Anaswali Na Kuacha Lakini Anasoma Qur-aan Je, Anahukumiwa Vipi?

 

SWALI:

 

Naomba munifafanulie, je ikiwa Muislam anaacha Sala mara kwa mara, mara atasalii mara hasali, lakini anapenda

 

sana kusoma Quraan takriban siku zote kila wakati anapopata nafasi. Je, ana malipo gani kwa mola mtu huyu?

 


 

JIBU:

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola i wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

Shukrani zetu za dhati kwa swali lako hilo zuri. Hakika ni kuwa kusoma Qur-aan kuna fadhila kubwa sana kwani Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:

Mwenye kusoma herufi kutoka kwa Kitabu cha Allaah atapata ujira mmoja, na ujira huu ni sawa na kumi mfano wake. Wala sisemi kuwa Alif Laam Miym ni herufi moja lakini Alif ni herufi na Laam ni herufi na Miym ni herufi” (At-Tirmidhiy, na akasema ni Hadiyth Hasan Swahiyh na ameipokea ad-Daarimiy nayo ni Sahihi). Qur-aan haifai kusomwa tu bali inatakiwa ifahamike na itiwe katika maisha kwa kufuata kimatendo. Hakika ni kuwa wenye kushikamana nayo wameokoka na wamefaulu na wenye kupuuza wamehiliki na wamepata hasara.

Ni ajabu kuwa Muislamu mfano wa huyu atapenda kuisoma Qur-aan lakini kukosa kuifuata. Tufahamu kuwa huyu Muislamu bado ana Imani hivyo ni juu yetu na yako kujaribu kumlingania ili arudi katika njia ya sawa na haki, Uislamu. Kusoma huko Qur-aan bila kuswali hakumnufaishi yeyote yule kwa chochote ila atubu na kujirekebisha.

Swalah ina fadhila kubwa sana, hivyo kukosa kuswali ni kosa kubwa. Swalah ni amali ya kwanza itakayokaguliwa Siku ya Qiyaama na ndio ufunguo wa Pepo. Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:

Faradhi ya mwanza atakayoulizwa Muislamu Siku ya Qiyaama kuwa kaitekeleza – na kaitekeleza vilivyo – ni Swalah. Ikiwa aliitekeleza vilivyo basi kunatarajiwa atafaulu. Ikiwa hakuitekeleza au kaitekeleza, lakini sivyo ndivyo, basi itatazamwa Swalah za Sunnah, na alizileta vilivyo … Ama ikiwa hana hata Sunnah au kaitekeleza sivyo ndivyo, basi keshapata khasara” (Ahmad, Abu Daawuud, at-Tirmidhiy, an-Nasaaiy na Ibn Maajah).

Amesema tena (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam):

Funguo za kufungulia milango ya Peponi ni Swalah” (Muslim).

Ubaya wa kuacha Swalah ni mkubwa sana kwani Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala) Anasema:

Lakini wakaja baada yao walio wabaya, wakaacha Swalah, na wakafuata matamanio. Basi watakuja kuta malipo ya ubaya” (19: 59).

Na pia: “Ni nini kilichokupelekeni Motoni? Waseme: Hatukuwa miongoni waliokuwa wakiswali” (74: 42 -43).

Na Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:

Kizuizi kilichoko baina ya mtu na ukafiri ni Swalah” (Muslim).

Pia: “Tofauti baina yetu Waislamu na wasio Waislamu ni Swalah” (Abu Daawuud, an-Nasaa’iy na Ibn Maajah).

Hivyo, tumeona kuwa kukosa kuswali kunafanya amali za Muislamu zote kupomoka na kutokuwa na faida yoyote. Lakini mkosa akitubia na kufanya matendo mazuri malipo yake yatakuwa makubwa. Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala) Anasema:

Isipokuwa waliotubu, wakaamini, na wakatenda mema. Hao, basi, wataingia Peponi wala hawatadhulumiwa chochote” (19: 60).  

Tafadhali ingia katika kiungo kifuatacho usome makala muhimu kabisa zinazohusu Swalah, makatazo ya kuacha kuswali, adhabu zake n.k na tunakupa nasaha kuwa usiache kabisa kuswali kwani hatari ya kuacha kuswali ni kubwa mno kama utakavyosoma katika hizi makala.

Swalah

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

Share