Afanyeje Ikiwa Mke Ni Mshindani Katika Ndoa?

SWALI:

 

Asaalamu aleikum warahamatullahi wabarakatu, Ama baad namshukuru Allah kwa kunipa fursa hii kuwauliza ndugu zangu Swali hili, Je Dini yasemaje kuhusu Mwanamke aliye mshindani kwa mumewe kwenye Ndoa? Shukran jazilaan

 


 

JIBU:

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

 

Shukrani zetu kwa swali lako kuhusu ushindani wa mke katika ndoa.

Ndoa ni maelewano baina ya mume na mke na huwa uhusiano na maelewano yao yanapelekea hadi mambo yao kuwa wanashauriana baina yao na kuafikiana kwa hilo.

Allaah Aliyetukuka Anatuambia:

Na mambo yao yakawa ni kwa kushauriana baina yao” (ash-Shuura 42: 38).

 

Katika maelewano ya watu wawili kukipatikana aina yoyote ya ushindani na mvutano, basi kunakuwa na matatizo ambayo yataleta mtetereko katika mahusiano hayo kwa jinsi ambayo jambo dogo tu linapofanyika kutapatikana na utesi ulio mkubwa sana. Mke kwa hali iliyo bora anatakiwa kuwa mnyenyekevu kwa mumewe na mtiifu ila tu inapofikia kuamrishwa kufanya maasiya.

 

Hivyo, ukihisi mke anakuwa mshindani inabidi ufuate njia zifuatazo ili kutatua tatizo hilo:

 

1.     Kuzungumza naye kwa njia ya kumnasihi na kufanikisha hilo tafuta wakati ambao ni munasibu na uzungumze naye kwa kumpa mawaidha mazuri na kwa upole.

 

2.     Ikiwa tatizo bado lipo basi itisha kikao baina yako wewe, mkeo na wazazi wake na wako ili kuzungumzia suala hilo ambalo linaharibu utulivu wa nyumba. Mazungumzo yawe ya upole na ulaini na huenda akafahamu makosa na akajirekebisha. Msisitizo katika kufanikisha hilo ni kila mmoja awe na ikhlaasw katika kikao hicho.

 

3.     Kuwashirikisha Mashaykh wenye elimu na taqwa ili wazungumze naye.

 

Tunatarajia na kuomba katika kufanya hivyo kutapatikana ufumbuzi.

 

Tunamuomba Allaah Aliyetukuka Awatilie tawfiki muweze kusuluhishiwa tatizo hilo.

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

Share