009-Hakimu Wa Kiislamu: Sura Ya Tatu

 

SURA YA TATU

 

HATI

 

 

 

Nyaraka

 

Mara nyengine, hati za karatasi zinakubaliwa kama ni mbadala wa kiapo cha mdomo. Lakini Mahkama hairuhusiwi kutoa maamuzi kwa kutegemea tu hati iliyopigwa muhuri au hati nyengine yoyote. Hadi pale inapoonekana kuwa ipo huru na udanganyifu na iwe ni kawaida ya watu kuingia kwenye mauziano kwa njia za hati. Kwa mfano, hati rasmi na kumbukumbu za Mahkama iliyo adilifu zinaweza kukubaliwa. Madaftari ya hisabu yaliyowekwa kwenye biashara na hati zilizotolewa mbele ya mashahidi wawili, pia zinaweza kutumika kama ni ushahidi.[1]

 

Ndani ya Sheria ya Ushahidi inaruhusu hati kuwasilishwa Mahkamani kama ni sehemu ya ushahidi. Hati hizi zipo za aina mbili. Aina ya kwanza ni zile za msingi (primary) ambazo ni za asili na aina ya pili ni zile ambazo zinathibitisha kuwepo hiyo aina ya kwanza (secondary). Kwa mfano nakala ya cheti cha ndoa inaweza kuwa ni ithbati kwamba kipo cheti halisi cha ndoa. Hivyo, nakala kwa hapa ni aina ya pili na kile cheti halisi ndio aina ya kwanza.[2] Pia maelezo ya mdomo juu ya kuthibitisha ukweli wa hati unatambulika kuangukia aina ya pili ya ushahidi wa hati.[3] Hakuna hati inayoruhusiwa kuthibitishwa Mahkamani isipokuwa pale yatakapotolewa maelezo ya shahidi.[4]

 

 

Wito Kwa Mdaiwa

 

Ni lazima Mahkama itoe wito kwa mdai pale taratibu za kufungua kesi zinapokamilika. Hata hivyo, wanachuoni hawakutoa maelezo ya kina kuhusiana na utoaji wa wito kwa mdai, isipokuwa Ibn Qudaamah na al-Khassaaf.[5]

 

Utaratibu wa wito wa kufika Mahkamani kwa mdaiwa unajulikana kwa al-Adwa wa l-l’adu (Bidii ya kumtafuta mdaiwa) na kuegemezwa hoja hiyo kwa Abu Yuusuf, ambaye ameeleza kwamba pale kesi inapofunguliwa Mahkamani na mdaiwa kutambuliwa kuwa anaishi mji huo huo, wito huo utapelekwa pamoja na aliyefungua kesi na tarishi ambao watamleta mdaiwa yeye binafsi au wakala wake.

 

Kwa mujibu wa Abu Yuusuf, utaratibu wa al-‘Adwa wa l-l’ada una msingi kutoka Istihsaan[6] na sio Qiyaas[7], na Maswahaba walifanya hivyo na hakuna aliyeukataa.[8]

 

Azad anaendelea kusema kwamba; inapotokea kuwa mdaiwa anaishi nje ya mji, kwa usafiri wa siku nzima. Hakimu ataandika ushahidi uliotolewa na mdai na kisha kumpelekea mdaiwa, akimpa amri ya kufika na kujibu madai. Kwa mujibu wa Ibn Qudaamah na al-Khassaf, maelezo hayo yanatolewa kutoka kwenye maamuzi precedence tofauti yaliyotolewa kutoka kwa Makhalifa waongofu.

 

Kwa mujibu wa kifungu 20 cha Sheria ya Mwenendo wa Madai ya Zanzibar, Mahkama kama ikipenda inaweza kutoa hati ya wito kwa mdaiwa pale kesi inapofunguliwa. Hati hiyo ni lazima iwe na saini ya Hakimu (au ofisa yeyote aliyeteuliwa na Hakimu kutia saini) pamoja na muhuri wa Mahkama.[9] Hati hiyo ni lazima imuelekeze mdaiwa huyo kufika yeye mwenyewe au kuwakilishwa na wakala wake. Pia kuna utaratibu maalum wa kumtafuta ili kumpata mdaiwa pale anapojaribu kukimbia sheria. Mfano anaweza kupelekewa afisa maalum kumuita[10], ikishindikana atabandikiwa hati hiyo mlangoni mwake.[11]

 

 

Ushahidi Wa Wito

 

Wito wowote unaopelekwa kwa mdaiwa kumtaka afike Mahkamani ni lazima uwe na ithibati kwamba umetoka Mahkamani na ni amri ya Hakimu. Hivyo, wito huo uwe na ushahidi wa Hakimu (mfano saini) na nembo ya Mahkama ukipelekwa na tarishi.

