40-Adabu Za Ndoa Katika Sunnah Iliyotakasika: Kukataa Kufanya Mambo Yanayopingana Na Shari'ah

 

   

Anapofanya mtu sherehe ya ndoa, inampasa akatae kuingiza jambo lolote ambalo linalopingana (liloharamishwa) na shari'ah. Hii ni muhimu zaidi kuzingatia khaswa kuhusu ada nyingi ambazo zimekuwa ni mazoea kutendwa na Waislamu katika sherehe za ndoa, na kwa vile Maulamaa wa Kiislamu wamenyamaza kimya hata zikadhaniwa na Waislamu kuwa ni mambo yanayoruhusiwa. Nitazitanabahisha hapa zilizo muhimu katika ada hizo:

 


Kutundika Picha


Imeharamishwa kutundika picha za binaadamu au wanyama katika ukuta. Hakuna tofauti ikiwa ni picha za kuchorwa au za kupigwa au sanamu za kuchongwa zenye kivuli na zisizo na kivuli. Zote hizo ni marufuku. Ni vizuri mtu
kama hawezi japo kuziteketeza basi angalau aziondoshe.
(Shaykh Al-Albaaniy baada ya kutaja kuharamishwa aina zote za picha, zilizochorwa kwa mkono, za kamera au za vinyago, kisha anataja zilizoruhusiwa
kama watoto wa sanamu kama ilivyo katika Hadiyth ya ‘Aaishah رضي الله عنها na vile vile amekubali zile ambazo zinabidi kwa manufaa ya Waislamu mfano; picha za matibabu, picha za majambazi wanaotafutwa na kadhalika).


Kuna Hadiyth mbali mbali kuhusu mas-ala haya:

 
Kwanza:

  عن عائشة رضي الله عنها قالت: دَخَلَ عَلَيَّ رَسُولُ اللّهِ وَقَدْ سَتَرْتُ سَهْوَةً لِي بِقِرَامٍ فِيهِ تَمَاثِيلُ.  ( وفي رواية: فيه الخيل ذوات الأجنحة)  فَلَمَّا رَآهُ هَتَكَهُ وَتَلَوَّنَ وَجْهُهُ وَقَالَ :((يَا عَائِشَةُ! أَشَدُّ النَّاسِ عَذَاباً عِنْدَ اللّهِ، يَوْمَ الْقيَامَةِ، الَّذِينَ يُضَاهُونَ بِخَلْقِ اللّهِ)) ( وفي رواية)

((إنَّ أصحابَ هذه الصُّورَ يُعذَّبُون، ويقال لهم: أحْيُوا ما خَلقتم،))  وقال: ((إن البيت الذي فيه الصُّورَ لا تدخله الملائكة)).  قَالَتْ عَائِشَةُ: فَقَطَعْنَاهُ فَجَعَلْنَا مِنْهُ وِسَادَةً أَوْ وِسَادَتَيْنِ.  [فَقَدْ رَأَيْتَهُ مُتَّكِئاً عَلى إِحْداهُمَا وَفِيهضا صُورَة] 

Kutoka kwa mama wa waumini ‘Aaishah رضي الله عنها ambaye amesema: "Nilifungua pazia la chumba cha hazina ambalo lilikuwa na picha" (katika maelezo mengine: "ambalo lilikuwa lina picha za farasi wenye mbawa"). Mtume صلى الله عليه وآله وسلم alipoliona, alilichana na uso wake ukabadilika kuwa mwekundu kisha akasema, ((Ewe ‘Aaishah, watu watakaopewa adhabu kali kabisa mbele ya Allaah siku ya Qiyaamah ni wale wanaoigiza maumbile ya Allaah)) (katika usemi mwingine) ((Hakika wanaochora picha hizi wataadhibiwa na wataambiwa: Tieni uhai vile mlivyoviumba!)) Mtume صلى الله عليه وآله وسلم akaendelea kusema, ((Hakika Malaika hawaingii nyumba ambayo ina picha)). ‘Aaishah akasema: Tukalikata pazia na tukalitumia kufanyia mto au mito miwili. Nimemuona akiegemea mto mmojawapo uliokuwa na picha"[1]

 


Pili:

