Kwa Nini Uislamu Unataka Ushahidi Wa Wanawake Wawili Badala Ya Mmoja Kama Wanaume?

 

Kwa Nini Uislamu Unataka Ushahidi  Wa Wanawake Wawili Badala Ya Mmoja Kama Wanaume?

 

Alhidaaya.com

 

SWALI:

 

Assalam alaykum.

Mimi ni mwislamu na nimekabiliwa na swali ambalo linanitatiza mimi kwa sababu nimeulizwa na wengi wasiokuwa waislamu.Ijapokuwa nimejaribu kulijibu kwa elimu nilionayo naona bado hawajaridhika. Maswali ni mawili na ni yafuatayo:

1. Katika Qur'an tukufu wanaume waumini wamebashiriwa pepo na wameahidiwa wanawake wazuri ambayo hawajaingiliwa na binadamu yeyote wala jini. Je wananwake wamebashiriwa hayo? NA kuna maulama wanaosema waumini wa kiislamu waaume watafufuliwa na wake zao.

2. Utamwelezaje asiye muislamu kwa nini mwanamke kauli yake ni nusu ya mwanamume. Yaani ikiwa ni shahidi basi wanawake wanne wanatakikana au wanaume wawili.

Ninavyoamini mimi kila jambo la kiislamu tulioamrishwa kuna maana yake na alhamdulillah mengi nimetafuta maana na nikayapata.Ningependa kusikia mwislamu mwenzangu angejibu nini akiulizwa na asiyekuwa mwislamu maswali haya.

Shukran wa jazakAllaahu kheir.

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na Salaam zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Hakika ni kuwa Uislamu ulikuja kumtoa mwanmke katika minyororo aliyokuwa amefungwa nayo. Suala la mwanamke limezua mjadala mkubwa sana katika ulimwengu kwa sababu ya ujahili. Hata Waislamu wamekuwa katika njia panda kwa sababu hiyo hiyo. Mbali na ujahili, athari ya tamaduni za kimagharibi zimewafanya watu wasijue uhakika kuwahusu.

 

Mengi yamesemwa kuhusu hadhi na majukumu ya mwanamke wa Kiislamu. Yote haya yametokea kwa sababu ya nadharia zisizokuwa na msingi wowote wa dini. Wapotofu wa Kimagharibi mpaka sasa wana fikra chafu dhidi ya Uislamu. Hii ni dhahiri kulingana na makala ya mwandishi wa Woman in Islam (Mwanamke katika Uislamu): "Katika kipindi cha miaka 15 kuanzia nilipoingia katika Uislamu, nimeulizwa maswali mengi kuhusu maisha ya Muislamu na wasiokuwa Waislamu na marafiki zangu… wanauliza: Je, katika Uislamu, mnaamini kuwa mwanamke ana roho? Waislamu wanawake hawaswali au kwenda Makkah, je wanafanya hayo? Pepo ni kwa wanaume peke yao au sivyo?" Mengi ni kuwa mwanamke hana haki ya ilimu, kutoa rai, kuwa na akiba yake ya rasilmali au pesa, na kadhalika. Haya ni maswali ambayo yanaulizwa na yataendelea kuulizwa.

 

Ukitaja kujua neema ambayo Uislamu imempatia mwanamke soma kuhusu wanawake wanavyofanywa katika staarabu nyingine. Utakuta kuwa Uislamu umemuenzi mwanamke kwa kumpatia uhuru wa kumiliki atakacho, kuchuma, anashirikiana na mwanaume katika kunyanyua viwango vya maadili, kufanya Da'wah, kupata ilimu na kufundisha, kutoa rai na maoni, kushiriki katika Jihadi na mengineo mengi. Amepatiwa hadhi ya kijamii kama mama, mke, dada, binti, na kadhalika.

 

Hakika ni kuwa Pepo katika Uislamu na utukufu unategemea utendaji kazi na amali zake njema anazofanya. Wapo wanawake ambao wataingia motoni kama vile wanaume, na wapo wanawake ambao wataingia Peponi kama vile wanaume. Amali njema ni muhimu sana katika kufanikisha wepesi wa kuingia Peponi. Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Anatueleza kuwa ubora mbele yake ni uchaji Mungu. Hivyo ikiwa mwanamke ana Imani na taqwa zaidi atakuwa karibu zaidi na Allaah kama Alivyosema Aliyetukuka:

 

