Kusujudu Baada Ya Kusoma Aayah Yenye Sajdah (Sijdah At-Tilaawah)

Kusujudu Baada Ya Kusoma Aayah Yenye Sajdah (Sijdah At-Tilaawah)

 

Alhidaaya.com

 

 

SWALI:

 

Kuhusu sijida ya kisomo, nataka kujua ulazima wake:  jee ni lazima mara tu ukizisikia ayah hizo kusujudu hata kama huna udhu japo kwa ishara. jee kuna ushahidi wowote.

    

JIBU:

 

AlhamduliLLaah; Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salamu zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho

 

Sajdah ya Tilaawah (ya kisomo) ni sijda ambayo husujudiwa wakati wa anaposoma mtu Qur-aan na kukutana na Aayah inazungumzia kusujudu au pia mtu anaposikia Aayah inasomwa ambayo inahusiana na kusujudu.

 

Fadhila zake:

 

عنْ أَبِي هُرَيْرَةَ، قَالَ قَالَ رَسُولُ اللَّهِ صلى الله عليه وسلم ‏ "‏ إِذَا قَرَأَ ابْنُ آدَمَ السَّجْدَةَ فَسَجَدَ اعْتَزَلَ الشَّيْطَانُ يَبْكِي يَقُولُ يَا وَيْلَهُ - وَفِي رِوَايَةِ أَبِي كُرَيْبٍ يَا وَيْلِي - أُمِرَ ابْنُ آدَمَ بِالسُّجُودِ فَسَجَدَ فَلَهُ الْجَنَّةُ وَأُمِرْتُ بِالسُّجُودِ فَأَبَيْتُ فَلِيَ النَّارُ ‏"‏  

 Abuu Hurayrah (Radhwiya Allaahu ‘anhu) amehadithia kwamba: Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)  amesema: ((Anaposoma mwanaadam (Aayah) ya kusujudu kisha akasujudu, shaytwaan atajitenga na kulia, kisha husema (kujiambia): “Ole wake ameamrishwa (mwanaadam) kusujudu akasujudu na ana Jannah (Pepo), nami niliamrishwa kusujudu nikaasi na nina moto.” [Muslim, Ibn Maajah na Ahmad]

 

Ama fadhila za kusujudu kwa ujumla, ziko Hadiyth nyingi ila tutatosheka na hiyo inayohusu swali.

 

Kila mwenye kusoma au kusikia kisomo cha Aayah zenye Sijdah anafaa asujudu, ili kutoa dalili ya kimatendo kwa kuonyesha unyenyekevu na utiifu kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)  na kwenda sambamba na Malaika Wake.

 

Katika Qur-aan zipo sehemu 15, ‘Ulamaa wengine  wamesema ni 14 kwani ipo tofauti katika ile sijdah ya Suwratu Swaad.

 

Zifuatazo ni Majina ya Suwrah na nambari za Aayah ambazo Muislamu anapaswa kusujudu anaposoma au anaposikia  zikisomwa.  ‘Ulamaa    wamekubaliana kuwa Sijdah ifanywe katika sehemu hizo, lakini wametofautiana kuhusu hadhi yake ya ulazima.

 

Kulingana na Imaam Ath Thawry, Abuu Haniyfah ni wajibu (lazima) na moja ya kauli ya Imaam Ahmad, na Imaam Ibn Taymiyyah kaendana na msimamo huo vilevile. Lakini ‘Ulamaa wengine pamoja na Imaam wakubwa waliobaki wamesema kuwa ni pendekezo (si lazima).

 

Inatakiwa ifahamike kuwa kitendo cha kupendezwa kufanya  hakina hadhi sawa na faradhi lakini kukiacha kwa makusudi japokuwa si dhambi inachukuliwa ni makosa kwa Muislamu mwema na mzuri na kukiacha kabisa ni makosa.

 

Namna ya kusujudu kwake ni sijdah moja tu. Anasujudu mtu kama anavyosujudu kwenye sijdah ya Swalaah kwa viungo vyake saba; kuweka viganja viwili ardhini (vidole vikiielekea Qiblah), magoti mawili, na matumbo ya vidole vya miguu (akijitahidi vidole vielekee Qiblah), na kipaji cha uso na pua (vikihesabika ni kitu kimoja) na ahakikishe kapanua viwiko vyake (asiibane mikono yake kwenye mbavu zake) na tumbo lisigusane na mapaja yake.