 

Itakapotokezea mdaiwa kutoweza kufika kwa sababu za msingi kama ugonjwa au wanawake wa mila ambao wamezuiwa kabisa kutoka, hawatapelekewa wito. Badala yake, kamati itaundwa ambayo itamtembelea mtu huyo aliyetajwa na atakuwepo Hakimu au naibu wake aliyepewa nguvu kuwa naibu. Kamati itaandika maelezo ya mdaiwa huyo na kuyafikisha Mahkamani. Kama mdaiwa wa namna hiyo atateua wakili, basi kamati haitaandika maelezo ya mdaiwa.

 

Imaam ash-Shafi’iy anakubaliana na Hakimu kuhamia kwenye eneo la mdaiwa ikiwa anayedaiwa ni mwanamke. Ametumia kisa cha Unays aliyeamrishwa na Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam):

 

“Nenda ewe Unays kwa mwanamke wa (kesi hii) hili, akikubali (tuhuma za zinaa nje ya ndoa), mpige mawe hadi kufa.”[12]

 

Sheria ya Mwenendo wa Madai inaeleza kama ilivyo hapo juu. Hivyo, ni lazima wito uwe na saini pamoja na muhuri wa Mahkama.[13] Halikadhalika nakala moja ya wito itarejeshwa Mahkamani ikionesha jina na saini ya mpokeaji, tarehe na wakati ilipopelekwa.[14] Sheria pia haimlazimishi mwanamke aliyefungika na mila kufika Mahkamani. Hawa ni wale wanawake ambao hawaruhusiki kutoka nje kwa mujibu wa mila na tamaduni zao.[15]

 

 

Kutotii Kwa Mdaiwa Na Kuvamia Eneo La Mdaiwa

 

Kama mdaiwa bila ya sababu za msingi atakataa kufika Mahkamani hali ya kuwa amepelekewa wito rasmi wa kumtaka afike. Hakimu ataandika maelezo hayo pamoja na ushahidi wa mashahidi wawili. Hakimu atamtaarifu walii (mkuu wa mamlaka ya shehia/kata/eneo/kijiji) na gharama za utaratibu huo utakuwa ni juu ya mdaiwa mwenyewe. Ataadhibiwa kwa mijeledi au kifungo kulingana na amri ya Hakimu, kwa sababu ameshindwa kufuata amri ya Hakimu, na hivyo mdaiwa amedharau Mahkama.

 

Mdaiwa atawajibika kuadhibiwa kwa kutofika Mahkamani siku aliyopangiwa kufika ikiwa amepokea na kuukubali wito. Ni kosa la jinai kuidharau Mahkama na atawajibika kuadhibiwa. Hata hivyo, adhabu ya aliyekataa kupokea wito na kutofika ni kubwa kuliko kwa mtu aliyepokea na kukataa kufika[16].

 

Kama mdaiwa atajificha na kumkimbia tarishi, Hakimu atamuandikia walii kwa lengo la kumfikisha.

 

Itakapotokezea kutolewa habari kwamba mdaiwa aliwahi kuonekana kwa ushahidi wa mdai na walii ambaye ameshindwa kumfikisha mdaiwa Mahkamani. Na kama upo ushahidi wa kuwa yupo nyumbani kwake, basi Hakimu atatoa amri ya kuizingira nyumba yake na kugeuzwa jela kwa siku tatu. Kila siku ataulizwa, kama akikaidi itaendelelea hadi siku ya pili, ataulizwa tena, akikaidi, utaratibu huu utaendelea hadi siku ya tatu. Ikifika siku ya tatu bado amekaidi kufika Mahkamani. Hakimu atamteua wakili aisimamie kesi kwa niaba ya mdaiwa.

 

Lakini kwa mujibu wa al-Mawardi kwenye kesi ya mdaiwa kutotii amri ya kufika Mahkamani. Hakimu anaweza kutumia moja kati ya njia zifuatazo:

 

1)    Kumlazimisha kwa msaada wa tarishi kufika Mahkamani.

2)    Kuihamisha kesi yake mamlaka ya juu ambayo itamlazimisha kufika Mahkamani.

3)    Kuteua watu wawili waadilifu ambao watamwita mbele ya mlango wa nyumba yake kufika Mahkamani na kujibu madai[17].

 

Kwa maoni ya Maliki anaeleza kwamba, Hakimu asimlazimishe mdaiwa, isipokuwa kama Hakimu ataridhika kwamba masuala ya fedha yalifanyika baina ya mdai na mdaiwa. Kwa sababu mtu anaweza tu kufungua kesi ili kumtia doa mwenziwe. Hata hivyo, Ibn Qudaamah[18] hakubaliani na mawazo haya kwani anasema kuwa mdaiwa ni lazima alazimishwe kufika Mahkamani.

