Laylatul-Qadr- Vipi Uweze Kuupata Usiku Huu?

 

Laylatul-Qadr- Vipi Uweze Kuupata Usiku Huu?

 

Imekusanywa Na:  Alhidaaya.com

 

 

Tunaingia kumi la mwisho la Ramadhwaan, kumi ambalo ndani yake kuna Laylatul-Qadr. ‘ibaadah yoyote itakayotendwa usiku huo, ni bora kuliko ‘ibaadah ya miezi elfu.

 

Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

بِسْمِ اللَّـهِ الرَّحْمَـٰنِ الرَّحِيمِ

 

إِنَّا أَنزَلْنَاهُ فِي لَيْلَةِ الْقَدْرِ ﴿١﴾

Hakika Sisi Tumeiteremsha Qur-aan katika Laylatil-Qadr (usiku wa Qadar).

 

وَمَا أَدْرَاكَ مَا لَيْلَةُ الْقَدْرِ ﴿٢﴾

Na nini kitakachokujulisha ni nini huo Laylatul-Qadr?

 

لَيْلَةُ الْقَدْرِ خَيْرٌ مِّنْ أَلْفِ شَهْرٍ ﴿٣﴾

Laylatul-Qadr ni mbora kuliko miezi elfu.

 

تَنَزَّلُ الْمَلَائِكَةُ وَالرُّوحُ فِيهَا بِإِذْنِ رَبِّهِم مِّن كُلِّ أَمْرٍ ﴿٤﴾

Wanateremka humo Malaika na Ar-Ruwh (Jibriyl) kwa idhini ya Rabb wao kwa kila jambo.

سَلَامٌ هِيَ حَتَّىٰ مَطْلَعِ الْفَجْرِ ﴿٥﴾

Amani mpaka kuchomoza Alfajiri.    [Al-Qadr: 1-5]

 

Hadiyth mbali mbali zimethibiti kuhusu fadhila za usiku huu mtukufu na jinsi Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alivyokuwa katika masiku kumi ya mwisho ya Ramadhwaan.

 

Hesabu ya thawabu za usiku huo ni kama ifuatavyo:

 

Miezi elfu moja ni sawa na miaka themanini na tatu na miezi mitatu takriban. (1000 ÷ 12 = 83.3)

Utakapokuwa umo katika ‘ibaadah usiku huo wa Laylatul-Qadr, basi utaandikiwa thawabu za miaka 83! Juu ya hivyo, ‘ibaadah ya usiku huo ni bora zaidi kuliko ‘ibaadah ya miaka themanini na tatu.  

 

 

Mazingatio kuhusu Laylatul-Qadr na yapasayo kutekelezwa:

 

1-Mwenye kukosa Laylatul-Qadr atakuwa ni mwenye kula hasara kwa dalili: 

 

عَنْ أَبِي هُرَيْرَة رَضِيَ اللَّه عَنْهُ قَالَ : لَمَّا حَضَرَ رَمَضَان قَالَ رَسُول اللَّه صَلَّى اللَّه عَلَيْهِ وَسَلَّمَ  (( قَدْ جَاءَكُمْ شَهْرُ رَمَضَان شَهْرٌ مُبَارَكٌ اِفْتَرَضَ اللَّهُ عَلَيْكُمْ صِيَامَهُ تُفْتَح فِيهِ أَبْوَاب الْجَنَّة وَتُغْلَق فِيهِ أَبْوَابُ الْجَحِيم وَتُغَلُّ فِيهِ الشَّيَاطِين فِيهِ لَيْلَة خَيْرٌ مِنْ أَلْف شَهْر مَنْ حَرُمَ خَيْرهَا فَقَدْ حُرِمَ)) وَرَوَاهُ النَّسَائِيّ

Imepokelewa kutoka kwa Abuu Huraryah (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba ilipofika Ramadhwaan, Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Umekujieni mwezi wa Ramadhwaan, ni mwezi wa Baraka.  Imefanywa Swawm kwenu kuwa ni fardhi, milango ya Jannah hufunguliwa na milango ya moto hufungwa na mashaytwaan hufungwa. Katika mwezi huu, kuna usiku ulio bora kuliko miezi elfu.  Atakayenyimwa kheri zake, basi hakika amenyimwa!)) [An-Nasaaiy]

 

2-Siku hiyo ni siku iliyoteremeshwa Qur-aan. Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa): 

 

بِسْمِ اللَّـهِ الرَّحْمَـٰنِ الرَّحِيمِ

 

حم﴿١﴾

Haa Miym.