عن عائشة رضيَ الله عنها قالت:  حَشَوتُ للنبيِّ صلى الله عليه وسلم وسادةً فيها تماثيُل كأنها نمرُقة، فجاءَ فقام بينَ البابين وجَعلَ يَتغيَّرُ وَجهُهُ، فقلتُ: ما لنا يا رسولَ الله؟  [أَتُوبُ إِلَى الله مِمَّا أَذْنَبْتُ]،  قَال: ((مَا بال هَذهِ ؟)) قُلْت: وِسَادة جَعلتُها لكَ لَتضْطَجِع عليها. قال:(( أما عَلِمْتِ أنَّ الْملائِكَةُ لا تََدْخلُ بَيْتاً فِيهِ صُورَة ؟ وَأنَّ مَنْ صَنَعََ الصُّورَةَ يُعذَّب يومَ القيامةِ فيقال: أحْيُوا ما خلقتم)) وفي رواية :((إنَّ أصحابَ هذه الصُّورِ يُعذَّبونَ يومَ القيامةِ))  [قَالَتْ: فَمَا دَخَل حَتَّى أَخْرَجتْها]    

Kutoka kwa ‘Aaishah رضي الله عنها ambaye amesema: "Niliujaza mto (pamba au sufi) kama wa kuegemea kwa ajili Mtume صلى الله عليه وآله وسلم ambao ulikuwa na picha. Alisimama baina ya milango miwili na uso wake ukabadilika rangi kwa ghadhabu. Nikasema: Nimefanya nini Ewe Mjumbe Wa Allaah? Nimetubu kwa Allaah kwa dhambi zozote nilizofanya. Mtume صلى الله عليه وآله وسلم akasema, ((Mto huu una nini?)) Nikasema: Nimueutengeneza kwa ajili yako ili uegemee. Mtume صلى الله عليه وآله وسلم akasema, ((Hukujua kama Malaika hawaingii katika nyumba ambayo ina picha na kwamba anayetengeneza picha hizi ataadhibiwa siku ya Qiyaamah na ataambiwa, huisha ulivyoviumba?)) (Na katika riwaaya) ((Wenye (kuchora) picha hizi wataadhibiwa siku ya Qiyaamah)). Akasema: Hakuingia hadi nilivyouondosha"[2]

 


Tatu:

قالَ رَسُولُ الله صلى الله عليه وسلم ((أتَانِي جِبْرَائِلُ فقالَ لِي أتَيْتُكَ الْبَارِحَةَ فَلَمْ يَمْنَعْنِي أنْ أكُونَ دَخَلْتُ إلاَّ أنَّهُ كانَ عَلَى الْبَابِ تَمَاثِيلُ وَكَانَ في الْبَيْتِ قِرَامُ سِتْرٍ فِيهِ تَمَاثِيلُ وَكَانَ في الْبَيْتِ كَلْبٌ، فَمُرْ بِرَأْسِ التَّمْثَالِ الَّذِي في الْبَيْتِ يُقْطَعُ فَيَصِيرُ كَهَيْئَةِ الشَّجَرَةِ وَمُرْ بالسِّتْرِ فَلْيُقْطَعْ فَلْيُجْعَلْ مِنْهُ وِسَادَتَيْنِ مَنْبُوذَتَيْنِ تُوطَآنِ ومُرْ بِالْكَلْبِ فَلْيَخْرُجْ،   فَإنَّا لاَ نَدْخُل بيتاً فِيهِ صُورِة وَلاَ كَلْب))  وَإذَا الْكَلْبُ  [جرو]  لِحَسَنٍ أوْ حُسَيْنٍ كانَ تَحْتَ نَضَدٍ لَهُمْ ( وفي رواية: تحت سريره ) فَقَال:  ((يَا عَائِشَةُ مَتَىٰ دَخَلَ هٰذَا الْكَلْبُ هٰهُنَا؟)) فَقَالَتْ: وَاللّهِ مَا دَرَيْتُ. فَأَمَرَ بِهِ فَأُخْرِجَ  (ثم أخذ بيده ماءً فنضح مكانه)

 

