Ukisahau Kusoma Suratul-Faatihah Katika Rakaa Ufanyeje?

 

SWALI

Hakuna Swalah bila ya "surratul-faat-ha". je ukiwa umesahau kusoma "suratul-faat-ha" katika rakaa moja ya Swalah ya rakaa tatu au nne, utafanya nini?

 


 

JIBU:

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola  wa walimwengu wote, Swalah na Salaam zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho

Ikiwa umesahau kusoma Suratul-Faatihah au hata kama umeikuosea kuisoma basi urudie kuisoma kwani Suratul-Faatihah ni nguzo katika Swalah. Mfano ukiwa umesahau kisha ukakakumbuka katika rukuu basi urudi kusimama na kuisoma upya kisha urudi kurukuu kwani hiyo rakaa ya mwanzo itakuwa haihesabiki tena kwa vile hukutimiza nguzo kwa kusoma Suratul-Faatihah.

Na ikiwa umesahau kuisoma ukakakumbuka baada ya kumaliza rukuu yaani mfano uko katika sujuud, basi rakaa hiyo haitahesabika kuwa imekamilika hadi kwanza utimize Suratul-Faatihah. Kwa hiyo utasimama na kuanza upya kuisoma Suratul-Faatihah na kufanya tena rukuu yake. Ikiwa hiyo ilikuwa ni mfano rakaa ya mwanzo basi ya pili yake utakayosimama kurekebisha kusoma Suratul-Faatihah itahesabika kuwa ni ya kwanza kwa sababu rakaa ya kwanza haikuhesabika kwa upungufu wa Suratul-Faatihah.

Na ikiwa umekumbuka baada ya kutoa Salaam, utainuka na kuleta Takbira kisha utaiswali rakaa moja kwa kuisoma Suratul-Faatihah, kisha kurukuu, na kumalizia kwa tashahhud.

Hili zaidi linahusiana zaidi ukiwa unaswali peke yako au ukiwa wewe ni Imaam. Ama ukiwa ni maamuma suala linatofautiana ukiwa hujasoma Suratul-Faatihah kwa sababu maamuma hutakiwa kumfuata Imaam kwa kila jambo ndani ya Swalah. Na pia maamuma huweza kuja na kumkuta Imaam katika rukuu na ikawa yeye maamuma hakupata kuisoma hiyo Suratul-Faatihah, na rakaa yake hiyo akawa ameipata japo aliikuta kwenye rukuu na hakusoma Suratul-Faatihah. Hili limethibiti.

Na Allaah Anajua zaidi  

 

Share