وَالْكِتَابِ الْمُبِينِ﴿٢﴾

Na Kitabu kinachobainisha.

 

إِنَّا أَنزَلْنَاهُ فِي لَيْلَةٍ مُّبَارَكَةٍ ۚ إِنَّا كُنَّا مُنذِرِينَ﴿٣﴾

Hakika Sisi Tumeiteremsha (Qur-aan) katika usiku uliobarikiwa, hakika Sisi daima ni Wenye kuonya.

فِيهَا يُفْرَقُ كُلُّ أَمْرٍ حَكِيمٍ﴿٤﴾

Katika (usiku) huo hupambanuliwa kila jambo la hikmah.     [Ad-Dukhaan: 1-4]

 

Maana ya: “(Usiku) Huo hupambanuliwa kila jambo la hikmah” ina maana: Usiku huo wa Laylatul-Qadr, majaaliwa yanahamishwa kutoka katika Al-Lawh Al-Mahfuwdhw (Ubao Uliohifadhiwa) kwenda kwa waandishi (Malaika) wanaoandika majaaliwa ya mwaka unaokuja; kuhusu uhai, rizki na yote yatakayomtokea mwana Aadam mpaka mwisho wa mwaka  [Imesimuliwa na Ibn 'Umar, Mujaahid, Abu Maalik, Adh-Dhwahaak na wengineo katika Salaf – Ibn Kathiyr: 8:671]

 

 

3-Kufanya juhudi kubwa katika ‘ibaadah masiku haya: 

 

Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa inapoingia kumi la mwisho alijitahidi kufanya ‘ibaadah kuliko siku zozote zingine:

 

عنْ  عائشة  رضي الله عنها : "كَانَ رَسُولُ اللَّهِ -صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ- يَجْتَهِدُ فِي الْعَشْرِ الْأَوَاخِرِ مَا لَا يَجْتَهِدُ فِي غَيْرِهِ

   

Imepokewa kwa 'Aaishah (Radhwiya Allaahu 'anhaa) kwamba: "Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)  alikuwa akijitahidi katika kumi la mwisho kuliko alivyojitahidi katika siku nyingine zozote" [Muslim]

 

Na katika Al-Bukhaariy na Muslim:  

 

  عنْ  عائشة  رضي الله عنها  قالت: "كَانَ النَّبِيُّ  صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ  إِذَا دَخَلَ الْعَشْرُ شَدَّ مِئْزَرَهُ وَأَحْيَا لَيْلَهُ وَأَيْقَظَ أَهْلَهُ"

  وفي رواية:  " أَحْيَا اللَّيْلَ وَأَيْقَظَ أَهْلَهُ وَجَدَّ وَشَدَّ الْمِئْزَرَ" رواه البخاري ومسلم.

Imepokewa kutoka kwa 'Aaishah (Radhwiya Allaahu 'anhaa):  "Ilipokuwa inaingia kumi (la mwisho) Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alikaza izaar (shuka) yake, akikesha usiku, na akiamsha ahli zake"

 

Na katika riwaayah nyingine:   “Akikesha usiku na akiamsha ahli zake na akijitahidi na kukaza shuka yake.” [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

 

4-Kwa Nini Umeitwa Laylatul-Qadr?

 

Imaam Ibn 'Uthaymiyn (Rahimahu-Allaah) amesema:

 

Kwanza: Kutokana na uwezo; nao ni utukufu kama vile kusema “fulani mwenye uwezo mkubwa" yaani mwenye hadhi au utukufu.   

 

Pili: Ni usiku ambao una makadirio na majaaliwa ya mwaka mzima na huandikwa yote yatakayotokea mwaka huo, na hii ni hikmah ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) na kuonyesha usanifu katika utengenezaji Wake na Uumbaji Wake.  

