34-Fadhila Za Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم): Amekubaliwa Ombi Lake Kutoka Mbingu Ya Saba Kupunguziwa Swalaah Khamsiyn Kwa Ummah Wake

 

Fadhila Za  Nabiy  (صلى الله عليه وآله وسلم)

 

34-Amekubaliwa Ombi Lake Kutoka Mbingu Ya Saba

Kupunguziwa Swalaah Khamsiyn Kwa Ummah Wake

 

www.alhidaaya.com

 

 

Juu ya kuwa Swalaah ni nguzo muhimu kabisa katika nguzo za Kiislamu, na ni msingi wa Dini, na kama alivyosema Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم) kuhusu mtu asiyeswali kwamba mwenye kuiacha amekufuru kwani baina ya mtu na shirki na ukafiri ni Swalaah, lakini Allaah (عزّ وجلّ)  Alimuitikia Nabiy Wake (صلى الله عليه وآله وسلم)  ombi lake la kupunguziwa Ummah wake Swalaah hizo kutoka khamsini kwa siku hadi tano. Na fardhi hii amefaridhishwa nayo Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم)  kutoka mbingu ya saba, jambo ambalo hakuna Nabiy yeyote aliyefadhilishwa kama hivi:

 

 

قالَ أَنَسُ بْنُ مَالِكٍ وَابْنُ حَزْمٍ قَالَ رَسُولُ اللَّهِ صلى الله عليه وسلم ‏ "‏ فَرَضَ اللَّهُ عَزَّ وَجَلَّ عَلَى أُمَّتِي خَمْسِينَ صَلاَةً فَرَجَعْتُ بِذَلِكَ حَتَّى أَمُرَّ بِمُوسَى عَلَيْهِ السَّلاَمُ فَقَالَ مَا فَرَضَ رَبُّكَ عَلَى أُمَّتِكَ قُلْتُ فَرَضَ عَلَيْهِمْ خَمْسِينَ صَلاَةً ‏.‏ قَالَ لِي مُوسَى فَرَاجِعْ رَبَّكَ عَزَّ وَجَلَّ فَإِنَّ أُمَّتَكَ لاَ تُطِيقُ ذَلِكَ ‏.‏ فَرَاجَعْتُ رَبِّي عَزَّ وَجَلَّ فَوَضَعَ شَطْرَهَا فَرَجَعْتُ إِلَى مُوسَى فَأَخْبَرْتُهُ فَقَالَ رَاجِعْ رَبَّكَ فَإِنَّ أُمَّتَكَ لاَ تُطِيقُ ذَلِكَ ‏.‏ فَرَاجَعْتُ رَبِّي عَزَّ وَجَلَّ فَقَالَ هِيَ خَمْسٌ وَهِيَ خَمْسُونَ لاَ يُبَدَّلُ الْقَوْلُ لَدَىَّ ‏.‏ فَرَجَعْتُ إِلَى مُوسَى فَقَالَ رَاجِعْ رَبَّكَ فَقُلْتُ قَدِ اسْتَحْيَيْتُ مِنْ رَبِّي عَزَّ وَجَلَّ ‏"‏ ‏.‏

 

Imepokelewa kutoka kwa Anas bin Maalik na Ibn Hazmi kwamba Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) amesema:  “Allaah (عزّ وجلّ) Amefaridhisha kwa Ummah wangu Swalaah khamsini, nikarudi nikiwa nimezikubali mpaka nikafikia kwa Muwsaa (عليه السلام) akauliza: Rabb wako Amefaridhisha nini kwa Ummah wako? Nikasema: Amewafaridhisha Swalaah khamsini.  Akaniambia: Rudi kwa Rabb wako Allaah (عزّ وجلّ) kwani ummah wako hawataziweza. Nikarudi kwa Rabb wangu Allaah (عزّ وجلّ) Akapunguza idadi fulani nikarudi kwa Muwsaa na kumjulisha akasema: Rejea kwa Rabb wako kwani Ummah wako hawataziweza. Nikarudi kwa Rabb wangu Allaah (عزّ وجلّ) mwisho Akasema: Hizo ni tano lakini (thawabu zake) ni khamsini; Haibadilishwi Kwangu kauli. Nikarudi kwa Muwsaa akasema: Rejea kwa Rabb wako, nikasema: Hakika ninamstahi Rabb wangu Allaah (عزّ وجلّ) [An-Nisaaiy, Ibn Maajah]

 

 

Share