Mtume صلى الله عليه وآله وسلم amesema, ((Jibriyl عليه السلام alinijia na akaniambia: Nilikujia jana usiku na kitu pekee kilichonizuia kuingia ndani ni picha (binaadamu, yaani vinyago) katika mlango na pazia na katika nyumba kulikuwa na picha na kulikuweko na mbwa. Kwa hiyo kata kichwa cha picha mpaka kiwe kama ni mti tu, liendee pazia na lifanye mito miwili ya kuikalia na amrisha mbwa aondoshwe. Hakika sisi hatuingii nyumba ambazo zina picha au mbwa)). Mbwa alikuwa ni wa Hasan na Husayn ambaye alijificha chini ya sehemu ya kutundikia nguo. (katika riwaya nyingine imesema chini ya kitanda cha Mtume صلى الله عليه وآله وسلم  .. Mtume صلى الله عليه وآله وسلم akasema, ((Ewe ‘Aaishah, wakati gani ameingia mbwa huyu?)) Akasema: WaLlaahi sijui. Akaamrisha atolewe kisha akarashia maji kwa mikono yake mahali alipokuweko mbwa"[3]

 


Kufunika Ukuta Kwa Zulia


Jambo la pili linalopaswa kujiepusha nalo katika sherehe za harusi ni kwamba kusiweko na kufunikwa kuta kwa zulia au vibusati hata
kama vimetengenezwa kwa isiyokuwa hariri. Hii ni gharama na israaf ambayo hairuhusiwi katika Sharia. Nayo ni kutokana na Hadiyth ifuatayo kutoka kwa ‘Aaishah رضي الله عنها:

كان رسول الله صلى الله عليه وسلم غائباً في غزاة غزاها ، فَلَمَّا تَحَيَّنت قُفُولَه، فأخذتُ نَمَطاً (فيه صورة)، كانت لي فسترتُه على المَعْرِضِ، فلما  دَخَلَ رَسوُل الله صلى الله عليه وسلم  تَلَقَّيْتُهُ  فِي الْحجرة، فقلتُ: السلامُ عليك ورحمةُ اللَّهِ، الحَمْدُ للَّهِ الذي أَعَزَّكَ ونَصَرَكَ  وَأقَرَّ عَيْنَيْك وأَكْرَمَكَ، قَالَتْ  فَلَمْ يَرُدَّ عليَّ شيئاً  وَعَرَفْتُ فِي وَجْهِه الْغَضَب، وَدَخَلَ الْبَيْتَ مُسْرِعاً  وَأخَذَ النَّمْط بِيَدِهِ، فجذبه حَتَّى هتكه،  ثُمَّ قالَ: ((أتسترين الجدار؟!))  ((بستر فيه تصاوير؟!))، ((إنَّ اللَّهَ لم يَأْمُرْنَا فِيمَا رَزَقَنَا أنْ نَكْسُوَ الحِجَارَةَ  والطِّيْنَ)) قالتْ: فقطعنا منه وسادتين، وحَشَوْتُهما لِيفاً، فلَمْ يَعِبْ ذٰلكَ عليَّ  ( فكان صلى الله عليه وسلم يرتفق عليهما)

"Mtume صلى الله عليه وآله وسلم alipokuwa amekwenda katika vita vimojawapo, na wakati nikimtarajia kurudi, nilichukua busati langu ambalo lilikuwa lina picha nikafunika upande mmoja wa ukuta. Alipoingia Mtume صلى الله عليه وآله وسلم nilikutana naye katika chumba cha nje na kumuambia: Assalaam 'Alaykum Ewe Mjumbe wa Allaah, Rahma na Baraka zikushukie. Sifa Zote ni za Allaah Aliyekuadhimisha?? Na Akakunusuru na adui wako, Akakutuliza macho?? Au Akawa pendezo la macho yako na Akukirimu". ‘Aaishah akaendelea: "Lakini hakunisemesha na nikatambua ghadhabu usoni mwake! Kisha akaingia ndani kwa haraka na akalivuta pazia kwa nguvu hadi akaliangusha kisha akasema, ((Unafunika ukuta na kwa pazia ambalo lina picha? Hakika Allaah Hakutuamrisha tuvishe mawe au saruji)). ‘Aaishah anaendelea: "Kwa hiyo tukalikata pazia na kulifanya mito miwili tukajaza na usumba. Mtume صلى الله عليه وآله وسلم hakulipinga hili na alikuwa akiegemea mito hiyo"[4]