يَا أَيُّهَا النَّاسُ إِنَّا خَلَقْنَاكُم مِّن ذَكَرٍ وَأُنثَىٰ وَجَعَلْنَاكُمْ شُعُوبًا وَقَبَائِلَ لِتَعَارَفُوا ۚ إِنَّ أَكْرَمَكُمْ عِندَ اللَّـهِ أَتْقَاكُمْ ۚ إِنَّ اللَّـهَ عَلِيمٌ خَبِيرٌ﴿١٣﴾

Enyi watu! Hakika Sisi Tumekuumbeni kutokana namwanamme na mwanamke, na Tukakujaalieni  mataifa na makabila ili mtambuane. Hakika aliye na hadhi zaidi miongoni mwenu mbele ya Allaah ni mwenye taqwa zaidi kati yenu. Hakika Allaah ni Mjuzi wa yote, Mwenye upeo wa khabari za dhahiri na za kufichika. [Al-Hujuraat: 13.]

 

Ama kuhusu kuingia Peponi Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) katika Ayah nyingi Anatufahamisha dhahiri shahiri:

 

مَنْ عَمِلَ سَيِّئَةً فَلَا يُجْزَىٰ إِلَّا مِثْلَهَا ۖ وَمَنْ عَمِلَ صَالِحًا مِّن ذَكَرٍ أَوْ أُنثَىٰ وَهُوَ مُؤْمِنٌ فَأُولَـٰئِكَ يَدْخُلُونَ الْجَنَّةَ يُرْزَقُونَ فِيهَا بِغَيْرِ حِسَابٍ﴿٤٠﴾

Yeyote atakayetenda uovu, basi hatolipwa isipokuwa mfano wake; na yeyote atakayetenda mema kati ya mwanamume au mwanamke, naye ni Muumini, basi hao wataingia Jannah wataruzukiwa humo bila ya hesabu. [Ghaafir: 40]

 

Pia,

فَاسْتَجَابَ لَهُمْ رَبُّهُمْ أَنِّي لَا أُضِيعُ عَمَلَ عَامِلٍ مِّنكُم مِّن ذَكَرٍ أَوْ أُنثَىٰ ۖ بَعْضُكُم مِّن بَعْضٍ ۖ فَالَّذِينَ هَاجَرُوا وَأُخْرِجُوا مِن دِيَارِهِمْ وَأُوذُوا فِي سَبِيلِي وَقَاتَلُوا وَقُتِلُوا لَأُكَفِّرَنَّ عَنْهُمْ سَيِّئَاتِهِمْ وَلَأُدْخِلَنَّهُمْ جَنَّاتٍ تَجْرِي مِن تَحْتِهَا الْأَنْهَارُ ثَوَابًا مِّنْ عِندِ اللَّـهِ ۗ وَاللَّـهُ عِندَهُ حُسْنُ الثَّوَابِ ﴿١٩٥﴾

Basi Rabb wao Akawaitikia  Hakika Mimi Sipotezi ‘amali za mtendaji yeyote yule miongoni mwenu akiwa mwanamume au mwanamke, nyinyi kwa nyinyi. Basi wale waliohajiri na wakatolewa majumbani mwao na wakaudhiwa katika njia Yangu, wakapigana na wakauliwa; bila shaka Nitawafutia makosa yao na bila shaka Nitawaingiza Jannaat zipitazo chini yake mito, ni thawabu kutoka kwa Allaah.  Na kwa Allaah kuna thawabu nzuri kabisa. [Aal- 'Imraan: 195]

 

Na Amesema:

مَنْ عَمِلَ صَالِحًا مِّن ذَكَرٍ أَوْ أُنثَىٰ وَهُوَ مُؤْمِنٌ فَلَنُحْيِيَنَّهُ حَيَاةً طَيِّبَةً ۖ وَلَنَجْزِيَنَّهُمْ أَجْرَهُم بِأَحْسَنِ مَا كَانُوا يَعْمَلُونَ﴿٩٧﴾

Mwenye kutenda mema miongoni mwa wanamume au wanawake naye ni Muumin, Tutamhuisha uhai mzuri, na bila shaka Tutawalipa ujira wao kwa mazuri zaidi ya yale waliyokuwa wakitenda. [An-Naml: 97]

 

Uislamu umetufanya sote, wanawake na wanaume kuwa ndugu moja kama Alivyosema:

إِنَّمَا الْمُؤْمِنُونَ إِخْوَةٌ فَأَصْلِحُوا بَيْنَ أَخَوَيْكُمْ ۚ وَاتَّقُوا اللَّـهَ لَعَلَّكُمْ تُرْحَمُونَ﴿١٠﴾

Hakika Waumini ni ndugu, basi suluhisheni baina ya ndugu zenu. Na mcheni Allaah ili mpate kurehemewa. [Al-Hujuraat: 10)]

