10-Riyaadhw Asw-Swaalihiyn: Mlango Wa Fadhila Ya Kwenda Msikitini

 

Riyaadhw Asw-Swaalihiyn

 

باب فضل المشي إلى المساجد

10-Mlango Wa Fadhila Ya Kwenda Msikitini

 

Alhidaaya.com

 

Hadiyth – 1

عن أبي هريرة رضي اللهُ عنه : أنَّ النبيَّ رسولَ اللهِ صلى الله عليه وسلم ، قَالَ : (( مَنْ غَدَا إلى المَسْجِدِ أَوْ رَاحَ ، أعَدَّ اللَّهُ لَهُ فِي الجَنَّةِ نُزُلاً كُلَّمَا غَدَا أوْ رَاحَ )) متفقٌ عَلَيْهِ .

Imepokewa kutoka kwa Abuu Huraiyrah (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: "Atakayetoks mapema kwenda Msikitini na akarudi Allaah atamuandalia makazi Peponi kila anapoenda au anaporudi." [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

Hadiyth – 2

عن أبي هريرة رضي اللهُ عنه : أنَّ النبيَّ صلى الله عليه وسلم ، قَالَ : (( مَنْ تَطَهَّرَ في بَيْتِهِ ، ثُمَّ مَضَى إلى بَيْتٍ مِنْ بُيُوتِ اللَّهِ ، لِيَقْضِي فَرِيضَةً مِنْ فَرَائِضِ اللَّهِ ، كَانَتْ خُطُواتُهُ ، إحْدَاهَا تَحُطُّ خَطِيئَةً ، وَالأُخْرَى تَرْفَعُ دَرَجَةً )) رواه مسلم .

Imepokewa kutoka kwake Abuu Huraiyrah (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: "Mwenye kujitwahirisha (kutawadha) nyumbani kwake kisha akaelekea kwenye nyumba miongoni mwa nyumba za Allaah ili atekeleze faradhi miongoni mwa faradhi za Allaah basi hatua yake moja inafuta dhambi na nyingine inanyanyua daraja yake." [Muslim]

 

Hadiyth – 3

 

وعن أُبيّ بن كعبٍ رضي اللهُ عنه ، قَالَ : كَانَ رَجُلٌ مِنَ الأنْصَارِ لاَ أَعْلمُ أَحَداً أبْعَدَ مِنَ المَسْجِدِ مِنْهُ ، وَكَانَتْ لا تُخْطِئُهُ صَلاَةٌ ، فَقيلَ لَهُ : لَوْ اشْتَرَيْتَ حِمَاراً لِتَرْكَبَهُ في الظَّلْمَاءِ وَفِي الرَّمْضَاءِ ، قَالَ : مَا يَسُرُّنِي أنَّ مَنْزِلِي إلى جَنْبِ المَسْجِدِ ، إنِّي أُرِيدُ أنْ يُكْتَبَ لِي مَمْشَايَ إلى المَسْجِدِ ، وَرُجُوعِي إذَا رَجَعْتُ إلى أهْلِي . فَقَالَ رَسُولُ اللهِ صلى الله عليه وسلم : (( قَدْ جَمَعَ اللَّهُ لكَ ذَلِكَ كُلَّه )) رواه مُسلِم .

Imepokewa kutoka kwake Ubayy bin Ka'ab (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba: "Kulikuwa na mtu katika Answaar wala simjui mtu yeyote aliyekuwa mbali na msikiti kama yeye. Na alikuwa hakosi Swalaah hata moja, hivyo akaambiwa: 'Lau kama ungenunua punda ili kumpanda wakati wa giza na wakati wa joto kali.' Akasema: 'Sipendelei kabisa nyumba yangu kuwa karibu na msikiti. Nami napenda niandikiwe kutembea kwangu kuelekea Msikitini na kurudi kwangu ninaporudi kwa familia yangu.' Akasema Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam): 'Hakika Allaah amekuandikia yote hayo katika hesabu yako'." [Muslim]

 

Hadiyth – 4

وعن جابر رضي اللهُ عنه ، قَالَ : خَلَت البِقاعُ حولَ المَسْجِدِ ، فَأَرَادَ بَنُو سَلمَةَ أنْ يَنْتَقِلُوا قُرْبَ المَسْجِدِ ، فَبَلَغَ ذَلِكَ النبي صلى الله عليه وسلم ، فَقَالَ لَهُمْ : (( بَلَغَنِي أنَّكُم تُريدُونَ أنْ تَنْتَقِلُوا قُرْبَ المَسْجِدِ ؟ )) قالوا : نعم ، يا رَسُول اللَّهِ ، قَدْ أرَدْنَا ذَلِكَ . فَقَالَ : (( بَنِي سَلِمَةَ دِيَارَكُم تُكْتَبْ آثارُكُمْ ، دِيَارَكُمْ تُكْتَبْ آثارُكُمْ )) فقالوا : مَا يَسُرُّنَا أنَّا كُنَّا تَحَوَّلْنَا . رواه مسلم ، وروى البخاري معناه من رواية أنس .