Hii ndio sababu kwamba Salafus Swaalih (wema waliotangulia) walikuwa wakigoma kuingia katika nyumba ambazo kuta zao zimefunikwa. Salim ibn 'Abdallaah kasema: "Niliona wakati wa maisha ya baba yangu. Alitangaza sherehe kwa watu na miongoni mwa walioalikwa alikuwa Abu Ayyuub. Walifunika kuta za nyumba yangu kwa kitambaa cha kijani. Abu Ayyuub alikaribia na kuingia katika nyumba na akaniona nimesimama. Kisha akatazama na akaona kuta za nyumba zimefunikiwa na mazulia ya kijani. Akasema:  'Ewe 'Abdallaah, umefunika kuta?' Baba yangu akaona hayaa akasema: 'Wanawake wana njia zao Ewe Abu Ayyuub!' (za kulazimisha jambo) Akajibu: 'Kuna wengine niliokhofu kuwa watatawaliwa na wanawake (yaani kwa kufanya makosa) lakini sikuwa na khofu kama hii kwako nawe'. Kisha akaondoka. Allaah Amrehemu."[5]

 


Kunyoa Nyusi


Jambo la tatu ovu la maasi ambalo Wanawake wengi wa Kiislamu wanalifanya ni kunyoa nyusi zao hadi zionekane
kama upinde au mwezi mwembamba. Wanafanya hivi wakidhania kuwa ni kuleta uzuri (wa sura) wakati ni jambo ambalo Mjumbe wa Allaah ameliharamisha na Allaah Anawalaani wanawake wanaonyoa nyusi.


Mtume
صلى الله عليه وآله وسلم   amesema:

((لَعَنَ اللّهُ الْوَاشِمَاتِ وَالْمُسْتَوْشِمَاتِ، وَالْوَاصِلاَتِ،  وَالنَّامِصَاتِ وَالْمُتَنَمِّصَاتِ، وَالْمُتَفَلِّجَاتِ لِلْحُسْنِ الْمُغَيِّرَاتِ خَلْقَ اللّهِ))

((Allaah Amemlaani mwanamke anayefanya tattoo (kuchorwa kwa kuchanjwa) Na mwenye kuomba kufanyiwa, na anayetoa nyusi na mwenye kuomba kutolewa na anayechonga meno kuweka nafasi (mwanya), kubadilisha maumbile ya Allaah kwa ajili ya kupata uzuri))[6]

 


Kupaka Rangi Kucha Na Kuzikuza Kuwa Refu

 
Hii ni mila/ada nyingine ya kuchukiza ambayo imepangwa na kutendwa na wanawake wengi wa Kiislamu kutokana na upotovu wa wanawake nchi za kimagharibi. Wanawake hao wanapaka kucha zao kwa rangi nyekundu ya vanishi (minicore) na huku wakiyaacha makucha kuwa marefu. Hata vijana wengine wa Kiislamu wanafuga makucha
yao. Hii sio tu aina moja ya kubadilisha maumbile ya Allaah ambayo inastahiki laana ya Allaah kama tulivyoona hapo juu, bali pia ni kujifananisha na makafiri iliyokatazwa katika Hadithi nyingi na hii ni dhidi ya Fitwrah (hali ya kimaumbile na desturi ya Mitume wote).


Kuhusu kujifananisha na makafiri Mtume
صلى الله عليه وآله وسلم   amesema:

((...وَمَنْ تَشَبَّهَ بِقَوْمٍ فَهُوَ مِنْهُمْ))

 ((Atakayejifananisha na watu, basi yeye ni miongoni mwao))[7] hali hii inakhalifu Fitwrah.


Na kuhusu kukata kucha, Mtume
صلى الله عليه وآله وسلم   amesema:

 

((الْفِطْرَةُ خَمْسٌ : الْخِتَانُ،  و حلق العانة   وَقَصُّ الشَّارِبِ  وَتَقْلِيمُ الأَظْفَارِ، وَنَتْفُ الإِبِطِ،))  وَقَالَ أَنَس  رضي الله عنه : وُقِّتَ لَنَا فِي قَصِّ الشَّارِبِ، وَتَقْلِيمِ الأَظْفَارِ، وَنَتْفِ الإِبِطِ، وَحَلْقِ الْعَانَةِ، أَنْ لاَ نَتْرُكَ أَكْثَرَ مِنْ أَرْبَعِينَ يَوْماً