 

Pia ifahamike kuwa maamrisho yote ya 'Ibadah yameamriwa kwa wanaume na wanawake bila kubagua. Vile vile mwanamke au mwanaume akifanya kosa wanapata adhabu sawa kabisa. Kwa mfano mwanamke au mwanaume akiiba, Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Amebaini adhabu zao:

وَالسَّارِقُ وَالسَّارِقَةُ فَاقْطَعُوا أَيْدِيَهُمَا جَزَاءً بِمَا كَسَبَا نَكَالًا مِّنَ اللَّـهِ ۗ وَاللَّـهُ عَزِيزٌ حَكِيمٌ ﴿٣٨﴾

Mwizi mwanamume na mwizi mwanamke ikateni (kitanga cha) mikono yao; ni malipo kwa yale waliyoyachuma, ndio adhabu ya kupigiwa mfano kutoka kwa Allaah. Na Allaah ni Mwenye enzi ya nguvu Asiyeshindika, Mwenye hikmah wa yote. [Al-Maaidah: 38 ]

 

Vile vile anapozini mwanamke anapatiwa adhabu sawa na mwanamme, kama Alivyosema Aliyetukuka:

الزَّانِيَةُ وَالزَّانِي فَاجْلِدُوا كُلَّ وَاحِدٍ مِّنْهُمَا مِائَةَ جَلْدَةٍ ۖ وَلَا تَأْخُذْكُم بِهِمَا رَأْفَةٌ فِي دِينِ اللَّـهِ إِن كُنتُمْ تُؤْمِنُونَ بِاللَّـهِ وَالْيَوْمِ الْآخِرِ ۖ وَلْيَشْهَدْ عَذَابَهُمَا طَائِفَةٌ مِّنَ الْمُؤْمِنِينَ ﴿٢﴾

Mzinifu mwanamke na mzinifu mwanamme mpigeni kila mmoja katika wawili hao mijeledi mia. Na wala isiwashikeni huruma kwa ajili yao katika hukmu ya Allaah mkiwa nyinyi mnamwamini Allaah na Siku ya Mwisho. Na washuhudie adhabu yao kundi la Waumini. [An-Nuwr: 2]

 

Katika Aayah moja, Allaah Aliyetukuka Amebaini matendo chungu nzima ambayo yanafaa yafanywe na jinsiya zote mbili. Hapo hapo akaahidi Aliyetukuka kuwa mwenye kufanya hayo basi atapata maghfira na ujira mkubwa. Allaah Anasema:

إِنَّ الْمُسْلِمِينَ وَالْمُسْلِمَاتِ وَالْمُؤْمِنِينَ وَالْمُؤْمِنَاتِ وَالْقَانِتِينَ وَالْقَانِتَاتِ وَالصَّادِقِينَ وَالصَّادِقَاتِ وَالصَّابِرِينَ وَالصَّابِرَاتِ وَالْخَاشِعِينَ وَالْخَاشِعَاتِ وَالْمُتَصَدِّقِينَ وَالْمُتَصَدِّقَاتِ وَالصَّائِمِينَ وَالصَّائِمَاتِ وَالْحَافِظِينَ فُرُوجَهُمْ وَالْحَافِظَاتِ وَالذَّاكِرِينَ اللَّـهَ كَثِيرًا وَالذَّاكِرَاتِ أَعَدَّ اللَّـهُ لَهُم مَّغْفِرَةً وَأَجْرًا عَظِيمًا ﴿٣٥﴾

Hakika Waislamu wanaume na wanawake, na Waumini wanaume na wanawake, na watiifu wanaume na wanawake, na wasemao kweli wanaume na wanawake, na wanaosubiri wanaume na wanawake, na wanyenyekevu wanaume na wanawake, na watoao swadaqah wanaume na wanawake, na wafungao Swawm wanaume na wanawake, wanaojihifadhi tupu zao wanaume na wanawake, na wanaomdhukuru Allaah kwa wingi wanaume na wanawake; Allaah Amewaandalia maghfirah na ujira adhimu. [Al-Ahzaab: 35]

 

Hivyo, wanawake wamebashiriwa Pepo na neema nyingi sana. Wakati wa Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) aliwabashiria wanawake miongoni mwa Swahabiyah ishirini kuwa wataingia Peponi kulingana na Hadiyth kadhaa. Miongoni mwao ni Khadiyjah bint Khuwaylid, 'Aaishah bint Abubakar, Zaynab bint Jahsh, Hafswah bint 'Umar, Faatwimah bint Rasuul, Asmaa bint Abubakar, Umm Sulaym Rumayswaa' bint Milhaan, Asmaa bint Yaziyd, Nusaybah bint Ka'b, Sumayyah bint Khabbaat, Barakah bint Tha'labah na wengineo.