 

Tatu: Usiku huo una uwezo mkubwa kama alivyosema Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam):  

 

((مَنْ قَامَ لَيْلَةَ الْقَدْرِ إِيمَانًا وَاحْتِسَابًا غُفِرَ لَهُ مَا تَقَدَّمَ مِنْ ذَنْبِهِ)) متفق عليه

((Atakayesimama usiku wa Laylatul-Qadr kwa iymaan na kutaraji malipo, ataghufuriwa madhambi yake yaliyotangulia)) [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

 

5-Sababu Ya Kupewa Waislamu Laylatul-Qadr:

 

Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) aliona umri wa Ummah za mwanzo ni mrefu, na umri wa Ummah wake ni mfupi akapewa usiku wa Laylatul-Qadr uwe ni bora kuliko miezi elfu. [Muwatw-twaa 1/321 (Muhammad Fuad 'Abdil-Baaqy]

 

 

6-‘Ibaadah Za Kufanya Masiku Kumi Ya Mwisho:

 

 

a-Qiyaamul-Layl: (Kisimamo cha usiku kuswali):

 

 

عَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ أَنَّ رَسُولَ اللَّهِ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ قَالَ : ((مَنْ قَامَ رَمَضَانَ إِيمَانًا وَاحْتِسَابًا غُفِرَ لَهُ مَا تَقَدَّمَ مِنْ ذَنْبِهِ)) رواه البخاري 37 ومسلم 759 . 

 

Imepokelewa kutoka kwa Abuu Hurayrah (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Atakayesimama (kuswali) Ramadhwaan kwa iymaan na kutaraji malipo, ataghufuriwa madhambi yake yaliyotangulia)) [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

 

b-Kukithirisha kuisoma Qur-aan:

 

Kukithirisha kuisoma Qur-aan khasa kwa vile usiku wa Laylatul-Qadr ndio usiku ulioteremeshwa Qur-aan kama ilivotajwa katika Aayah zilizotangulia. Na imetajwa pia kuwa Qur-aan imeteremshwa katika mwezi wa Ramadhwaan kwa hiyo Muislamu inampasa aisome kwa wingi masiku yote ya Ramadhwaan. Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)

 

شَهْرُ رَمَضَانَ الَّذِي أُنزِلَ فِيهِ الْقُرْآنُ هُدًى لِّلنَّاسِ وَبَيِّنَاتٍ مِّنَ الْهُدَىٰ وَالْفُرْقَانِ ۚ  

Mwezi wa Ramadhwaan ambao imeteremshwa humo Qur-aan ili iwe mwongozo kwa watu na hoja bayana za mwongozo na upambanuo (wa haki na batili). [Al-Baqarah: 185]

 

Jibriyl ('Alayhis-Salaam) alikuwa akimteremkia Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kila usiku wa Ramadhwaan akimsomesha na kumsikiliza Qur-aan:

 

"كَانَ رَسُولُ اللَّهِ  صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ  أَجْوَدَ النَّاسِ وَكَانَ أَجْوَدُ مَا يَكُونُ فِي رَمَضَانَ حِينَ يَلْقَاهُ جِبْرِيلُ وَكَانَ يَلْقَاهُ فِي كُلِّ لَيْلَةٍ مِنْ رَمَضَانَ فَيُدَارِسُهُ الْقُرْآنَ"  رواه البخاري   

Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa ni   mkarimu zaidi  kuliko watu, na alikuwa mkarimu zaidi katika Ramadhwaan,  Jibriyl alikuwa akimjia kila usiku wa Ramadhwaan akimfundisha Qur-aan)) [Al-Bukhaariy]

 

 

c-I’tikaaf Msikitini:               

 

Kutia niyyah kubakia Msikitini kwa kufanya ‘ibaadah humo kwani Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akifanya hivyo:

 

 عن عائشة  رضي الله عنها  قالت: كَانَ النَّبِيُّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ  يَعْتَكِفُ فِي كُلِّ رَمَضَانٍ عَشْرَةَ أَيَّامٍ, فَلَمَّا كَانَ الْعَامُ الَّذِي قُبِضَ فِيهِ اعْتَكَفَ عِشْرِينَ يَوْمًا"   البخاري    

Imepokelewa kutoka kwa ‘Aaishah (Radhwiya Allaahu 'anhaa) kwamba: Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akifanya I'tikaaf kila Ramadhwaan siku kumi, ulipofika mwaka wake wa kuaga dunia alifanya I'tikaaf siku ishirini" [Al-Bukhaariy]

 

 

d-Kuomba Maghfirah:

 

Kwa sababu ni hatari mtu amalize Ramadhwaan bila ya Allaah kumghufuria madhambi!