 

((Fitwrah ni mambo matano; khitaan (kutahiri), kunyoa nywele sehemu za siri, kukata masharubu, kukata kucha, na kunyofoa nywele za kwapa)) [8]

 
Anas
رضي الله عنه alisema, "Mtume صلى الله عليه وآله وسلم alituwekea muda wa kukata masharubu, kukata kucha, kunyoa nywele za kwapa, na kunyoa nywele za sehemu za siri kuwa tusiziache zaidi ya siku arubaini".[9]

 


Kunyoa Ndevu


Mila nyingine ya kuchukiza kama hizo nyingine au hata kuchukiza zaidi ni kama zile za kuwaiga makafiri na kuitakidi kuwa kunyoa ndevu ndio usafi na ni ustaarabu kuwaiga wazungu makafiri, hata imefikia hadi kuwa mume hawezi kuingia kwa mke wake siku ya harusi kama hajanyoa ndevu. Hii ni kinyume kabisa na sheria na inavunja sheria kwa njia nyingi
kama zifuatazo:

 


A. Kubadilisha Maumbile Ya Allaah.

 

Allaah سبحانه وتعالى Amesema Kuhusu Shaytwaan

 

((وَلأُضِلَّنَّهُمْ وَلأُمَنِّيَنَّهُمْ وَلآمُرَنَّهُمْ فَلَيُبَتِّكُنَّ آذَانَ الأَنْعَامِ وَلآمُرَنَّهُمْ فَلَيُغَيِّرُنَّ خَلْقَ اللّهِ وَمَن يَتَّخِذِ الشَّيْطَانَ وَلِيًّا مِّن دُونِ اللّهِ فَقَدْ خَسِرَ خُسْرَانًا مُّبِينًا))

 

 

((Na hakika nitawapoteza na nitawatia matamanio, na nitawaamrisha, basi watakata masikio ya wanyama, na nitawaamrisha, basi watabadili Aliyoumba Allaah. Na mwenye kumfanya shaytwaan kuwa ni mlinzi wake badala ya Allaah, basi huyo amekhasiri khasara ya dhaahiri)) (An-Nisaa: 119)


Hii ni matini na dalili iliyo dhahiri inayosema kwamba kubadilisha maumbile ya Allaah bila ya ruhusa Yake ni kutii amri ya shaytwaan na ni kumuasi Mola Mtukufu Mwenye Huruma. Kwa hiyo hakuna shaka kwamba Mtume
صلى الله عليه وآله وسلم kuwalaani wanawake wanaobadilisha maumbile ya Allaah kwa ajili ya kuleta uzuri uliyotajwa kabla inawahusu pia wale wanaonyoa ndevu zao wakifikiri pia kama hii ni aina ya kuleta uzuri. Kwa hiyo laana inawahusu wao pia, khaswa kwa vile mas-ala mawili haya yanashirikiana katika sababu na zote zinasababisha laana ya Allaah. Sababu ya kusema hivyo "bila ya ruhusa ya Allaah" hapo juu, ni kwa vile hakuna atakayefikiria kwamba kunyoa nywele za siri na mengineyo yaliyotajwa katika Fitwrah kuwa yanahusiana na kubadilisha maumbile ya Allaah. Bali mambo haya yameruhusiwa na hata kusisitizwa na sheria.




B. Kuasi Amri za Mtume
صلى الله عليه وآله وسلم

 

Juu ya hivyo, ni kumuasi Mtume صلى الله عليه وآله وسلم ambaye amesema:

((قُصُّوا الشَّوَارِبَ، واعْفُوا اللِّحى))

 

((Kateni masharubu na acheni ndevu)).[10] Kama inavyojulikana katika Misingi ya Sheria ya Kiislamu (Usuulul-Fiqh) kuwa amri ya Mtume صلى الله عليه وآله وسلم ni wajibu isipokuwa mpaka upatikane muunganisho wa kufananisha, ambao ni kufanana na Kafiri (Qariynah) ipatikane ambayo itathibitisha kuwa yale yaliyokusudiwa katika amri ni mapendekezo na si wajibu.