 

Hilo la kuwa wanaume watakaoingia Peponi wamebashiriwa wanawake ambao ni hurul 'ayn (wanawake wenye macho mazuri na makubwa) ni kweli kwani Aayah za Qur-aan zipo wazi kuhusu hilo. Zipo Aayah kadha kuhusu hili lakini inatosha kunukuu moja. Allaah Aliyetukuka Anatueleza:

فِيهِنَّ قَاصِرَاتُ الطَّرْفِ لَمْ يَطْمِثْهُنَّ إِنسٌ قَبْلَهُمْ وَلَا جَانٌّ ﴿٥٦﴾

Mna humo wanawake wenye staha wanaoinamisha macho, hajawabikiri binadamu kabla yao wala jini. [Ar-Rahmaan: 56]

 

Sehemu hii ya pili ambayo tumeipigia msitari imekaririwa tena katika surah hii hii aayah ya 74.

 

Wanawake Peponi watakuwa ni aina mbili. Aina ya kwanza ni wale wanawake wa duniani waliotenda matendo mema, Allaah Aliyetukuka Atawajazi na kuwaingiza Peponi pamoja na waume zao ikiwa walikuwa wema pia. Anasema Allaah Mtukufu:

إِنَّا أَنشَأْنَاهُنَّ إِنشَاءً ﴿٣٥﴾فَجَعَلْنَاهُنَّ أَبْكَارًا ﴿٣٦﴾عُرُبًا أَتْرَابًا ﴿٣٧﴾

Hakika Sisi Tunawaanzisha (huwrun-’iyn) uanzishaji. Tunawafanya mabikra. Wenye mahaba, ashiki na bashasha kwa waume zao, hirimu moja. [Al-Waaqi'ah: 35 – 37]

 

Pia,

وَالَّذِينَ آمَنُوا وَاتَّبَعَتْهُمْ ذُرِّيَّتُهُم بِإِيمَانٍ أَلْحَقْنَا بِهِمْ ذُرِّيَّتَهُمْ وَمَا أَلَتْنَاهُم مِّنْ عَمَلِهِم مِّن شَيْءٍ ۚ كُلُّ امْرِئٍ بِمَا كَسَبَ رَهِينٌ ﴿٢١﴾

Na wale walioamini na wakafuatwa na dhuriya wao kwa iymaan, Tutawakutanisha nao dhuriya wao na Hatutawapunguzia katika ‘amali zao kitu chochote. Kila mtu atawekewa rehani kwa yale aliyoyachuma. [Atw-Twuwr: 21]

 

Hizi Aayah zinaonyesha ikiwa mumeishi hapa duniani kama mume na mke kwa wema Allaah kwa rehema Yake Atawaungisha tena muishi pamoja lakini wakati huu nyote mtakuwa vijana hata kama mlikufa mkiwa wazee.

 

Wanawake aina ya pili ni wale walioumbwa na Allaah Aliyetukuka kwa ajili ya Pepo tu. Hawa watakuwa ni wenye kupewa wanaume waliowema kama jazaa yao. Kwa vile wanaume kimaumbile kuanzia hapa duniani ni wenye kuoa wake wengi Allaah pia Akhera Atawatunukia hadhi hiyo hiyo. Hekima ya hilo linajulikana na Allaah. Lakini kwa kuzingatia hekima ya mwanamume kuruhusiwa kuoa zaidi ya mke mmoja tutapata busara ya hilo ndilo hilo litakavyokuwa Peponi. Huku si kuwadunisha wanawake bali ni Muumba kuangalia maslahi na maumbile ya kila mmoja. Hapa leo ikiwa utamfanya mke mmoja awe na waume wanne basi utampatia shida na mtihani mkubwa mwanamke huyo, lakini kwa mwanaume ni jambo la kawaida tu.

 

Ama kuhusu swali lako la pili ni jambo ambalo liko wazi kabisa kwa udhaifu wa wanawake katika kukumbuka mas-ala ya nambari na hesabu.

 

Hakika ni kuwa kauli ya mwanamke si nusu. Inaonyesha hapa mmechanganya baina ya mambo mawili tofauti.