 

عَنْ أَنَس وَغَيْره أَنَّ النَّبِيّ صَلَّى اللَّه عَلَيْهِ وَسَلَّمَ لَمَّا صَعِدَ الْمِنْبَر ثُمَّ قَالَ  (( آمِينَ آمِينَ آمِينَ)) " قِيلَ يَا رَسُول اللَّه عَلَامَ مَا أَمَّنْت ؟ قَالَ (( أَتَانِي جِبْرِيل فَقَالَ يَا مُحَمَّد رَغِمَ أَنْف رَجُل ذُكِرْت عِنْده فَلَمْ يُصَلِّ عَلَيْك قُلْ آمِينَ فَقُلْت آمِينَ ثُمَّ قَالَ رَغِمَ أَنْف رَجُل دَخَلَ عَلَيْهِ شَهْر رَمَضَان ثُمَّ خَرَجَ فَلَمْ يُغْفَر لَهُ قُلْ آمِينَ فَقُلْت آمِينَ ثُمَّ قَالَ رَغِمَ أَنْف رَجُل أَدْرَكَ وَالِدَيْهِ أَوْ أَحَدهمَا فَلَمْ يُدْخِلَاهُ الْجَنَّة قُلْ آمِينَ فَقُلْت آمِين))  صحيح الترمذي و قال الشيخ الأباني حسن صحيح  

Imepokelewa kutoka kwa Anas na wengineo kwamba Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alipopanda juu ya minbar aliitikia ((Aamiyn, Aamiyn, Aamiyn)). Alipoulizwa kwa nini ameitikia hivyo akasema: ((Amenijia Jibriyl akasema: “Ee Muhammad, ole wake yule ambaye unapotajwa hakuswalii, hivyo sema Aamiyn”. Nikasema Aamiyn. Kisha akasema: “Ole wake yule ambaye umeingia mwezi wa Ramadhwaan kisha akatoka bila ya kughufuriwa, kwa hiyo sema Aamiyn”. Nikasema Aamiyn. Kisha akasema: “Ole wake yule ambaye amewakuta wazazi wake au mmoja wa wazazi wake lakini wasimuingize Peponi. Hivyo sema Aamiyn”. Nikasema Aamiyn)) [Swahiyh At-Tirmidhiy na kasema Shaykh Al-Albaaniy kuwa Hadiyth hiyo ina daraja ya Hasan Swahiyh]

 

 

e-Du'aa Ya Kuomba Katika Siku Kumi Hizi za Mwisho:  

 

عن عَائِشَةَ، قالَتْ: قُلْتُ: يا رَسُولَ اللهِ، أرَأيْتَ إنْ عَلِمْتُ أيُّ لَيْلَةٍ لَيْلَةُ الْقَدْرِ، مَا أقُولُ فِيها؟ قَالَ: ((قُولي: اللَّهُمَّ إنَّكَ عَفُوٌّ تُحِبُّ العَفْوَ فَاعْفُ عَنِّي)).

Imepokelewa toka kwa ‘Aaishah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) kwamba amesema: “Ee Rasuli wa Allaah! Nieleze ikiwa nitajua usiku fulani ndio wa Laylatul-Qadr, niseme nini?” Akasema: ((Sema:

اللَّهُمَّ إنَّكَ عَفُوٌّ تُحِبُّ العَفْوَ فَاعْفُ عَنِّي

Allaahumma Innaka 'Afuwwun Tuhibbul-'Afwa fa'fu 'anniy.” (Ee Allaah Hakika Wewe ni Mwingi wa kusamehe, Unapenda kusamehe basi Nisamehe)) [An-Nasaaiy, Sunan Al-Kubraa (7712) Ibn Maajah (3850), Ahmad (25384)]

 

 

f-Kumdhukuru Allaah Kwa wingi kwa:

 

Tasbiyh: Kumsabbih kwa kusema:

سُبْحانَ الله

Subhaanah Allaah 

 

Tahmiyd: Kumhimidi kwa kusema:

الْحَمْدُ لِلَّه

AlhamduliLLaah

 

Tahliyl: Kumpwekesha kwa kusema:

لا إلهَ إلاّ الله

Laa ilaaha illa-Allaah

 

Takbiyr: Kumtukuza kwa kusema:

اَللهُ اَكْبَر

Allaahu Akbar  

 

 

g-Kuomba Du'aa:

 

Ramadhwaan ni mwezi wa kuzidisha kuomba du’aa kwa sababu Aayah za kuomba du’aa zipo kati ya Aayah za kuhusu Swawm:

 

