Hedhi: Amepata Hedhi Karibu Magharibi Je Alipe Swawm?

SWALI:

asalam aleykum,nina suali nataka kuliuliza,nilimaliza period yangu tarehe

1.10.06 na siku ya ijumaa tarehe 6.10.06 nataka kuswali maghrib nikaiyona damu kwa umbali ,haikutoka tena leo tarehe 8.10.06 nimeiyona lakini sio rangi ya damu sasa naweza kuendelea na saumu yangu na swala au mpaka nioshe?au siruhusiwi kuswali nakufunga?shukran jazakumu llah

 

 


 JIBU:

Sifa zote njema anastahiki Allah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu 'anhum)  na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 Tunategemea kuwa siku zako za hedhi na kama kawaida ya wengine wa wanawake kupata baina ya siku tano na nane takriban.  

Katika mas-ala haya ya muda wa hedhi na nifaas, Maulamaa wamekhtilafiana kuhusu muda wa hedhi, na kauli iliyokubalika zaidi ni kwamba hakuna muda maalum wa siku za hedhi au nifaas ingawa pia wengine wameona kuwa ihesabiwe tokea siku ya mwanzo ya damu hadi ifikie siku kumi na tano ihesabike kuwa ni hedhi na baada ya hapo mwanamke anaweza kuswali na kufunga na endapo baada ya hapo mwanamke ataona damu itakuwa ni 'istihaadhwah'.   (Damu ya kawaida mbali na ya hedhi au nifaas).

Kitu kitakachowajulisha kuwa ni damu ya hedhi au nifaas ni kwamba sifa zifuatazo ziangaliwe katika damu kutambua ni aina gani ya damu:

Rangi:       

Damu ya hedhi huwa ni nyekundu iliyoiva kukaribia kuwa nyeusi na damu ya 'istihaadhwah' ni nyekundu inayong'aa (bright red)

Shakili yake: 

Damu ya hedhi huwa nzito, ama ya 'istihaadhwah' huwa ni nyepesi.

Harufu:     

Damu ya hedhi huwa ina harufu ya kukirihisha, ama damu ya 'istihaadhwah' haina harufu kwani huwa inatoka katika mishipa ya kawaida katika mwili wa binaadamu.

Hivyo baada ya kuhakikisha sifa hizo utaweza kujua ni aina gani ya damu hiyo. Na ikiwa ni damu ya hedhi basi, kwa vile umeona damu ulipotaka kuswali Magharibi, bila shaka itakuwa imetoka kabla ya Magharibi, na hata kama ni muda wa dakika chache tu kabla ya Magharibi, basi Swawm yako itakuwa haifai, itakubidi ulipe siku hiyo.

Na Allah Anajua zaidi

 

Share