 

Suala la kwanza ni je, ushahidi wa mwanamke ni nusu wa ule wa mwanamme? Hakika jambo hili lipo wazi kabisa kwa kila mwenye kutaka ukweli bila ya kuwa na ubaguzi wala nadharia zake mwenyewe za awali. Kwa hukumu hii mwanamke hajadunishwa wala kudharauliwa. Hakika ni kuwa hukumu hii inakwenda sambamba na maumbile yake na saikolojia ya mwanamke inakuwa wazi kulingana na dondoo za wana-saikolojia, wataalamu wa magonjwa ya akili na tafiti za kitabibu.

 

Aayah hii ya Qur-aan:

 

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا إِذَا تَدَايَنتُم بِدَيْنٍ إِلَىٰ أَجَلٍ مُّسَمًّى فَاكْتُبُوهُ ۚ وَلْيَكْتُب بَّيْنَكُمْ كَاتِبٌ بِالْعَدْلِ ۚ وَلَا يَأْبَ كَاتِبٌ أَن يَكْتُبَ كَمَا عَلَّمَهُ اللَّـهُ ۚ فَلْيَكْتُبْ وَلْيُمْلِلِ الَّذِي عَلَيْهِ الْحَقُّ وَلْيَتَّقِ اللَّـهَ رَبَّهُ وَلَا يَبْخَسْ مِنْهُ شَيْئًا ۚ فَإِن كَانَ الَّذِي عَلَيْهِ الْحَقُّ سَفِيهًا أَوْ ضَعِيفًا أَوْ لَا يَسْتَطِيعُ أَن يُمِلَّ هُوَ فَلْيُمْلِلْ وَلِيُّهُ بِالْعَدْلِ ۚ وَاسْتَشْهِدُوا شَهِيدَيْنِ مِن رِّجَالِكُمْ ۖ فَإِن لَّمْ يَكُونَا رَجُلَيْنِ فَرَجُلٌ وَامْرَأَتَانِ مِمَّن تَرْضَوْنَ مِنَ الشُّهَدَاءِ أَن تَضِلَّ إِحْدَاهُمَا فَتُذَكِّرَ إِحْدَاهُمَا الْأُخْرَىٰ ۚ وَلَا يَأْبَ الشُّهَدَاءُ إِذَا مَا دُعُوا ۚ وَلَا تَسْأَمُوا أَن تَكْتُبُوهُ صَغِيرًا أَوْ كَبِيرًا إِلَىٰ أَجَلِهِ ۚ ذَٰلِكُمْ أَقْسَطُ عِندَ اللَّـهِ وَأَقْوَمُ لِلشَّهَادَةِ وَأَدْنَىٰ أَلَّا تَرْتَابُوا ۖ إِلَّا أَن تَكُونَ تِجَارَةً حَاضِرَةً تُدِيرُونَهَا بَيْنَكُمْ فَلَيْسَ عَلَيْكُمْ جُنَاحٌ أَلَّا تَكْتُبُوهَا ۗ وَأَشْهِدُوا إِذَا تَبَايَعْتُمْ ۚ وَلَا يُضَارَّ كَاتِبٌ وَلَا شَهِيدٌ ۚ وَإِن تَفْعَلُوا فَإِنَّهُ فُسُوقٌ بِكُمْ ۗ وَاتَّقُوا اللَّـهَ ۖ وَيُعَلِّمُكُمُ اللَّـهُ ۗ وَاللَّـهُ بِكُلِّ شَيْءٍ عَلِيمٌ ﴿٢٨٢﴾ 

Enyi walioamini! Mtakapokopeshana deni mpaka muda maalumu uliopangwa, basi liandikeni. Na aandike baina yenu mwandishi kwa uadilifu. Na wala asikatae mwandishi kuandika kama Allaah Alivyomfunza. Basi aandikishe kwa imla yule ambaye ana haki (mdai) na amuogope Allaah, Rabb wake, na wala asipunguze humo kitu chochote. Basi ikiwa yule ambaye ana haki amepumbaa kiakili au mnyonge, au hawezi kuandikisha mwenyewe, basi aandikishe msimamizi wake kwa uadilifu. Na mshuhudishe mashahidi wawili wanaume miongoni mwenu. Na ikiwa hakuna wanaume wawili, basi mwanamme mmoja na wanawake wawili katika wale mnaowaridhia miongoni mwa mashahidi, ili kama mmoja wao hao wanawake wawili akikosea (akasahau), basi mmoja wao atamkumbusha mwengine. Na mashahidi wasikatae watapoitwa. Na wala msichukie kuliandika (deni) dogo au kubwa mpaka muda wake. Hivyo kwenu ndiyo uadilifu upasavyo mbele ya Allaah na ndio unyoofu zaidi kwa ushahidi; na ni karibu zaidi ili msiwe na shaka; isipokuwa itakapokuwa biashara taslimu mnayoiendesha baina yenu, basi si dhambi kwenu msipoiandika. Na shuhudisheni mnapouziana. Na wala asidhuriwe mwandishi wala shahidi; na mkifanya basi hakika huo ni ufasiki kwenu. Na mcheni Allaah, na Allaah Anakufunzeni, na Allaah kwa kila kitu ni Mjuzi.