 وَإِذَا سَأَلَكَ عِبَادِي عَنِّي فَإِنِّي قَرِيبٌ ۖ أُجِيبُ دَعْوَةَ الدَّاعِ إِذَا دَعَانِ ۖ فَلْيَسْتَجِيبُوا لِي وَلْيُؤْمِنُوا بِي لَعَلَّهُمْ يَرْشُدُونَ ﴿١٨٦﴾

Na watakapokuuliza waja Wangu kuhusu Mimi, basi Mimi ni Niko karibu (kwa ujuzi); Naitikia du’aa ya muombaji anaponiomba. Basi waniitikie Mimi na waniamini Mimi, wapate kuongoka.  [Al-Baqarah: 186]

 

 

7-Usiku Gani Unapatikana Laylatul-Qadr? 

 

Hadiyth kadhaa zimetaja kuhusu usiku wa Laylatul-Qadr. Imetajwa kuwa ni katika masiku kumi ya mwisho; siku ya ishirini na moja, au ishirini na tatu, au ishirini na tano au ishirini na saba au ishirini na tisa kwa dalili zifuatazo:

 

Ilothibiti Kuwa Ni Siku zote za Witr:

 

عائشة أن رسول الله صلى الله عليه وسلم قال: ((تَحرُّوا لَيلةَ القَدْرِ في الوَتْر من العَشرِ الأواخِرِ من رمضانَ)) رواه البخاري

 

Imepokelewa kutoka kwa  'Aaishah (Radhwiya Allaahu 'anhaa) kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)  amesema: ((Utafuteni usiku wa Laylatul-Qadr katika siku za witir kwenye siku kumi za mwisho za Ramadhwaan)) [Al-Bukhaariy]

 

Ilothibiti kuwa ni usiku wa ishirini na tisa, ishirini na saba, ishirini na tano:

 

عن ابنِ عبَّاس رضِيَ اللهُ عنهُما أنَّ النبيَّ صلَّى الله عليه وسلَّمَ قال: ((الْتمِسوها في العَشر الأواخِر من رمضانَ؛ لَيلةَ القَدْر في تاسعةٍ تَبقَى، في سابعةٍ تَبقَى، في خامسةٍ تَبْقَى )) رواه البخاريُّ (2021)

 

Imepokelewa kutoka kwa  Ibn 'Abbaas (Radhwiya Allaahu 'anhumaa) kwamba Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Utafuteni usiku wa Laylatul-Qadr katika siku kumi za mwisho za Ramadhwaan; katika (usiku wa) tisa, saba, na wa tano utakaobakia)) [Al-Bukhaariy]

 

 

Ilothibiti kuwa ni usiku wa ishirini na tatu:

 

 

عَنْ عَبْدِ اللَّهِ بْنِ أُنَيْسٍ، أَنَّ رَسُولَ اللَّهِ صلى الله عليه وسلم قَالَ ‏ ((أُرِيتُ لَيْلَةَ الْقَدْرِ ثُمَّ أُنْسِيتُهَا وَأَرَانِي صُبْحَهَا أَسْجُدُ فِي مَاءٍ وَطِينٍ))‏ ‏.‏ قَالَ فَمُطِرْنَا لَيْلَةَ ثَلاَثٍ وَعِشْرِينَ فَصَلَّى بِنَا رَسُولُ اللَّهِ صلى الله عليه وسلم فَانْصَرَفَ وَإِنَّ أَثَرَ الْمَاءِ وَالطِّينِ عَلَى جَبْهَتِهِ وَأَنْفِهِ ‏.‏ قَالَ وَكَانَ عَبْدُ اللَّهِ بْنُ أُنَيْسٍ يَقُولُ ثَلاَثٍ وَعِشْرِينَ ‏.‏

 

Imepokelewa kutoka kwa ‘Abdullaah bin Unays (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:  ((Nilionyeshwa Laylatul-Qadr kisha nikafanywa niusahau na nikaona kuwa asubuhi yake  nasujudu katika maji na udongo)) Akasema msimuliaji: “Tukanyeshewa mvua  usiku wa ishirini na tatu na Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akatuswalisha  na pindi alipoondoka kulikuweko na alama ya maji na udongo katika kipaja chake cha uso na puani mwake.”  Akasema: “‘Abdullaah bin Unays alikuwa akisema kwamba ulikuwa ni usiku wa ishirini na tatu.”  [Muslim]

 

