Kujisafisha Masikio Kunabatilisha Swawm?

 
 
 
SWALI:
 
 
Swali langu ninauliza je mtu anpojisafisha masikio kwa kutumia kijiti bila ya kujuwa wakati amefunga ,funga yake ni batili Shehe naomba unisaidi
 
 

 
JIBU:
 
Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu 'anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho
 
Kusafisha masikio hakubatilishi Swawm kwani sio miongoni mwa mambo yanayoharibu Swawm.
 
Yafuatayo ni mambo yanayobatilisha Swawm na yasiyobatilisha:
 
 
 
Yanayobatilisha (Yanayoharibu) Swawm:
 
1.       Kula na kunywa kwa makusudi. Na sio kwa kusahau wala kwa bahati mbaya au kwa kulazimishwa, katika mchana wa Swawm.
2.       Kujitapisha kwa makusudi. Kuwe kujitapisha huko kwa kutia kidole mdomoni au kunusa kitu kitachopelekea kutapika.
3.       Mume kumuingilia Mke wake. Na pia kumkumbatia au kumchezea hadi yakamtoka manii.
4.       Kujichua (kuyatoa manii) kwa makusudi ima kwa mkono au kwa kuchezewa na Mkeo au kwa njia yoyote ile. Ama manii hayo yakitoka kwa kuota (ndoto) au kutazama (bila kukusudia) basi haiharibu Swawm.
5.       Kupatwa na Hedhi au Nifasi kwa Mwanamke. Hata kukiwa kutokea huko kuwa ni wakati wa kukaribia kufuturu/kufutari.
6.       Mwenye kutia Nia ya kula wakati amefunga, kwa sharti kuwa kaazimia tendo hilo hata kama hakulitekeleza.
7.       Kudhania kuwa jua lishazama magharibi au bado hakujapambazuka (yaani haujaanza wakati wa kufunga), kisha akala akanywa au akamuingilia mke wake.
Yasiyobatilisha (Yasiyoharibu) Swawm)
 
1.       Kula au kunywa kwa kusahau, kimakosa au kulazimishwa.
2.       Kuingia maji ndani ya matundu ya mwili bila kukusudia, kwa mfano wakati wa kuoga.
3.       Kudungwa sindano mwilini wakati wa maradhi.
4.       Dawa ya maji idondoshewayo machoni.
5.       Kujipulizia dawa ya asthma mdomoni (puffer au inhaler).
6.       Kuoga na kujimwagia maji mwilini wakati wa joto kali.
7.       Kuonja chakula kwa mpishi kwa sharti asimeze kile akionjacho.
8.       Kumbusu au kumkumbatia mkeo, kwa sharti awe mtu ana uwezo wa kujizuia na kudhibiti matamanio yake.
9.       Kupiga chuku (cupping), ikiwa kupika chuku huko hakutomfanya huyo mtu adhoofike. Ingawa kuna baadhi ya Maulamaa wanaona kuwa haifai.
10.   Haitobatilika Swawm ya mtu atakayeamka na janaba au atakayeota mchana wa Swawm akatokwa na manii.
11.   Kuingia harufu ya manukato au udi puani mwake. Ingawa baadhi ya Maulamaa wanasema ni vizuri kujiepusha moshi usiingie hadi kufika tumboni.
12.   Kupiga mswaki, kusukutua au kusafisha pua kwa kutia maji puani bila kuzidisha.
 
 
Na Allaah Anajua zaidi
 
 
Share