[Al-Baqarah: 282] inazungumzia hitaji hilo la ushahidi kuhusu kukopeshana.

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Anatoa muongozo kwa mambo yanayohusiana na majukumu ya pesa. Katika kipengele hiki, hitaji la kuandika mahusiano ya pesa limenukuliwa kwa mkazo, "Basi liandikeni". Baada ya hapo ayah inazungumzia kuhusu wajibu wa mwandishi au mhusika wa kutayarisha mkataba kwa ibara za kisasa. Ayah pia, inagusia ikiwa mhusika (mkopaji) ni mpumbavu au mnyonge au hawezi kuandikisha, basi walii wake awe ni mwenye kuchukua jukumu hilo kwa niaba yake na achague mashahidi wawili walio waadilifu. Ifahamike kuwa hili linatokea tu ikiwa mhusika hana uwezo wa kuandika mkataba. Kwa hiyo, mashahidi wanakuwa ndio wenye kuchunga kuwa haki lazima ifanyike.

 

Baada ya hapo ndio Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Anaweka sharti la kuita mashahidi wawili wanaume na ikiwa hawapo basi mwanaume na wanawake wawili. Kisha Aayah inaelezea umuhimu wa kuandikiana ikiwa mkataba wenyewe ni mkubwa au mdogo. Qur-aan inazidi kutuelimisha kuwa kuwa si mara zote inawezekana kuandikiana mikataba hivyo, ikiwa haiwezekani basi kuwe na mashahidi wenye kushuhudia hilo.

 

Lengo hasa la kutoa utangulizi huo ni kuwavutia watu kwa ile hakika kuwa ushahidi wa wanawake hapa hauhusiani na hadhi yao bali ni juu ya mikataba ya kibiashara. Hapa Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Anatubainishia wazi kuwa wanaotakiwa ni mashahidi wanne bila kubagua kama ni wanawake au wanaume. Pale ambapo Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Anatulezea kuhusu ushahidi wa wanaume wawili au mwanaume na wanawake wawili ni katika mas-ala ya deni. Anasema Aliyetukuka:

 

وَاسْتَشْهِدُوا شَهِيدَيْنِ مِن رِّجَالِكُمْ ۖ فَإِن لَّمْ يَكُونَا رَجُلَيْنِ فَرَجُلٌ وَامْرَأَتَانِ مِمَّن تَرْضَوْنَ مِنَ الشُّهَدَاءِ أَن تَضِلَّ إِحْدَاهُمَا فَتُذَكِّرَ إِحْدَاهُمَا الْأُخْرَىٰ

Na mshuhudishe mashahidi wawili wanaume miongoni mwenu. Na ikiwa hakuna wanaume wawili, basi mwanamme mmoja na wanawake wawili katika wale mnaowaridhia miongoni mwa mashahidi, ili kama mmoja wao hao wanawake wawili akikosea (akasahau), basi mmoja wao atamkumbusha mwengine. [Al-Baqarah: 282]

 

Ifahamike kuwa Allaah, Muumbaji, kwa hekima Yake isiyo kifani Anatoa maagizo ambayo yana manufaa tele kwa wanadamu. Yeye ndiye Muumbaji, hivyo, Anajua jambo ambalo litamsaidia mwanadamu mwenyewe. Katika mas-ala haya Allaah   (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kwa hekima Yake iliyo ya juu Ameweka hivyo kwa sababu ya kuwa wanawake si wazoefu katika mas-ala ya hesabu, hivyo wakiwa wawili wanaweza kukumbushana ikiwa mmoja wao ataghafilika. Wanawake hawakuwa ni wenye kujishughulisha katika biashara, hivyo kuwa jambo zito kwao na kwa kuwa halipo akili mwao anaweza kusahau mara moja.

 

Katika enzi hii ya sayansi tunaweza kupata umuhimu wa hukumu na sharia hii. Mengi yamevumbuliwa kuanzia wakati wa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam). Kila kukicha uvumbuzi mwingi zaidi unakuwa ni wenye kufanyika. Wanawake huwa wana duara la matatizo ya kisaikolojia kila mwezi. Alama za mfadhaiko zinakuwa ni zenye kuonekana mwanzo wa mimba, wakati wa mimba na baada yake, hali ya kukakita damu, shida ya kifiziolojia na saikolojia kwa ajili ya utasa na matatizo ya kisaikolojia baada ya kutisha (kuharibika mimba). Ni katika hali hizi ndio wanawake wanapata uchovu wa kisaikolojia ambao unaleta mfadhaiko, kukosa umakinifu, akili kuwa pole na ukosefu wa hifdhi kwa muda mfupi.

