴿٣٦﴾

36. Je, anadhani binaadam ataachwa huru bila jukumu?

 

 

 

أَلَمْ يَكُ نُطْفَةً مِّن مَّنِيٍّ يُمْنَىٰ﴿٣٧﴾

37. Kwani hakuwa tone kutokana na manii yanayomwagwa kwa nguvu?

 

 

 

ثُمَّ كَانَ عَلَقَةً فَخَلَقَ فَسَوَّىٰ﴿٣٨﴾

38. Kisha akawa pande la damu, (Allaah) Akamuumba na Akamsawazisha?

 

 

 

فَجَعَلَ مِنْهُ الزَّوْجَيْنِ الذَّكَرَ وَالْأُنثَىٰ﴿٣٩﴾

39. Akamfanya namna mbili; mwanamume na mwanamke?

 

 

 

 

أَلَيْسَ ذَٰلِكَ بِقَادِرٍ عَلَىٰ أَن يُحْيِيَ الْمَوْتَىٰ﴿٤٠﴾

40. Je Huyo (Allaah Anayeumba) Si Muweza wa Kuhuisha wafu?![11]

 

 

 

 

[1] Siku Ya Qiyaamah Na Majina Mengineyo Ya Siku Hii Adhimu:

 

Majina ya Siku ya Qiyaamah yamenukuliwa kufikia zaidi ya themanini [Imaam Ibn Kathiyr – An-Nihaayah Al-Fitan Wal-Malaahim]

 

Jina mojawapo ni Al-Qiyaamah ambalo ndilo la Suwrah hii, na limetajwa mara nyingi mno katika Qur-aan. Miongoni mwa Aayah zilizotaja jina hili ni Kauli Yake Allaah (سبحانه وتعالى):

 

قُلِ اللَّـهُ يُحْيِيكُمْ ثُمَّ يُمِيتُكُمْ ثُمَّ يَجْمَعُكُمْ إِلَىٰ يَوْمِ الْقِيَامَةِ لَا رَيْبَ فِيهِ وَلَـٰكِنَّ أَكْثَرَ النَّاسِ لَا يَعْلَمُونَ﴿٢٦﴾

“Sema: Allaah Anakuhuisheni, kisha Atakufisheni, kisha Atakukusanyeni Siku ya Qiyaamah isiyo na shaka ndani yake, lakini watu wengi hawajui.” [Al-Jaathiyah (45:26)]

 

Baadhi ya majina mengineyo ni yafuatayo pamoja na baadhi ya rejea zake:  

 

يوم الآخر – Siku ya Akhirah (Mwisho): An-Nisaa (4:38-39), (4:59), (4:136).

 

السّاعة  - Saa: Al-Hajj (22:1), (22:7), (22:55).

 

 يوم الدِّين - Siku ya malipo: Al-Faatihah (1:4), Al-Infitwaar 82:15,17-18).

 

يوم الحِساب Siku ya hesabu: Swaad (38:16), (38:26), (38:53).

 

يوم البعث – Siku ya kufufuliwa: Ar-Ruwm (30:56).

 

يوم الخُروج – Siku ya kutoka (makaburini) Qaaf (50:42).

 

يوم الفَصل -  Siku ya hukumu na kutenganisha: Al-Mursalaat (77:13-14), (77:38), An-Nabaa (78:17).

 

يوم الجَمع – Siku ya mjumuiko au mkusanyiko: Ash-Shuwraa (42:7), At-Taghaabun (64:9).

 

يوم الوعيد – Siku ya makamio: Qaaf (50:20).

 

يوم المعود  - Siku iliyoahidiwa: Al-Buruwj (85:2)

 

يوم الحسرة – Siku ya majuto: Maryam (19:39).

 

يوم عقيم  - Siku ya ukame: Al-Hajj (22:55)

 

يوم الخُلود –  Siku ya kudumu milele: Qaaf (50:34).

 

يوم ثقيل – Siku nzito: Al-Insaan (76:27)

 

يوم التَّناد – Siku ya kuitana: Ghaafir (40:32).

 

يوم الحقّ – Siku ya haki: An-Nabaa (78:39).

 

 يوم التغابن - Siku ya kupata na kukosa: At-Taghaabun (64:9) 

 

يوم الظيم  - Siku kubwa kabisa au adhimu: Al-An’aam (6:15).

 

يوم كبير - Siku kubwa: Huwd (11:3).

 

يوم اليم  - Siku inayoumiza: Huwd (11:26).

 

يوم محيط  - Siku inayozingira – Huwd (11:84).