 

Hakujawekewa hukmu ya kuleta takbiyrah  ukitaka kusujudu sijdah hiyo wala kutoa salaam baada ya kusujudu.

 

Kunapendezwa kupiga takbiyrah wakati wa kusujudu na wakati wa kunyanyuka baada ya kusujudu kwa kauli ya ‘Ulamaa wengi.

 

Ni bora anayetaka kusujudu sijdah hiyo asimame kwanza kisha ashuke kusujudu sijdah hiyo ya kisomo, na hii ni rai ya madhehebu ya Hanbali, wanazuoni wa ki Hanafi na moja ya muono wa Imaam Shaafi’iy, na wamechukua msimamo huo kuegemea katika Aayah ifuatayo:

 

قُلْ آمِنُوا بِهِ أَوْ لَا تُؤْمِنُوا ۚ إِنَّ الَّذِينَ أُوتُوا الْعِلْمَ مِن قَبْلِهِ إِذَا يُتْلَىٰ عَلَيْهِمْ يَخِرُّونَ لِلْأَذْقَانِ سُجَّدًا ﴿١٠٧﴾

Sema: Iaminini au msiamini. Hakika wale waliopewa elimu kabla yake wanaposomewa (Qur-aan) wanaporomoka kifudifudi wanasujudu.    [Al Israa:107]

 

Na ingawa Wanazuoni wengi wanaonelea kuwa ni sharti mtu kuwa na wudhuu anapotaka kusujudu sijdah ya tilaawah kwa hoja kuwa masharti ya Swalaah ndiyo masharti ya sijdah hiyo, lakini Imaam Ibn Hazm, Shaykhul-Islaam Ibn Taymiyyah, Imaam Al-Bukhaariy na Ash Sha’by wanatoa hoja ya kuwa haiwezi kuwekewa sharti ya twahaarah kwa sababu sijdah ya kisomo si Swalaah bali ni tendo la ‘ibaadah na kwa hivyo halihitajii ulazima wa twahaarah. Na huo ndiyo msimamo wa Swahabah Ibn ‘Umar (Radhwiya Allaahu ‘anhumaa). Na dalili ni Hadiyth ya Ibn ‘Abbaas kuwa Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)  alisujudu kwenye (kisomo cha) Suwrah ya An-Najm na wakasujudu pamoja naye waislam, washirikina, majini na binaadam)) [Al Bukhaariy na At-Tirmidhy]

 

Hata hivyo, pamoja ni kuwa si lazima kuwa na wudhuu au kuelekea Qiblah kwa sijdah hiyo, lakini ni bora na afadhali zaidi kusujudu ukiwa na wudhuu na kuelekea Qiblah, na haipendezi kuacha kufanya hivyo ikiwa huna udhuru ingawa kama ilivyotajwa nyuma kuwa si sharti.

 

Ama kuhusu jinsi ya kufanya sijdah hii, tunajifunza kutoka kwenye Hadiyth kuwa ilikuwa tofauti katika hali na sehemu tofauti. Wakati mwengine Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)  alipokuwa akisoma Aayah inayohitajia sijdah, alikuwa anasujudu papo hapo na kila mmoja katika kikao hicho alikuwa akifanya hivyo, kwa kiasi kwamba wapo watu ambao walikuwa wanakosa nafasi ya kusujudia kwayo hivyo kumfanya asujudu kwenye mgongo wa mwenziwe. [Al-Bukhaariy na Muslim kutoka kwa Ibn ‘Umar  Radhwiya Allaahu 'anhumaa] 

 

Pia tunakuta Hadiyth kuwa wakati wa kutekwa kwa Makkah, Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'Alayhi wa aalihi wa sallam)  alikuwa akisoma kisomo na akafika katika Aayah inayohitaji sijdah. Wale waliokuwa wamesimama walisujudu kwenye sakafu na wale waliokuwa juu ya vipando (farasi na ngamia) waliitekeleza hapo hapo juu ya wanyama wao.