 

8-Alama Zinazobainisha Laylatul-Qadr:

 

 

a-Mwezi kuwa na umbo la nusu sinia kutokana na Hadiyth:

 

عَنْ أَبِي حَازِمٍ، عَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ،  رضى الله عنه  قَالَ تَذَاكَرْنَا لَيْلَةَ الْقَدْرِ عِنْدَ رَسُولِ اللَّهِ صلى الله عليه وسلم فَقَالَ: ((أَيُّكُمْ يَذْكُرُ حِينَ طَلَعَ الْقَمَرُ وَهُوَ مِثْلُ شِقِّ جَفْنَةٍ)) مسلم

Imepokelewa kutoka kwa Abuu Haazim, kutoka kwa Abuu Hurayrah (Radhwiya Allaahu ‘anhu) aliyesema: “Tulitajiana Laylatul-Qadr kwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)  naye akasema: ((Yupi kati yenu ana kumbuka wakati ulipochomoza mwezi ukiwa mithili ya nusu sinia?)) [Muslim]

 

b-Kauli nyenginezo za baadhi ya Salaf:

 

  • Usiku huo unakuwa na mwanga zaidi. 
  • Upepo siku hiyo hutulia, yaani siku hiyo hautokei upepo mkali.
  • Hali ya hewa huwa nzuri.
  • Nyoyo za Waumini usiku huo huwa zina utulivu kuliko siku nyingine.
  • Baadhi ya watu wema huoteshwa usiku huo kama walivyokuwa wakioteshwa Salafus-Swaalih (wema waliotangulia) 

 

c-Asubuhi Yake:

 

عن أُبيِّ بنِ كَعبٍ رضِيَ اللهُ عنهُ قال: ((هي ليلةُ صَبيحةِ سَبعٍ وعِشرين، وأمارتُها أنْ تطلُعَ الشَّمسُ في صَبيحةِ يومِها بيضاءَ لا شُعاعَ لها  ((رواه مسلم (762)

 

Imepokelewa kutoka kwa ‘Ubay bin Ka'ab (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba: ((Huo ni usiku wa ishirini na saba na    alama yake jua siku hiyo hutoka likiwa halina mishale (mikali)" [Muslim]

 

Pia,

 

 

عَنِ ابْنِ عَبَّاسٍ رَضِيَ اللهُ عَنْهُمَا: أَنَّ رَسُولَ اللهِ قَالَ فِي لَيْلَة الْقَدْر: ((لَيْلَةٌ سَمْحَةٌ طَلقةٌ لاَ حَارَّة وَلاَ بَارِدَة تُصْبِح شَمْسُها صَبِيحَتَهَا ضَعِيفَة حَمْرَاء صحيح مسند الطيالسي (2680)، تعليق الألباني "صحيح"، صحيح الجامع (5475).

 

Imepokelewa kutoka kwa Ibn ‘Abbaas (Radhwiya Allaahu ‘anhumaa) kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Usiku ulio katika hali ya ukunjufu, hauna joto wala baridi, jua la asubuhi yake ni jekundu dhaifu)) [Swahiyh ameisahihisha Al-Albaaniy: Swahiyh Al-Jaami’ 5475]   

 

 Pia,

 

((ليلَةُ القَدْرِ لَيْلَةٌ بَلْجَةٌ ، لا حارَّةٌ ولا بارِدَةٌ ، ولا يُرْمَى فيها بنَجْمٍ ، ومِنْ علامةِ يومِها تَطلُعُ الشمْسُ لا شُعاعَ لَهَا)) رواه الطبراني  ومسند أحمد  

((Laylatul-Qadr usiku wa kung'aa [yaani wenye mwanga] sio joto wala baridi, na vimondo (nyota za kufyatuliwa) havitotumwa)) [At-Twabaraaniy na Ahmad na ameisahihisha Al-Albaaniy: Swahiyh Al-Jaami’ 5472 – Hadiyth ya ‘Ubaadah bin Asw-Swaamit na Waathilah bin Al-Asqa’ (Radhwiya Allaahu ‘anhumaa] 

 

Tunamuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Tawfiyq ya kutuwezesha  kukesha masiku kumi ya Ramadhwaan ili tujaaliwe kuupata usiku huu mtukufu, tutoke katika Ramadhwaan tukiwa tumeghufuriwa madhambi yetu yote. Aamiyn.

 

 

 

Share