002-Hakimu Wa Kiislamu: Shukurani

 

SHUKRANI

 

 

 إنَّ الْحَمْدَ لِلَّهِ نَحْمَدُهُ وَنَسْتَعِينُهُ وَنَسْتَغْفِرُهُ وَنَعُوذُ بِاللَّهِ مِنْ شُرُورِ أَنْفُسِنَا وَمِنْ سَيِّئَاتِ أَعْمَالِنَا مَنْ يَهْدِهِ اللَّهُ فَلَا مُضِلَّ لَهُ وَمَنْ يُضْلِلْ فَلَا هَادِيَ لَهُ وَأَشْهَدُ أَنْ لَا إِلَهَ إِلَّا اللَّهُ وَحْدَهُ لَا شَرِيكَ لَهُ وَأَشْهَدُ أَنَّ مُحَمَّدًا عَبْدُهُ وَرَسُولُهُ. اللّهُـمَّ صَلِّ عَلـى مُحمَّـد، وَعَلـى آلِ مُحمَّد، كَمـا صَلَّيـتَ عَلـى إبْراهـيمَ وَعَلـى آلِ إبْراهـيم، إِنَّكَ حَمـيدٌ مَجـيد ، اللّهُـمَّ بارِكْ عَلـى مُحمَّـد، وَعَلـى آلِ مُحمَّـد،  كَمـا بارِكْتَ عَلـى إبْراهـيمَ وَعَلـى آلِ إبْراهيم، إِنَّكَ حَمـيدٌ مَجـيد .

أمّاَ بعد, إِنَّ أَصْدَقَ الْحَدِيثِ كِتَابُ اللَّهِ وَأَحْسَنَ الْهَدْيِ هَدْيُ مُحَمَّدٍ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَ سَلَّم,  وَشَرَّ الْأُمُورِ مُحْدَثَاتُهَا وَكُلَّ مُحْدَثَةٍ بِدْعَةٍ وَكُلَّ بِدْعَةٍ ضَلَالَةٍ وَكُلَّ ضَلَالَةٍ فِي النَّارِ

 

Vyovyote nitakavyojitahidi kumshukuru Mola wangu Mtukufu kwa Neema na Fadhila Zake, basi shukurani hizo hazitafikia chembe ya usawa wa Neema na Fadhila hizo, kwani hakuna awezaye kuzihesabu. Lakini sina budi kutaja shukurani zangu Kwake kwa kuniwezesha kuifanikisha kazi hii.

 

Kwa hakika mengi ninayapatia katika kujifunza kwangu. Ni katika pirika pirika hizi ndipo nilipotambua kwamba nina mzigo mkubwa mno kwa jamii inayonizunguka. Hicho kidogo nilichojifunza kwa hakika wengi hawakielewi. Ndio nikachukua jitihada za kuwafikishia Waislamu wenzangu ili waelewe yale yanayowazunguka katika mambo ya Sheria. Na ukweli ni kwamba, Waislamu wengi sio wenye kuipigia mbizi nyanja hii.

  

Bila ya shaka ni wajibu wa kila Muislamu kujifunza Uislamu wake ili aweze kufahamu yale ya halali na haramu. Hapo ndipo ataweza kuzichunga amali zake kwa lengo la kupata mafanikio duniani na Akhera. Na tunatamka kwamba hakuna njia iliyo sahihi ya wanaadamu kuifuata isipokuwa ni njia ya Uislamu. Ni Uislamu wetu ndio utatupatia mafanikio makubwa.

  

Hamu, utashi na matamanio makubwa yalinizidi ya kuipatia jamii yetu msaada wa masuala ya Sheria nilipokuja kujua kwamba wanafunzi wengi wanapata taabu katika somo hili kutokana na elimu hii kukuwepo katika lugha ya Kiarabu na Kiingereza. Halikadhalika, wana jamii wengi ninaokutana nao Mahkamani ni wenye kukosa ufahamu wa masuala haya ya Sheria.

 

Pia sina budi kukiri kwamba kitabu hiki ni zao la bidii na juhudi ya muda mrefu usiopungua miezi kumi na nane.

 

Lakini nisingeliweza kuikamilisha kazi hii bila ya usaidizi na ushauri wa ndugu yangu katika Uislaam, Muhammad Baawaziyr. Namshukuru kwa nasaha, ushauri, na namna alivyonitia moyo na ari kwa ajili ya kuitenda kazi hii. Shukurani na du’aa zangu za dhati zimfikie na Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Amlipe kwa juhudi yake kubwa anayochangia katika kazi hii, Aamiyn.

 

Pia shukurani zangu kwa familia yangu, nikianza na mama  yangu, kisha kwa baba yangu, Dr. Hamed R. H. Hikmany ambaye amenipa wasaa wa kila aina kuniwezesha kutekeleza kazi hii, kunitayarishia na kuninunulia vitabu pamoja na vifaa vinavyohitajika kuiwezesha kazi hii itendeke kwa hali na mali. Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Awalipe wazee wangu Pepo ya Firdaws, Aamiyn.  Pili shukurani nyingi kwa tashji’i kubwa na uvumilivu wa hali ya juu kutoka kwa Ahli yangu ambaye amenisaidia kwa kiasi kikubwa na amenipa fursa ya kutosha ya kushughulika na majukumu haya matukufu bila kuchoshwa wala kuvunjika moyo. Namuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Amlipe malipo mema, Ambariki, Amuongoze na Amzidishie elimu ya dini yake na taqwa. Aamiyn.

 

Shukurani za dhati pia kwa Ukhti yetu katika Uislaam Ummu Iyyaad ambaye amenipa fursa na ruhusa adhimu ya kutumia rejeo za kazi zake. Namuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Amjaalie tawfiyq na Amfanyie wepesi katika kazi zake hizi. Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Azijaalie kazi zake zizae matunda ya khayr kwa familia yake na jamii nzima.

 

Namuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Aijaalie kazi hii ilete manufaa makubwa kwa jamii yetu, iwe ni sababu ya wengi kupata haki zao. Aijaalie iwe ni ufunuo kwa wale waliozama katika ujahili wa kufuata Umagharibi zaidi kuliko Uislamu wao. Aijaalie iwe ni alhidaaya (uongofu) wao kwa Idhni Yake.

 

Namuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Anitakabalie amali hii iwe nzito katika mizani ya mambo mema siku ya Qiyaamah.  Aamiyn Yaa Rabbal ’Aalaamiyn.

 

 

Naaswir Haamid

01 Muharram 1430H – 01/01/2009M

 

 

 

Share