 

Al-Khassaaf anasema kwamba wanachuoni wetu wanaruhusu kufanya uvamizi kwenye eneo la mdaiwa wa fedha (mwenye deni) ambaye kwa makusudi anajificha. Hakimu Abu Yuusuf ameshawahi kutumia njia hii. Kwa maelezo ya as-Sarkhasi, utaratibu huu haufai.

 

Mfumo wa kuvamia kwenye kesi kama hii utakuwa kama ifuatavyo:

 

Hakimu atawapeleka watu wawili madhubuti, matarishi, wanawake na wahudumu. Matarishi watasimama kuizunguka nyuma ili kama akitoroka wamkamate. Wanawake na wahudumu wataingia ndani kumtafuta ili kumtoa hata kama amefichwa na wanawake wa familia yake.

 

Kwa kutetea hoja hiyo, al-Khassaaf ametoa vigezo vya Makhalifa waongofu, lakini uvamizi waliofanya unahusu maeneo yanayotuhumiwa kwa jinai, kama ulevi na kucheza dansi.

 

Ikiwa kwa njia hizo zote hazijafanikisha kumleta mdaiwa Mahkamani, Hakimu ataandika ushahidi uliotolewa na mdai na akiukubali ushahidi huo atatoa hukumu ya upande mmoja (bila ya kumsikiliza mdaiwa)[19].

 

Maelezo yote hapo juu yanaonesha wazi kwamba Mahakimu wa mwanzo wa Kiislamu walikuwa na hadhari kuhusiana na wito na huduma hizo. Ilikuwa ni wajibu wa Mahkama ya mamlaka ya juu kumtaarifu mdaiwa kuhusiana na hatua hiyo ili aweze kufika Mahkamani kujibu madai. Tofautisha na maoni ya Joseph Schacht kama ifuatavyo:

 

“Shari’ah za Kiislamu bado zinatumia njia za zamani za kuanzisha vitendo, ambavyo vinahusisha mdai kumkamata mdaiwa na kumburuza mbele ya Jaji (Hakimu)”[20].

 

Sheria inaruhusu kubandikwa hati ya wito kwenye nyumba ya mdaiwa. Njia hii hufuatwa iwapo Mahkama imeamini kwamba mdaiwa anakwepa kupatiwa wito huo au iwapo hapatikani kabisa au ameshindwa yeye binafsi au wakala wake kupokea wito huo.[21]Iwapo mpeleka notisi ametumia taratibu ya kuibandika hati ya wito, atatakiwa kula kiapo au Mahkama inaweza kumuamuru kwenda Mahkama nyengine ili kuthibitisha maelezo yake.[22]

 

Mahkama inaweza kuamuru mambo yafuatayo juu ya mtu ambaye amepatiwa hati ya wito na ameshindwa kufuata amri ya kufika:

 

a)    Kutoa hati ya kukamatwa (arrest warrant)

b)    Kushikilia na kuiuza mali yake/zake

c)     Kumtoza faini

d)    Kuamuru kuwasilisha dhamana ya mali na atakaposhindwa atahukumiwa kifungo cha jela kisichokuwa cha jinai (civil prison).[23]

 

Kufika Mdaiwa Mahkamani

 

Pale madai yatakapotolewa na kukamilisha taratibu kama zilivyo hapo juu na kuithibitisha Mahkama kwamba kweli ipo kesi ya kujibu. Mara nyengine, madai huweza kuwa hayana msingi na kupelekea kutupwa.[24] Prima facie, Hakimu atamuamuru mdaiwa kufika na kujibu madai.

 

Kila dai linalofunguliwa mbele ya Hakimu, ni lazima lifuate taratibu maalum za Sheria. Dai lililofuata taratibu za Sheria katika ufunguzi wake, itamlazimu mdaiwa kufika mbele ya Hakimu kujibu madai. [25]

 

 

Majibu Kwa Njia Ya Kujitoa

 

Pale wadaawa wanapofika Mahkamani, mdai ataulizwa kueleza kesi yake na kama ameweka kwa maandishi madai yake ayathibitishe. Baadaye Mahkama itamuita mdaiwa kutoa jibu lake, kama ina lazima. Mdaiwa kiurahisi anaweza kukataa dai hilo au kujitetea kwa njia ya kujitoa (daf’a). Ndani ya majibu kwa njia ya kujitoa inakuwa na madai ambayo yanaletwa mbele na mdaiwa mwenyewe, ambayo inatosa kujibu madai ya mdai. Kwa mfano, mtu anapodai kwa mwengine idadi fulani ya pesa kama ni deni analomdai, na mdaiwa kueleza kwamba alikuwa akidaiwa pesa hiyo lakini ameshalipa au mdai amemsamehe deni hilo au kwamba yeye na mdai wamewafikiana kulimaliza au kiasi hicho hakikuwa ni deni lakini ni gharama ya bidhaa fulani, ambazo yeye mdaiwa amenunua kwa ajili ya mdai. Kama mdaiwa atathibitisha dai lake la kujitoa, kesi ya mdai itafeli.

