05 - Mambo Ya Haramu Kwa Vinyozi: Kukosa Swalaah Au Kukosa Swalaah Kwa Wakati

Mambo ya Haramu yanayofanyika katika kazi ya Unyozi:

 

5. Aghlabu Vinyozi Wengi Hukosa Swalaah Au Kwa Uchache Kukosa Swalaah Kwa Wakati

 

Kama tulivyogusia katika kipengele kilichotangulia, vinyozi wengi hawaswali na wale wanaoswali hawaswali kwa kipindi. Wengi wanapitwa na Swalaah kwa khofu ya kumuacha mteja wake anamsubiri au khofu ya wateja kumkimbia!

Maskini hawatambui kuwa rizki yao ishakadiriwa na Allaah, na hata wafanye ujanja wote na hila zote na mbinu zote hawatoweza kuongeza kile walichokadiriwa.

Khofu hiyo ya rizki na pia zaidi ni tamaa ya kupata zaidi na kutajirika na kuwa na maisha mazuri na kushindana na walio juu yao kidunia, huwapelekea hata vinyozi wengine katika baadhi ya miji wakionekana kwenda kufanya vibarua vingine vya ziada vya kuzidisha kipato japo utaona kazi yake inamuingizia kipato cha kutosha – japo kwa haramu nyingi kama tulivyoona juu -.

Tamaa na kukosa kuridhika, kunachangia sana katika kukiukwa maamrisho ya Allaah na Mtume Wake na ni sababu ya maasi kuzidi.

Saluni zingine ziko karibu na Misikiti lakini hata hawajui nyakati za Jamaa’ah hususan kuna maeneo Adhana haisikiki nje. Kuna mteja mmoja alikwenda kukatwa nywele na ilipofika karibu na Swalaah ya Maghrib akauliza Maghrib bado dakika ngapi, basi hakuna katika waliokuwemo humo ndani aliyemjibu. Akaaga na kuwahimiza kwenda kuswali, wakamwambia tunakuja “ya kumtoa njiani”!

Hiyo ndio misiba katika misiba mingi iliyomo kwenye maeneo hayo.

Wale wanaojitahidi kuswali, basi hupishana hapo hapo saluni, mmoja ataingia pembeni kuswali "Swalaah ya kuwahi mteja asiondoke", na kisha mwenzake kukipungua wateja naye ndio atakwenda kuswali hata kama muda wa Swalaah umekwisha au zimepandiana Swalaah mbili au tatu kwa wakati mmoja!

Tunawazindua umuhimu wa Swalaah na madhara ya mwenye kutokuswali au kuzipuuza Swalaah kwa kuswali atakavyo au kuswali na kuacha.

Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) kwa wale wanaopoteza Swalah zao:

"Lakini wakaja baada yao walio wabaya, wakaacha Swalah, na wakafuata matamanio. Basi watakuja kuta malipo ya ubaya." [Maryam: 59]

Kutoka kwa Jaabir bin 'Abdillaah kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: "Hakika Baina ya mtu na shirki, na kufru, ni kuacha Swalaah." [Muslim]

Kutoka kwa Buraydah bin Al-Haswiyb (Radhiya Allaahu 'anhu ambaye amesema: "Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akisema: "Ahadi (mafungamano) baina yetu na baina yao (wasio Waislam) ni Swalaah, atakayeiacha atakuwa amekufuru." [Ahmad, Abu Daawuwd, An-Nasaaiy na Ibn Maajah]

Anasema Ibn Hazm;

“Imepokelewa kutoka kwa 'Umar bin Khatwtwaab na 'Abdur-Rahmaan bin 'Awf na Mu'aadh bin Jabal na Abu Hurayrah na Maswahaba wengi (Radhwiya Allaahu 'anhum) kuwa: “Atakayeacha kuswali (Swalaah moja tu ya) fardhi kusudi (bila ya udhuru wowote) mpaka wakati wake (Swalaah hiyo) ukatoka, anakuwa kafiri.”

Imaam Ash-Shawkaaniy amesema: 

“Kwa hakika asiyeswali ni Kafiri, kwa sababu Hadiyth zote zilizopokelewa katika maudhui haya zinamwita hivyo (kuwa ni kafiri), na mpaka uliowekwa baina ya mtu anayestahiki kuitwa kafiri na yule asiyestahiki kuitwa kafiri ni Swalaah.”

Vile vile asiyeswali atafufuliwa na watu waovu kabisa siku ya Qiyaamah kama alivyosema Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) katika riwaya ifuatayo:

Kutoka kwa 'Abdullaah bin 'Amru bin Al-'Aasw: "Atakayeihifadhi atakuwa na mwanga na uongofu, na kufuzu siku ya Qiyaamah, na asiyeihifadhi hatokuwa na mwanga wala uongofu wala kufuzu, na siku ya Qiyaamah atakuwa pamoja na Qaaruwn, Fir'awn, Haamaan na Ubayy bin Khalaf." [Musnad Ahmad ikiwa na isnaad Swahiyh]

Katika kuifasiri Hadiyth hii, anasema mwanachuoni maarufu Ibn Qayyim Al-Jawziyyah:

“Mwenye kuacha Swalah huwa ameshughulika na mojawapo kati ya yafuatayo; ama atakuwa imemshughulisha mali yake au ufalme wake au cheo chake au biashara zake. Yule aliyeshughulika na mali yake, atafufuliwa pamoja na Qaaruwn, na aliyeshughulika na ufalme wake, huyo atakuwa pamoja na Fir'awn, na aliyeshughulika na cheo chake atakuwa pamoja na Haamaan na yule aliyeshughulika na biashara zake (akaacha kuswali), huyo atakuwa pamoja na Ubayy bin Khalaf.”

 

Share