Wakati mwengine alipokuwa akihutubu na akafika katika Aayah ya sijdah alikuwa Nabiy (Swalla Allaahu 'Alayhi wa aalihi wa sallam) anateremka chini ya minbar kusujudu kisha akapanda tena na kuendelea na khutbah. Na ‘Umar (Radhwiya Allaahu 'anhu) naye alikuwa anafanya hivyo hivyo wakati mwengine na maamuma wote nao wakimfuata na mara nyengine alikuwa hasujudu [Al-Bukhaariy]. 

 

Baadhi ya Wanazuoni wana rai kuwa masharti ya kufanya sijdah hii ni kama yale ya kutekeleza Swalaah, lakini hakuna dalili kwa rai hii kutoka kwenye Hadiyth. Tunapata kutoka kwa Swahaba kuwa alipokuwa akisikia Aayah mojawapo ya sijdah ikisomwa basi akiinamisha kichwa chake katika hali yoyote ile. Alikuwa hajali kama ana wudhuu au la; ikiwa anaweza kuelekea Qiblah au la; ikiwa anaweza kusujudu juu ya sakafu au ardhini au la. Tunapata mifano ya wasomi na Salaf Swaalih wakifanya hivyo. Kulingana na Imaam Al-Bukhaariy, ‘Abdullah bin ‘Umar (Radhwiya Allaahu 'anhumaa) alikuwa akisujudu akiwa na wudhuu au hata bila ya wudhuu. Imenukuliwa katika Fat-hul Baariy kuwa Abu ‘Abdir-Rahmaan As-Sulaamiy (Radhwiya Allaahu 'anhu) alikuwa akisoma Qur-aan katika hali ya kuwa anatembea na alikuwa akiinamisha kichwa chake tu anaposoma Aayah ya sijdah, hakukuwa na tofauti akiwa ana wudhuu au hapana, na wala akiwa ameelekea Qiblah au popote.

 

Kwa haya tunahitimisha kuwa japokuwa wengi wanakubaliana katika njia ya kusujudu lakini mtu asikemewe akifanya njia nyengine iliyofanywa Salaf Swaalih kama tulivyoona hapo juu kwani hii njia ya wengi haina dalili katika Sunnah.

 

Hadiyth kadhaa za Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) zinatufundisha kusujudu papo hapo unaposoma au unaposikia Aayah hiyo ya sijdah.

 

Al-Bukhaariy na Muslim wametaja Hadiyth ya Ibn ‘Umar, Abuu Hurayrah na Ibn ‘Abbaas (Radhiya Allaahu 'anhum) kuhusu hilo. Ndio Sayyid Saabiq katika Fiqhus Sunnah akasema: “Ikiwa mtu hakusujudu baada ya kuisoma au kuisikia mojawapo ya Aayah hizo basi hakuna kulipa baada ya muda kupita.”

 

Katika sijdah hiyo, mtu atasema:

 

الله أكْبَر

Allaahu Akbar

 

wakati anataka kusujudu na akisujudu atasema:

سُبْـحانَ رَبِّـيَ الأَعْلـى  

 

 

Kisha akinyanyuka atasema    

 الله أكْبَر

Allaahu Akbar

 

Suwrah pamoja na Aayah zake ambazo inampasa Muislamu asujudu kwayo ni kama zifuatazo:

 

 

Suwrah

 

Namba ya Suwrah

Namba ya Aayah

 

1

الأعراف

Al-A’raaf

 

7

(mwisho wa Suwrah)

206

 

 

الرّعد

Ar-Ra’d

 

13

 

15

 

3

النّحل

An-Nahl

 

16

 

50

 

4

الإسراء

Al-Israa

 

17

 

109

 

5

مريم

Maryam

 

19

 

58

 

6

الحجّ

Al-Hajj

 

22

 

18

 

7

الحجّ

Al-Hajj

 

22

 

77

 

8

الفرقان

Al-Furqaan

 

25

 

60

 

9

النّمل

An-Naml

 

27

 

26

 

10

السّجدة

As-Sajdah

 

32

 

15

 

11

ص

Swaad

 

38

 

24

 

12

فصّلت

Fusswilat

 

41

 

38

 

13

النّجم

An-Najm

 

53

 

62

 

14

الإنشقاق

Al-Inshiqaaq

 

84

 

21

 

15

العلق

Al-‘Alaq

 

96

 

19

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share