Yanayompasa Bwana Harusi Na Bibi Harusi Siku Ya kufunga Ndoa

 

SWALI:

Namshukuru Allah kwa kunipa nafasi hii na namtakia rehema na amani Mtume wetu Mtukufu (SAW). Mimi Inshaallah natarajia kuoa hivi karibini na nimesoma mambo yanapofaa na yasiofaa kufanywa katika ndoa kama mlivyomjibu mwenzangu aliyetaka kujua yanayopaswa na yasiopaswa kufanywa katika ndoa, ila nilikuwa naomba ufafanuzi kidogo kwenye kipengele 2 (d) na (e) katika yanayopaswa kufanywa. 2(d) inasema kuwa 'Mume aweke mkono wake juu ya sehemu ya mbele ya kichwa cha mkewe na kumuombea dua Swali ni je kuna ulazima wa kuomba hii dua (Nimeiona duaa yenyewe) kwa sauti au hata kimoyo moyo inafaa? na 2(e) inasema 'Mume na mke waswali rakaa mbili, mke nyuma ya mume'. Swali ni je mume asalishe kwa kusoma sura kwa sauti au kimya kimya na je kuna sura zozote zinazofaa kusoma hapa?

Ninaelewa kuwa mna kazi nyingi katika kutuelimisha sisi ndugu zenu na tunawaombea wepesi Inshaallah.

 


 

JIBU:

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

Kwanza kabla hatujajibu swali lako, tunakukumbusha kuwa unapoandika jina la Allaah au Mtume, usifupishe mbele yake kwa kuweka (S.W.) au (S.A.W.) kama ilivyozoelekea na wengi, bali andika kwa kirefu maneno hayo bila ya kuyafupisha. Andika (Subhaanahu wa Ta’ala) baada ya kumtaja Allaah, na andika Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) au (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) baada ya kumtaja Mtume. Hivyo ndivyo inavyopaswa, na ndio heshima zaidi na utukufu na ndivyo inavyotamkwa na si kama inavyofupishwa na wengi kimazoea na kivivu

Shukrani zetu za dhati kwa swali lako. Hakika hakuna tatizo katika kuisoma duaa hiyo kwa kutoa sauti au kimoyo moyo. Hata hivyo, ni bora kuisoma kwa sauti ili naye mkeo aweze kuisikia na kuwa pamoja nawe katika hayo unayosoma.

Kitabu katika kiungo kifuatacho ni kitabu muhimu kabisa chenye mafunzo mengi yanayohusu wanandoa:

Adabu Za Ndoa Katika Sunnah Iliyotakasika (Aadabu Az-Zafaaf Fiy As-Sunnat Al-Mutwahharah)

Ama kuhusu Swalah ambayo unafaa kuwa Imaam ukimswalisha mkeo usiku wa mwanzo inatakiwa usome kwa sauti kwani Sunnah zote zinazoswaliwa kwa kwa jamaa huwa ni kwa namna hiyo. Mfano wa hizo ni kama Swalah ya Tarewehe, Tahajjud, Witr na nyenginezo. Pia Surah za kusomwa baada ya al-Faatihah katika Swalah hiyo hazikutajwa hivyo kukupatia nafasi wewe kama Imaam kusoma Surah unazotaka.

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share