161-Aayah Na Mafunzo: Tahadharisho La Kufanya Khiyana

Aayah Na Mafunzo

Aal-‘Imraan

Tahadharisho La Kufanya Khiyana

Alhidaaya.com

 

 

Anasema Allaah (سبحانه وتعالى):

 

 وَمَا كَانَ لِنَبِيٍّ أَن يَغُلَّ ۚ وَمَن يَغْلُلْ يَأْتِ بِمَا غَلَّ يَوْمَ الْقِيَامَةِ ۚ ثُمَّ تُوَفَّىٰ كُلُّ نَفْسٍ مَّا كَسَبَتْ وَهُمْ لَا يُظْلَمُونَ ﴿١٦١﴾

Na haikuwa (ni tabia) kwa Nabiy yeyote kukhini (ngawira). Na yeyote atakayekhini atakuja na kile alichokikhini Siku ya Qiyaamah. Kisha italipwa kamilifu kila nafsi yale iliyoyachuma nao hawatodhulumiwa. [Aal-'Imraan: 161]

 

 

Mafunzo:

 

Abuu Maalik Al-Ashja’iy amehadithia kwamba Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) amesema: “Ghuluwl (khiyaana ya wizi) kubwa mbele ya Allaah ni kipande cha ardhi ambacho utakuta watu wawili majirani katika ardhi au katika nyumba kisha mmoja wapo akakata kipande cha ardhi ya mwenziwe (bila haki), basi akifanya hivyo, atafungwa nacho kutoka ardhi saba mpaka Siku ya Qiyaamah.” [Ahmad].

 

Pia,

 

Abuu Hurayrah (رضي الله عنه) amehadithia kwamba: Alisimama mbele yetu Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) akataja suala la kuiba ngawira, akalishadidia na kulitilia umuhimu jambo hilo, akasema: “Nisije kumkuta mmoja wenu siku ya Qiyaamah juu ya shingo yake kuna mbuzi anatoa sauti, juu yake kuna farasi anatoa sauti aseme: Ee Rasuli wa Allaah! Niokoe! Nitamwambia: Similiki kwako kitu chochote, hakika nilikubalighishia. Na juu ya shingo yake kuna ngamia anatoa sauti aseme: Ee Rasuli wa Allaah! Niokoe! Nitamwambia: Similiki kwako kitu chochote hakika nilikubalighishia. Na juu ya shingo yake kuna nguo zilizo chanikachanika zinapepea kisha aseme: Ee Rasuli wa Allaah! Niokoe! Nitamwambia: Similiki kwako kitu chochote hakika nilikubalighishia.[Al-Bukhaariy (2891)].

 

Na pia,

 

‘Umar bin Al-Khattwaab (رضي الله عنه) amehadithia kwamba: Siku ya vita vya Khaybar, Maswahaba wa Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) walimwendea na kusema: Fulani na fulani wamekufa shahidi, fulani na fulani wamekufa shahidi. Walipomtaja mmojawapo kuwa kafariki shahidi, Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) akasema: “Hapana! Nimemuona motoni kwa sababu ya kanzu aliyoiiba (katika ngawira).” [Ahmad na Muslim kwa riwaayah nyingine].

 

 

Share