 

Utafiti unaonyesha kuwa wasichana kabla ya kupata ada yao ya mwezi wanapata mabadiliko ya kisaikolojia. Maelezo ni kama yafuatayo: "Tafiti nyingi zimeripoti kuwa kuna ongezo la athari hasi katika kipindi kabla ada ya mwezi. Katika hayo ni hisia nyingi ikijumlisha kusumbua, mfadhaiko, wasiwasi, huzuni, kujihisi kuwa hako salama, machofu, upweke, kudondokwa na machozi, kukosa utulivu na mabadiliko ya hali. Katika tafiti nyingi, watafiti wameona shida kutofautisha baina ya athari hasi…" (Psychological Medicine, Monograph Suppliment 4, 1983, Cambridge University Press, uk. 6).

 

Naye C. Shreeves ameandika: "Nguvu za umakinifu na hifadhi zinapungua ni jambo la kawaida katika kipindi kabla ya mwanamke kuingia katika ada yake. tatizo hili linaweza kutatuliwa tu ugonjwa wenyewe utatibiwa" (The Pre-Menstrual Syndrome).

 

Wakati wanawake wakiwa na mimba wanapata mfadhaiko na matatizo ya kiakili na hofu (Psychiatry in Practice, Oktoba-Novemba 1986, uk. 6). Matatizo kama haya yanaendelea mimba inapokua kubwa. Nako kukatika kwa damu ambako kunaanza katikati ya miaka thelathini hadi hamsini kunakuja na shida zake nyengine. Kuhusu hili Dkt. Jennifer al-Knopf anasema: "…Wanawake hawajui miili yao inawafanya nini.. Baadhi yao wanaripoti ishara ya udhoofu kwa kutokwa jasho usiku, kutopata usingizi, mwasho, mbadiliko wa hali, kupoteza hifdhi kwa muda, kuumwa na kichwa, kupatwa na kukojoa ambao si kawaida na kuongeza mwili. Mabadiliko haya yanapatikana kwa kupungua kwa hormoni za kike kama oestrogen na progesterone, ambazo zinatawala mduara wa uzazi" (Newsweek International, 25 Mei 1992) 

 

Kuharibu mimba kwa mwanamke kunamletea mabadiliko mengine ya kisaikolojia na athari nyingine hasi. Wanawake wanakuwa na wasiwasi kwa asilimia kubwa zaidi kuliko wanaume pamoja na kuwa na hamu.

 

Kwa yaliyopatikana na wana-saikolojia, wataalamu wa akili na watafiti kama tulivyonukuu hapo juu tunaweza kuelewa kauli ya Aliyetukuka:

 

وَاسْتَشْهِدُوا شَهِيدَيْنِ مِن رِّجَالِكُمْ ۖ فَإِن لَّمْ يَكُونَا رَجُلَيْنِ فَرَجُلٌ وَامْرَأَتَانِ مِمَّن تَرْضَوْنَ مِنَ الشُّهَدَاءِ أَن تَضِلَّ إِحْدَاهُمَا فَتُذَكِّرَ إِحْدَاهُمَا الْأُخْرَىٰ

Na mshuhudishe mashahidi wawili wanaume miongoni mwenu. Na ikiwa hakuna wanaume wawili, basi mwanamme mmoja na wanawake wawili katika wale mnaowaridhia miongoni mwa mashahidi, ili kama mmoja wao hao wanawake wawili akikosea (akasahau), basi mmoja wao atamkumbusha mwengine. [Al-Baqarah: 282]

 

Ndio Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akatuusia: " Wafanyieni wema wanawake. Mwanamke ameumbwa na ubavu, na sehemu iliyopinda zaidi ni ya juu. Ukijaribu kuinyoosha itavunjika, na ukiiacha itabaki kama ilivyo. Kwa hiyo, watendeeni wema wanawake". Katika riwaya nyingine: " Ukijaribu kuunyoosha utamvunja na kumvunja ni kumtaliki" [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

Maneno ya Aayah hii yaonyesha kwa uwazi kabisa kuwa msingi wa kanuni hii si kubagua baina ya jinsia lakini ni uwezo wa kuhifadhi wa wanawake. Aayah inatoa hakika ya kibayolojia – kuwa wanawake si wazuri katika kukumbuka vitu kama wanaume. Hii ndio sababu, ikiwa tutakubali ushahidi wa wanawake katika kesi za deni, ni lazima wawe wawili, ili kwa wakati wowote wa mustakbali, ikiwa wanahitajika kutoa ushahidi, mmoja wao ataweza kufidia udhaifu wa hifdhi wa mwenziwe.