 

Pale mdaiwa anapobisha dai hilo, mdai ataitwa ili kuthibitisha madai yake. Kama mdai ataweza kutoa ushahidi wa kutosha unaokubalika, atalazimika kupatiwa maamuzi kwa ajili yake na kama si hivyo, anaweza tu kuita upande wa pili kuchukua kiapo kuthibitisha kukataa kwake. Kama upande wa pili utachukua kiapo, dai hilo dhidi yake litatupwa, lakini kama atakataa kula kiapo, utatolewa uamuzi wa hukumu. Hakimu, kwa mujibu wa hukumu za zamani precedence, anaweza kuegemeza amri zake kwenye uoni wake binafsi wa ukweli. Lakini siku hizi, anasema mwandishi wa Durru’l-Mukhtaar, hili halitokubaliwa kwa sababu ya maofisa kushiriki kwenye rushwa.[26]

 

Sheria inaeleza kwamba, mdaiwa atahitajika kuwasilisha majibu ya madai siku ya mwanzo ya kusikilizwa kesi yake au pale Mahkama itakapoamuru vyenginevyo.[27]

 

Mdaiwa katika kesi anaweza kujitoa dhidi ya madai ya mdai, kwa msingi wa kudai haki au dai. Kujitoa kwake hakutakuwa na ulazima kwamba iwe ni kwa misingi ya kulipwa au kutolipwa haki yake. Kujitoa huku kutakuwa na nguvu kama vile ni dai la pingamizi na Hakimu anaweza kutamka hukumu ya mwisho.

 

Iwapo kujitoa kwa mdaiwa kumezuiliwa na Mahkama au haiwezekani kwa mujibu wa hati ya mdai, mdaiwa atatakiwa kufungua dai jengine jipya kwa ajili ya kujitoa.

 

Iwapo imethibiti kwamba dai la kujitoa kwa mdaiwa ni la msingi, Mahkama inaweza kutoa amri ya kumvua mdaiwa dhidi ya madai ya mdai. Mahkama pia inaweza kuamuru malipo yoyote kutoka kwa mdai kwenda kwa mdaiwa.[28]

 





[1] Fataawa ‘Alamgiri, Juzuu ya III, uk. 584; al-Majallah, uk. 297; pia angalia Sheria ya Ushahidi ya Daftari la Benki, Sura ya 6, S. 3 – 6.

[2]  Sheria ya Ushahidi, S. cha 63

[3] Sheria ya Ushahidi, S. 63 (e)

[4] Sheria ya Ushahidi, S. 67

[5] Azad, Judicial System of Islam, uk. 80.

[6] Twaha Jaabir al-Alwany katika kitabu cha Uswuulul al-Fiqh ametafsiri Al Istihsaan: Kuikubali Qiyaas-kufananisha ambayo inaonekana kuwa juu kisheria kwa kulinganisha na mfananisho ulio dhahiri. Ni katika maelezo hayo ambapo al Istihsaan inakuja kwa mara kadhaa kutafsiriwa kama ni “Hiari ya Mwanachuoni”.

[7] Qiyaas: inahusu suala kwa kulifananisha na jengine, pia suala hilo linazungumzwa ndani ya Qur-aan au Sunnah.

[8] Azad, Judicial System of Islam, uk. 81.

[9] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. V, r. 1 (2) na (3).

[10] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. V, r. 16.

[11] Ibid, O. V, r. 17.

[12] Azad, Judicial System of Islam, uk. 83.

[13] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. V, r. 10; angalia pia Sheria ya Mahkama ya Ardhi no. 12 ya 1994, S. 23 – 25.

[14] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. V, r. 18.

[15] Sheria ya Mwenendo wa Madai, S. 111 (1).

[16] Azad, Judicial System of Islam, uk. 82.

[17] Azad, Judicial System of Islam, uk. 83.

[18] Azad, Judicial System of Islam, uk. 83.

[19] Ibn Qudamah; Akhbaar al-Qudhaat, IX, uk. 109.

[20] An Introduction to Islamic Law, uk. 16.

[21] Sheria ya Mwenendo wa madai, O. V, r. 17 na 20.

[22] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. V, r. 19.

[23] Sheria ya Mwenendo wa Madai, S. 24.

[24] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. VII, r. 12.

[25] Sheria ya Mwenendo wa Madai, S. 19 na 20.

[26] Durru’l-Mukhtaar’, Juzuu ya IV, uk. 391, pia Raddu’l-Mukhtaar.

[27] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. VIII, r. 1.

[28] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. VIII, r. 6 (1) na (8).

Share