 
Kuhusu ndevu, Mtume
صلى الله عليه وآله وسلم hakupata kunyoa ndevu zake, hakumruhusu yeyote kunyoa ndevu na wala hakushuhudia mtu aliyenyoa na kisha akaruhusu au kwa kukaa kimya. Kwa kifupi, dalili zote katika mas-ala haya yanatia nguvu ufahamu wa mwanzo wa amri ya Mtume صلى الله عليه وآله وسلم kwamba ni wajibu kuziacha ndevu kukua na imeharamishwa kuzinyoa. Zifuatazo ni dalili za nyinginezo:

 


C. Kujifananisha na makafiri.

 

Mtume صلى الله عليه وآله وسلم amesema:

 

((جُزُّوا الشَّوارِبَ وارْخُوا اللِّـحَى خالِفُوا الـمَـجُوسَ))

((Punguzeni masharubu na acheni ndevu zenu ziwe ndefu, kuweni tofauti na Majusi))[11]

 



D. Kujishabihisha na Wanawake.

لَعَنَ رسول الله  صلى الله عليه وسلم  الْمُتَشَبِّهِينَ مِنَ الرِّجَالِ بِالنِّسَاءِ  وَالْمُتَشَبِّهَاتِ مِنَ النِّسَاءِ بِالرِّجَالِ

((Mtume صلى الله عليه وآله وسلم amewalaani wanaume wanaojishabihisha na wanawake na wanawake wanaojishabihisha na wanaume))[12]

 

Kwa hakika mwanamume kunyoa ndevu zake ni kujifananisha na wanawake. Natumai kwamba dalili hizo tulizo zinukuu zitatosha kuwakinaisha wale waliofikwa na msiba wa kuhalifu amri za dini Namuomba Allaah Atujaalie sisi na wao usalama na kila Asilolipenda na Asiloridhika nalo.

 


Pete Ya Uchumba


Sita:


Waislamu wengi wanafuata na kutekeleza mila na desturi za kuvalishana pete ambayo inaitwa 'pete ya uchumba' (engagement ring). Mbali ya kuwa ni kigezo cha mila za makafiri kwa vile chanzo chake ni kutoka kwa manaswara, bali pia ni kukhalifu wazi wazi makatazo yaliyokuja katika nasw (matini) zilizo Swahiyh ambazo zimeharamisha kuvaa pete za dhahabu kwa Waislamu wanaume na wanawake kama tutakavyoeleze katika nasw (matini) zifuatazo:


Kwanza:

 

Kukatazwa Kwa Pete Ya Dhahabu

 

  ((نَهَى صَلَّى الله عَلَيْهِ وَسَلَّمَ عَنْ خَاتم الذَّهَب )).

 

Mtume صلى الله عليه وآله وسلم ameharamisha pete za dhahabu. (Al-Bukhaariy na Muslim)[13]

 


Pili:

عَنْ إبْنِ عَبَّاسٍ أَنَّ رَسُولَ اللّهِ رَأَىٰ خَاتِماً مِنْ ذَهَبٍ فِي يَدِ رَجُلٍ  فَنَزَعَهُ فَطَرَحَهُ وَقَالَ: ((يَعْمِدُ أَحَدُكُمْ إِلَىٰ جَمْرَةٍ مِنْ نَارٍ فَيَجْعَلُهَا فِي يَدِهِ))  فَقِيلَ لِلرَّجُلِ، بَعْدَ مَا ذَهَبَ رَسُولُ اللّهِ : خُذْ خَاتَمَكَ انْتَفِعْ بِهِ. قَالَ: لاَ. وَاللّهِ لاَ آخُذُهُ أَبَداً. وَقَدْ طَرَحَهُ رَسُولُ اللّهِ .

Kutoka kwa Ibn 'Abbaas رضي الله عنهما kwamba Mtume صلى الله عليه وآله وسلم aliona pete ya dhahabu katika kidole cha mwanamume, akaitoa na kuitupilia mbali na akasema, ((Je, mnataka mmoja wenu achukue kaa la moto na ajiwekee mkononi mwake?)) Baada ya Mtumeصلى الله عليه وآله وسلم kuondoka mtu yule aliambiwa na watu, "Chukua pete yako na faidika nayo" (kwa kuiuza). Mtu huyo alisema: "Hapana, WaLlaahi, sitoichukua baada ya kutupwa na Mjumbe wa Allaah"[14]


Tatu:

 