 

Utafiti wa sasa kuhusu suala hili umeyakinisha ukweli huu wa Qur-aan, kuwa hifdhi na kumbukumbu za wanawake ni dhaifu kuliko za wanaume. Wanasayansi wa Urusi wametafiti hili kwa kina, na hitimisho lao lilichapishwa katika kitabu. Ufupisho wake ulitokea katika gazeti moja India ukiwa na anwani, "Uwezo wa Kuhifadhi S". "Wanaume wana uwezo mkubwa zaidi wa kuhifadhi na kufanyia kazi maalumati ya hesabu kuliko wanawake, lakini wanawake ni wazuri zaidi kwa maneno na kauli". Alisema mwanasayansi wa Urusi , "Wanaume wanatawala masomo ya hesabu kwa kuwa na sifa ya kuhifadhi ya kipekee" (Dr. Vladimir Konovalov, Memorising Ability, New Delhi edition of the Times of India, Januari 18, 1985).

 

Mbali na serikali ya Kenya kutaka kuona kuwa wasichana nao wanafanikiwa katika somo la hesabu pamoja na masomo ya sayansi utakuta kila matokeo yanapotoka yanakuwa ni kama yale ya miaka iliyopita. Ni wasichana wachache wanaofaulu katika mitihani hiyo kuliko wavulana.

 

Mas-ala ya pili ni kuwa, je ushahidi wa mwanamke ni sawa na wa mwanaume au wake ni duni zaidi? Hili lipo wazi kabisa katika Aayah kadhaa ila hii ya deni. Tunaposoma katika Suwrah An Nuwr pale ambapo Allaah Aliyetukuka Anatufahamisha:

وَالَّذِينَ يَرْمُونَ الْمُحْصَنَاتِ ثُمَّ لَمْ يَأْتُوا بِأَرْبَعَةِ شُهَدَاءَ 

Na wale wanaowasingizia wanawake watwaharifu kisha hawaleti mashahidi wanne.. [An-Nuwr: 4]

 

Pia tunasoma kuhusu mashahidi wa wasiya:

 يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا شَهَادَةُ بَيْنِكُمْ إِذَا حَضَرَ أَحَدَكُمُ الْمَوْتُ حِينَ الْوَصِيَّةِ اثْنَانِ ذَوَا عَدْلٍ مِّنكُمْ أَوْ آخَرَانِ مِنْ غَيْرِكُمْ إِنْ أَنتُمْ ضَرَبْتُمْ فِي الْأَرْضِ فَأَصَابَتْكُم مُّصِيبَةُ الْمَوْتِ ۚ  

Enyi walioamini! Mauti yanapomfikia mmoja wenu wakati anapousia, basi chukueni ushahidi wa wawili wenye uadilifu miongoni mwenu; au wawili wengineo wasiokuwa nyinyi pale mnapokuwa safarini ukakufikeni msiba wa mauti. [Al-Maaidah: 106]

 

Pia:

وَالَّذِينَ يَرْمُونَ أَزْوَاجَهُمْ وَلَمْ يَكُن لَّهُمْ شُهَدَاءُ إِلَّا أَنفُسُهُمْ فَشَهَادَةُ أَحَدِهِمْ أَرْبَعُ شَهَادَاتٍ بِاللَّـهِ ۙ إِنَّهُ لَمِنَ الصَّادِقِينَ ﴿٦﴾

Na wale wanaowasingizia wake zao na hawana mashahidi isipokuwa nafsi zao, basi ushahidi wa mmoja wao utakuwa ni kushuhudia.. [An-Nuwr: 6]

 

Pia kuhusu talaka, anasema Aliyetukuka:

فَإِذَا بَلَغْنَ أَجَلَهُنَّ فَأَمْسِكُوهُنَّ بِمَعْرُوفٍ أَوْ فَارِقُوهُنَّ بِمَعْرُوفٍ وَأَشْهِدُوا ذَوَيْ عَدْلٍ مِّنكُمْ

Na watakapokaribia kufikia muda wao, basi wazuieni kwa wema, au farikianeni nao kwa wema, na mshuhudishe mashahidi wawili wenye uadilifu miongoni mwenu.. [Atw-Twalaaq: 2]

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

Share