Imepokewa kutoka kwake Jaabir (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba: Ardhi kando ya msikiti ilikuwa tupu "Wakataka Banu (ukoo wa) Salamah kuhamia karibu na Msikiti. Habari hiyo ilimfikia Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam), ambaye aliwaambia: 'Hakika imenifikia mimi kuwa nyinyi mnataka kuhamia karibu na Msikiti?' Wakasema: 'Ndio, ee Rasuli wa Allaah, hakika sisi tumetaka kufanya hivyo.' Akasema: 'Bani Salamah, kaeni katika nyumba zenu kwani nyayo zenu zinaandikwa. Bani Salamah, kaeni katika nyumba zenu kwani nyao zenu zinaandikwa." [Muslim]

 

Hadiyth – 5

وعن أبي موسى رضي اللهُ عنه ، قَالَ : قال رَسُول اللَّهِ صلى الله عليه وسلم : (( إنَّ أَعْظَمَ النَّاسِ أجْراً في الصَّلاةِ أبْعَدُهُمْ إلَيْهَا مَمْشىً ، فَأَبْعَدُهُمْ ، وَالَّذِي يَنْتَظِرُ الصَّلاَةَ حَتَّى يُصَلِّيَهَا مَعَ الإمَامِ أعظَمُ أجْراً مِنَ الَّذِي يُصَلِّيهَا ثُمَّ يَنَامُ )) متفقٌ عَلَيْهِ .

Imepokewa kutoka kwa Abuu Muwsaa (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: "Mtu anayepata malipo zaidi katika Swalaah, ni yule anayekaa mbali zaidi na anyetembea mbali zaidi. Na pia yule anayesubiri Swalaah mpaka anaswali pamoja na Imamu malipo yake ni makubwa zaidi kuliko yule anayeswali kisha akalala." [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

Hadiyth – 6

وعن بُريدَة رضي اللهُ عنه ، عن النبيِّ صلى الله عليه وسلم ، قَالَ : (( بَشِّرُوا المَشَّائِينَ في الظُّلَمِ إلى المَسَاجِدِ بِالنُّورِ التَّامِّ يَوْمَ القِيَامَةِ )) رواه أبُو دَاوُدَ وَالتِّرمِذِيُّ .

Imepokewa kutoka kwa Buraydah (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: "Wapeni bishara njema wenye kutembea kuelekea Misikitini katika giza kuwa watapata nuru timilifu (kamili) Siku ya Qiyaamah." [Abuu Daawuwd na At-Tirmidhiy]

 

Hadiyth – 7

وعن أبي هريرة رضي اللهُ عنه : أنَّ رَسُول الله صلى الله عليه وسلم ، قَالَ : (( ألا أدُلُّكُمْ عَلَى مَا يَمْحُو اللهُ بِهِ الخَطَايَا ، وَيَرْفَعُ بِهِ الدَّرَجَاتِ ؟ )) قَالُوا : بَلَى يا رَسُول اللهِ ؟ قَالَ : (( إسْبَاغُ الوُضُوءِ عَلَى المَكَارِهِ ، وَكَثْرَةُ الخُطَا إلَى المَسَاجِدِ ، وَانْتِظَارُ الصَّلاَةِ بَعْدَ الصَّلاَةِ ، فَذَلِكُمُ الرِّبَاطُ ، فذَلِكُمُ الرِّبَاطُ )) رواه مسلِم .

Imepokewa kutoka kwa Abuu Huraiyrah (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: "Hivi niwafahamishe juu ya kile ambacho Allaah anafutia nacho makosa na ananyanyua nacho daraja?" Wakasema: "Kwa nini ee Rasuli wa Allaah, tufahamishe." Akasema: "Kujieneza wudhuu pamoja na machukivu ( kiviosha viungo pamoja na kutunza adabu na ukamilifu wake mbali na kuwa na taabu mfano wa ubaridi, hali ya hewa mbaya, kuumwa, n.k.) na wingi wa kupiga hatua kwenda Msikitini na kuingoja Swalaah baada ya Swalaah, huo ndio ulindaji." [Muslim]

 

Hadiyth – 8

وعن أبي سعيد الخدري رضي اللهُ عنه ، عن النبيِّ صلى الله عليه وسلم ، قَالَ : (( إذا رَأَيْتُمُ الرَّجُلَ يَعْتَادُ المَسَاجِدَ فَاشْهَدُوا لَهُ بالإيمَانِ ، قال اللهُ عزوجل : ( إِنَّمَا يَعْمُرُ مَسَاجِدَ اللهِ مَنْ آمَنَ بِاللهِ وَالْيَوْمِ الآخِرِ ) الآية )) رواه الترمذي، وقال: (( حديث حسن )).

Imepokewa kutoka kwa Abuu Sa'iyd Al-Khudriy (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: "Mnapomuona mtu anazoea Msikitini mshuhudie kuwa ana Imani. Amesema Allaah Ta'aalaa: 'Hakika wanaoamirisha Misikiti ya Allaah ni wale wanaomwamini Allaah na Siku ya Mwisho, na wakasimamisha Swalaah na wakatoa Zakaah na hawamkhofu (yeyote) isipokuwa Allaah. Basi asaa hao wakawa miongoni mwa walioongoka'. [At-Tawbah: 18]." [At-Tirmidhiy, na akasema Hadiyth Hasan]

 

 

 

Share