عَنْ أَبِي ثَعْلَبَةَ الْخُشَنِيِّ ،: أَنَّ النَّبِيَّ صلى الله عليه وسلم أَبْصَرَ فِي يَدِهِ خَاتَما مِنْ ذَهَبٍ فَجَعَلَ يَقْرَعُهُ بِقَضِيبٍ مَعَهُ فَلَمَّا غَفَلَ النَّبِيُّ صلى الله عليه وسلم أَلْقَاهُ (فنظر النبي صلى الله عليه وسلم فلم يره في يده)   قَالَ: ((مَا أُرَانَا إلاَّ قَدْ أَوْجَعْنَاكَ وَأَغْرَمْنَاكَ))

 

Kutoka kwa Abu Tha'alabah Al-Khushaniy رضي الله عنه ambaye amesema kwamba Mtume صلى الله عليه وآله وسلم aliona pete ya dhahabu katika kidole chake akawa anaipiga kwa kijiti alichokuwa nacho. Alipokuwa Mtume صلى الله عليه وآله وسلم hamtazami aliitupilia mbali. Kisha Mtume صلى الله عليه وآله وسلم aliitazama na hakuiona tena akasema, ((Umeitupa baada ya kukuumiza na kukutia maumivu))[15]


Nne:

عن عبد الله بن عمرو أنَّ النَّبِيِّ صلى الله عليه وسلم رَأَى عَلىَ بَعْض أَصْحَابه خَاتماً مِن ذَهَب، فَأَعْرَضَ عَنْهُ، فَألْقَاه وَاتَّخَذَ خَاتِماً مِنْ حَديد قال: فَقال هذا شرٌّ هذا حلية أَهْل النَّار. فألقَاه وَاتَّخَذ خاتماً مِنْ وَرَق، فَسَكت عنه

Kutoka kwa 'Abdullaah ibn 'Amr رضي الله عنه ambaye amesema kwamba Mtume صلى الله عليه وآله وسلم alimuona Swahaba mmoja amevaa pete ya dhahabu, akamgeuzia uso. Swahaba akaitupilia mbali pete na akavaa pete ya chuma. Mtume صلى الله عليه وآله وسلم akamwambia, ((Hii ni mbaya zaidi. Pambo la watu wa motoni)). Kwa hiyo Swahaba akaitupilia mbali akavaa pete ya fedha. Mtume صلى الله عليه وآله وسلم hakusema kitu kuhusu hiyo"[16]

 


Tano:

((مَنْ كَانَ يُؤْمِن بالله وَالْيَوْم الآخِر فَلاَ يَلْبس حَرِيراً وَلاَ ذَهَباً))

 

((Yeyote anayemuamini Allaah na Siku Ya Qiyaamah, basi asivae pete ya dhahabu))[17]

 


Sita:

 

((مَنْ لَبِسَ الذَّهَبَ مِنْ أُمَّتِي، فمَاتَ وَهُوَ يَلْبَسُهُ، حَرَّمَ الله عَلَيْهِ ذَهَبَ الجَنَّةِ))

 

((Yeyote atakayevaa dhahabu katika Umma wangu, na akifa akiwa ameivaa, ataharamishiwa na Allaah dhahabu ya Peponi))[18]

 

 



[1]Al-Bukhaariy, Muslim na wengineo

[2] Al-Bukhaariy, Muslim na wengineo

[3]Abu Daawuud, An-Nasaaiy, At-Tirmidhiy na wengineo : Swahiyh

[4] Muslim, Abu 'Awwaanah na wengineo

[5] Al-Bukhaariy, Muslim na wengineo

[6] Al-Bukhaariy, Muslim na wengineo

[7] Abu Daawuud na Ahmad: Hasan

[8] Al-Bukhaariy, Muslim na wengineo

[9] Muslim, Abu Daawuud na wengineo

[10] Al-Bukhaariy, Muslim na wengineo

[11] Muslim na Abu 'Awwaanah

[12] Al-Bukhaariy, At-Tirmidiy na wengineo

[13] Al-Bukhaariy na Muslim

[14] Muslim, Ibn Hibbaan na At-Twabaraaniy

[15] An-Nasaaiy, Ahmad na wengineo: Swahiyh

[16] Al-Bukhaariy, Ahmad

[17] Ahmad: Hasan

[18] Ahmad: Swahiyh

 

Share