Anaishi Katika Nyumba Isiyokuwa Na Masikilizano Aombe Du’aa Gani Naye Apate Mume Atoke Katika Nyumba

SWALI:

 

Asalaam Alaikum Warahmatullahi Wabarakaatu

 

Tuna ndugu yetu anaomba msaada yeye anaishi na kaka yake na wifi yake, ndani ya nyumba hiyo hamna masikilizano mazuri na yeye hana mume. Suala lake iko dua ambayo ataweza kuomba ili Mola Subhana Wataala amjaalie apate mume na yeye awe na kwake.


 

JIBU:

 

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

 

Shukrani zetu za dhati kwa swali lako kuhusu kuwa ndani ya nyumba iliyo na matatizo

.

Tufahamu kuwa tatizo moja au jengine ni katika mitihani ambayo mwanaadamu anakumbana nayo kwa njia moja au nyingine. Katika hali hiyo inafaa mtu asubiri sana kwani Allaah Aliyetukuka Amesema:

Hakika Allaah yu pamoja na wanaosubiri”.

 

Na hakika subira huvuta kheri.

 

Pia tufahamu kuwa hakuna dhiki juu ya dhiki; baada ya dhiki ni faraji. Na minajili hiyo, Anasema Aliyetukuka: “Hakika pamoja na dhiki huja faraji” (94: 6). Na faraji kwako huenda ikawa ipo karibu.

 

Ama kuhusu du’aa hakuna du’aa maalumu kuhusu hilo. Unachohitajika kufanya ni kumuomba Allaah Aliyetukuka katika nyakati ambazo du’aa hukubaliwa. Nyakati hizo ni kama zifuatazo:

 

1.     Baina ya Adhana na Swalah ya faradhi.

2.     Wakati umefunga.

3.     Wakati wa kufungua mwadhini siku unayofunga.

4.     Ukiwa katika sijdah.

5.    Baada ya kumaliza Tahiyyaatu kabla ya kutoa Salaam ndani ya Swalah.

6.     Wakati wa usiku unapoinuka kwa ajili ya Swalah ya Tahajjud.

7.     Wakati uko katika safari, na kadhalika.

 

Tunakuombea kila la kheri utoke katika balaa na mtihani huo.

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

Share