Mume Wangu Aliyesilimu Haswali Nifanyeje?

SWALI:

Asalaam alykum,

Sifa zote njema anastahiki Allaah mola wa viumbe wote, aliyetukuka Mola mlezi wa ulimwengu wote.

Mimi Naitwa ………. , Nimeolewa na nina mtoto mmoja wa kike. Namshukuru Mwenyeezi mungu kwa kunipatia mume, ila nina tatizo katika ndoa yangu.

Kwanza ningependa nitoe History kidogo ya ndoa yangu labda ndo utaweza kufahamu swali langu lina lengo lipi ili mimi niweze kuelewa vizuri.

Kabla sijaolewa nilikuwa naishi na mama yangu mdogo ambaye yeye ni Mkristo, ndo kanielea kwa asilimia kubwa ya maisha yangu ingawa wazazi wangu wote wapo ila kwa upande wa mama alikuwa anaishi mbali sana na mimi, Baba yangu nilikuwa naishi nae hapa dar ila ameoa wake wawili na mama angu aliwa ni mke wa tatu lakini ndie bi mkubwa.

Katika maisha ya pale kwa mama yangu mdogo, tulikuwa na maisha magumu sana, mpaka ikafikia mahali nikamwambia Baba yangu mzazi kuwa hapa ninaishi maisha magumu kwani hawa wanakula nguruwe, halafu siwezi kuswali wala kufunga kwani vyombo ninavyotumika vinakuwa tayari vimeshatumika na nyama ya nguruwe. (ni mambo mengi siwezi kusimulia yote) Basi baba hakuweza kunisaidia chochote ndio kwanza aliniambia nitafute mchumba niolewe niwe na kwangu.

Mwenyeezi mungu akanijaalia nikapata mchumba lakini alikuwa Mkristo, kufatana na hali niliyokuwa nayo nikaona nibora niolewe hata na huyu mkristo ili niondokane na mama yangu mdogo.

Mwenyeezi mungu akanijaalia tukafunga ndoa kanisani ila mimi si kubadili dini nikabaki katika dini yangu ya uislam. Wakati tunaendelea na maisha yetu ya ndoa Baba yangu mzazi akawa hataki maisha yangu ya kuishi na mume ambae ni mkristo, lakini kwa nguvu za Mwenyeezi mungu mume wangu akabadili dini akawa muislam ila hataki wazazi wake wajue kuwa yeye ni muislam, na tutakafunga ndoa tena kwa dini ya Kiislam.

sasa swali langu ni hivi mume wangu ni muislam, ramadhani anafunga, ila hataki kuswali sio kwamba anaenda kanisani hapana hata mtoto wetu anasisitiza kuwa asome dini ya kiislam.

JE MIMI NIFANYE NINI ILI MUME WANGU AWEZE KUSWALI NA ASIWASIKILIZE NDUGU ZAKE ingawa mimi naswali na kufunga sunna kila Juma tatu na alhamis???

Ahsante.....

 


JIBU:

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Shukran zetu za dhati kwa dada yetu katika Imani kwa swali lako muhimu. Hili ni tatizo sugu katika jamii yetu kwa watoto kukosa malezi mema kutoka kwa wazazi wao. Ikiwa malezi hayo mema ya Kiislamu hayakuwa ni yenye kupatikana basi vijana na wasichana wanakuwa nje na twaa na hivyo kufanya wanavyotaka. Hili ni suala ambalo tunafaa tulizingatie sana ili kizazi kijacho kisiingie katika kidimbwi cha maasi na uchafu.

 

Dada yetu hayo uliyoyapata ukiwa mdogo ni katika mitihani ambayo kila mmoja wetu anapata kulingana na Imani yake. Allaah Aliyetukuka Anasema: “Hapana shaka Tutakujaribuni kwa chembe ya khofu, na njaa, na upungufu wa mali na watu na matunda. Na wabashirie wanao subiri” (2: 155).

 

Kwa mtihani huu wa awali ilionekana dhahiri kulingana na maelezo yako kuwa uliweza kuupita kwa kuweza kushindana na vishawishi chungu nzima na kutoka hapo ikiwa Imani yako ni barabara. Mbali na matatizo nyumbani kwa baba na mama mdogo Alhamdulillah, uliendelea kujihifadhi na kufuata maelekezo ya Dini hii Tukufu.

 

Lakini lililonishangaza mimi ni kushawishika kuolewa na asiyekuwa Muislamu hivyo kuanguka mtihani ambao ulikuwa ni rahisi na wenye dalili ya katazo la moja kwa moja la Qur-aan. Mume Mkristo hawezi kabisa kuwa mchumba wa mwanamke ambaye ni Muislamu. Hakika huko ni kujivua na Imani uliyokuwa nayo. Hivyo, uliyumba wakati ambao ulikuwa hufai kuwa na sifa hiyo. Chaguo lako hilo halikuwa bora kwani Allaah Aliyetukuka Amekataza tangamano baina ya mume Mkristo na mwanamke Muislamu kwa kauli Yake: “Wala msiwaoe wanawake washirikina mpaka waamini. Na mjakazi Muumini ni bora kuliko mshirikina hata akikupendezeni. Wala msiwaoze (binti zenu) wanaume washirikina mpaka waamini. Na mtumwa mwanamume Muumini ni bora kuliko mshirikina hata akikupendezeni. Hao wanaitia kwenye Moto, na Allaah Anaitia kwenye Pepo na maghafira kwa idhini yake. Naye huzibainisha Aya zake kwa watu ili wapate kukumbuka” (2: 221).

 

Hivyo, mwanzo unatakiwa utubie kabisa toba ya sawa sawa ili Allaah Aliyetukuka Akusamehe kwa kosa hilo la zinaa na huyo ambaye sasa ni mumeo. Allaah Aliyetukuka Anasema: “Enyi mlioamini! Tubuni kwa Allaah toba iliyo ya kweli!” (66: 8).

 

Na Allaah Anasamehe nadhambi yote: “Sema: Enyi waja Wangu walio jidhulumu nafsi zao! Msikate tamaa na rehema ya Mwenyeezi Mungu. Hakika Allaah husamehe dhambi zote. Hakika Yeye ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu” (39: 53).

 

Ni ajabu kwa baba yako kwake kuliwa nguruwe na kukataa wewe kuolewa na Mkristo na yote ni madhambi na hilo la pili ni madhambi zaidi. Allaah Aliyetukuka Ametuamuru: “Enyi mlioamini! Ingieni katika Uislamu kwa ukamilifu, wala msifuate nyayo za Shetani; hakika yeye kwenu ni adui aliye wazi” (2: 208).

 

Mume wako kwa kusilimu kwake bado ni Muislamu lakini ni asi na ni dhambi kwake kutoswali. Kila mwanadamu ana makosa yake na udhaifu wake wa kibinadamu, hivyo ni juu yako kumpatia nasaha mumeo kwa njia nzuri na kutumia njia zote. Unaweza kutumia watu katika Mashaykh na wengineo ambao wanaweza kuzungumza naye kwa njia nzuri. Allaah Aliyetukuka Anasema: “Waite waelekee kwenye Njia ya Mola wako Mlezi kwa hikima na mawaidha mema, na ujadiliane nao kwa namna iliyo bora” (16: 125).

 

Huu ni mtihani mwingine kwako kuwa wewe unafanya Ibadah lakini mume wako hayuko katika hilo. Fanya subira na InshaAllaah mambo yote yatakuwa sawa.

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share