Surat Yuusuf Ukisoma Inaondosha Wivu? Na Zipi Surah Zilotajwa Fadhila Zake Katika Qur-aan

 

Suwrah Yuwsuf Ukisoma Inaondosha Wivu?

Na Zipi Suwrah Zilizotajwa Fadhila Zake Katika Qur-aan?

 

Alhidaaya.com

 

 

SWALI:

 

Assalam Alleikum Sheikh,

 

Ningependa kama utanielimisha kuhusu faida ya kila surah katika Quran, nilipata forward inayosema faida ya kila surah k.m Surat Yusuf - kuondoa wivu, Suwrah Al-Anfaal - kutimiziwa haja zako n.k Pia inasema kusoma Suwrah Yasin ni kama kusoma Qur-aan 12 na kufanya Hajj 20.

 

Tafadhali nielimishe. Shukran

 

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na Salaam zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Fadhila za Suwrah nyingi zimepatikana kutokana kwa Hadiyth dhaifu au maudhu’ (za kutungwa; za uongo), hivyo kutoweza kutegemewa.

 

Mfano wa fadhila zilizoenea kutajwa, ni za Suwrah Yaasiyn ambazo si sahihi.

 

Ama Suwrah Yuwsuf, Ibn Kathiyr ametaja Hadiyth ya kutoka kwa Ubayy bin Ka’b (Radhwiya Allaahu ‘anhu) ambayo Ibn Kathiyr kaeleza kuwa ni dhaifu, nayo inasema:

 

“Wafundisheni wasichana wenu Suwrah Yuwsuf, kwani hakuna Muislamu atakayeisoma au kumfundisha mkewe au aliyemmiliki kwa mkono wake wa kuume ila Allaah Humpunguzia machungu ya umauti na kumpatia nguvu ya kutomhusudu Muislamu yeyote”. Kisha akasema Ibn Kathiyr: “Na hii (Hadiyth) katika njia hii haisihi kwa sababu ya udhaifu kabisa wa Isnadi yake”.

 

Ama Suwrah Al-Anfaal hatukupata fadhila zake.

 

Zipo Suwrah zenye fadhila zinazofahamika kwa Hadiyth zilizo sahihi kama Suwrah Al- Ikhlaasw, ambapo Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema ni thuluthi ya Qur-aan, kusomwa Suwrah Al-Kahf siku ya Ijumaa kunamuepusha mtu na fitnah za Dajjal n.k.

 

Soma ndani ya kiungo hichi kwa maelezo zaidi:

 

Fadhila Za Surat Yaasiyn Na Al-An'aam

 

Nataka kujua matumizi ya Surah Yaasiyn na Ayatul Kursiy

 

Surat Yaasiyn Inafaa Kumsomea Mtu Anayekata Roho

 

Vijitabu Vya Surat Yaasiyn Na Surah Maalum Za Kusomwa Na Yaasiyn, Vinafaa Kuvitumia?

 

Fadhila Za Suratul-Kahf Surah Namba: 18

 

Surah Saba Ziitwazo Sabaa Munjiyaat Ni Swahiyh Kuzisoma Kila Siku?

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share