 

يوم مشهود – Siku ya kushuhudiwa: Huwd (11:84).

 

يوم الآزفة  - Siku inayokurubia sana: Ghaafir (40:18).

 

يوم عبوس قمطرير  - Siku ya masononeko, ngumu na ndefu mno.

 

[2] Aina Tatu Za Nafsi:

 

Rejea Yuwsuf (12:53) kwenye maelezo.

 

[3] Ukanushaji Wa Makafiri Kuhusu Kufufuliwa Na Kuumbwa Katika Umbo Jipya:

 

Aayah hii namba (3) na zinazofuatia hadi (6) zinataja ukanushaji wa makafiri kutokuamini Siku ya kufufuliwa Siku ya Qiyaamah, na pia Uthibitisho wa Allaah (سبحانه وتعالى) wa kufufua viumbe katika umbo kamilifu hadi alama za vidole vyao, ili kila mtu ajulikane barabara umbo lake aliloumbiwa nalo. Rejea Al-Israa (17:49) kwenye maelezo na rejea mbalimbali. Rejea pia Yaasiyn (77-83).

 

[4] Swali La Makafiri Kuuliza Lini Ahadi Ya Qiyaamah:

 

Makafiri walikuwa wakiuliza kwa istihzai lini ahadi ya Qiyaamah itatokea. Na swali lao hilo limekariri katika Aayah kadhaa. Miongoni mwazo ni ifuatayo:

 

وَيَقُولُونَ مَتَىٰ هَـٰذَا الْوَعْدُ إِن كُنتُمْ صَادِقِينَ﴿٢٥﴾

“Na wanasema: Ni lini hiyo ahadi (ya kufufuliwa), mkiwa ni wasemao kweli?” [Al-Mulk (67:25)]

 

Rejea Yuwnus (10:48) kwenye faida na rejea kadhaa za kauli kama hiyo ya makafiri.

 

[5] Khusuwf Na Kusuwf (Kupatwa Mwezi Na Jua):

 

Aayah hii namba (8) na inayofuatia namba (9) inataja khusuwf (kupatwa kwa mwezi) na kusuwf (kupatwa jua).  

 

Kusuwf ni kupotea mwanga wa jua au mwezi au sehemu ya mwanga na kubadilika kuwa weusi, na Khusuwf ni kisawe chake. Wataalamu wengine wanasema kwamba Kusuwf ni kupatwa jua na Khusuwf ni kupatwa mwezi, na tafsiri hii ndiyo mashuhuri zaidi katika lugha. [Swahiyhh Fiqh As-Sunnah - Lisaan Al-‘Arab, Kash-Shaaf Al-Qinaa (2/60) na Asnaa Al-Matwaalib (1/385)]

 

Mwezi au jua vinapopatwa Waislamu wanatakiwa waswali Swalaah ya Kusuwf. Swalaah ya Kusuwf ni Swalaah inayoswaliwa kwa mtindo maalumu wakati jua au mwezi ukipatwa wote au sehemu. [Mawaahibul Jaliyl (2/199), Nihaayatul-Muhtaaj (2/394) na Kash-Shaaful Qinaa (2/60)]

 

Bonyeza viungo vifuatavyo vyenye faida tele:

 

16-Swahiyh Al-Bukhaariy: Kitabu Cha Al-Kusuwf (Kupatwa Mwezi Au Jua) - كتاب الكسوف

 

032-Swahiyh Fiqh As-Sunnah: Mlango Wa Swalaah: Swalaah Ya Kupatwa Jua (Kusuwf)

 

15-Buluwgh Al-Maraam: Kitabu Cha Swalaah: Mlango Wa Swalaatul-Kusuwf (Swalaah Ya Kupatwa Jua Au Mwezi)

 

[6] Viumbe Watadhihirishiwa Amali Zao Zote Za Kheri Na Za Shari:

 

Miongoni mwa Kauli Zake Allaah (سبحانه وتعالى) ni:

 

يَوْمَئِذٍ يَصْدُرُ النَّاسُ أَشْتَاتًا لِّيُرَوْا أَعْمَالَهُمْ ﴿٦﴾ فَمَن يَعْمَلْ مِثْقَالَ ذَرَّةٍ خَيْرًا يَرَهُ ﴿٧﴾ وَمَن يَعْمَلْ مِثْقَالَ ذَرَّةٍ شَرًّا يَرَهُ ﴿٨﴾

“Siku hiyo watatoka watu makundi mbalimbali wamefarakiana ili waonyeshwe amali zao. Basi yule atakayetenda kheri uzito wa chembe (kama atomu) ataiona. Na yule atakayetenda shari uzito wa chembe (kama atomu) ataiona.” [Az-Zalzalah (99:6-8)

 

Rejea katika Suwrah hiyo kupata rejea nyenginezo.

