03 - Mambo Ya Haramu Kwa Vinyozi: Kunyoa Nyusi

Mambo ya Haramu yanayofanyika katika kazi ya Unyozi:

 

 

3. Kunyoa Nyusi

 

Vilevile baadhi ya vinyozi hukata vijana wa kiume nyusi. Vijana wanaoiga wanamuziki na wachezaji mpira. Kijana akiona mcheza mpira maarufu kaweka mistari kwenye nyusi zake naye aenda kumuiga.

Vinyozi wanapoendewa na vijana kama hao, wao “pesa mbele dini baadae” wanatekeleza wateja wao wanavyotaka. Mteja akikaa tu kwenye kiti, akiamrisha afanyiwe mtindo wowote, basi naye kinyozi asiyejitambua ambaye ima hajui chochote kuhusu mafunzo ya dini yake na hataki kujishughulisha kujua, au anajua lakini pesa imegeuka kuwa ndio dini yake, basi hutekeleza yale mteja anayoyataka tena wakati mwengine kwa fakhari aonekane mnyoaji mahiri na hakuna mtindo unaomshinda!

Kutoka kwa 'Abdullah bin Mas'uwd (Radhwiya Allahu 'anhu) kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Allaah Amewalaani watu wenye kuwachanja wenzao (tattoo) na wenye kuchanjwa, na wenye kuwanyoa wenzao nyusi na wenye kunyolewa na wenye kuchonga meno yao (kama kufanya mwanya) kwa ajili ya kujipamba kubadilisha maumbile ya Allaah) [Al-Bukhaariy na Muslim]

Kitendo cha unyoaji nyusi japo kwa mazoea kinafanywa na wanawake, na laana hizo zinawaendea wanaofanya na kuwafanyia wenzao hivyo, lakini kwa mwanamme laana inakuwa ni kali zaidi kwani kunapatikana maharamisho mawili ndani yake; ya kunyoa nyusi na ya kujifanananisha na wanawake.

Eee mja ikiwa unamuogopa Mola wako na Siku ya Mwisho na adhabu ya Moto, jiepushe na matamanio hayo machafu ya kipumbavu ambayo hayakunufaishi chochote wala kukuongezea zaidi ya kumuasi Mola wako na kujipalilia adhabu Yake isiyostahamilika.

Share