 

[7] Binaadam Atajishuhudia Mwenyewe Matendo Yake:

 

Makafiri na waliamuasi Allaah (سبحانه وتعالى) Siku ya Qiyaamah watataka kukanusha matendo yao ya kufru na maovu, lakini hakuna atakayeweza kukanusha kwa sababu amali zimehifadhiwa katika rekodi za kila mmoja. Juu ya hivyo, viungo vya mwanaadam vitashuhudia matendo. Rejea Al-Israa (17:13-14) kwenye maelezo na rejea mbalimbali. Rejea pia Yaasiyn (36:65), Fusw-Swilat: (41:20-22), An-Nuwr (24:24).

 

[8] Nyudhuri Za Kujitetea Hazitapokelewa Wala Hazitamfaa Mtu Siku Ya Qiyaamah:

 

Anathitibisha hayo Allaah (سبحانه وتعالى) katika Kauli Zake kadhaa, miongoni mwazo ni Kauli Yake:

 

وَلَا يُؤْذَنُ لَهُمْ فَيَعْتَذِرُونَ﴿٣٦﴾

“Na wala hawatopewa idhini ili watoe nyudhuru.” [Al-Mursalaat (77:36)]

 

Rejea pia Ar-Ruwm (30:57).

 

[9] Sababun-Nuzuwl (Sababu Ya Kuteremshwa) Aayah Au Suwrah:

 

Bonyeza kiungo kifuatacho:  

 

075-Asbaabun Nuzuwl: Al-Qiyaamah Aayah 16-19: لَا تُحَرِّكْ بِهِ لِسَانَكَ لِتَعْجَلَ بِهِ

 

Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم) Alikuwa Ana Pupa Ya Kupokea Wahy Na Kuisoma Qur-aan:

 

Jibriyl (عليه السّلام) alipomjia Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم) na Wahy na akaanza kumsomea (Qur-aan), Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم) aliharakisha kuisoma kwa shauku kabla ya Jibriyl kumaliza kuisoma, na alikuwa anaisoma pamoja naye. [Tafsiyr As-Sa’diy]

 

[10]  ‘Aqiydah Ya Ahlus-Sunnah Wal-Jam’aah Kwamba Waumini Watamuona Allaah (عزّ وجلّ)  Katika Jannah (Peponi):

 

Rejea Yuwnus (10:26) kuna maelezo na dalili bayana. Rejea Al-Mutwaffifiyn (83:15).

 

[11] Kuitikia Subhaanak! Naam! Baada Ya Kusoma Kauli Hii:

 

 

عَنْ مُوسَى بْنِ أَبِي عَائِشَةَ قَالَ : كَانَ رَجُلٌ يُصَلِّي فَوْقَ بَيْتِهِ ، وَكَانَ إِذَا قَرَأَ : (أَلَيْسَ ذَلِكَ بِقَادِرٍ عَلَى أَنْ يُحْيِيَ الْمَوْتَى) قَالَ : سُبْحَانَكَ فَبَلَى . فَسَأَلُوهُ عَنْ ذَلِكَ ، فَقَالَ : سَمِعْتُهُ مِنْ رَسُولِ اللَّهِ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ . صححه الألباني في صحيح أبي داود .

Amesimulia Muwsaa Bin Abiy ‘Aaishah (رضي الله عنه): Mtu mmoja alikuwa akiswali juu ya paa la nyumba yake na aliposoma:

 

أَلَيْسَ ذَٰلِكَ بِقَادِرٍ عَلَىٰ أَن يُحْيِيَ الْمَوْتَىٰ﴿٤٠﴾

“Je Huyo (Allaah Anayeumba) Si Muweza wa Kuhuisha wafu?”

 

Alisema:

سُبْحَانَكَ فَبَلَى

Subhaanaka Fabalaa (Ametakasika Allaah. Naam!)

 

Wakamuuliza kuhusu kusema hivyo, akasema: Nimesikia Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم).  Abuu Daawuwd amesema: Ahmad (Bin Hanbal) amesema: Imenifurahisha kwamba mtu asome katika Swalaah ya fardhi duaa ambazo zimo katika Qur-aan.” [Swahiyh Abiy Daawuwd (884)]

 

 

Share